Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, inafaa dada ajifunike kichwa anapotafsiri kwa lugha ya ishara hotuba za Biblia kwenye mikutano ya Kikristo, au kwenye makusanyiko?

Kwa kawaida, mwanamke Mkristo anapaswa kujifunika kichwa anapotimiza migawo ambayo inapaswa kutimizwa na mume wake au ndugu katika kutaniko. Jambo hilo linapatana na kanuni iliyotolewa na mtume Paulo kwamba “kila mwanamke ambaye husali au kutoa unabii kichwa chake kikiwa hakijafunikwa hukiaibisha kichwa chake” kwa sababu “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Kor. 11:3-10) Dada anapojifunika kitambaa kizuri na kinachofaa katika hali kama hizo, anaonyesha kwamba anajitiisha kwa mpango wa kitheokrasi katika kutaniko la Kikristo.—1 Tim. 2:11, 12. *

Namna gani ikiwa dada anatafsiri katika lugha ya ishara hotuba ambayo inatolewa na ndugu? Kwa kweli, dada huyo anawapitishia tu wahudhuriaji habari inayotolewa na msemaji. Hilo linamaanisha kwamba si yeye anayefundisha bali ni yule ndugu anayetoa hotuba. Hata hivyo, kutafsiri lugha ya ishara ni tofauti sana na kutafsiri lugha zinazozungumzwa. Kuhusu lugha zinazozungumzwa, wasikilizaji wanaweza kumkazia fikira msemaji na wakati uleule wamsikilize yule anayetafsiri. Pia, tofauti na dada wanaotafsiri lugha ya ishara, kwa kawaida, dada wanaotafsiri lugha zinazozungumzwa hawasimami mahali ambapo wanakaziwa fikira sana. Huenda nyakati nyingine wakaketi wanapotafsiri, au ikiwa wamesimama huenda wakamtazama msemaji badala ya kuwatazama wasikilizaji. Kwa hiyo, si lazima dada anayetafsiri lugha inayozungumzwa ajifunike kichwa.

Kwa kuongezea, kwa sababu ya maendeleo katika tekinolojia ambayo inatumiwa wakati hotuba zinapotafsiriwa katika lugha ya ishara, mara nyingi wahudhuriaji wanamkazia fikira yule anayetafsiri. Kwa kawaida, yule anayetafsiri anaonekana kwenye televisheni au kitambaa kikubwa, na huenda hata wahudhuriaji wasimwone msemaji. Hivyo, ingefaa dada anayetafsiri katika lugha ya ishara ajifunike kichwa ili aonyeshe kwamba si yeye anayetoa hotuba ila anatafsiri tu.

Mwongozo huu uliorekebishwa utatumiwa jinsi gani wakati wa kutafsiri katika lugha ya ishara sehemu za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, maonyesho, maelezo wakati wa Funzo la Biblia la Kutaniko, Mkutano wa Utumishi, na Funzo la Mnara wa Mlinzi? Je, dada ambaye anatafsiri katika lugha ya ishara anapaswa vilevile kujifunika kichwa katika pindi hizo? Katika hali fulani huenda isiwe lazima kwa dada kujifunika kichwa, kwa sababu wote wanaohudhuria wanapaswa kuelewa kwamba kwa kweli si yeye anayeongoza mkutano. Kwa mfano, inaweza kuwa hivyo wakati dada huyo anapotafsiri maelezo ya wahudhuriaji, hotuba zinazotolewa na akina dada, au maonyesho. Hata hivyo, anapaswa kujifunika kichwa anapotafsiri hotuba zinazotolewa na akina ndugu wakati wa mikutano hiyo, anapomtafsiria kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi, kiongozi wa Funzo la Biblia la Kutaniko, au anapoongoza katika kutoa ishara wakati wa kuimba nyimbo. Mkutano unapoendelea, huenda dada akawatafsiria ndugu, dada, watoto, na wazee wa kutaniko. Kwa sababu hiyo, huenda ikafaa zaidi ajifunike kichwa wakati wote wa mkutano.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Kwa habari zaidi kuhusu wakati ambapo wanawake Wakristo wanapaswa kujifunika kichwa, ona ukurasa wa 209 mpaka 212 wa kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu.”