Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sala Zako Zinafunua Nini Kukuhusu?

Sala Zako Zinafunua Nini Kukuhusu?

Sala Zako Zinafunua Nini Kukuhusu?

“Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.”—ZAB. 65:2.

1, 2. Kwa nini watumishi wa Yehova wanaweza kusali kwake wakiwa na hakika kwamba anawasikiliza?

YEHOVA hapuuzi kamwe maombi ya watumishi wake waaminifu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba anatusikiliza. Hata ikiwa mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wangesali kwa Mungu wakati uleule, bado angemsikiliza kila mmoja wao.

2 Akiwa na hakika kwamba Mungu alisikiliza maombi yake, mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.” (Zab. 65:2) Sala za Daudi zilijibiwa kwa sababu alikuwa mwabudu mshikamanifu wa Yehova. Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, dua zangu zinaonyesha kwamba ninamtumaini Yehova na kwamba ibada safi ndiyo hangaiko langu kuu? Sala zangu zinafunua nini kunihusu?’

Sali kwa Yehova kwa Unyenyekevu

3, 4. (a) Tunapaswa kusali kwa Mungu tukiwa na mtazamo gani? (b) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunasumbuliwa na ‘fikira zinazofadhaisha’ kwa sababu ya dhambi nzito?

3 Ili sala zetu zijibiwe, ni lazima tusali kwa Mungu kwa unyenyekevu. (Zab. 138:6) Tunapaswa kumwomba Yehova atuchunguze, kama Daudi alivyofanya aliposema hivi: “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.” (Zab. 139:23, 24) Badala ya kusali tu tunapaswa pia kumruhusu Mungu atuchunguze na tunapaswa kutii mashauri ya Neno lake. Yehova anaweza kutuongoza kwenye “njia ya mpaka wakati usio na kipimo,” na kutusaidia kufuata njia inayoongoza kwenye uzima wa milele.

4 Namna gani ikiwa tunasumbuliwa na ‘fikira zinazofadhaisha’ kwa sababu ya dhambi nzito? (Soma Zaburi 32:1-5.) Kujaribu kuinyamazisha dhamiri yenye hatia kunaweza kutufanya tunyauke kama mti ambao unapoteza maji yake wakati wa majira ya joto kali. Kwa sababu ya dhambi aliyotenda, Daudi alipoteza shangwe yake na hata labda akawa mgonjwa. Lakini alipata kitulizo kama nini alipoungama dhambi yake kwa Mungu! Fikiria shangwe ya Daudi alipohisi kwamba Yehova alikuwa ‘amemsamehe maasi yake.’ Kuungama dhambi kwa Mungu kunaweza kuleta kitulizo, na msaada wa wazee Wakristo utamsaidia mkosaji kuwa tena na hali nzuri ya kiroho.—Met. 28:13; Yak. 5:13-16.

Msihi Mungu na Kumshukuru

5. Kutoa dua kwa Yehova kunamaanisha nini?

5 Ikiwa mambo fulani yanatufanya tuwe na mahangaiko mengi, tunapaswa kufuata shauri hili la Paulo: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Flp. 4:6) “Kutoa dua” kunamaanisha “kusihi kwa unyenyekevu.” Tunapaswa kumsihi sana Yehova atusaidie na kutuongoza hasa wakati wa hatari au mateso.

6, 7. Kwa nini tunapaswa kumshukuru Mungu katika sala zetu?

6 Hata hivyo, tukisali tu wakati tunapohitaji kitu fulani, hilo linafunua nini kuhusu nia yetu? Paulo alisema kwamba tunapaswa kutoa maombi yetu ili yajulikane na Mungu “pamoja na kutoa shukrani.” Bila shaka, tuna sababu nzuri ya kumshukuru Mungu kutoka moyoni kama Daudi aliyesema hivi: “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na utukufu na heshima; kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako. Ufalme ni wako, Ee Yehova, Wewe unayejiinua kuwa kichwa juu ya wote. . . . Ee Mungu wetu, tunakushukuru na kulisifu jina lako zuri.”—1 Nya. 29:11-13.

7 Yesu alimshukuru Mungu kwa ajili ya chakula na kwa ajili ya mkate na divai ambayo ilitumiwa wakati wa Mlo wa Jioni wa Bwana. (Mt. 15:36; Marko 14:22, 23) Zaidi ya kuonyesha shukrani kama hiyo, tunapaswa ‘kumshukuru Yehova’ kwa ajili ya “kazi zake za ajabu kwa wana wa binadamu,” ‘maamuzi yake ya hukumu ya uadilifu,’ na kwa ajili ya neno lake, au ujumbe ambao unapatikana sasa katika Biblia.—Zab. 107:15; 119:62, 105.

Sali kwa Ajili ya Wengine

8, 9. Kwa nini tunapaswa kusali kwa ajili ya Wakristo wenzetu?

8 Bila shaka, tunasali kwa ajili yetu wenyewe, lakini tunapaswa pia kusali kwa ajili ya wengine, hata Wakristo ambao hatuwajui kwa jina. Hata ingawa huenda mtume Paulo hakuwajua waamini wote huko Kolosai, aliandika hivi: “Sikuzote sisi humshukuru Mungu Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo tunaposali kwa ajili yenu, kwa kuwa tulisikia juu ya imani yenu kuhusiana na Kristo Yesu na upendo mlio nao kwa watakatifu wote.” (Kol. 1:3, 4) Paulo alisali pia kwa ajili ya Wakristo wa Thesalonike. (2 The. 1:11, 12) Sala za aina hiyo zinafunua mengi kutuhusu na kuhusu jinsi tunavyowaona ndugu na dada zetu katika imani.

9 Sala zetu kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta na kwa ajili ya waandamani wao wa “kondoo wengine” zinaonyesha wazi hangaiko letu kwa ajili ya tengenezo la Mungu. (Yoh. 10:16) Paulo aliwaomba waabudu wenzake wasali kusudi ‘apewe uwezo wa kusema ili ajulishe siri takatifu ya habari njema.’ (Efe. 6:17-20) Je, tunasali kibinafsi kwa njia hiyo kwa ajili ya Wakristo wengine?

10. Kusali kwa ajili ya wengine huenda kukawa na uvutano gani juu yetu?

10 Kusali kwa ajili ya wengine kunaweza kubadili mtazamo wetu kuwaelekea. Tukisali kwa ajili ya mtu ambaye hatumpendi sana inaelekea hilo litabadili mtazamo wetu kumwelekea mtu huyo. (1 Yoh. 4:20, 21) Sala za aina hiyo zinajenga na zinachangia umoja pamoja na ndugu zetu. Zaidi ya hayo, sala kama hizo zinaonyesha kwamba tuna upendo kama wa Kristo. (Yoh. 13:34, 35) Sifa hiyo ni sehemu ya matunda ya roho ya Mungu. Je, tunasali kibinafsi ili tupewe roho takatifu, tukimwomba Yehova atusaidie kuonyesha matunda ya roho, yaani, upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia? (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Ikiwa ndivyo, maneno na matendo yetu yataonyesha kwamba tunatembea na kuishi kwa roho.—Soma Wagalatia 5:16, 25.

11. Kwa nini unaweza kusema kwamba ni jambo linalofaa kuwaomba wengine wasali kwa ajili yetu?

11 Tukipata habari kwamba watoto wetu wanashawishiwa kuiba mitihani shuleni, tunapaswa kusali kwa ajili yao na pia kutumia Maandiko ili kuwasaidia watende kwa unyoofu na kuepuka kufanya jambo lolote baya. Paulo aliwaambia Wakristo wa Korintho hivi: “Tunasali kwa Mungu kwamba msifanye kosa.” (2 Kor. 13:7) Sala za unyenyekevu za aina hiyo zinampendeza Yehova na zinafunua sifa zetu nzuri. (Soma Methali 15:8.) Tunaweza kuwaomba wengine wasali kwa ajili yetu, kama mtume Paulo alivyofanya. Aliandika hivi: “Endeleeni kusali kwa ajili yetu, kwa maana sisi tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Ebr. 13:18.

Sala Zetu Zinafunua Mambo Mengi Zaidi Kutuhusu

12. Ni mambo gani yanayopaswa kuwa ya maana sana katika sala zetu?

12 Je, sala zetu zinaonyesha kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova wenye furaha na bidii? Je, dua zetu zinakazia hasa kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu, kuhubiriwa kwa ujumbe wa Ufalme, kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, na kutakaswa kwa jina lake? Hayo yanapaswa kuwa mambo ya maana sana katika sala zetu, kama inavyoonyeshwa na sala ya Yesu ya kielelezo, ambayo inaanza kwa maneno haya: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mt. 6:9, 10.

13, 14. Sala zetu zinafunua nini kutuhusu?

13 Sala zetu kwa Mungu zinafunua nia, mapendezi, na tamaa zetu. Yehova anajua sisi ni watu wa aina gani. Andiko la Methali 17:3 linasema hivi: “Chungu cha kusafishia ni kwa ajili ya fedha na tanuru ni kwa ajili ya dhahabu, lakini Yehova ndiye mchunguzaji wa mioyo.” Mungu anaona yale yaliyo katika mioyo yetu. (1 Sam. 16:7) Anajua jinsi tunavyohisi kuhusu mikutano yetu, huduma yetu, na ndugu na dada zetu wa kiroho. Yehova anajua jinsi tunavyofikiri kuhusu “ndugu” za Kristo. (Mt. 25:40) Anajua ikiwa kwa kweli tunataka mambo tunayoomba katika sala au tunarudia-rudia tu maneno fulani. Yesu alisema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza [kimakosa] watasikiwa kwa kutumia maneno mengi.”—Mt. 6:7.

14 Mambo tunayosema katika sala yanafunua ni kwa kadiri gani tunamtegemea Mungu. Daudi alisema hivi: “[Yehova] umekuwa kimbilio langu, mnara wenye nguvu mbele ya uso wa adui. Nitakuwa mgeni katika hema lako mpaka nyakati zisizo na kipimo; nitakimbilia maficho ya mabawa yako.” (Zab. 61:3, 4) Kwa njia ya mfano, Mungu ‘anapotandaza hema lake juu yetu,’ tunafurahia usalama na ulinzi wake. (Ufu. 7:15) Inafariji kama nini kumkaribia Yehova katika sala tukiwa na uhakika wa kwamba yuko ‘upande wetu’ tunapokabili jaribu lolote la imani yetu!—Soma Zaburi 118:5-9.

15, 16. Sala inaweza kutusaidia kutambua nini kuhusu tamaa yetu ya kufikia mapendeleo ya utumishi?

15 Sala ya unyoofu kwa Yehova kuhusu nia yetu inaweza kutusaidia kutambua ukweli kuhusu nia hiyo. Kwa mfano, je, tunataka sana kutumikia katika pendeleo fulani la uangalizi kati ya watu wa Mungu kwa sababu tunatamani kwa unyenyekevu kusaidia na kufanya yote tunayoweza ili kuendeleza mambo ya Ufalme? Au je, inawezekana kwamba tunataka kuwa “mahali pa kwanza” au hata tunatamani ‘kupiga ubwana juu’ ya wengine? Mambo hayapaswi kuwa hivyo kati ya watu wa Yehova. (Soma 3 Yohana 9, 10; Luka 22:24-27.) Ikiwa tuna tamaa mbaya, kusali kwa unyoofu kwa Yehova Mungu kunaweza kufunua tamaa hizo na kutusaidia kubadilika kabla hazijatia mizizi.

16 Huenda wake Wakristo wakatamani sana waume wao watumike wakiwa watumishi wa huduma na labda baadaye wakiwa waangalizi, au wazee. Dada hao wanaweza kutenda kupatana na hisia ambazo wanaeleza katika sala zao za faraghani kwa kujitahidi kujiendesha wenyewe kwa njia nzuri. Hilo ni jambo la maana kwa sababu maneno na mwenendo wa familia unaweza kumfanya mtu aonwe na kutaniko kwa njia inayofaa au isiyofaa.

Kuwakilisha Wengine Katika Sala ya Watu Wote

17. Kwa nini ni vizuri kuwa peke yetu tunaposali faraghani?

17 Mara nyingi, Yesu alijitenga na umati wa watu ili asali kwa Baba yake faraghani. (Mt. 14:13; Luka 5:16; 6:12) Sisi pia, tunahitaji wakati fulani kuwa peke yetu. Tunaposali kwa utulivu katika mazingira yenye amani, inaelekea kwamba tutafanya maamuzi yatakayompendeza Yehova na ambayo yatatusaidia sana kubaki wenye nguvu kiroho. Hata hivyo, Yesu alisali pia hadharani, na ni vizuri kuchunguza jinsi tunavyoweza kusali hadharani kwa njia nzuri.

18. Ni mambo gani ambayo ndugu wanapaswa kukumbuka wanapoliwakilisha kutaniko katika sala ya watu wote?

18 Kwenye mikutano yetu, wanaume washikamanifu wanaliwakilisha kutaniko katika sala ya watu wote. (1 Tim. 2:8) Waamini wenzetu wanapaswa kusema “amina,” kumaanisha “na iwe hivyo,” mwishoni mwa sala hiyo. Hata hivyo, ili waseme “amina” ni lazima wakubaliane na yale yaliyosemwa. Katika ile sala ya kielelezo, Yesu hakusema jambo lolote lisilo la busara au lenye kushtua. (Luka 11:2-4) Zaidi ya hayo, hakutaja mahitaji yote au matatizo ya kila mtu kati ya wasikilizaji wake. Ni vizuri kutaja mahangaiko ya kibinafsi katika sala ya faraghani, bali si katika sala ya watu wote. Na tunapowakilisha kikundi cha watu katika sala, tunapaswa kuepuka kutaja mambo ya siri.

19. Tunapaswa kujiendesha jinsi gani wakati wa sala ya watu wote?

19 Tunapowakilishwa katika sala ya watu wote, tunapaswa kuonyesha heshima inayotokana na ‘kumwogopa Mungu.’ (1 Pet. 2:17) Kuna wakati unaofaa na mahali panapofaa pa kufanya mambo fulani ambayo si vizuri kuyafanya kwenye mkutano wa Kikristo. (Mhu. 3:1) Kwa mfano, tuseme kwamba mtu fulani anawahimiza watu wote katika kikundi washikane mikono wakati wa sala. Hilo linaweza kuwaudhi au kuwakengeusha wengine, kutia ndani wageni ambao si waamini wenzetu. Wenzi fulani wa ndoa wanaweza kushikana mikono kwa busara, lakini wakikumbatiana wakati wa sala ya watu wote, wanaweza kuwakwaza wale ambao wanaona mwenendo huo. Huenda wakafikiri au kuwa na maoni ya kwamba wenzi hao wanakazia fikira uhusiano wao wa kimahaba badala ya kumheshimu Yehova. Kwa sababu ya kumheshimu Mungu, acheni ‘tufanye mambo yote kwa utukufu wa Mungu’ na kuepuka mwenendo ambao unaweza kumkengeusha, kumshtua, au kumkwaza mtu yeyote.—1 Kor. 10:31, 32; 2 Kor. 6:3.

Tusali kwa Ajili ya Mambo Gani?

20. Unaweza kufafanua Waroma 8:26, 27 kwa njia gani?

20 Nyakati nyingine, huenda tusijue jambo la kusema katika sala zetu za faraghani. Paulo aliandika hivi: “Lile tatizo kuhusu tunalohitaji kusali hatujui, lakini roho [takatifu] yenyewe hutuombea pamoja na kuugua kusikotamkwa. Lakini [Mungu] ambaye huichunguza mioyo anajua ni nini maana ya roho.” (Rom. 8:26, 27) Yehova aliongoza mambo ili sala nyingi ziandikwe katika Maandiko. Anakubali maombi hayo yaliyoongozwa na roho yake kana kwamba ni maombi yetu wenyewe na hivyo anayatimiza. Mungu anatujua na anajua pia maana ya mambo ambayo aliongoza roho yake iseme kupitia waandikaji wa Biblia. Yehova anajibu dua zetu wakati roho ‘inapoomba,’ au kusihi, kwa ajili yetu. Lakini kadiri tunavyojua vizuri zaidi Neno la Mungu, ndivyo tunavyokumbuka kwa urahisi zaidi mambo tunayohitaji kuomba.

21. Tutachunguza nini katika habari ambayo inafuata?

21 Kama tulivyoona, sala zetu zinafunua mengi kutuhusu. Kwa mfano, zinaweza kufunua jinsi tulivyo na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova na jinsi tunavyolijua vizuri Neno lake. (Yak. 4:8) Katika habari inayofuata, tutachunguza sala na maombi fulani yaliyoandikwa katika Biblia. Inaelekea uchunguzi huo wa Maandiko utaboresha jinsi gani sala zetu kwa Mungu?

Ungesema Nini?

• Tunapaswa kuwa na mtazamo gani tunaposali kwa Yehova?

• Kwa nini tunapaswa kusali kwa ajili ya waamini wenzetu?

• Sala zetu zinaweza kufunua nini kutuhusu na kuhusu nia yetu?

• Tunapaswa kujiendesha jinsi gani wakati wa sala ya watu wote?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Je, unamsifu na kumshukuru Yehova kwa ukawaida?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Sikuzote mwenendo wetu wakati wa sala ya watu wote unapaswa kumheshimu Yehova