Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thamini Sana Mahali Pako Katika Kutaniko

Thamini Sana Mahali Pako Katika Kutaniko

Thamini Sana Mahali Pako Katika Kutaniko

“Mungu ameviweka viungo katika mwili, kila kimoja, kama vile alivyopenda.”—1 KOR. 12:18.

1, 2. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba kila mtu katika kutaniko anaweza kupata mahali ambapo anaweza kuthamini? (b) Ni maswali gani ambayo yatazungumziwa katika habari hii?

TANGU siku za Waisraeli wa kale, Yehova amekuwa akitumia mpango wa kutaniko ili kuwalisha watu wake kiroho na kuwapa mwongozo. Kwa mfano, baada ya Waisraeli kulishinda jiji la Ai, Yoshua ‘alisoma kwa sauti maneno yote ya sheria, baraka na laana, kulingana na yote ambayo yaliandikwa katika kitabu cha sheria mbele ya kutaniko lote la Israeli.’—Yos. 8:34, 35.

2 Katika karne ya kwanza W.K., mtume Paulo alimwambia mzee Mkristo Timotheo kwamba kutaniko la Kikristo lilikuwa “nyumba ya Mungu” na “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Tim. 3:15) “Nyumba” ya Mungu leo ni undugu wa ulimwenguni pote wa Wakristo wa kweli. Katika sura ya 12 ya barua yake ya kwanza kwa Wakorintho ambayo iliongozwa na roho ya Mungu, Paulo analinganisha kutaniko na mwili wa mwanadamu. Anasema kwamba hata ingawa kila kiungo kinafanya kazi tofauti, viungo vyote ni vya maana. Paulo anaandika hivi: “Mungu ameviweka viungo katika mwili, kila kimoja, kama vile alivyopenda.” Hata anataja kwamba “zile sehemu za mwili ambazo tunafikiri kuwa zina heshima kidogo, hizo tunazizungushia heshima nyingi zaidi.” (1 Kor. 12:18, 23) Hivyo, daraka la mtu mmoja mnyoofu katika nyumba ya Mungu si bora zaidi wala si baya zaidi linapolinganishwa na daraka la Mkristo mwingine mwaminifu. Daraka lake ni tofauti tu. Hivyo basi, tunaweza kupata jinsi gani na kuthamini sana mahali petu katika mpango wa Mungu? Ni mambo gani yanayoweza kuamua mahali petu katika kutaniko? Na tunaweza kufanya nini ili ‘maendeleo yetu yawe wazi kwa watu wote’?—1 Tim. 4:15.

Tunaweza Kuthamini Jinsi Gani Mahali Petu?

3. Ni njia gani moja ya kupata na kuonyesha kwamba tunathamini mahali petu katika kutaniko?

3 Njia moja ya kupata na kuonyesha kwamba tunathamini mahali petu katika kutaniko ni kushirikiana kikamili na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na Baraza Linaloongoza ambalo linamwakilisha. (Soma Mathayo 24:45-47.) Tunahitaji kuchunguza jinsi tunavyoitikia mwongozo tunaopata kutoka kwa jamii ya mtumwa. Kwa mfano, kwa miaka mingi tumekuwa tukipokea maagizo ya moja kwa moja kuhusu kuvaa na kujipamba, burudani, na matumizi yasiyofaa ya Intaneti. Je, tunatii kabisa mashauri hayo mazuri ili tulindwe kiroho? Namna gani shauri la kuwa na programu ya kawaida ya ibada ya familia? Je, tumetii kutoka moyoni shauri hilo na kutenga jioni moja kwa ajili ya kusudi hilo? Ikiwa sisi ni waseja, je, tunatenga wakati wa kujifunza kibinafsi Maandiko? Yehova atambariki kila mmoja wetu na pia familia zetu tukifuata mwongozo wa jamii ya mtumwa.

4. Tunapaswa kufikiria nini tunapofanya maamuzi ya kibinafsi?

4 Huenda watu fulani wakasema kwamba mambo kama vile kuvaa, kujipamba, na burudani ni mambo ya kibinafsi. Hata hivyo, Mkristo aliyejiweka wakfu ambaye anathamini sana mahali pake katika kutaniko, hapaswi kufikiria tu mapendezi yake mwenyewe anapofanya maamuzi. Ni lazima tufikirie hasa maoni ya Yehova ambayo yamefunuliwa kupitia Neno lake, Biblia. Ujumbe wa Biblia unapaswa kuwa ‘taa ya mguu wetu, na nuru kwa barabara yetu.’ (Zab. 119:105) Pia, ni jambo la hekima kufikiria jinsi maamuzi tunayofanya katika mambo ya kibinafsi yatavyokuwa na matokeo juu ya huduma yetu na watu wengine, ndani na nje ya kutaniko.—Soma 2 Wakorintho 6:3, 4.

5. Kwa nini tunapaswa kujilinda ili tusisitawishe roho ya kujitegemea?

5 “Roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii” imeenea sana hivi kwamba ni kama hewa tunayopumua. (Efe. 2:2) Roho hiyo inaweza kutufanya tufikiri kwamba hatuhitaji mwongozo kutoka kwa tengenezo la Yehova. Bila shaka, hatutaki kuwa kama Diotrefe, ambaye ‘hakupokea kwa heshima jambo lolote kutoka kwa mtume Yohana.’ (3 Yoh. 9, 10) Tunahitaji kujilinda ili tusisitawishe roho ya kujitegemea. Hatupaswi kamwe kusema au kufanya jambo lolote ambalo litaonyesha kwamba hatuheshimu njia ambayo Yehova anatumia leo kuwasiliana na sisi. (Hes. 16:1-3) Kinyume chake, tunapaswa kuthamini pendeleo letu la kushirikiana na jamii ya mtumwa. Na je, hatupaswi kujitahidi kuwatii na kuwanyenyekea wale wanaoongoza katika kutaniko letu?—Soma Waebrania 13:7, 17.

6. Kwa nini tunapaswa kuchunguza hali zetu wenyewe?

6 Njia nyingine ya kuonyesha kwamba tunathamini mahali petu katika kutaniko ni kuchunguza kwa uangalifu hali zetu wenyewe na kufanya yote tunayoweza ili ‘kuitukuza huduma yetu’ na kumletea Yehova heshima. (Rom. 11:13) Wahubiri fulani wanatumika wakiwa mapainia wa kawaida. Wengine wanatumika katika utumishi wa pekee wa wakati wote wakiwa wamishonari, waangalizi wanaosafiri, na washiriki wa familia za Betheli ulimwenguni pote. Ndugu na dada wengi wanasaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Wengi kati ya watu wa Yehova wanafanya yote wanayoweza ili kutimiza mahitaji ya kiroho ya familia zao na kushiriki kikamili katika huduma kila juma. (Soma Wakolosai 3:23, 24.) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunapojitoa kwa kupenda katika utumishi wa Mungu na kufanya yote tunayoweza ili kumtumikia kwa nafsi yote, sikuzote tutakuwa na mahali petu katika mpango wake.

Hali Zinazoamua Mambo Tunayoweza Kutimiza Kutanikoni

7. Eleza jinsi hali zetu zinavyoweza kuamua mahali petu katika kutaniko.

7 Ni jambo la maana kuchunguza hali zetu kwa sababu, kwa kadiri fulani, mahali petu au mambo tunayotimiza katika kutaniko yanategemea hali zetu na yale ambayo tunaweza kufanya. Kwa mfano, mambo ambayo ndugu anatimiza katika kutaniko yanatofautiana kwa njia fulani na yale ambayo dada anatimiza. Umri, afya, na hali nyingine zinaweza pia kuamua mambo tunayoweza kutimiza katika utumishi wa Yehova. Andiko la Methali 20:29 linasema, “Uzuri wa vijana ni nguvu zao, na utukufu wa wazee ni kichwa chao chenye mvi.” Washiriki wa kutaniko ambao ni vijana wanaweza kufanya mambo mengi zaidi yanayohitaji nguvu za kimwili kwa sababu ya nguvu zao za ujana, na wale waliozeeka wanaweza kulisaidia sana kutaniko kwa sababu ya hekima na uzoefu wao. Pia, tunahitaji kukumbuka kwamba jambo lolote ambalo tunaweza kufanya katika tengenezo la Yehova linategemea fadhili zisizostahiliwa za Mungu.—Mdo. 14:26; Rom. 12:6-8.

8. Tamaa ina matokeo gani kwa yale tunayofanya katika kutaniko?

8 Mfano wa dada wawili wa kimwili ambao ni vijana unakazia jambo lingine ambalo linaamua mahali petu katika kutaniko. Wote wawili wanamaliza masomo ya shule ya sekondari. Hali zao zinalingana. Wazazi wao wamejitahidi kabisa kuwatia moyo wote wawili wafanye utumishi wa painia wa kawaida baada ya kumaliza shule. Baada ya kumaliza shule, mmoja wao anakuwa painia, lakini yule mwingine anaanza kufanya kazi ya wakati wote ya mshahara. Ni nini kilichowaongoza kufanya maamuzi tofauti? Ni tamaa yao. Mwishowe, kila mmoja wao alifanya kile alichotaka kufanya. Je, hilo si jambo la kweli kwa wengi wetu? Tunahitaji kufikiria kwa uzito kuhusu yale ambayo tungependa kufanya katika utumishi wa Mungu. Je, tunaweza kuongeza muda tunaotumia katika utumishi huo, hata ikiwa ni lazima turekebishe hali zetu?—2 Kor. 9:7.

9, 10. Tunapaswa kufanya nini ikiwa hatuna tamaa ya kufanya mengi katika utumishi wa Yehova?

9 Namna gani ikiwa hatuna tamaa ya kufanya mengi katika utumishi wa Yehova na tuna mwelekeo wa kutimiza machache katika kutaniko? Katika barua yake kwa Wafilipi, Paulo alisema hivi: “Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” Ndiyo, Yehova anaweza kutenda ndani yetu na kuongoza nia yetu, au tamaa zetu.—Flp. 2:13; 4:13.

10 Hivyo basi, ni jambo zuri kumwomba Yehova atuchochee kuwa na tamaa ya kutaka kufanya mapenzi yake. Hivyo ndivyo Mfalme Daudi wa Israeli la kale alivyofanya. Alisali hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe. Nitembeze katika kweli yako na kunifundisha, kwa maana wewe ni Mungu wangu wa wokovu. Nimekutumainia mchana kutwa.” (Zab. 25:4, 5) Tunaweza kufanya vivyo hivyo kwa kusali kwamba Yehova atuchochee kuwa na tamaa ya kutaka kufanya mambo yanayompendeza. Tunapofikiria jinsi Yehova Mungu na Mwana wake wanavyohisi kuhusu mambo tunayotimiza kwa ajili yao, tunachochewa kuwathamini kwa moyo wetu wote. (Mt. 26:6-10; Luka 21:1-4) Hisia hiyo ya shukrani inaweza kutusukuma tumsihi Yehova atuchochee tukuze tamaa ya kutaka kufanya maendeleo ya kiroho. Nabii Isaya ametuwekea mfano kuhusu mtazamo ambao tunapaswa kusitawisha. Aliposikia sauti ya Yehova ikiuliza: “Nitamtuma nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?” nabii huyo alijibu hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.”—Isa. 6:8.

Unaweza Kufanya Maendeleo Jinsi Gani?

11. (a) Kwa nini kuna uhitaji wa ndugu kufikia mapendeleo katika tengenezo? (b) Ndugu anaweza kufikia jinsi gani mapendeleo ya utumishi?

11 Watu 289,678 walibatizwa ulimwenguni pote katika mwaka wa utumishi wa 2008, na hilo linaonyesha wazi kwamba kuna uhitaji mkubwa wa ndugu wa kuongoza. Ndugu anapaswa kufanya nini ili kutimiza uhitaji huo? Kwa ufupi, anapaswa kujitahidi kutimiza sifa za kustahili za wazee na watumishi wa huduma ambazo zimeonyeshwa katika Maandiko. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Ndugu anaweza kujitahidi jinsi gani ili kutimiza matakwa hayo ya Kimaandiko? Kwa kushiriki kwa bidii katika huduma, kutimiza kwa bidii migawo yake katika kutaniko, kujitahidi kuboresha maelezo yake kwenye mikutano ya Kikristo, na kupendezwa kibinafsi na waamini wenzake. Anapofanya hivyo anaonyesha kwamba anathamini sana mahali pake katika kutaniko.

12. Vijana wanaweza kuonyesha namna gani bidii yao kwa ajili ya kweli?

12 Ndugu vijana, hasa wale ambao ni matineja, wanaweza kufanya maendeleo jinsi gani katika kutaniko? Wanaweza kujitahidi kukua katika ‘hekima na utambuzi wa kiroho’ kwa kuendelea kupata ujuzi wa Maandiko. (Kol. 1:9) Kuwa wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu na kushiriki kwa bidii katika mikutano ya kutaniko bila shaka kutawasaidia kufanya maendeleo. Vijana wanaume wanaweza pia kufikia mapendeleo kwa kujitahidi kustahili kuingia kwenye “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji” mbalimbali katika utumishi wa wakati wote. (1 Kor. 16:9) Kufuatia mradi wa kumtumikia Yehova maishani ni njia inayoridhisha kwelikweli na inaleta baraka nyingi sana.—Soma Mhubiri 12:1.

13, 14. Akina dada wanaweza kuonyesha katika njia gani kwamba wanathamini sana daraka lao katika kutaniko?

13 Akina dada pia wanaweza kuonyesha kwamba wanathamini sana pendeleo lao la kushiriki kibinafsi katika kutimiza andiko la Zaburi 68:11. Andiko hilo linasema hivi: “Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.” Moja kati ya njia kuu zaidi ambazo akina dada wanaweza kuonyesha kwamba wanathamini mahali pao katika kutaniko ni kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Hivyo, dada wanaposhiriki kikamili katika huduma na kujidhabihu kwa kupenda kwa ajili ya kazi hiyo, wanathibitisha kwamba wanathamini sana daraka lao katika kutaniko.

14 Paulo alisema hivi alipomwandikia Tito: “Wanawake wenye umri mkubwa wawe wenye tabia ya kumhofu Mungu, . . . walimu wa yaliyo mema; ili kuziamsha akili za wanawake vijana wawapende waume zao, wawapende watoto wao, wawe na utimamu wa akili, safi kiadili, wafanyakazi nyumbani, wema, wakijitiisha kwa waume zao wenyewe, ili neno la Mungu lisitukanwe.” (Tito 2:3-5) Dada wakomavu wanaweza kuwachochea sana wengine katika kutaniko wafanye mema! Kwa kuwaheshimu ndugu ambao wanaongoza na kwa kufanya maamuzi yenye hekima maishani kuhusiana na mambo kama vile kuvaa, kujipamba, na burudani, wanawawekea wengine mfano mzuri na wanaonyesha kwamba wanathamini sana mahali pao katika kutaniko.

15. Dada mseja anaweza kufanya nini ili kukabiliana na upweke?

15 Nyakati nyingine, huenda ikawa vigumu kwa dada ambaye hajaolewa kutambua mahali pake katika kutaniko. Dada mmoja ambaye amekabili hali hiyo alisema hivi: “Mara kwa mara, maisha ya useja yanakuwa yenye upweke.” Alipoulizwa jinsi anavyokabiliana na hali hiyo, alisema hivi: “Kusali na kujifunza kunanisaidia kutambua tena mahali pangu. Ninajifunza kuhusu jinsi Yehova anavyoniona. Kisha ninajitahidi kujitolea kuwasaidia wengine katika kutaniko. Hilo linanisaidia kuwafikiria wengine badala ya kujifikiria tu.” Kulingana na Zaburi 32:8, Yehova alimwambia Daudi hivi: “Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” Ndiyo, Yehova anapendezwa kibinafsi na watumishi wake wote, kutia ndani dada waseja, naye atawasaidia wote kuona mahali pao katika kutaniko.

Kaa Mahali Pako!

16, 17. (a) Kwa nini kukubali mwaliko wa Yehova wa kuwa sehemu ya tengenezo lake ndio uamuzi bora zaidi tunaoweza kufanya? (b) Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kukaa mahali petu katika tengenezo la Yehova?

16 Kwa upendo, Yehova amemvuta kila mmoja wa watumishi wake ili awe na uhusiano pamoja naye. Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” (Yoh. 6:44) Kati ya mabilioni ya watu walio duniani, Yehova ametualika sisi binafsi ili tuwe sehemu ya kutaniko lake leo. Kukubali mwaliko huo ndio uamuzi bora zaidi ambao tumewahi kufanya. Mwaliko huo umefanya maisha yetu yawe na kusudi na maana. Tumepata shangwe na uradhi mkubwa kama nini kwa sababu tuna mahali petu katika kutaniko!

17 Mtunga-zaburi alisema hivi: “Yehova, nimependa makao ya nyumba yako.” Pia, aliimba hivi: “Mguu wangu utasimama mahali tambarare; kati ya makundi yaliyokutanika nitambariki Yehova.” (Zab. 26:8, 12) Mungu wa kweli ana mahali kwa ajili ya kila mmoja wetu katika tengenezo lake. Tukiendelea kufuata mwongozo wa kitheokrasi na kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu, tutaendelea kukaa mahali petu penye thamani katika mpango wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba Wakristo wote wana mahali pao katika kutaniko?

• Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunathamini sana mahali petu katika tengenezo la Mungu?

• Ni mambo gani yanayoweza kuamua mahali petu katika kutaniko?

• Watu wazima na vijana Wakristo wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanathamini sana mahali pao katika mpango wa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Ndugu wanaweza kufanya nini ili wafikie mapendeleo katika kutaniko?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Akina dada wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanathamini sana mahali pao katika kutaniko?