Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wathamini Ndugu na Dada Zako Viziwi!

Wathamini Ndugu na Dada Zako Viziwi!

Wathamini Ndugu na Dada Zako Viziwi!

LEO, watu wa Mungu ni familia kubwa ya ndugu na dada wa kiroho ambao urithi wao wa kiroho ulianza na wanaume na wanawake wa nyakati za kale. Wanatia ndani Samweli, Daudi, Samsoni, Rahabu, Musa, Abrahamu, Sara, Noa, na Abeli. Kuna watumishi wengi waaminifu wa Yehova ambao ni viziwi. Kwa mfano, watu wawili ambao walikuwa Mashahidi wa kwanza wa Yehova nchini Mongolia walikuwa wenzi wa ndoa viziwi. Na kwa sababu ya utimilifu wa waamini wenzetu walio viziwi huko Urusi, tulishinda kesi katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu.

Katika nyakati za kisasa, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameandaa vichapo katika lugha ya ishara na ameanzisha makutaniko na makusanyiko katika lugha ya ishara. (Mt. 24:45) Mambo hayo yote yamewasaidia sana viziwi. * Lakini je, umewahi kufikiria jinsi viziwi walivyojifunza kumhusu Mungu wa kweli na kufanya maendeleo katika kweli bila maandalizi hayo? Je, umefikiria jambo ambalo unaweza kufanya ili kuwasaidia viziwi wanaoishi katika eneo lenu?

Kabla ya Maandalizi ya Leo

Ikiwa ungewauliza viziwi fulani wenye umri mkubwa jinsi walivyojifunza kumhusu Mungu wangejibu namna gani? Huenda wangekuambia jinsi walivyohisi walipojifunza kwa mara ya kwanza kwamba Mungu ana jina—jinsi kujifunza kweli hiyo kulivyobadili maisha yao na kuwategemeza kwa miaka mingi kabla video au DVD za lugha ya ishara hazijatolewa ili kuwasaidia wajifunze mambo mazito zaidi kuhusu kweli za Kimaandiko. Huenda wakaeleza jinsi ilivyokuwa wakati ambapo mikutano ya Kikristo haikuwa ikiongozwa au kutafsiriwa katika lugha ya ishara. Badala yake, mtu fulani alikuwa akiketi kando yao na kuandika mambo makuu kwenye karatasi ili kuwasaidia waelewe mambo ambayo yalikuwa yanasemwa. Ndugu mmoja ambaye ni kiziwi alijifunza kweli za Biblia kwa njia hiyo kwa miaka saba kabla mtu wa kutafsiri mikutano katika lugha ya ishara hajapatikana.

Viziwi wenye umri mkubwa wanakumbuka jinsi walivyowahubiria watu wanaosikia. Kwenye mkono mmoja walishika kadi iliyokuwa imeandikwa ujumbe mfupi wa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwenye mkono mwingine walishika magazeti ya karibuni zaidi ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ilikuwa vigumu sana kuongoza funzo la Biblia pamoja na mtu mwingine aliye kiziwi wakitumia vichapo ambavyo wote wawili hawakuvielewa vizuri kabisa. Huenda wahubiri wenye umri mkubwa walio viziwi wanakumbuka jinsi walivyovunjika moyo wakati ambapo watu hawakuwaelewa na hivyo hawangeweza kuendelea kuzungumza nao kuhusu kweli za kiroho. Pia, wanaelewa jinsi mtu anavyohisi wakati anapompenda sana Yehova lakini hawezi kuonyesha upendo huo akiwa na uhakika. Kwa nini? Kwa sababu hawakuwa na uhakika ikiwa walielewa habari fulani kwa usahihi.

Hata ingawa wamekabili vizuizi hivyo vyote, ndugu na dada zetu viziwi wameendelea kushikilia utimilifu wao. (Ayu. 2:3) Wameendelea kumngojea Yehova kwa kutamani. (Zab. 37:7) Na sasa anawabariki kwa kuwapa vitu vingi kuliko wengi wao walivyotarajia.

Fikiria jitihada ambazo zilifanywa na ndugu mmoja kiziwi ambaye ni mume na baba. Kabla ya video za lugha ya ishara kutolewa, aliendelea kuongoza funzo la familia kwa uaminifu. Mwana wake anakumbuka hivi: “Sikuzote ilikuwa vigumu kwa baba kuongoza funzo la familia, kwa sababu mambo yote ambayo alitufundisha yalikuwa yameandikwa katika vichapo. Mara nyingi, hakuelewa vizuri habari zilizokuwa zimeandikwa. Nasi watoto tulifanya iwe vigumu hata zaidi. Tulimkosoa haraka wakati ambapo hakueleza mambo kwa usahihi. Ijapokuwa alikabili mambo hayo yote, sikuzote aliongoza funzo la familia. Alihisi kwamba ingawa nyakati nyingine aliaibika kwa sababu hakuelewa Kiingereza vizuri, lilikuwa jambo la maana sana kwetu kujifunza jambo fulani kumhusu Yehova.”

Pia, kuna mfano wa Richard, ndugu mwenye umri wa miaka 70 na kitu ambaye ni kiziwi na pia kipofu anayeishi huko Brooklyn, New York, Marekani. Richard anajulikana sana kwa sababu amezoea kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Ili ahudhurie mikutano, anasafiri kwa gari-moshi la chini ya ardhi akiwa peke yake. Anahesabu mara ambazo gari-moshi linasimama katika vituo mbalimbali ili ajue wakati wa kushuka. Wakati fulani wa majira ya baridi kali, kulikuwa na dhoruba kubwa ya theluji hivi kwamba mikutano haingeweza kufanywa. Wote katika kutaniko walijulishwa lakini kwa sababu fulani, Richard hakujulishwa. Wakati ndugu walipotambua jambo hilo walianza kumtafuta, walimkuta Richard akiwa amesimama nje ya Jumba la Ufalme, akingojea kwa subira milango ifunguliwe. Alipoulizwa ni kwa nini alitembea katika dhoruba, alijibu hivi: “Ninampenda Yehova.”

Unaweza Kufanya Nini?

Je, kuna viziwi ambao wanaishi katika eneo lenu? Je, unaweza kujifunza lugha ya ishara kwa kadiri fulani ili uweze kuwasiliana nao? Kwa kawaida, watu walio viziwi wanakuwa wenye fadhili na subira sana wanapowafundisha watu wengine lugha yao. Huenda ukakutana na kiziwi ukiwa katika shughuli zako za kibinafsi au katika huduma. Unaweza kufanya nini? Jaribu kuwasiliana. Tumia ishara, maandishi, michoro, picha, au tumia mambo hayo yote. Hata ikiwa mtu huyo anasema kwamba hapendezwi na kweli, mweleze Shahidi ambaye ni kiziwi au ambaye anajua lugha ya ishara kumhusu. Ujumbe wetu unaweza kumvutia zaidi mtu aliye kiziwi unapotolewa katika lugha ya ishara.

Labda unajifunza lugha ya ishara na kuhudhuria mikutano ya kutaniko la lugha ya ishara. Unaweza jinsi gani kupata ustadi zaidi katika kutoa ishara na kuelewa lugha hiyo? Ingawa huenda kuna wahubiri wengine ambao wanasikia katika kutaniko lenu, kwa nini msizungumze kwa kutumia lugha ya ishara? Hilo litawasaidia kufikiria katika lugha ya ishara, yaani, kwa kutazama. Nyakati nyingine, huenda ukashawishiwa kufanya jambo lililo rahisi, yaani, kuzungumza badala ya kutumia lugha ya ishara. Hata hivyo, unapojifunza lugha yoyote ile, ni lazima ujitahidi kabisa ili uzungumze kwa ufasaha.

Kujitahidi kabisa kutumia lugha ya ishara kunaonyesha kwamba tunawapenda na kuwaheshimu ndugu na dada zetu walio viziwi. Fikiria jinsi viziwi wanavyovunjika moyo kila siku kwa sababu hawawezi kuwaelewa watu kazini au shuleni. Ndugu mmoja ambaye ni kiziwi alisema hivi: “Kila siku, watu wanaonizunguka wanazungumza. Mara nyingi ninahisi upweke na pia ninahisi kwamba watu wananipuuza na hivyo ninaudhika, au hata kukasirika. Maneno hayawezi kueleza kikamili jinsi ninavyohisi nyakati nyingine.” Mikutano yetu inapaswa kuwa mahali penye kuburudisha ambapo ndugu na dada zetu viziwi wanapokea chakula cha kiroho na kufurahia mazungumzo na ushirika mchangamfu.—Yoh. 13:34, 35.

Pia, hatuwezi kusahau vikundi vingi vidogo zaidi vya viziwi ambavyo vinakutana pamoja na makutaniko ya wahubiri wenye uwezo wa kusikia. Mikutano inatafsiriwa kwa ajili yao. Ili waelewe kikamili habari zinazozungumziwa, washiriki wa kutaniko ambao ni viziwi wanaketi mbele katika Jumba la Ufalme. Hilo linawawezesha kumwona yule anayetafsiri na pia msemaji wakati uleule bila kuzuiwa na kitu chochote. Imeonekana kwamba washiriki wengine wa kutaniko wanazoea hali hiyo haraka, na hawaoni kuwa inawakengeusha. Mipango kama hiyo pia inatumiwa katika makusanyiko ambayo yana sehemu ya kutafsiri katika lugha ya ishara. Washiriki wenye bidii wa kutaniko wanahitaji kupongezwa kutoka moyoni kwa kutafsiri kama vile tu ambavyo kiziwi angeweza kueleza ujumbe huo, yaani, kwa njia ya kawaida na iliyo wazi.

Huenda unashirikiana na kutaniko ambalo lina kikundi cha lugha ya ishara au ambalo lina watu wachache ambao ni viziwi na hivyo mikutano inatafsiriwa kwa ajili yao. Unaweza kufanya nini ili uwaonyeshe upendezi wa kibinafsi ndugu hao viziwi? Wakaribishe nyumbani kwako. Ikiwezekana, jifunze ishara chache. Usiogope kwamba hutaweza kuwasiliana nao. Utapata njia ya kuwasiliana, na ukionyesha upendo kama huo utapata mambo mengi yenye kufurahisha ambayo utakumbuka. (1 Yoh. 4:8) Tunaweza kujifunza mambo mengi kutoka kwa Mashahidi wenzetu ambao ni viziwi. Wana uwezo mkubwa wa kuendeleza mazungumzo, wanaona mambo kwa undani kabisa, na ni wacheshi kwelikweli. Ndugu mmoja ambaye wazazi wake wote ni viziwi anasema hivi: “Nimeshirikiana na viziwi katika maisha yangu yote, na wamenipa vitu vingi ambavyo siwezi kuwalipa. Tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa ndugu na dada zetu viziwi.”

Yehova anawapenda waabudu wake waaminifu, kutia ndani wale ambao ni viziwi. Bila shaka, mfano wao wa imani na uvumilivu unafanya tengenezo la Yehova liwe bora zaidi. Basi acheni tuwathamini ndugu na dada zetu walio viziwi!

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Ona makala yenye kichwa “Yehova Ameufanya Uso Wake Ung’ae Kuwaelekea” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 2009 (15/8/2009).

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ujumbe wa Ufalme unaweza kumvutia zaidi mtu aliye kiziwi unapotolewa kwa lugha ya ishara

[Picha katika ukurasa wa 32]

Mikutano yetu inapaswa kuwa mahali penye kuburudisha ambapo ndugu na dada zetu viziwi wanatiwa moyo kiroho