Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Upendo Ambao Haushindwi Kamwe

Sitawisha Upendo Ambao Haushindwi Kamwe

Sitawisha Upendo Ambao Haushindwi Kamwe

‘Upendo huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.’—1 KOR. 13:7, 8.

1. (a) Mara nyingi watu wana maoni gani kuhusu upendo? (b) Watu wengi wanapenda nani na nini?

MAMBO mengi yameandikwa na kuchapishwa kuhusu upendo. Sifa hiyo imetukuzwa na kutungiwa nyimbo za mahaba. Upendo ni uhitaji wa msingi wa wanadamu. Lakini mara nyingi vitabu na sinema zimeonyesha hadithi za uwongo kuhusu upendo, na kuna habari nyingi kama hizo zinazouzwa kwa wingi. Hata hivyo, inasikitisha kwamba watu wengi hawampendi kikweli Mungu na jirani yao. Tunaona mambo ambayo Biblia ilitabiri kwamba yangetukia katika siku hizi za mwisho. Watu ‘wanajipenda wenyewe, wanapenda pesa, wanapenda raha badala ya kumpenda Mungu.’—2 Tim. 3:1-5.

2. Biblia inatoa onyo gani kuhusu upendo usiofaa?

2 Wanadamu wana uwezo wa kuonyesha upendo, hata hivyo Neno la Mungu linatuonya kuhusu upendo usiofaa. Na Biblia inaeleza yale yanayotukia wakati upendo huo unapotia mizizi katika moyo wa mtu. (1 Tim. 6:9, 10) Je, unakumbuka mtume Paulo aliandika nini kumhusu Dema? Ingawa Dema alishirikiana na Paulo, alianza kupenda mambo ya ulimwengu. (2 Tim. 4:10) Mtume Yohana aliwaonya Wakristo kuhusu hatari hiyo. (Soma 1 Yohana 2:15, 16.) Kuupenda ulimwengu, njia zake na mambo yake yanayopitilia mbali hakupatani na kumpenda Mungu na mambo yanayotokana naye.

3. Tunakabili tatizo gani, na hilo linatokeza maswali gani?

3 Sisi si sehemu ya ulimwengu, ingawa tunaishi katika ulimwengu huu. Kwa hiyo, si jambo rahisi kuepuka maoni yaliyopotoka ya ulimwengu kuhusu upendo. Ni jambo la maana kutojiruhusu tunaswe na mtego wa kuonyesha upendo usiofaa au uliopotoka. Basi, tunapaswa kusitawisha na kuwaonyesha nani upendo unaotegemea kanuni? Ni maandalizi gani yanayotuwezesha kusitawisha upendo ambao unavumilia mambo yote na ambao haushindwi kamwe? Tutapata faida gani sasa na wakati ujao tukifanya hivyo? Tunahitaji kujua maoni ya Mungu ili tupate mwongozo unaofaa.

Sitawisha Upendo Kumwelekea Yehova

4. Upendo kumwelekea Mungu unakua jinsi gani?

4 Kusitawisha kunaweza kumaanisha kutayarisha na kuchochea ukuzi wa kitu fulani. Fikiria mkulima ambaye anafanya kazi kwa bidii ili kutayarisha udongo na kupanda mbegu. Anatazamia mbegu zikue. (Ebr. 6:7) Vivyo hivyo, upendo wetu kumwelekea Mungu unapaswa kukua. Ni nini kinachohitajiwa ili upendo huo ukue? Ni lazima tutayarishe udongo mzuri wa moyo wetu, mahali ambapo mbegu ya kweli ya Ufalme ilipandwa. Tunaweza kufanya hivyo kwa kujifunza kwa bidii Neno la Mungu ili tuongeze ujuzi wetu kumhusu. (Kol. 1:10) Kuhudhuria kwa ukawaida na kushiriki katika mikutano ya kutaniko kutatusaidia pia kuongeza ujuzi wetu. Tukiwa mtu mmoja-mmoja, je, tunajitahidi daima kupata ujuzi mwingi zaidi?—Met. 2:1-7.

5. (a) Tunaweza kujifunza jinsi gani sifa kuu za Yehova? (b) Unaweza kusema nini kuhusu haki, hekima, na nguvu za Mungu?

5 Yehova anafunua utu wake kupitia Neno lake. Kwa kujifunza Maandiko na kupata ujuzi kumhusu Yehova hatua kwa hatua, tutathamini zaidi sifa zake, kama vile haki, nguvu, hekima, na zaidi ya yote, upendo wake mkuu zaidi. Yehova anaonyesha haki katika njia zake zote na katika sheria yake kamilifu. (Kum. 32:4; Zab. 19:7) Tunaweza kutafakari juu ya kazi zote za uumbaji za Yehova na kustaajabia hekima yake kuu. (Zab. 104:24) Pia, ulimwengu wote unathibitisha kwamba Yehova ndiye Chanzo cha nguvu zenye msukumo na kwamba ana nguvu nyingi zisizokwisha.—Isa. 40:26.

6. Mungu ametuonyesha upendo jinsi gani, na upendo huo umekuchochea jinsi gani?

6 Tunaweza kusema nini kuhusu sifa kuu zaidi ya Mungu, yaani, upendo wake? Sifa hiyo ni pana na inatufaidi sisi sote. Alionyesha upendo huo kwa kuandaa fidia au dhabihu ya kuwakomboa wanadamu. (Soma Waroma 5:8.) Uandalizi huo unatolewa kwa wanadamu ulimwenguni pote, lakini ni wale tu wanaothamini upendo wa Mungu na kumwamini Mwana wake ndio watakaofaidika na uandalizi huo. (Yoh. 3:16, 36) Hatua ya Mungu ya kumtoa Yesu kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu inapaswa kutuchochea sisi pia tumpende Mungu.

7, 8. (a) Tunapaswa kufanya nini ili kuonyesha kwamba tunampenda Mungu? (b) Watu wa Mungu wanashika amri zake ingawa wanakabili hali gani?

7 Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunampenda Mungu kwa yote ambayo ametufanyia? Jibu hili lililoongozwa na roho ya Mungu linaonyesha wazi jambo tunalopaswa kufanya: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yoh. 5:3) Ndiyo, kumpenda Yehova Mungu kunatuchochea kushika amri zake. Hiyo ni moja ya sababu zinazotufanya tutoe ushahidi kuhusu jina na Ufalme wake, ushahidi ambao unawafaidi wengine. Tunapofanya hivyo huku tukichochewa na moyo uliojaa mambo mema, tunathibitisha kwamba tunashika amri za Mungu tukiwa na nia nzuri.—Mt. 12:34.

8 Ndugu zetu ulimwenguni pote wanaendelea kushika amri za Mungu ingawa wanakabiliana na watu wenye ubaridi na watu wanaokataa kabisa ujumbe wa Ufalme. Wanaendelea kujitahidi kutimiza kikamili huduma yao bila kuacha. (2 Tim. 4:5) Vivyo hivyo, tunachochewa kushika amri zote za Mungu na kushiriki na wengine ujuzi kumhusu Mungu.

Sababu Inayotufanya Tumpende Bwana Wetu Yesu Kristo

9. Kristo alivumilia nini, na alichochewa na nini?

9 Zaidi ya kumpenda Mungu, kuna sababu nyingi zinazotufanya tusitawishe upendo kumwelekea Mwana wake. Ingawa hatukuwahi kamwe kumwona Yesu, kadiri tunavyojifunza mengi kumhusu, ndivyo upendo wetu kumwelekea unavyoongezeka. (1 Pet. 1:8) Ni mambo gani ambayo Yesu alivumilia? Alipokuwa akifanya mapenzi ya Baba yake, Yesu alichukiwa bila sababu, aliteswa, alishtakiwa kwa uwongo, alitukanwa, na alitendewa pia mambo mengine mengi ya dharau. (Soma Yohana 15:25.) Yesu alivumilia majaribu hayo kwa sababu alimpenda Baba yake wa mbinguni. Na kwa sababu ya upendo, alikufa na hivyo kuandaa fidia au dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya wengi.—Mt. 20:28.

10, 11. Kwa sababu ya yale ambayo Kristo alitufanyia, tuna mradi gani?

10 Maisha ya Yesu yanatuchochea sana. Tunapofikiria mambo ambayo Kristo ametufanyia, tunachochewa kumpenda hata zaidi. Tukiwa wafuasi wake, tunapaswa kujiwekea mradi wa kusitawisha na kuendelea kuonyesha upendo kama wa Kristo ili tuweze kuvumilia tunaposhika amri yake ya kutoa ushahidi kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.

11 Ili kuonyesha kwamba tunathamini upendo wa Kristo kwa wanadamu wote, tunachochewa kumaliza mgawo wetu kabla ya mwisho kufika. (Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.) Upendo ambao Kristo alionyesha ulikuwa muhimu sana katika kutimiza yale ambayo Mungu alikusudia kwa ajili ya wanadamu. Na kielelezo ambacho Kristo alituachia tufuate kwa ukaribu kinamwezesha kila mmoja wetu kushiriki katika kutimiza kusudi hilo la Mungu. Ili kufanya hivyo tunahitaji kusitawisha kikamili zaidi upendo kwa Mungu. (Mt. 22:37) Tunapofuata mambo ambayo Yesu alifundisha na kushika amri zake, tunaonyesha kwamba tunampenda na kwamba tumeazimia kwa vyovyote vile kuunga mkono enzi kuu ya Mungu, kama alivyofanya Yesu.—Yoh. 14:23, 24; 15:10.

Kufuatia Njia Iliyo Bora Zaidi ya Upendo

12. Paulo alimaanisha nini alipotumia usemi “njia iliyo bora zaidi”?

12 Mtume Paulo alimwiga Kristo. Kwa sababu ya kufuata kwa ukaribu sana hatua za Kristo, Paulo alikuwa na uhuru wa kusema alipowahimiza ndugu zake wamwige yeye. (1 Kor. 11:1) Ingawa aliwahimiza Wakristo Wakorintho waendelee kutafuta kwa bidii zawadi fulani za roho ambazo zilikuwapo katika karne ya kwanza, kama vile kuponya na kusema kwa lugha, Paulo aliwaonyesha kwamba kulikuwa na kitu fulani bora zaidi ambacho walipaswa kufuatia. Kwenye 1 Wakorintho 12:31, alisema hivi: “Bado nawaonyesha ninyi njia iliyo bora zaidi.” Mistari mingine katika sura hiyo inaonyesha kwamba njia hiyo ilikuwa njia iliyo bora zaidi ya upendo. Njia hiyo ilikuwa bora zaidi katika maana gani? Paulo alitoa mfano ili kuonyesha kile alichokuwa akimaanisha. (Soma 1 Wakorintho 13:1-3.) Ikiwa Paulo alikuwa na uwezo fulani wa pekee na hata ikiwa angetimiza mambo makubwa lakini asiwe na upendo, hilo lingemfaidi jinsi gani? Halingemfaidi hata kidogo! Akichochewa na roho ya Mungu, alikazia kweli hiyo ya maana sana. Jambo aliloeleza linatuchochea kama nini!

13. (a) Ni andiko gani litakalokuwa andiko la mwaka wa 2010? (b) Upendo haushindwi kamwe katika maana gani?

13 Kisha, Paulo anatueleza kile ambacho upendo unamaanisha na kile ambacho haumaanishi. (Soma 1 Wakorintho 13:4-8.) Sasa, chunguza ikiwa unatimiza yale ambayo upendo unamaanisha. Kazia fikira hasa sentensi ya mwisho ya mstari wa 7 na sentensi ya kwanza ya mstari wa 8: ‘Upendo huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.’ Hilo ndilo andiko letu la mwaka wa 2010. Ona kwamba katika mstari wa 8, Paulo alisema kwamba zawadi za roho, kutia ndani kutoa unabii na kusema kwa lugha, zawadi ambazo zilitumiwa mwanzoni mwa kutaniko la Kikristo, zingeondolewa mbali. Zingekoma. Lakini upendo utakuwepo sikuzote. Yehova ndiye chanzo cha upendo, naye anaishi milele. Hivyo, upendo hautashindwa kamwe, au kukoma. Utaendelea kuwepo milele ukiwa sifa ya Mungu wetu anayeishi milele.—1 Yoh. 4:8.

Upendo Unavumilia Mambo Yote

14, 15. (a) Upendo unaweza kutusaidia jinsi gani kuvumilia majaribu? (b) Kwa nini ndugu mmoja kijana alikataa kulegeza msimamo wake?

14 Ni nini kinachowawezesha Wakristo kuvumilia hata wanapokabili majaribu, hali ngumu, na matatizo yoyote yale? Hasa ni upendo ambao unategemea kanuni. Upendo huo unapita nguvu za kuachana tu na vitu vyetu vya kimwili. Unatuchochea kufikia hatua ya kuwa tayari kudumisha utimilifu wetu na hata kupoteza uhai wetu kwa ajili ya Kristo. (Luka 9:24, 25) Tafakari juu ya uaminifu wa Mashahidi walioteseka katika kambi za mateso, kambi za kazi ngumu, na katika magereza wakati na baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu.

15 Mfano wa kijana mmoja Shahidi Mjerumani anayeitwa Wilhelm unaonyesha hilo. Badala ya kulegeza msimamo wake, alibaki mshikamanifu alipokuwa akingoja kuuawa kwa kupigwa risasi na kikundi cha askari wa Nazi. Katika barua ya kuaga familia yake, aliandika hivi: “Zaidi ya mambo yote tunapaswa kumpenda Mungu, kama Kiongozi wetu Yesu Kristo alivyoamuru. Tukisimama imara upande wa Mungu, atatuthawabisha.” Baadaye, katika gazeti moja la Mnara wa Mlinzi, mtu mmoja wa familia ya Wilhelm aliandika hivi: “Katika hali zenye misukosuko, sikuzote tumehakikisha kwamba tukiwa familia tunatanguliza upendo wetu kwa Mungu.” Na huo ndio mtazamo wa ndugu wengi ambao kwa sasa wanavumilia vifungo gerezani huko Armenia, Eritrea, Korea Kusini, na nchi nyinginezo. Ndugu hao wanaendelea kuwa imara katika upendo wao kwa Yehova.

16. Ndugu zetu nchini Malawi walivumilia mateso gani?

16 Katika maeneo mengi, majaribu ya aina mbalimbali yanajaribu imani na uvumilivu wa ndugu zetu. Kwa miaka 26, Mashahidi wa Yehova nchini Malawi walivumilia marufuku ya serikali, upinzani mkali, na ukatili mwingi. Walibarikiwa kwa sababu ya uvumilivu wao. Mateso yalipoanza, kulikuwa na Mashahidi 18,000 hivi katika nchi hiyo. Miaka 30 baadaye hesabu yao iliongezeka zaidi ya mara mbili kufikia 38,393. Matokeo kama hayo yameonekana katika nchi nyingine.

17. Mashahidi fulani wanakabili hali gani katika familia zilizogawanyika kidini, na kwa nini wanavumilia mateso?

17 Ingawa mashambulizi ya moja kwa moja kuelekea watu wa Mungu kwa ujumla yanaweza kuwa makali, hali inakuwa tofauti kabisa wakati Mkristo mmoja-mmoja anapopingwa na watu wa familia yake. Huenda tukapata mikazo kutoka kwa washiriki wa familia au watu wa karibu wa ukoo. Je, Yesu hakutabiri kwamba mambo hayo yangetukia? Ndiyo, na watu wengi wamejionea ukweli wa maneno yake. (Mt. 10:35, 36) Vijana fulani wamevumilia upinzani kutoka kwa wazazi wasio waamini. Wengine hata wamefukuzwa kutoka nyumbani, lakini wamekaribishwa na Mashahidi wenye fadhili. Wengine wamekataliwa na familia zao. Ni nini kilichowawezesha Mashahidi hao kuvumilia mateso? Si kwa sababu tu wanawapenda ndugu zao, bali kwa sababu hasa wanampenda kikweli Yehova na Mwana wake.—1 Pet. 1:22; 1 Yoh. 4:21.

18. Upendo ambao unavumilia mambo yote unawasaidia jinsi gani Wakristo waliofunga ndoa?

18 Tunahitaji pia kuonyesha upendo ambao unavumilia mambo yote tunapokabili hali nyingine nyingi maishani. Katika kifungo cha ndoa, upendo unawawezesha wenzi wa ndoa kuheshimu maneno haya ya Yesu: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:6) Wanapopatwa na “dhiki katika mwili wao,” Wakristo waliofunga ndoa wanapaswa kujikumbusha kwamba Yehova ni mtu muhimu sana katika ndoa yao. (1 Kor. 7:28) Neno lake linasema kwamba ‘upendo huvumilia mambo yote,’ na mume na mke ambao wanajivika sifa hiyo wanapata nguvu za kushikamana pamoja na kudumisha ndoa yao.—Kol. 3:14.

19. Watu wa Mungu wamefanya nini baada ya misiba ya asili?

19 Upendo unatusaidia kuvumilia mambo yote wakati wa misiba ya asili. Ndivyo ilivyokuwa wakati tetemeko la nchi lilipotikisa eneo la kusini la Peru na Kimbunga Katrina kilipoharibu sehemu fulani za eneo la Ghuba huko Marekani. Ndugu zetu wengi walipoteza nyumba zao au mali zao katika misiba hiyo. Upendo ulichochea kutaniko la ulimwenguni pote kuandaa misaada, na wajitoleaji walisaidia kujenga upya nyumba na kurekebisha Majumba ya Ufalme. Matendo kama hayo yanathibitisha kwamba ndugu zetu wanapendana na wanawajali wenzao nyakati zote na chini ya hali yoyote ile.—Yoh. 13:34, 35; 1 Pet. 2:17.

Upendo Haushindwi Kamwe

20, 21. (a) Kwa nini upendo ni wenye thamani bora zaidi? (b) Kwa nini umeazimia kufuatia ile njia ya upendo?

20 Watu wa Yehova leo wanaonyesha kwamba ni jambo la hekima kufuatia ile njia iliyo bora zaidi ya upendo. Kwa kweli, njia hiyo inashinda hali yoyote ile. Ona jinsi mtume Paulo alivyokazia ukweli huo. Kwanza, alitaja kwamba zawadi za roho zingepitilia mbali na kwamba kutaniko la Kikristo lingekua na kufikia ukomavu. Kisha, akakata kauli hivi: “Sasa, hata hivyo, inabaki imani, tumaini, upendo, hayo matatu; lakini lililo kubwa zaidi kati ya hayo ni upendo.”—1 Kor. 13:13.

21 Mwishowe, mambo ambayo tunaamini yatakuwa halisi, na hivyo hatutahitaji tena kuonyesha imani katika mambo hayo. Tumaini katika ahadi ambazo tunatamani sana kuona zikitimizwa halitahitajiwa tena baada ya mambo yote kuwa mapya. Lakini namna gani upendo? Upendo hautashindwa kamwe, au kukoma. Utabaki. Huku tukitazamia kuishi milele, bila shaka tutaona na kuelewa zaidi sehemu mbalimbali za upendo wa Mungu. Ukifanya mapenzi ya Mungu kwa kuendelea kufuatia ile njia iliyo bora zaidi ya upendo ambayo haishindwi kamwe, huenda utadumu milele.—1 Yoh. 2:17.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunapaswa kujihadhari na upendo usiofaa?

• Upendo unaweza kutusaidia kuvumilia nini?

• Upendo haushindwi kamwe katika maana gani?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Andiko la mwaka wa 2010 ni: ‘Upendo huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.’—1 Kor. 13:7, 8.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kumpenda Mungu kunatuchochea kutoa ushahidi

[Picha katika ukurasa wa 26]

Upendo usioshindwa uliwawezesha ndugu na dada zetu nchini Malawi kuvumilia majaribu