Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa Mali ya Yehova Ni Fadhili Zisizostahiliwa

Kuwa Mali ya Yehova Ni Fadhili Zisizostahiliwa

Kuwa Mali ya Yehova Ni Fadhili Zisizostahiliwa

“Sisi ni wa Yehova.”—ROM. 14:8.

1, 2. (a) Tuna pendeleo gani? (b) Tutazungumzia maswali gani?

TAIFA la Israeli lilipata pendeleo la pekee sana wakati Yehova alipoliambia hivi: ‘Hakika mtakuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu.’ (Kut. 19:5) Leo, washiriki wa kutaniko la Kikristo pia wana pendeleo la pekee la kuwa mali ya Yehova. (1 Pet. 2:9; Ufu. 7:9, 14, 15) Ni pendeleo ambalo linaweza kutunufaisha milele.

2 Kuwa mali ya Yehova ni pendeleo, lakini pia ni daraka. Huenda wengine wakajiuliza: ‘Je, nitaweza kufanya yale ambayo Yehova anataka nifanye? Ikiwa nitatumbukia katika dhambi, je, atanitupa? Je, nikiwa mali ya Yehova nitapoteza uhuru wangu?’ Mahangaiko hayo yanapaswa kutiliwa maanani. Hata hivyo, kwanza kuna swali lingine ambalo linastahili kufikiriwa kwa makini: Kuna faida gani za kuwa mali ya Yehova?

Kuwa Mali ya Yehova Kunaleta Furaha

3. Rahabu alipata faida gani kwa sababu ya kuchagua kumtumikia Yehova?

3 Je, watu ambao ni mali ya Yehova wanapata faida yoyote? Mfikirie Rahabu, kahaba aliyeishi katika jiji la kale la Yeriko. Bila shaka, alilelewa katika ibada yenye upotovu ya miungu ya Kanaani. Hata hivyo, alipopata habari kuhusu ushindi ambao Yehova alikuwa amewapa Waisraeli, alitambua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli. Kwa hiyo, alihatarisha uhai wake ili awalinde watu wa Mungu na hivyo akawaachia daraka la kumwokoa. Biblia inauliza hivi: “Je, Rahabu yule kahaba hakutangazwa pia kuwa mwadilifu kwa matendo, baada ya kuwakaribisha wale wajumbe na kuwatoa nje kwa njia nyingine?” (Yak. 2:25) Hebu wazia faida alizopata baada ya kuwa sehemu ya watu safi wa Mungu, watu ambao walifundishwa na Sheria ya Mungu kuonyesha upendo na haki. Bila shaka, alifurahi sana kuacha maisha yake ya zamani. Aliolewa na Mwisraeli naye akamlea Boazi, mwana wake, ambaye alikuja kuwa mwanamume mzuri sana aliyemwogopa Mungu.—Yos. 6:25; Rut. 2:4-12; Mt. 1:5, 6.

4. Ruthu alifaidika jinsi gani kwa sababu ya kuamua kumtumikia Yehova?

4 Ruthu wa Moabu pia aliamua kumtumikia Yehova. Akiwa msichana mdogo, huenda aliabudu Kemoshi na miungu mingine ya Moabu, lakini baadaye alimjua Mungu wa kweli, Yehova, akaolewa na Mwisraeli ambaye alikuwa amekimbilia katika nchi yao. (Soma Ruthu 1:1-6.) Baadaye, Ruthu na Orpa walipoanza safari ya kwenda Bethlehemu wakiwa na mama-mkwe wao, Naomi, aliwahimiza vijana hao warudi nyumbani. Haingekuwa rahisi kwao kuishi Israeli. Kwa kweli, Orpa ‘alirudi kwa watu wake na kwa miungu yake,’ lakini Ruthu hakurudi. Alitenda kwa imani na alijua alitaka kuwa mali ya nani. Alimwambia hivi Naomi: “Usiniombe nikuache, nigeuke nisifuatane nawe; kwa maana uendako nitaenda, na mahali utakapokaa usiku kucha nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.” (Rut. 1:15, 16) Kwa sababu ya kuchagua kumtumikia Yehova, Ruthu alifaidika kutokana na Sheria ya Mungu, ambayo iliandaa mipango ya pekee kwa ajili ya wajane, maskini, na wale wasio na mashamba. Alipata furaha, ulinzi, na usalama chini ya mabawa ya Yehova.

5. Umeona nini kuhusu watu ambao wanamtumikia Yehova kwa uaminifu?

5 Labda unajua watu fulani ambao baada ya kujiweka wakfu kwa Yehova wamekuwa wakimtumikia kwa uaminifu kwa miaka mingi. Waulize wamefaidika jinsi gani kwa sababu ya kumtumikia Yehova. Ingawa kila mtu anakabili matatizo, mambo ya hakika yanaonyesha kwamba maneno haya ya mtunga-zaburi ni ya kweli kabisa: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—Zab. 144:15.

Matakwa ya Yehova Si Mazito

6. Kwa nini hatupaswi kuogopa kwamba hatuwezi kutimiza matakwa ya Yehova?

6 Huenda uliogopa kwamba huwezi kutimiza matakwa ya Yehova. Ni rahisi kuhisi kwamba huwezi kumtumikia Mungu, kuishi kupatana na sheria yake, na kutangaza jina lake. Kwa mfano, Musa alipotumwa kuzungumza na Waisraeli na mfalme wa Misri alihisi kwamba hastahili. Lakini Mungu hakumtaka Musa atimize mambo ambayo yalipita uwezo wake. Yehova ‘alimfundisha mambo ya kufanya.’ (Soma Kutoka 3:11; 4:1, 10, 13-15.) Kwa kuwa Musa alikubali msaada wa Yehova, alipata shangwe ya kutimiza mapenzi ya Mungu. Leo pia, mambo ambayo Yehova anataka tufanye, hayapiti uwezo wetu. Anaelewa hali yetu ya kutokamilika, naye anataka kutusaidia. (Zab. 103:14) Kumtumikia Mungu tukiwa wafuasi wa Yesu kunatuburudisha badala ya kutulemea kwa sababu njia hiyo ya maisha inawanufaisha wengine na kuufanya moyo wa Yehova ushangilie. Yesu alisema hivi: “Njooni kwangu . . . nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni.”—Mt. 11:28, 29.

7. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakuwezesha kufanya yale anayotaka ufanye?

7 Sikuzote Yehova yuko tayari kututia moyo tukihitaji kutiwa moyo, maadamu tu tunamtegemea ili atutie nguvu. Kwa mfano, inaonekana kwamba Yeremia hakuwa msemaji mwenye ujasiri. Kwa hiyo, Yehova alipompa mgawo wa kuwa nabii Wake, Yeremia alisema hivi: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama, mimi hakika sijui jinsi ya kusema, kwa sababu mimi ni mvulana tu.” Baadaye, hata alisema hivi: “Sitamtaja tena, wala sitasema tena katika jina lake.” (Yer. 1:6; 20:9) Hata hivyo, Yehova alimtia moyo, na Yeremia akafaulu kuhubiri kwa miaka 40 ujumbe ambao haukupendwa na watu wengi. Yehova alimhakikishia hivi tena na tena: “Mimi niko pamoja nawe ili kukukomboa.”—Yer. 1:8, 19; 15:20.

8. Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunamtegemea Yehova?

8 Yehova anaweza kutusaidia tufanye yale ambayo anataka Wakristo wafanye leo, kama vile tu alivyomtia nguvu Musa na Yeremia. Jambo kuu ni kumtegemea Mungu. Biblia inasema hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” (Met. 3:5, 6) Tunaonyesha kwamba tunamtegemea Yehova tunapotumia mashauri anayotoa kupitia Neno lake na kutaniko. Tukimruhusu Yehova aongoze hatua zetu maishani, hakuna kitu ambacho kitatuzuia tusiwe waaminifu kwake.

Yehova Anamjali Kila Mmoja wa Watumishi Wake

9, 10. Zaburi ya 91 inaahidi ulinzi wa aina gani?

9 Watu fulani wanapofikiria kujiweka wakfu kwa Yehova, huenda wakaogopa kuanguka katika dhambi, kutostahili, na kukataliwa na Yehova. Inafurahisha kwamba Yehova anatupatia msaada wote ambao tunahitaji ili kulinda uhusiano wetu wenye thamani pamoja naye. Hebu tuone jinsi hilo linavyoelezwa katika Zaburi ya 91.

10 Zaburi hiyo inaanza hivi: “Yeyote anayekaa mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi atajipatia makao katika kivuli cha Mweza-Yote. Nitamwambia Yehova: ‘Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtegemea.’ Kwa maana yeye mwenyewe atakukomboa kutoka katika mtego wa mwindaji wa ndege.” (Zab. 91:1-3) Ona kwamba Mungu anaahidi kuwalinda wale ambao wanampenda na kumtegemea. (Soma Zaburi 91:9, 14.) Alimaanisha ulinzi wa aina gani? Kwa kweli, Yehova aliwalinda kimwili watumishi wake fulani wa zamani, nyakati nyingine alifanya hivyo ili kulinda ukoo ambao ungemtokeza Masihi aliyeahidiwa. Hata hivyo, watumishi wake wengi waaminifu walifungwa gerezani, waliteswa, na kuuawa kikatili katika jitihada za Ibilisi za kuwafanya wamwasi Mungu. (Ebr. 11:34-39) Walipata ujasiri waliohitaji ili kuvumilia mateso kwa sababu Yehova aliwalinda kiroho kutokana na hatari ya kuvunja utimilifu wao. Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba Zaburi ya 91 inaahidi ulinzi wa kiroho.

11. “Mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi” ni nini, na Mungu anawalinda watu gani mahali hapo?

11 Kwa hiyo, “mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi,” panapotajwa na mtunga-zaburi, ni mahali pa mfano penye ulinzi wa kiroho. Wale wanaokaa pamoja na Mungu mahali hapo wakiwa wageni wake wamelindwa salama kutokana na kitu chochote na mtu yeyote ambaye anaweza kuhatarisha imani yao na upendo wao kwa Mungu. (Zab. 15:1, 2; 121:5) Ni mahali pa siri kwa sababu watu ambao si waamini hawawezi kupatambua. Yehova anawalinda mahali hapo watu ambao wanasema hivi kwa njia ya mfano: ‘Wewe ni Mungu wangu, ambaye nitamtegemea.’ Tukikaa mahali hapo pa kimbilio, hatuhitaji kuogopa kwamba tutapoteza kibali cha Mungu kwa kuanguka katika mtego wa Shetani, “mwindaji wa ndege.”

12. Ni mambo gani ambayo yanahatarisha uhusiano wetu pamoja na Mungu?

12 Ni mambo gani ambayo yanahatarisha uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Mungu? Mtunga-zaburi anataja hatari mbalimbali, kama vile “tauni inayotembea gizani, . . . [na] maangamizi yanayopora katikati ya mchana.” (Zab. 91:5, 6) Yule “mwindaji wa ndege” amenasa watu wengi akitumia tamaa ya kichoyo ya kupata uhuru. (2 Kor. 11:3) Anawanasa wengine kwa kuwachochea kuwa na pupa, kiburi, na kupenda vitu vya kimwili. Anawapotosha wengine pia kwa kutumia falsafa kama vile uzalendo, mageuzi, na dini ya uwongo. (Kol. 2:8) Na wengi wameshawishiwa kutumbukia katika mtego wa mahusiano haramu ya ngono. Mapigo hayo ambayo yana madhara kiroho yamewafanya mamilioni ya watu kupoteza upendo wao kumwelekea Mungu.—Soma Zaburi 91:7-10; Mt. 24:12.

Kuulinda Upendo Wako kwa Mungu

13. Yehova anatulinda jinsi gani kutokana na mambo ambayo yanahatarisha hali yetu ya kiroho?

13 Yehova anawalinda jinsi gani watu wake kutokana na hatari hizo za kiroho? Zaburi inasema hivi: “Atawaamuru malaika zake kukuhusu wewe, ili kukulinda katika njia zako zote.” (Zab. 91:11) Malaika wa mbinguni wanatuongoza na kutulinda ili tuweze kuhubiri habari njema. (Ufu. 14:6) Mbali na malaika, wazee Wakristo wanashika imara Maandiko wanapofundisha na hivyo kutulinda ili tusidanganywe na mawazo ya uwongo. Wanaweza kumsaidia kila Mkristo ambaye anapambana ili kushinda mitazamo ya ulimwengu. (Tito 1:9; 1 Pet. 5:2) Pia, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anaandaa chakula cha kiroho ili kutulinda kutokana na fundisho la mageuzi, kishawishi cha tamaa potovu za kingono, kutafuta utajiri na umashuhuri, na tamaa na mambo mengine mengi yenye kudhuru. (Mt. 24:45) Ni nini ambacho kimekusaidia kushinda hatari hizo?

14. Tunaweza kufanya nini ili tufaidike kutokana na ulinzi ambao Mungu anaandaa?

14 Ni lazima tufanye nini ili tuendelee kukaa “mahali pa siri” pa Mungu penye ulinzi? Ni lazima tujilinde daima kutokana na hatari za kiroho kama tunavyojilinda daima kutokana na hatari za kimwili, kama vile aksidenti, wahalifu, au magonjwa. Hivyo, tunapaswa kufuata kwa ukawaida mwongozo ambao Yehova anatuandalia kupitia vichapo vyetu na katika mikutano ya kutaniko na makusanyiko. Tunapaswa kuwaomba wazee mashauri. Na je, hatufaidiki kutokana na sifa mbalimbali ambazo ndugu na dada zetu Wakristo wanaonyesha? Kwa kweli, kushirikiana na kutaniko kunatusaidia kuwa wenye hekima.—Met. 13:20; soma 1 Petro 4:10.

15. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anaweza kukulinda kutokana na kitu chochote ambacho kinaweza kufanya upoteze kibali chake?

15 Hatuna sababu yoyote ya kuwa na shaka kwamba Yehova anaweza kutulinda kutokana na kitu chochote ambacho kinaweza kutufanya tupoteze kibali chake. (Rom. 8:38, 39) Amelilinda kutaniko kutokana na maadui wa kidini na wa kisiasa wenye nguvu ambao kwa kawaida kusudi lao, si kutuua, bali kututenga na Mungu wetu mtakatifu. Ahadi hii ya Yehova imethibitika kuwa ya kweli: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.”—Isa. 54:17.

Ni Nani Anayetupatia Uhuru?

16. Kwa nini ulimwengu hauwezi kutupatia uhuru?

16 Je, tukiwa mali ya Yehova tutapoteza uhuru wetu? Hapana, tutapoteza uhuru wetu tukiwa mali ya ulimwengu. Ulimwengu umetengwa mbali na Yehova na unatawaliwa na mungu mjeuri ambaye anawafanya watu wawe watumwa. (Yoh. 14:30) Kwa mfano, mfumo wa mambo wa Shetani unatumia hali ngumu ya kiuchumi kuwanyang’anya watu uhuru wao. (Linganisha na Ufunuo 13:16, 17.) Dhambi pia ina nguvu za udanganyifu ambazo zinawafanya watu wawe watumwa. (Yoh. 8:34; Ebr. 3:13) Kwa hiyo, hata ingawa watu wasio waamini wanaweza kuahidi uhuru wanapotetea njia ya maisha ambayo haipatani na mafundisho ya Yehova, punde si punde, mtu yeyote anayewasikiliza atajikuta amekuwa mtumwa wa maisha mapotovu ya dhambi.—Rom. 1:24-32.

17. Yehova anatuahidi uhuru gani?

17 Kwa upande mwingine, tukijitiisha chini ya Yehova, atatuweka huru kutokana na kila kitu ambacho kinaweza kutudhuru kiroho. Kwa njia fulani, hali yetu ni kama ya mtu ambaye anaacha uhai wake mikononi mwa daktari stadi sana wa upasuaji ambaye anaweza kumtibu ugonjwa ambao unasababisha kifo. Sisi sote tuna ugonjwa ambao unasababisha kifo, yaani, dhambi tuliyorithi. Ni kwa kujitiisha tu kwa Yehova, kwa msingi wa dhabihu ya Kristo, ndipo tunapoweza kuwa na tumaini la kuepuka matokeo mabaya ya dhambi, kisha tuishi milele. (Yoh. 3:36) Kama vile tu ambavyo imani yetu katika daktari inavyoweza kuongezeka tunaposikia kuhusu sifa zake, ndivyo tutakavyomtegemea Yehova zaidi tunapoendelea kujifunza kumhusu. Kwa hiyo, tunaendelea kujifunza Neno la Mungu kwa makini kwa sababu kufanya hivyo kutatusaidia kumpenda sana hivi kwamba hatutaogopa kuwa mali yake.—1 Yoh. 4:18.

18. Wale ambao ni mali ya Yehova watapata nini?

18 Yehova anawapa watu wote uhuru wa kuchagua. Neno lake linasema hivi: “Lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako.” (Kum. 30:19, 20) Anataka tuonyeshe kwamba tunampenda kwa kuchagua kumtumikia bila kulazimishwa. Bila shaka, tukiwa mali ya Mungu ambaye tunampenda tutapata furaha ya kudumu, hatutapoteza uhuru wetu.

19. Kwa nini kuwa mali ya Yehova ni fadhili zisizostahiliwa?

19 Tukiwa watenda-dhambi hatustahili kuwa mali ya Mungu mkamilifu. Tunaweza kuwa mali ya Mungu kwa sababu tu ya fadhili zake zisizostahiliwa. (2 Tim. 1:9) Hivyo, Paulo aliandika hivi: “Tukiishi, tunaishi kwa ajili ya Yehova, na tukifa, tunakufa kwa ajili ya Yehova. Kwa hiyo tukiishi na tukifa, sisi ni wa Yehova.” (Rom. 14:8) Bila shaka, hatutajuta kamwe kwa sababu ya kuchagua kuwa mali ya Yehova.

Ungesema Nini?

• Kuna faida gani za kuwa mali ya Yehova?

• Kwa nini tunaweza kufanya yale ambayo Mungu anataka tufanye?

• Yehova anawalinda watumishi wake kupitia njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Waulize wengine jinsi ambavyo wamefaidika kwa sababu ya kuwa mali ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yehova anatulinda akitumia njia gani mbalimbali?