Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesha Kwamba Wewe Ni Mfuasi wa Kweli wa Kristo

Onyesha Kwamba Wewe Ni Mfuasi wa Kweli wa Kristo

Onyesha Kwamba Wewe Ni Mfuasi wa Kweli wa Kristo

“Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa.”—MT. 7:17.

1, 2. Tunaweza kuwatofautisha jinsi gani wafuasi wa kweli wa Kristo na wale wa uwongo, hasa nyakati hizi za mwisho?

YESU alisema kwamba tunaweza kuwatofautisha wafuasi wake wa kweli na wale wanaodai kwa uwongo kwamba wanamtumikia kwa kuchunguza matunda yao, yaani, mafundisho yao na mwenendo wao. (Mt. 7:15-17, 20) Bila shaka, mambo ambayo watu wanaruhusu yaingie katika akili na mioyo yao ndiyo yanayowasukuma kutenda kwa njia fulani. (Mt. 15:18, 19) Watu wanaofundishwa uwongo wanazaa “matunda yasiyofaa,” lakini wale ambao wanafundishwa kweli ya kiroho wanazaa “matunda mazuri.”

2 Matunda hayo ya aina mbili yameonekana wazi nyakati hizi za mwisho. (Soma Danieli 12:3, 10.) Wakristo wa uwongo wana maoni yaliyopotoka kumhusu Mungu na kwa kawaida wana ujitoaji-kimungu wa kinafiki, lakini wale ambao wana ufahamu wa kiroho wanamwabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Yoh. 4:24; 2 Tim. 3:1-5) Wanajitahidi kuonyesha sifa kama za Kristo. Lakini namna gani sisi binafsi? Unapochunguza mambo matano yafuatayo ambayo yanawatambulisha Wakristo wa kweli, jiulize hivi: ‘Je, inaonekana wazi kwamba mwenendo na mafundisho yangu yanapatana na Neno la Mungu? Je, ninaifanya kweli iwavutie wale wanaoitafuta?’

Ishi Kulingana na Neno la Mungu

3. Yehova anapendezwa na nini, na hilo linahusisha nini kwa Wakristo wa kweli?

3 Yesu alisema hivi: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.” (Mt. 7:21) Ndiyo, Yehova anapendezwa na wale wanaoishi kupatana na Ukristo bali si wale wanaodai tu kuwa Wakristo. Kwa wafuasi wa kweli wa Kristo, hilo linahusisha maisha yao yote, kutia ndani na mtazamo wao kuelekea pesa, kazi ya kimwili, burudani, desturi na sherehe za kilimwengu, ndoa na mahusiano yao na wanadamu wenzao. Hata hivyo, Wakristo wa uwongo wanafuata mawazo na njia za ulimwengu, ambazo zinazidi kumchukiza Mungu katika siku hizi za mwisho.—Zab. 92:7.

4, 5. Tunaweza kutumia jinsi gani maneno ya Yehova yaliyo katika Malaki 3:18 maishani mwetu?

4 Hivyo, nabii Malaki aliandika hivi: “Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mwadilifu na mwovu, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hajamtumikia.” (Mal. 3:18) Unapotafakari kuhusu maneno hayo, jiulize hivi: ‘Je, ninatenda kama watu wa ulimwengu au niko tofauti? Je, sikuzote ninajaribu kuwaiga marafiki wangu wa ulimwengu, iwe shuleni au kazini, au ninashikamana kabisa na kanuni za Biblia, na kuzitetea waziwazi inapofaa?’ (Soma 1 Petro 3:16.) Bila shaka, hatutaki tuonekane kuwa waadilifu kupita kiasi, lakini tunapaswa kuwa tofauti na wale ambao hawampendi wala hawamtumikii Yehova.

5 Ikiwa kuna jambo unalohitaji kurekebisha, kwa nini usisali kuhusu jambo hilo na utafute nguvu za kiroho za kufanya hivyo kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida, kusali, na kuhudhuria mikutano? Kadiri unavyotumia Neno la Mungu katika maisha yako, ndivyo utakavyozaa “matunda mazuri” kwa wingi zaidi, kutia ndani ‘tunda la midomo ambalo hulifanyia jina [la Mungu] tangazo la hadharani.’—Ebr. 13:15.

Tangaza Ufalme wa Mungu

6, 7. Inapohusu ujumbe wa Ufalme, kuna tofauti gani kati ya Wakristo wa kweli na Wakristo wa uwongo?

6 Yesu alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kwa nini Yesu alikazia hasa Ufalme wa Mungu katika huduma yake? Alijua kwamba akiwa Mfalme wa Ufalme huo, pamoja na ndugu zake waliofufuliwa ambao wamezaliwa kwa roho, wataondoa kabisa vyanzo vya mateso ya wanadamu, yaani, dhambi na Ibilisi. (Rom. 5:12; Ufu. 20:10) Kwa hiyo, aliwaamuru wafuasi wake watangaze Ufalme huo mpaka mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Mt. 24:14) Watu ambao wanadai tu kuwa wafuasi wa Kristo hawafanyi kazi hiyo, na kwa kweli, hawawezi kuifanya. Kwa nini? Kuna sababu tatu hivi: Kwanza, hawawezi kuhubiri mambo ambayo hawaelewi. Pili, wengi wao hawana unyenyekevu na ujasiri unaohitajiwa ili kuvumilia dhihaka na upinzani ambao huenda wakakabili wanapowahubiria majirani wao ujumbe wa Ufalme. (Mt. 24:9; 1 Pet. 2:23) Na tatu, Wakristo wa uwongo hawana roho ya Mungu.—Yoh. 14:16, 17.

7 Lakini wafuasi wa kweli wa Kristo, wanaelewa Ufalme wa Mungu ni nini na wanajua yale ambayo utatimiza. Zaidi ya hayo, wanatanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yao, wakiutangaza ulimwenguni pote, kwa msaada wa roho ya Yehova. (Zek. 4:6) Je, unashiriki kwa ukawaida katika kazi hiyo? Je, unajitahidi kuwa mtangazaji wa Ufalme mwenye ustadi, labda kwa kutumia muda zaidi katika huduma au kwa kuboresha ufundishaji wako? Wengine wamejitahidi kuboresha huduma yao kwa kutumia Biblia vizuri zaidi. Mtume Paulo ambaye alikuwa na desturi ya kujadiliana na watu kwa kutumia Maandiko aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—Ebr. 4:12; Mdo. 17:2, 3.

8, 9. (a) Ni mambo gani yaliyoonwa ambayo yanakazia umuhimu wa kutumia Biblia katika huduma yetu? (b) Tunaweza kuboresha jinsi gani ustadi wetu wa kutumia Neno la Mungu?

8 Ndugu mmoja alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, alimsomea mwanamume fulani Mkatoliki andiko la Danieli 2:44 na kumweleza jinsi Ufalme wa Mungu utakavyoleta amani ya kweli na usalama. Mwanamume huyo akasema hivi: “Ninashukuru sana kwamba umefungua Biblia na kunionyesha jinsi andiko hilo linavyosema badala tu ya kuniambia kwa mdomo.” Ndugu mwingine alipomsomea andiko fulani mwanamke wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki, mwanamke huyo aliuliza maswali mengi mazuri. Katika kisa hiki pia, ndugu huyo pamoja na mke wake, walitumia Biblia kujibu maswali hayo. Baadaye, mwanamke huyo aliuliza: “Mnajua kwa nini niliamua kuzungumza nanyi? Mlikuja hapa kwangu na Biblia, kisha mkaisoma.”

9 Bila shaka, vichapo vyetu ni vya maana na tunapaswa kuwaachia watu tunapohubiri. Hata hivyo, kifaa chetu kikuu ni Biblia. Kwa hiyo, ikiwa huna mazoea ya kuitumia kwa ukawaida katika huduma yako, kwa nini usiweke mradi wa kufanya hivyo? Labda unaweza kuchagua maandiko machache ya msingi ambayo yanaeleza Ufalme wa Mungu ni nini na jinsi utakavyotatua matatizo fulani hususa ambayo yanawahangaisha watu katika eneo lenu. Kisha uwe tayari kusoma maandiko hayo unapohubiri nyumba kwa nyumba.

Jivunie Pendeleo la Kuitwa kwa Jina la Mungu

10, 11. Kuhusu kutumia jina la Mungu, kuna tofauti gani kati ya Yesu na watu wengi wanaodai kwamba wanamfuata?

10 “‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ asema Yehova, ‘nami ni Mungu.’” (Isa. 43:12) Yesu Kristo, Shahidi mkuu zaidi wa Yehova, aliona kwamba ni pendeleo kuitwa kwa jina la Mungu na kulitangaza. (Soma Kutoka 3:15; Yohana 17:6; Waebrania 2:12.) Kwa hakika, Yesu aliitwa “Shahidi Mwaminifu,” kwa sababu alitangaza jina la Baba yake.—Ufu. 1:5; Mt. 6:9.

11 Tofauti na Yesu, wale ambao wanadai kwamba wanamwakilisha Mungu na Mwana wake wamelionea aibu jina la Mungu, hata wameliondoa katika tafsiri zao za Biblia. Ili kuonyesha mtazamo huohuo, barua iliyotumwa hivi karibuni kwa maaskofu Wakatoliki ilisema kwamba “jina la Mungu ambalo linawakilishwa na herufi YHWH za tetragamatoni halipaswi kutumiwa wala kutamkwa” wakati wa ibada. * Mawazo hayo yanachukiza kama nini!

12. Watumishi wa Yehova walikuja kuhusianishwa hata zaidi na Yehova jinsi gani mwaka wa 1931?

12 Wakristo wa kweli wanafurahi sana kutumia jina la Mungu na hivyo wanamwiga Kristo na ‘wingu kubwa la mashahidi’ waliomtangulia. (Ebr. 12:1) Kwa kweli, katika mwaka wa 1931, watumishi wa Mungu walihusianishwa hata zaidi na Yehova kwa kukubali jina Mashahidi wa Yehova. (Soma Isaya 43:10-12.) Hivyo, kwa njia ya pekee sana, wafuasi wa kweli wa Kristo wakawa “watu wanaoitwa kwa jina [la Mungu].”—Mdo. 15:14, 17.

13. Tunaweza kuishi jinsi gani kupatana na jina letu ambalo tumepewa na Mungu?

13 Kila mmoja wetu anaweza kuishi jinsi gani kupatana na jina letu la pekee? Kwanza, ni lazima tutoe ushahidi kwa uaminifu kumhusu Mungu. Paulo aliandika hivi: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa. Hata hivyo, watawezaje kumwitia yeye ambaye hawajamwamini? Nao watamwaminije yeye ambaye hawajamsikia? Nao watasikiaje bila mtu wa kuhubiri? Nao watahubirije isipokuwa wawe wametumwa?” (Rom. 10:13-15) Pia, tunapaswa kufunua kwa busara uwongo wa dini ambao unamharibia sifa Muumba wetu, kama vile fundisho la moto wa mateso, ambalo kwa kweli linamaanisha kwamba Mungu wa upendo ni mkatili kama Ibilisi.—Yer. 7:31; 1 Yoh. 4:8; linganisha na Marko 9:17-27.

14. Watu fulani wanatenda jinsi gani wanapojifunza jina la Mungu?

14 Je, unajivunia pendeleo la kuitwa kwa jina la Baba yako wa mbinguni? Je, unawasaidia wengine kujua jina hilo takatifu? Mwanamke fulani huko Paris, Ufaransa, alisikia kwamba Mashahidi wa Yehova wanajua jina la Mungu, kwa hiyo mara tu alipokutana na Shahidi alimwomba amwonyeshe jina hilo katika Biblia yake. Aliposoma Zaburi 83:18, aliguswa moyo sana. Alianza kujifunza Biblia na sasa anatumika katika nchi nyingine akiwa dada mwaminifu. Mwanamke mmoja Mkatoliki anayeishi Australia alipoona jina la Mungu katika Biblia kwa mara ya kwanza, alilia kwa shangwe. Kwa miaka mingi sasa, amekuwa painia wa kawaida. Hivi karibuni, Mashahidi fulani huko Jamaika walipomwonyesha mwanamke mmoja jina la Mungu katika Biblia yake, yeye pia alitokwa na machozi ya shangwe. Kwa hiyo, jivunie pendeleo la kuitwa kwa jina la Mungu na umwige Yesu kwa kuwatangazia watu wote jina hilo lenye thamani.

“Msiwe Mkiupenda Ulimwengu”

15, 16. Wakristo wa kweli wana maoni gani kuhusu ulimwengu, na tunapaswa kujiuliza maswali gani?

15 “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake.” (1 Yoh. 2:15) Ulimwengu na roho yake ya kupenda vitu vya kimwili haupatani kamwe na Yehova na roho yake takatifu. Hivyo, wafuasi wa kweli wa Kristo hawaepuki tu kuwa sehemu ya ulimwengu. Wanakataa kwa moyo wote kuupenda ulimwengu, huku wakijua kama mwanafunzi Yakobo alivyoandika, “urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu.”—Yak. 4:4.

16 Inaweza kuwa vigumu kutii maneno hayo ya Yakobo katika ulimwengu huu wenye vishawishi vingi sana. (2 Tim. 4:10) Hivyo, Yesu alisali hivi kwa ajili ya wafuasi wake: “Ninakuomba, si kwamba uwatoe ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 17:15, 16) Jiulize hivi: ‘Je, ninajitahidi kutokuwa sehemu ya ulimwengu? Je, wengine wanajua msimamo wangu kuhusiana na sherehe na desturi ambazo hazipatani na Maandiko na pia zile ambazo huenda si za kipagani lakini zinaonyesha waziwazi roho ya ulimwengu?’—2 Kor. 6:17; 1 Pet. 4:3, 4.

17. Ni nini kinachoweza kuwachochea watu wenye mioyo minyoofu wachukue msimamo upande wa Yehova?

17 Ni wazi kwamba hatuwezi kupendwa na ulimwengu kwa sababu ya msimamo wetu unaotegemea Biblia, lakini tunaweza kuwavutia watu wenye mioyo minyoofu wanaotaka kujua kweli. Kwa wazi, watu kama hao wanapoona kwamba imani yetu imetia mizizi katika Maandiko na inaongoza maisha yetu yote, huenda wakachukua hatua ya kuwaambia hivi kwa njia ya mfano watiwa-mafuta: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.”—Zek. 8:23.

Onyesha Upendo wa Kweli wa Kikristo

18. Kumpenda Yehova na jirani yetu kunahusisha nini?

18 Yesu alisema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote” na “mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mt. 22:37, 39) Upendo huo (a·gaʹpe katika Kigiriki) ni upendo wa kimaadili ambao unahusisha wajibu, kanuni, na mwenendo wa heshima, lakini mara nyingi unatia ndani hisia zenye nguvu. Unaweza kuwa mchangamfu na wenye nguvu sana. (1 Pet. 1:22) Ni tofauti kabisa na roho ya ubinafsi au uchoyo, kwa kuwa unaonyeshwa kwa maneno na matendo yasiyo ya kichoyo.—Soma 1 Wakorintho 13:4-7.

19, 20. Simulia mambo fulani ambayo yanaonyesha kwamba upendo wa Kikristo una nguvu.

19 Kwa sababu upendo ni sifa ya roho takatifu ya Mungu, unawawezesha Wakristo wa kweli kufanya mambo ambayo wengine hawawezi kufanya, kama vile kushinda tofauti za kijamii, kitamaduni, na kisiasa. (Soma Yohana 13:34, 35; Gal. 5:22) Watu wenye mfano wa kondoo wanaguswa moyo sana wanapoona upendo huo. Kwa mfano, mwanamume fulani kijana Myahudi huko Israel alipohudhuria kwa mara ya kwanza mkutano wa Kikristo, alishangaa sana kuona ndugu Wayahudi na Waarabu wakimwabudu Yehova pamoja. Kwa hiyo, alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na akakubali kujifunza Biblia. Je, unawaonyesha ndugu zako upendo huo wa kutoka moyoni? Na je, unajitahidi kuwakaribisha kwa uchangamfu watu wapya kwenye Jumba lenu la Ufalme, bila kufikiria taifa lao, rangi yao ya ngozi, au cheo chao katika jamii?

20 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunajitahidi kuwapenda watu wote. Huko El Salvador, mhubiri mmoja kijana alikuwa akijifunza Biblia na mwanamke fulani Mkatoliki mwenye umri wa miaka 87 ambaye alishikamana sana na kanisa lake. Siku moja, mwanamke huyo alikuwa mgonjwa sana na akalazwa hospitalini. Mwanamke huyo aliporudi nyumbani, Mashahidi walimtembelea na kuhakikisha kwamba alikuwa na chakula. Walifanya hivyo kwa mwezi mmoja hivi. Mwanamke huyo hakutembelewa na mtu yeyote kutoka katika kanisa lake. Matokeo yakawa nini? Mwanamke huyo alitupa sanamu zake, akaacha kanisa lake, na kuanza tena kujifunza Biblia. Ndiyo, upendo wa Kikristo una nguvu! Upendo unaweza kugusa sana mioyo ya watu kuliko maneno.

21. Tunaweza kufanya nini ili tuwe na wakati ujao salama?

21 Hivi karibuni, Yesu atawaambia hivi wote ambao wanadai kwa uwongo kwamba wanamtumikia: “Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.” (Mt. 7:23) Kwa hiyo, acheni tuzae matunda ambayo yanamletea heshima Baba yetu na Mwana wake. Yesu alisema hivi: “Kila mtu anayesikia maneno yangu haya na kuyatenda atafananishwa na mtu mwenye busara, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba.” (Mt. 7:24) Ndiyo, tukionyesha kwamba sisi ni wafuasi wa kweli wa Kristo, tutapata kibali cha Mungu, na wakati wetu ujao utakuwa salama kana kwamba umejengwa juu ya mwamba!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Vitabu fulani vya karibuni vya Wakatoliki vya Kiingereza, kutia ndani The Jerusalem Bible, vinatafsiri tetragramatoni kuwa “Yahweh.”

Je, Unakumbuka?

• Tunaweza kuwatofautisha jinsi gani wafuasi wa kweli wa Kristo na wa uwongo?

• Taja “matunda” fulani ambayo yanawatambulisha Wakristo wa kweli.

• Unaweza kuweka miradi gani kuhusiana na kuzaa matunda ya Kikristo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, una mazoea ya kutumia Biblia kwa ukawaida katika huduma yako?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je, wengine wanajua msimamo wako kuhusu sherehe ambazo hazipatani na Maandiko?