Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Haki ya Mtoto ya Kukua Kiroho”

“Haki ya Mtoto ya Kukua Kiroho”

“Haki ya Mtoto ya Kukua Kiroho”

MNAMO Desemba 9, 2008, Chuo cha Haki za Mtoto cha Sweden kilifanya mkutano wa pekee wenye kichwa “Haki ya Mtoto ya Kukua Kiroho.” Maoni mengi yalitolewa na wasemaji waliowakilisha Waislamu, Kanisa la Sweden, dini nyingine zinazodai kuwa za Kikristo, na kikundi cha kutetea haki za binadamu.

Kasisi mmoja alisema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kueleza vizuri kabisa jinsi masimulizi ya Biblia yanavyowasaidia watoto kiroho.” Masimulizi ya Maandiko yanatosheleza jinsi gani mahitaji ya kiroho ya watoto?

Kasisi huyo alisema: “Maandiko na masimulizi yanawapa watoto mambo ya kufikiria na kutafakari wakiwa peke yao.” Alitaja “hadithi ya Adamu na Hawa, Kaini na Abeli, Daudi na Goliathi, kuzaliwa kwa Yesu, hadithi ya mkusanya-kodi aliyeitwa Zakayo, masimulizi kuhusu mwana mpotevu, na Msamaria mwema.” Hadithi hizo zilitajwa kuwa “kati ya masimulizi ambayo yanaweza kumfundisha [mtoto] mambo ya maana sana maishani kama vile kutosema uwongo, kusamehe, kufanya amani na wengine, kuepuka chuki, kuwaheshimu wengine, kufanya mapatano, na kuonyesha upendo wa kindugu usio wa kichoyo.” Aliongezea hivi: “Maandiko hayo yanatoa kielelezo ambacho mtu anaweza kufuata maishani, kutenda na kuishi kulingana nacho.”

Kwa kweli, ni jambo zuri kuwatia watu moyo wasome Biblia. Hata hivyo, je, kweli watoto wanaweza “kufikiria na kutafakari wakiwa peke yao” kuhusu mambo wanayosoma katika Maandiko na kufanya maamuzi yanayofaa?

Hata watu wazima wanahitaji kufafanuliwa maana ya Maandiko. Kwa mfano, Biblia inatuambia kuhusu mwanamume ambaye hakuweza kutimiza mahitaji yake ya kiroho kwa “kufikiria na kutafakari akiwa peke yake.” Mwanamume huyo alikuwa ofisa Mwethiopia. Alikuwa anasoma unabii wa Isaya lakini hakuelewa maana yake. Kwa kuwa alitaka kuelewa ujumbe wa nabii huyo, alikubali maelezo aliyopewa na mwanafunzi Filipo. (Mdo. 8:26-40) Si Mwethiopia huyo tu aliyehitaji msaada wa kiroho. Sisi sote, na hasa watoto, tunahitaji kufafanuliwa maana ya Maandiko.

Biblia inatuonya hivi: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” (Met. 22:15) Watoto wanahitaji mwongozo na mwelekezo, na wazazi wao wana daraka la kuwapa elimu ya kiadili na kiroho inayotegemea Biblia na mambo yanayofundishwa katika kutaniko la Kikristo. Watoto wana haki ya kupata mazoezi hayo. Tangu utotoni, wanahitaji kusaidiwa kujenga msingi imara unaotegemea Biblia ili wakue kiroho na kuwa “watu wakomavu . . . ambao kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.”—Ebr. 5:14.