Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamwona Yehova Kuwa Baba Yako?

Je, Unamwona Yehova Kuwa Baba Yako?

Je, Unamwona Yehova Kuwa Baba Yako?

“BWANA, tufundishe jinsi ya kusali.” Wakati mmoja wa wanafunzi wake alipotoa ombi hilo, Yesu alijibu hivi: “Wakati wowote mnaposali, semeni, ‘Baba, jina lako na litakaswe.’” (Luka 11:1, 2) Yesu angetumia majina ya cheo yenye kuvutia ya Yehova kama vile “Mweza-Yote,” “Mfundishaji Mkuu,” “Muumba,” “Mzee wa Siku,” na “Mfalme wa umilele.” (Mwa. 49:25; Isa. 30:20; 40:28; Dan. 7:9; 1 Tim. 1:17) Badala yake, Yesu alitumia neno “Baba.” Kwa nini? Labda ni kwa sababu anataka tumkaribie Mungu ambaye ndiye mkuu zaidi katika ulimwengu wote kama vile mtoto mnyenyekevu anavyomkaribia baba mwenye upendo.

Hata hivyo, watu fulani wanaona kwamba ni vigumu kumwona Mungu kuwa Baba yao. Mkristo anayeitwa Atsuko * anasema hivi: “Kwa miaka mingi baada ya kubatizwa, ilikuwa vigumu kwangu kumkaribia Yehova na kusali kwake akiwa Baba.” Akitaja sababu iliyomfanya afikirie hivyo, anasema hivi: “Baba yangu mzazi hakunionyesha upendo hata kidogo.”

Katika siku hizi za mwisho zenye hatari, baba wengi hawawaonyeshi watoto wao “upendo wa asili.” (2 Tim. 3:1, 3) Kwa hiyo, ni jambo la kawaida kwa watu kuhisi kama Atsuko. Hata hivyo, inatia moyo kujua kwamba tuna sababu nzuri za kumwona Yehova kuwa Baba mwenye upendo.

Yehova Ni Mwandalizi Mwenye Upendo

Ili tumwone Yehova kuwa Baba yetu, tunahitaji kumfahamu vizuri zaidi. Yesu alisema hivi: “Hakuna yeyote anayemjua Mwana kabisa ila Baba, wala yeyote hamjui Baba kabisa ila Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Mt. 11:27) Njia bora kabisa ya kujua Yehova ni Baba wa aina gani, ni kufikiria yale ambayo Yesu alifunua kumhusu Mungu wa kweli. Hivyo basi, Yesu alifunua nini kumhusu Baba?

Yesu alionyesha kwamba Yehova ndiye Chanzo cha uhai wake aliposema hivi: “Ninaishi kwa sababu ya Baba.” (Yoh. 6:57) Sisi pia tuko hai kwa sababu ya Baba. (Zab. 36:9; Mdo. 17:28) Ni nini kilichomfanya Yehova awape wengine uhai? Je, haikuwa ni kwa sababu ya upendo? Bila shaka, tunapaswa pia kumpenda Baba yetu wa mbinguni kwa kuwa ametupatia zawadi hiyo.

Mungu amewaonyesha wanadamu upendo kwa njia kubwa zaidi kwa kuandaa dhabihu ya ukombozi ya Yesu. Tendo hilo la upendo linawawezesha wanadamu wenye dhambi kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kupitia Mwana wake mpendwa. (Rom. 5:12; 1 Yoh. 4:9, 10) Na kwa sababu Baba yetu wa mbinguni ni Mtimizaji wa ahadi zake, tunaweza kuwa na hakika kwamba mwishowe wote wanaompenda na kumtii watafurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Rom. 8:21.

Pia, Baba yetu wa mbinguni “hulichomoza jua lake juu” yetu kila siku. (Mt. 5:45) Kwa kawaida hata hatufikirii kusali ili jua lichomoze. Hata hivyo, tunalihitaji sana na tunafurahia joto lake. Kwa kuongezea, Baba yetu ni Mwandalizi asiye na kifani, ambaye anajua mahitaji yetu ya kimwili hata kabla hatujamwomba. Kwa hiyo, je, hatupaswi kutenga wakati wa kuchunguza na kutafakari kwa uthamini jinsi Baba yetu wa mbinguni anavyojali viumbe wake?—Mt. 6:8, 26.

Baba Yetu Ni ‘Mtunzaji Mwenye Upendo’

Unabii wa Isaya uliwahakikishia hivi watu wa kale wa Mungu: “Milima itaondolewa na vilima vitayumba-yumba, lakini urafiki wangu hautaondolewa kamwe kwako wala agano langu la amani halitayumba-yumba, asema mtunzaji wako mwenye upendo Yehova.” (Isa. 54:10, The Bible in Living English) Sala ambayo Yesu alitoa katika usiku wake wa mwisho duniani inakazia kwamba kwa kweli Yehova ni ‘mtunzaji mwenye upendo.’ Yesu alisali hivi kuhusu wanafunzi wake: “Wao wamo ulimwenguni nami ninakuja kwako. Baba Mtakatifu, walinde kwa sababu ya jina lako.” (Yoh. 17:11, 14) Yehova amewatunza na kuwalinda wafuasi wa Yesu.

Njia moja ambayo Mungu anatulinda kutoka kwa hila za Shetani leo ni kwa kutuandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Ili ‘tuvae mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,’ ni jambo la maana kula chakula hicho kinachotutia nguvu. Kwa mfano, fikiria “ngao kubwa ya imani,” ambayo inaweza kutusaidia “kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.” (Efe. 6:11, 16) Imani yetu inatulinda kutokana na madhara ya kiroho na inaonyesha kwamba tunakubali Baba yetu atulinde.

Tunaweza kuelewa zaidi jinsi Baba yetu wa mbinguni anavyotulinda kwa upendo kwa kuchunguza jinsi Mwana wa Mungu alivyotenda alipokuwa duniani. Hebu fikiria simulizi lililoandikwa kwenye Marko 10:13-16. Katika simulizi hilo, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu.” Watoto hao walipokusanyika karibu naye, Yesu aliwakumbatia kwa wororo na akawabariki. Bila shaka, walitabasamu kwa shangwe! Tunajua kwamba Mungu wa kweli anataka tumkaribie kwa sababu Yesu alisema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yoh. 14:9.

Yehova Mungu ndiye Chanzo kikuu cha upendo. Yeye ni Mwandalizi asiye na kifani na Mlinzi asiyeweza kulinganishwa na yeyote na anataka tumkaribie. (Yak. 4:8) Kwa hiyo, bila shaka, Yehova ndiye Baba bora zaidi!

Tunafaidika Kwelikweli!

Tunafaidika sana tunapomtegemea Yehova na kumwona kuwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo mwororo. (Met. 3:5, 6) Yesu alifaidika kwa kuwa alimtegemea kabisa Baba yake. Kristo aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Siko peke yangu, bali Baba aliyenituma yuko pamoja nami.” (Yoh. 8:16) Sikuzote, Yesu alikuwa na hakika kwamba Yehova angemtegemeza. Kwa mfano, wakati alipobatizwa, Baba yake alimhakikishia hivi kwa upendo: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mt. 3:15-17) Na muda mfupi tu kabla ya kifo chake, Yesu alipaaza sauti hivi: “Baba, ninaikabidhi roho yangu mikononi mwako.” (Luka 23:46) Bado Yesu alimtegemea kabisa Baba yake.

Inaweza kuwa vivyo hivyo kwetu. Yehova akiwa upande wetu, hatuwezi kuogopa chochote. (Zab. 118:6) Atsuko ambaye alitajwa mwanzoni, alizoea kutegemea nguvu zake alipokabili matatizo. Lakini akaanza kujifunza kuhusu maisha na huduma ya Yesu, hasa akikazia fikira uhusiano wa karibu kati ya Yesu na Baba yake wa mbinguni. Matokeo yalikuwa nini? Atsuko anasema: “Nilijifunza maana ya kuwa na Baba na kumtegemea.” Anaongezea hivi: “Nilipata amani ya kweli na furaha. Kwa kweli, hatuna sababu ya kuogopa chochote.”

Tunafaidika kwa njia gani nyingine tunapomwona Yehova kuwa Baba yetu? Kwa kawaida, watoto wanawapenda wazazi wao na wanataka kuwapendeza. Kwa sababu ya upendo, Mwana wa Mungu ‘sikuzote alifanya mambo yanayompendeza Baba yake.’ (Yoh. 8:29) Vivyo hivyo, upendo wetu kwa Baba yetu wa mbinguni unaweza kutuchochea tutende kwa hekima na ‘kumsifu hadharani.’—Mt. 11:25; Yoh. 5:19.

Baba Yetu ‘Anaushika Mkono Wetu wa Kuume’

Baba yetu wa mbinguni ametupatia pia “msaidizi”—roho yake takatifu. Yesu alisema kwamba ‘itawaongoza ninyi ndani ya kweli yote.’ (Yoh. 14:15-17; 16:12, 13) Roho takatifu ya Mungu inaweza kutusaidia kumwelewa vizuri zaidi Baba yetu. Inaweza kutusaidia “kupindua ngome zenye nguvu,” yaani, maoni yaliyo moyoni mwetu, mawazo mabaya, au mawazo yaliyopotoka, na hivyo ‘kuiteka kila fikira ili kuifanya imtii Kristo.’ (2 Kor. 10:4, 5) Basi, acheni tumwombe Yehova atupe “msaidizi” aliyeahidiwa, tukiwa na uhakika kwamba ‘Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ (Luka 11:13) Pia, ni jambo linalofaa kusali ili roho takatifu itusaidie tuendelee kumkaribia Yehova zaidi.

Mtoto mchanga anahisi akiwa salama na bila wasiwasi anapotembea akiwa ameshikwa mkono na baba yake. Ikiwa kwa kweli unamwona Yehova kuwa Baba yako, unaweza kuwa na hakika na maneno haya yenye kutia moyo: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’” (Isa. 41:13) Unaweza kuwa na pendeleo zuri ajabu la “kutembea” na Mungu milele. (Mika 6:8) Endelea kufanya mapenzi yake, na utapata upendo, shangwe, na usalama ambao watu wanaomwona Yehova kuwa Baba wanapata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jina limebadilishwa.