Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Karibu Kwenye Njia Bora Zaidi ya Maisha!

Karibu Kwenye Njia Bora Zaidi ya Maisha!

Karibu Kwenye Njia Bora Zaidi ya Maisha!

“Tukiishi na tukifa, sisi ni wa Yehova.”—ROM. 14:8.

1. Yesu alifundisha nini kuhusu njia bora zaidi ya maisha?

YEHOVA anataka tufurahie njia bora zaidi ya maisha. Watu wanaweza kuishi kwa njia mbalimbali, lakini kuna njia moja tu ya maisha ambayo ni bora zaidi. Njia bora zaidi ya kutumia maisha yetu ni kuishi kulingana na Neno la Mungu na kujifunza kutoka kwa Mwana wake, Yesu Kristo. Yesu aliwafundisha wafuasi wake wamwabudu Mungu kwa roho na kweli, kisha akawaagiza wafanye wanafunzi. (Mt. 28:19, 20; Yoh. 4:24) Tunapoishi kulingana na maagizo ya Yesu, tunampendeza Yehova na kufurahia baraka Zake.

2. Watu wengi katika karne ya kwanza walitenda jinsi gani baada ya kusikia ujumbe wa Ufalme, na ilimaanisha nini kuwa watu wa “Ile Njia”?

2 Watu ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’ wanapoamini na kubatizwa, tunakuwa na sababu nzuri za kuwaambia, “Karibuni kwenye njia bora zaidi ya maisha!” (Mdo. 13:48) Katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, maelfu ya watu kutoka katika mataifa mbalimbali walikubali kweli na kubatizwa ili kuonyesha waziwazi kwamba walikuwa wamejitoa kwa Mungu. (Mdo. 2:41) Wanafunzi hao wa kale walikuwa watu wa “Ile Njia.” (Mdo. 9:2; 19:23) Usemi huo ulifaa kwa sababu wale ambao walikuwa wafuasi wa Kristo waliishi maisha ambayo yalitegemea imani katika Yesu Kristo na waliiga mfano wake.—1 Pet. 2:21.

3. Ni nini kinachowachochea watu wa Yehova wabatizwe, na ni wangapi ambao wamebatizwa katika kipindi cha miaka kumi iliyopita?

3 Kazi ya kufanya wanafunzi imesonga kwa kasi sana katika siku hizi za mwisho na sasa inafanywa katika nchi zaidi ya 230. Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, watu zaidi ya 2,700,000 wameamua kumtumikia Yehova na wamebatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwake. Idadi hiyo inaonyesha kwamba kwa wastani watu zaidi ya 5,000 wanabatizwa kila juma! Uamuzi wa kubatizwa unategemea kumpenda Mungu, kuwa na ujuzi wa Maandiko, na kuamini mafundisho yaliyomo. Ubatizo ni hatua ya maana sana katika maisha yetu, kwa sababu ni mwanzo wa kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova. Pia, ubatizo unaonyesha kwamba tuna hakika atatusaidia tumtumikie kwa uaminifu, kama vile alivyowasaidia watumishi wake wa kale watembee katika njia yake.—Isa. 30:21.

Kwa Nini Ubatizwe?

4, 5. Taja baraka na faida fulani za kubatizwa.

4 Labda umepata ujuzi kumhusu Mungu, umefanya mabadiliko katika maisha yako, na sasa wewe ni mhubiri ambaye hajabatizwa. Unastahili kupongezwa kwa sababu ya maendeleo hayo. Lakini je, umejiweka wakfu kwa Mungu katika sala, na je, unatazamia kubatizwa? Kutokana na mambo ambayo umejifunza katika Biblia, inaelekea unajua kwamba unapaswa kutumia maisha yako kumsifu Yehova, bali si kujipendeza mwenyewe tu au kujikusanyia vitu vya kimwili. (Soma Zaburi 148:11-13; Luka 12:15) Hivyo basi, utapata baraka na faida gani ukibatizwa?

5 Ukiwa Mkristo aliyejiweka wakfu, maisha yako yatakuwa na kusudi bora zaidi. Utakuwa na furaha kwa sababu unafanya mapenzi ya Mungu. (Rom. 12:1, 2) Roho takatifu ya Yehova itakusaidia kusitawisha sifa za Kikristo kama vile amani na imani. (Gal. 5:22, 23) Mungu atajibu sala zako na atabariki jitihada zako za kuishi kulingana na Neno lake. Ukiishi kulingana na mapenzi ya Mungu, utapata shangwe katika huduma yako na utaimarisha tumaini lako la kupata uzima wa milele. Kwa kuongezea, ukijiweka wakfu na kubatizwa utaonyesha kwamba unataka kwa kweli kuwa Shahidi wa Yehova.—Isa. 43:10-12.

6. Ubatizo wetu unaonyesha nini?

6 Tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa, tunaonyesha waziwazi kwamba sisi ni mali ya Yehova. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa kweli, hakuna hata mmoja wetu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe tu, na hakuna yeyote anayekufa kwa ajili yake mwenyewe tu; kwa maana tukiishi, tunaishi kwa ajili ya Yehova, na tukifa, tunakufa kwa ajili ya Yehova. Kwa hiyo tukiishi na tukifa, sisi ni wa Yehova.” (Rom. 14:7, 8) Mungu ameonyesha kwamba anatuthamini kwa kutupatia uhuru wa kuchagua. Tunapoamua kutoka moyoni kufuata njia hii ya maisha kwa sababu tunampenda Mungu, tunafanya moyo wake ushangilie. (Met. 27:11) Ubatizo wetu unaonyesha kwamba tumejiweka wakfu kwa Mungu na ni tangazo la waziwazi kwamba Yehova ndiye Mtawala wetu. Unaonyesha kwamba tunamuunga mkono katika lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. (Mdo. 5:29, 32) Naye Yehova, anakuwa upande wetu. (Soma Zaburi 118:6.) Pia, ubatizo unatufungulia njia ya kupata baraka nyingine nyingi za kiroho sasa na wakati ujao.

Baraka ya Kuwa Sehemu ya Undugu Wenye Upendo

7-9. (a) Yesu aliwahakikishia nini wale ambao waliacha vitu vyote na kumfuata? (b) Ahadi ya Yesu kwenye Marko 10:29, 30 inatimizwa jinsi gani?

7 Mtume Petro alimwambia Yesu hivi: “Tazama! Tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe; kwa kweli kutakuwa na nini kwa ajili yetu?” (Mt. 19:27) Petro alitaka kujua yeye na wanafunzi wengine wa Yesu wangepata nini wakati ujao. Walijidhabihu sana ili wajitoe kabisa kwa kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. (Mt. 4:18-22) Yesu aliwahakikishia nini?

8 Kulingana na simulizi la Marko, Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangekuwa sehemu ya undugu wa kiroho. Alisema hivi: “Hakuna mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara mia sasa katika kipindi hiki cha wakati, nyumba na ndugu na dada na mama na watoto na mashamba, pamoja na mateso, na katika mfumo wa mambo unaokuja uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30) Wakristo wa karne ya kwanza kama vile Lidia, Akila, Prisila, na Gayo, walikuwa kati ya wale ambao walitoa “nyumba” zao na pia wakawa “ndugu na dada na mama” kwa waamini wenzao, kama Yesu alivyokuwa ameahidi.—Mdo. 16:14, 15; 18:2-4; 3 Yoh. 1, 5-8.

9 Mambo ambayo Yesu alisema yanatimizwa kwa kiwango kikubwa leo. “Mashamba” ambayo wafuasi wake wanaacha leo yanamaanisha maisha ambayo wengi, kutia ndani wamishonari, washiriki wa familia ya Betheli, watumishi wa kimataifa, na wengine, wanaacha kwa kupenda ili wafanye kazi ya Ufalme katika nchi mbalimbali. Akina ndugu na dada wengi wameacha nyumba zao ili waishi maisha rahisi, na tunafurahi sana kusikia masimulizi yao yanayoonyesha jinsi ambavyo Yehova amewatunza na furaha ambayo wamepata kwa kumtumikia. (Mdo. 20:35) Kwa kuongezea, watumishi wote wa Yehova ambao wamebatizwa wanaweza kufurahia baraka zinazotokana na “kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu]” wakiwa sehemu ya undugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote.—Mt. 6:33.

Kukaa Salama “Mahali pa Siri”

10, 11. “Mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi” ni nini, na tunaweza kuingia jinsi gani mahali hapo?

10 Baraka nyingine tunayopata kwa kujiweka wakfu na kubatizwa ni pendeleo la kukaa katika “mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi.” (Soma Zaburi 91:1.) Hapa ni mahali pa mfano penye usalama na ulinzi, yaani, ni hali ya kulindwa kutokana na madhara ya kiroho. Ni “mahali pa siri” kwa sababu hapatambuliwi na watu walio katika giza la kiroho ambao hawamtegemei Mungu. Tunapoishi kulingana na wakfu wetu na kumtegemea Yehova kabisa, ni kana kwamba tunamwambia hivi: “Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ambaye nitamtegemea.” (Zab. 91:2) Yehova Mungu anakuwa makao yetu salama. (Zab. 91:9) Hakuna makao mengine yaliyo bora au salama zaidi kuliko makao hayo.

11 Kuingia “mahali pa siri” pa Yehova kunamaanisha pia kwamba tumepata pendeleo la kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Tunapata pendeleo hilo tunapojiweka wakfu na kubatizwa. Baada ya hapo, tunaendelea kujenga uhusiano wetu pamoja na Mungu kwa kumkaribia kupitia funzo la Biblia, sala inayotoka moyoni, na kumtii kikamili. (Yak. 4:8) Hakuna mtu mwingine yeyote ambaye amewahi kuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova isipokuwa Yesu, na sikuzote amemtegemea Muumba bila kuyumbayumba. (Yoh. 8:29) Kwa hiyo, tusiwe na shaka kamwe kwamba Yehova anatamani na anaweza kutusaidia kutimiza nadhiri yetu ya kujiweka wakfu. (Mhu. 5:4) Maandalizi ya kiroho ambayo Mungu amewapa watu wake yanathibitisha kabisa kwamba anatupenda kikweli naye anataka tufanikiwe tunapomtumikia.

Thamini Paradiso Yetu ya Kiroho

12, 13. (a) Paradiso ya kiroho ni nini? (b) Tunaweza kuwasaidia jinsi gani wapya?

12 Tunapojiweka wakfu na kubatizwa tunapata pia pendeleo la kukaa katika paradiso ya kiroho yenye baraka. Paradiso hiyo ni mazingira ya pekee ya kiroho ambayo tunafurahia pamoja na waabudu wenzetu ambao wana uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu na waamini wenzao. (Zab. 29:11; Isa. 54:13) Hakuna kitu chochote ulimwenguni ambacho kinaweza kulinganishwa na paradiso yetu ya kiroho. Hilo linaonekana wazi hasa kwenye makusanyiko ya kimataifa, ambapo ndugu na dada zetu kutoka mataifa, lugha, na jamii mbalimbali wanakusanyika katika mazingira yenye amani, umoja, na upendo wa kindugu.

13 Paradiso ya kiroho ambayo tunafurahia ni tofauti kabisa na hali zenye kusikitisha zilizo ulimwenguni leo. (Soma Isaya 65:13, 14.) Tunapotangaza ujumbe wa Ufalme, tunapata pendeleo la kuwaalika wengine waingie katika paradiso ya kiroho. Ni baraka pia kuwasaidia wale ambao wamejiunga na kutaniko hivi karibuni na ambao wanahitaji kuzoezwa katika huduma. Huenda tukapata baraka na pendeleo la kuwasaidia watu fulani wapya tunapoombwa na wazee tufanye hivyo, kama vile Akila na Prisila ‘walivyomfafanulia Apolo kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.’—Mdo. 18:24-26.

Endelea Kujifunza Kutoka kwa Yesu

14, 15. Tuna sababu gani nzuri za kuendelea kujifunza kutoka kwa Yesu?

14 Tuna sababu nzuri kabisa za kuendelea kujifunza kutoka kwa Yesu. Kabla ya kuja duniani, Yesu alifanya kazi pamoja na Baba yake kwa maelfu ya miaka. (Met. 8:22, 30) Alijua kwamba njia bora zaidi ya maisha ni kumtumikia Mungu na kutoa ushahidi kuhusu kweli. (Yoh. 18:37) Yesu alielewa vizuri kabisa kwamba ikiwa angefuata njia nyingine ya maisha angeishi maisha ya ubinafsi na hangekuwa na tumaini la wakati ujao. Alijua kwamba angejaribiwa vikali na angeuawa. (Mt. 20:18, 19; Ebr. 4:15) Akiwa Kielelezo chetu, alitufundisha jinsi ya kuendelea kuwa watimilifu.

15 Muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa, Shetani alijaribu kumshawishi aache njia bora zaidi ya maisha, lakini hakufanikiwa. (Mt. 4:1-11) Hilo linatufundisha kwamba hata Shetani afanye nini, tunaweza kudumisha utimilifu wetu. Inaelekea kwamba Shetani anawakazia fikira wale wanaokaribia kubatizwa na vilevile wale waliobatizwa hivi karibuni. (1 Pet. 5:8) Huenda tukapingwa na washiriki wa familia zetu wenye nia nzuri ambao wameelezwa mambo ya uwongo kuhusu Mashahidi. Hata hivyo, majaribu kama hayo yanatupa nafasi ya kuonyesha sifa nzuri za Kikristo, kama vile heshima na busara, tunapojibu maswali yao na kutoa ushahidi. (1 Pet. 3:15) Mambo kama hayo yanaweza kuwa na matokeo mazuri kwa wale wanaotusikiliza.—1 Tim. 4:16.

Endelea Kufuata Njia Bora Zaidi ya Maisha!

16, 17. (a) Andiko la Kumbukumbu la Torati 30:19, 20 lina matakwa gani matatu ya msingi ya kupata uzima? (b) Yesu, Yohana, na Paulo waliunga mkono jinsi gani maneno yaliyoandikwa na Musa?

16 Miaka 1,500 hivi kabla ya Yesu kuja duniani, Musa aliwahimiza Waisraeli wachague njia bora zaidi ya maisha. Alisema hivi: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.” (Kum. 30:19, 20) Waisraeli hawakuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu, lakini matakwa matatu ya msingi ya kupata uzima ambayo yalitajwa na Musa hayajabadilika. Yesu na wengine pia waliyataja matakwa hayo.

17 Kwanza, ‘ni lazima tumpende Yehova Mungu wetu.’ Tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa kutenda kulingana na njia zake za uadilifu. (Mt. 22:37) Pili, ‘ni lazima tusikilize sauti ya Yehova’ kwa kujifunza Neno la Mungu na kutii amri zake. (1 Yoh. 5:3) Ili tufanye hivyo, tunahitaji kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo, ambamo Biblia inazungumziwa. (Ebr. 10:23-25) Tatu, ‘ni lazima tushikamane na Yehova.’ Hata tukikabili hali gani, acheni sikuzote tumtegemee Mungu na kumfuata Mwana wake.—2 Kor. 4:16-18.

18. (a) Gazeti la Mnara wa Mlinzi lilisema nini kuhusu kweli mwaka wa 1914? (b) Tunapaswa kuhisi namna gani kuhusu nuru ya kweli leo?

18 Tunabarikiwa sana tunapoishi kulingana na kweli za Biblia. Mwaka wa 1914, maneno haya ya pekee yalichapishwa katika Mnara wa Mlinzi: “Je, si kweli kwamba sisi ni watu wenye furaha na waliobarikiwa? Je, si kweli kwamba Mungu wetu ni mwaminifu? Ikiwa kuna mtu ambaye anajua njia nyingine ambayo ni bora zaidi, na aifuate. Ikiwa mmoja wenu atapata kitu kilicho bora zaidi, tunatumaini kwamba atatuambia. Hatujui jambo lingine bora au linalokaribia hata kidogo mambo bora ambayo tumepata katika Neno la Mungu. . . . Hatuwezi kamwe kueleza amani, shangwe, na baraka ambazo tumepata moyoni na maishani mwetu baada ya kupata ujuzi ulio wazi kuhusu Mungu wa kweli. Habari kuhusu Hekima, Haki, Nguvu, na Upendo wa Mungu zinatosheleza kabisa mahitaji yetu ya kiakili na ya kihisia. Hatuna cha kutafuta tena. Hatuhitaji kitu kingine chochote ila tu kuelewa vizuri zaidi Habari hii nzuri ajabu.” (Gazeti la Mnara wa Mlinzi, Desemba 15, 1914 [15/12/1914] la Kiingereza, ukurasa wa 377-378) Bado tunathamini sana ile nuru ya kiroho na kweli. Bila shaka, sasa tuna sababu nzuri hata zaidi ya kushangilia kwamba ‘tunatembea katika nuru ya Yehova.’—Isa. 2:5; Zab. 43:3; Met. 4:18.

19. Kwa nini wale ambao wanastahili kubatizwa wanapaswa kuchukua hatua hiyo bila kukawia?

19 Ikiwa unataka ‘kutembea katika nuru ya Yehova’ lakini bado hujajiweka wakfu na kuwa Mkristo aliyebatizwa, usikawie kufanya hivyo. Chukua hatua yoyote inayohitajiwa ili utimize matakwa ya Biblia yanayohusu ubatizo—njia ya pekee ya kumshukuru Mungu na Kristo kwa ajili ya yale ambayo wametufanyia. Mpe Yehova mali yako ya kimwili yenye thamani zaidi, yaani, uhai wako. Onyesha kwamba unataka kufanya mapenzi ya Mungu kwa kumfuata Mwana wake. (2 Kor. 5:14, 15) Bila shaka, hiyo ndiyo njia bora zaidi ya maisha!

Ungesema Nini?

• Ubatizo wetu unaonyesha nini?

• Tunapata baraka gani tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa?

• Kwa nini ni jambo la maana sana kujifunza kutoka kwa Yesu?

• Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kufuata njia bora zaidi ya maisha?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Unapobatizwa unaonyesha kwamba umechagua njia bora zaidi ya maisha

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, umekaa salama “mahali pa siri”?