Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kifaa cha Kuwasaidia Vijana Wamkumbuke Muumba Wao

Kifaa cha Kuwasaidia Vijana Wamkumbuke Muumba Wao

Kifaa cha Kuwasaidia Vijana Wamkumbuke Muumba Wao

MIAKA 3,000 hivi iliyopita, mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” (Mhu. 12:1) Sasa vijana Wakristo wana kifaa kingine cha kuwasaidia kufanya hivyo. Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, ambacho kilitolewa kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova yenye kichwa “Kuongozwa na Roho ya Mungu,” ambayo yalifanywa ulimwenguni pote kuanzia Mei (Mwezi wa 5) 2008 mpaka Januari (Mwezi wa 1) 2009.

Kwenye upande wa ndani wa jalada la mbele la kitabu hicho kuna barua kwa vijana kutoka kwa Baraza Linaloongoza. Kwa sehemu, barua hiyo inasema hivi: “Tunasali kwa bidii kwamba habari iliyo katika kitabu hiki itakusaidia kushinda mikazo na vishawishi vinavyowakabili vijana leo na kitakuonyesha jinsi unavyoweza kufanya maamuzi yanayopatana na mapenzi ya Mungu.”

Kwa kufaa, wazazi wangependa kuwalea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Hata hivyo, vijana wengi wanapobalehe hawajiamini nao wanahitaji mwongozo. Ikiwa wewe ni mzazi wa kijana ambaye anabalehe, unaweza kumsaidia jinsi gani mtoto wako afaidike zaidi na kitabu hicho? Yafuatayo ni baadhi ya mapendekezo.

Uwe na nakala yako ya kitabu hicho na ukielewe vizuri kabisa. Ili ukielewe vizuri, haitoshi tu kukisoma. Jaribu pia kuelewa jinsi ambavyo mawazo yanaelezwa katika kitabu hicho. Badala tu ya kuwaambia vijana mambo yanayofaa na yasiyofaa, kitabu hicho kinazoeza “nguvu zao za ufahamu.” (Ebr. 5:14) Pia, kinawapa mapendekezo yanayofaa kuhusu jinsi wanavyoweza kushikamana na mambo yanayofaa. Kwa mfano, Sura ya 15 (“Nitashindaje Mkazo Kutoka kwa Vijana Wenzangu?”) inawasaidia vijana wachukue hatua zaidi badala tu ya kusema hapana. Inaonyesha jinsi ya kutumia kanuni za Biblia ili kutatua matatizo na inawasaidia vijana wajue jinsi ya “kumjibu kila mtu” wanaposhawishiwa.—Kol. 4:6.

Tumia sehemu ambazo zinamwomba kijana atoe maoni yake. Ingawa sehemu hizo zimekusudiwa kutumiwa na vijana, kwa nini usiandike katika nakala yako inapofaa? * Kwa mfano, unapochunguza maswali mawili yanayohitaji kujibiwa kuhusu urafiki wa kimapenzi kwenye ukurasa wa 16, jaribu kukumbuka jinsi ulivyohisi ulipokuwa na umri kama wa mtoto wako. Huenda ukataka kuandika majibu ambayo ungetoa ulipokuwa kijana. Kisha unaweza kujiuliza hivi: ‘Maoni yangu kuhusu jambo hili yamebadilika jinsi gani baada ya miaka mingi kupita? Nimejifunza mambo gani tangu nilipobalehe, na ninaweza kumweleza jinsi gani mtoto wangu mambo hayo kwa njia nzuri kabisa?’

Heshimu faragha ya kijana wako. Sehemu za kitabu hicho ambazo zinahitaji mtu atoe maoni yake zimekusudiwa kumfanya mtoto wako ajieleze na kumfanya aandike majibu yake au ajibu kimoyomoyo. Lengo lako ni kujua yaliyo moyoni mwake, si yale yaliyo katika kitabu chake. Katika ukurasa wa 3 wa kitabu hicho, sehemu yenye kichwa “Taarifa kwa Wazazi” inasema hivi: “Ili vijana wenu waandike majibu yao kwa unyoofu, acheni walichoandika katika nakala zao kiwe siri yao. Baadaye, huenda hata wakawa huru kuzungumza nanyi kuhusu mambo ambayo wameandika katika vitabu vyao.”

Kitabu Kinachofaa kwa Ajili ya Funzo la Biblia la Familia

Kitabu Vijana Huuliza, Buku la 2, kinafaa sana kutumiwa katika Ibada yenu ya Familia. Kwa kuwa kitabu hicho hakina maswali mwishoni mwa kila fungu, mnaweza kukitumia jinsi gani? Kwa nini msitumie njia ambayo inawafaa zaidi watoto wenu?

Kwa mfano, huenda familia fulani zikawa na vipindi vya mazoezi zinapozungumzia sehemu yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” kwenye ukurasa wa 132 na 133. Swali la kwanza katika sehemu hiyo linaweza kumsaidia mwana au binti yako aeleze hali ambayo ni ngumu zaidi kwake. Swali la pili linaonyesha mazingira ambayo yanaweza kuchangia hali hiyo itokee. Baada ya kuchunguza jambo linaloweza kutokea ikiwa mtoto wako atalegeza msimamo au ikiwa atashinda mkazo kutoka kwa vijana wenzake, mtoto wako anaombwa atoe majibu ambayo ama anakubali, anapiga chenga, au anakabiliana moja kwa moja na mkazo huo. Msaidie mwana au binti yako awe mbunifu na atayarishe majibu ambayo anahisi kwamba atayatoa kwa uhuru, kwa uhakika, na usadikisho.—Zab. 119:46.

Kifaa cha Kuwasiliana

Kitabu Vijana Huuliza, Buku la 2, kinawatia moyo vijana wawasiliane na wazazi wao. Kwa mfano, masanduku yenye kichwa “Ninaweza Kuzungumza Namna Gani na Baba Yangu au Mama Yangu Kuhusu Ngono?” (ukurasa wa 63-64) na “Zungumza na Wazazi Wako!” (ukurasa wa 189) kuna mapendekezo yanayofaa kuhusu jinsi ya kuanza kuzungumzia mambo ambayo si rahisi kuzungumzia. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 13 aliandika hivi: “Kitabu hicho kilinipa ujasiri wa kuzungumza na wazazi wangu kuhusu mambo ambayo nilikuwa nikifikiria—hata yale ambayo nilikuwa nimefanya.”

Kitabu hicho kinachochea mazungumzo kwa njia nyingine mbalimbali. Mwishoni mwa kila sura kuna sanduku lenye kichwa “Una Maoni Gani?” Badala tu ya kurudia mambo makuu, linaweza kutumiwa kama muhtasari wa mazungumzo ya familia. Karibu mwisho wa kila sura, kuna sanduku lingine lenye kichwa “Hatua za Kuchukua!” Sanduku hilo linawapa vijana nafasi ya kuandika njia hususa ambazo wanaweza kutumia yale ambayo wamejifunza katika sura hiyo. Kila sehemu ya mwisho ya sanduku “Hatua za Kuchukua!” inasema hivi: “Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni . . . ” Sehemu hiyo inaweza kuwasaidia vijana watafute mashauri yanayofaa kutoka kwa wazazi wao.

Gusa Moyo!

Ukiwa mzazi, lengo lako ni kugusa moyo wa mtoto wako. Kitabu Vijana Huuliza, Buku la 2, kinaweza kukusaidia ufanye hivyo. Fikiria jinsi ambavyo baba mmoja ametumia kitabu hicho kuzungumza kutoka moyoni pamoja na binti yake.

“Mimi na Rebekah tuna sehemu nzuri ambazo tunapenda kwenda kwa miguu, baiskeli, au kwa gari. Nimeona kwamba mazingira hayo yanamfanya awe huru kujieleza.

“Sehemu ya kwanza ya kitabu hicho ambayo tulizungumzia ni barua kutoka kwa Baraza Linaloongoza na ‘Taarifa kwa Wazazi.’ Nilitaka binti yangu ajue kwamba kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 3, anaweza kuandika chochote kwenye kitabu chake. Singechunguza ili kuona alichokuwa ameandika.

“Nilimruhusu Rebekah achague sura ambazo alipenda tuzungumzie na mpangilio ambao alitaka tufuate. Moja ya sura ambazo alichagua kwanza ilikuwa na kichwa ‘Nicheze Michezo ya Kompyuta?’ Singefikiria kwamba angechagua sura hiyo! Hata hivyo, alikuwa na sababu. Baadhi ya marafiki wake walikuwa wanacheza mchezo wa kompyuta wenye kutisha sana. Sikujua kwamba mchezo huo ulionyesha jeuri waziwazi na ulikuwa na lugha chafu! Lakini nilitambua mambo hayo yote tulipokuwa tukizungumzia sanduku lenye kichwa ‘Hatua za Kuchukua!’ kwenye ukurasa wa 251. Pia, sanduku hilo lilimsaidia Rebekah atayarishe jinsi ambavyo angejibu ikiwa mtu fulani angemshinikiza kucheza mchezo huo.

“Kufikia sasa, Rebekah haogopi kuniambia mambo ambayo ameandika katika kitabu chake. Wakati wa funzo, tunazungumza kwa uhuru. Tunasoma kwa zamu kisha anataka kuzungumzia kila jambo, kutia ndani picha na masanduku. Hilo linanipa nafasi ya kumweleza jinsi hali ilivyokuwa nilipokuwa kijana, kisha ananieleza jinsi hali ilivyo leo. Anafurahia kunieleza kila jambo!”

Ikiwa wewe ni mzazi, bila shaka ulisisimuka sana kitabu hicho kilipotolewa. Sasa una nafasi ya kukitumia vizuri. Baraza Linaloongoza linatumaini kwamba kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, kitainufaisha familia yako. Na kiwasaidie wote—hasa vijana wetu wapendwa—‘kuendelea kutembea kwa roho.’—Gal. 5:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Baadhi ya kurasa ambazo zinahitaji mtu aandike maoni yake zinaweza kutumiwa na watu wa umri wowote. Kwa mfano, sanduku “Dhibiti Hasira Yako,” (ukurasa wa 221), linaweza kukusaidia kama tu linavyoweza kumsaidia mwana au binti yako. Ndivyo pia na sehemu yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” (ukurasa wa 132-133), “Bajeti Yangu ya Kila Mwezi” (ukurasa wa 163), na “Miradi Yangu” (ukurasa wa 314).

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

Mambo Ambayo Vijana Fulani Wanasema

“Hiki ni kitabu ambacho unapaswa kusoma ukiwa na kalamu huku ukitafakari. Kwa kuwa kina nafasi za kuandika maoni yako, unaweza kutafakari faraghani ukiwa na kusudi la kuboresha maisha yako.”—Nicola.

“Ninashinikizwa sana kuanzisha urafiki wa kimapenzi, hata na watu ambao hawana nia mbaya. Sehemu ya kwanza ya kitabu hicho ilinisadikisha kwamba, kwa sasa, hata mtu aseme nini, siko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi.”—Katrina.

“Sanduku lenye kichwa ‘Unafikiria Kubatizwa?’ limenisaidia nithamini hata zaidi ubatizo wangu. Lilinichochea kuchunguza tena mazoea yangu ya kujifunza na kusali.”—Ashley.

“Ingawa wazazi wangu Wakristo wamenifundisha tangu nilipokuwa mchanga, kitabu hiki kimenifanya nifikirie hatua ambazo ninapaswa kuchukua maishani. Pia, kimenisaidia kuzungumza kwa uhuru zaidi pamoja na wazazi wangu.”—Zamira.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wazazi, mnapaswa kukielewa kabisa kitabu hiki

[Picha katika ukurasa wa 32]

Uwe na mradi wa kugusa moyo wa mtoto wako