Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni hali gani ambazo zinaweza kufanya mtu abatizwe tena?

Katika hali fulani, huenda mtu aliyebatizwa akatilia shaka uhalali wa ubatizo wake na huenda akataka kubatizwa tena. Kwa mfano, huenda wakati wa ubatizo mtu huyo alikuwa anaishi katika hali fulani au alikuwa anazoea kutenda jambo fulani kwa siri ambalo lingefanya atengwe na ushirika ikiwa angekuwa amebatizwa kihalali. Je, angeweza kujiweka wakfu kwa Mungu chini ya hali kama hizo? Mtu huyo, angeweza kujiweka wakfu kwa Yehova kihalali ikiwa tu angekuwa ameacha zoea lisilopatana na Maandiko. Kwa hiyo, mtu ambaye alibatizwa akiwa katika hali hiyo mbaya anaweza kuona kwamba ni jambo linalofaa kubatizwa tena.

Namna gani mtu ambaye hakuwa na zoea la kufanya dhambi wakati alipobatizwa lakini baada ya kubatizwa alifanya dhambi ambayo ilihitaji kushughulikiwa na halmashauri ya hukumu? Namna gani akisema kwamba hakuelewa kikamili jambo alilokuwa akifanya wakati wa ubatizo na hivyo ubatizo wake haukuwa halali? Wazee wanapokutana na mkosaji, hawapaswi kuuliza maswali kuhusu ubatizo wake au kumuuliza ikiwa anahisi kwamba wakfu na ubatizo wake ulikuwa halali. Bila shaka, alisikiliza hotuba inayotegemea Maandiko kuhusu maana ya ubatizo. Akajibu kwa uhakika maswali ya wakfu na ubatizo. Kisha akabadili mavazi yake na kubatizwa kwa kutumbukizwa ndani ya maji. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba alielewa kikamili uzito wa jambo alilokuwa akifanya. Kwa hiyo, wazee watashughulika naye kama mtu aliyebatizwa.

Mtu huyo akisema kwamba ubatizo wake haukuwa halali, wazee watamwomba achunguze gazeti Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Machi 1, 1960, ukurasa wa 159 na 160, na Februari 15, 1964 (15/2/1964), ukurasa wa 123 mpaka 126, ambapo suala la kubatizwa tena linazungumziwa kwa undani. Kubatizwa tena kwa sababu ya hali fulani (kama vile, kutoelewa Biblia vizuri wakati wa ubatizo) ni uamuzi wa mtu binafsi.

Wakristo wanapaswa kukumbuka mambo gani wanapoamua kuishi katika nyumba moja na watu wengine?

Kila mtu anahitaji mahali pa kuishi. Hata hivyo, watu wengi leo hawana nyumba zao wenyewe. Hali ya mtu ya kiuchumi, kiafya, au mambo mengine yanaweza kulazimu familia ziishi pamoja na watu wa ukoo. Katika maeneo fulani ya ulimwengu, watu wengi wa ukoo wanaweza kuishi katika chumba kimoja ambacho hakina faragha.

Si daraka la tengenezo la Yehova kuweka sheria nyingi kuhusu makao yanayofaa kwa ajili ya washiriki wote wa kutaniko la ulimwenguni pote. Wakristo wanahimizwa watumie kanuni za Kimaandiko kuamua ikiwa wanaishi katika hali zinazokubalika machoni pa Mungu. Ni kanuni gani hizo?

Jambo tunalopaswa kufikiria kwanza ni watu tunaoishi nao watakuwa na uvutano gani juu yetu na juu ya hali yetu ya kiroho. Ni watu wa aina gani? Je, ni waabudu wa Yehova? Je, wanaishi kulingana na viwango vya Biblia? Mtume Paulo aliandika hivi: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Kor. 15:33.

Maandiko yanaeleza kwamba Yehova anashutumu uasherati na uzinzi. (Ebr. 13:4) Hivyo, mpango wowote wa kulala ambao unaruhusu watu wa jinsia tofauti ambao hawajafunga ndoa waishi pamoja kama mume na mke, bila shaka haukubaliwi na Mungu. Mkristo hangependa kuishi mahali ambapo maadili mapotovu yanakubaliwa.

Kwa kuongezea, Biblia inawahimiza wale wanaotamani kupata kibali cha Mungu ‘waukimbie uasherati.’ (1 Kor. 6:18) Kwa hiyo, ni jambo la hekima kwa Wakristo kuepuka mpango wowote wa kuishi ambao unaweza kufanya washawishiwe kushiriki katika mwenendo mpotovu. Kwa mfano, fikiria mahali ambapo Wakristo wengi wanalala katika nyumba moja. Je, mpango kama huo unaweza kutokeza vishawishi? Namna gani ikiwa watu wawili ambao si wenzi wa ndoa wanajikuta wakiwa peke yao kwa sababu watu wengine wanaoishi katika nyumba hiyo wameondoka? Vivyo hivyo, kungekuwa na hatari ya kutenda dhambi ikiwa watu wawili ambao ni waseja na walio na uhusiano wa kimapenzi wanaishi katika nyumba moja. Ni jambo la hekima kuepuka kuishi katika hali kama hiyo.

Pia, haingefaa kwa watu ambao wametalikiana kuendelea kuishi katika nyumba moja. Kwa sababu walizoea kuwa na uhusiano wa karibu, ni rahisi sana kwao kutumbukia katika mwenendo mpotovu kimaadili.—Met. 22:3.

Jambo lingine la maana la kufikiria ni jinsi majirani wanavyoona maamuzi ambayo mtu anafanya. Mipango ya mahali pa kuishi ambayo Mkristo anaona inafaa lakini inafanya majirani waseme maneno yasiyofaa si mizuri. Hatungependa kamwe mwenendo wetu uliletee suto jina la Yehova. Paulo alisema hivi: “Epukeni kuwa vikwazo kwa Wayahudi na vilevile kwa Wagiriki na kwa kutaniko la Mungu, kama vile mimi ninavyowapendeza watu wote katika mambo yote, bila kutafuta faida yangu mwenyewe bali ile ya walio wengi, ili wapate kuokolewa.”—1 Kor. 10:32, 33.

Inaweza kuwa vigumu kwa wale ambao wanataka kuishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Yehova kupata mahali pazuri pa kuishi. Hata hivyo, ni lazima Wakristo ‘waendelee kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.’ Wanapaswa kuhakikisha kwamba hakuna jambo lolote chafu linalofanywa katika nyumba zao. (Efe. 5:5, 10) Hivyo, Wakristo wanahitaji kusali ili wapate mwongozo kutoka kwa Mungu, kisha wafanye yote wanayoweza ili kulindana kimwili na kimaadili na pia kulilinda jina zuri la Yehova.