Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Roho na Bibi-arusi Huendelea Kusema: ‘Njoo!’”

“Roho na Bibi-arusi Huendelea Kusema: ‘Njoo!’”

“Roho na Bibi-arusi Huendelea Kusema: ‘Njoo!’”

“Roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’ . . . Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”—UFU. 22:17.

1, 2. Mambo ya Ufalme yanapaswa kuwa ya maana kadiri gani katika maisha yetu, na kwa nini?

MAMBO ya Ufalme yanapaswa kuwa ya maana kadiri gani katika maisha yetu? Yesu aliwahimiza wafuasi wake ‘waendelee kuutafuta kwanza ufalme,’ na akawahakikishia kwamba ikiwa wangefanya hivyo, Mungu angewapa vitu walivyohitaji. (Mt. 6:25-33) Alilinganisha Ufalme wa Mungu na lulu yenye thamani kubwa sana hivi kwamba mwanabiashara msafiri alipoipata, ‘aliuza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.’ (Mt. 13:45, 46) Je, hatupaswi kuiona kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi kuwa kazi ya maana sana?

2 Kama tulivyoona katika makala mbili zilizotangulia, tunapohubiri kwa ujasiri na kutumia Neno la Mungu kwa ustadi katika huduma tunaonyesha kwamba tunaongozwa na roho ya Mungu. Roho hiyo pia inatimiza sehemu ya maana katika kutuchochea kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Acheni tuone jinsi inavyotuchochea.

Watu Wote Wamealikwa!

3. Wanadamu wote wanaalikwa ‘waje’ wanywe maji ya aina gani?

3 Wanadamu wote wamealikwa kupitia roho takatifu. (Soma Ufunuo 22:17.) Wanaalikwa ‘waje’ kutosheleza kiu yao kwa kunywa maji ya pekee sana. Si maji ya kawaida yenye hidrojeni na oksijeni. Hata ingawa maji halisi ni ya maana ili kuendeleza uhai duniani, Yesu alikuwa akizungumza kuhusu maji tofauti alipomwambia hivi yule mwanamke Msamaria kwenye kisima: “Yule atakayekunywa maji ambayo nitampa hatapatwa na kiu hata kidogo, lakini maji ambayo nitampa yatakuwa chemchemi ya maji ndani yake, inayobubujika ili kutokeza uzima wa milele.” (Yoh. 4:14) Maji hayo yasiyo ya kawaida ambayo wanadamu wanaalikwa waje wanywe yanawapa uzima wa milele.

4. Uhitaji wa maji ya uzima ulitokea jinsi gani, na maji hayo yanawakilisha nini?

4 Uhitaji wa maji hayo ulitokea wakati mwanadamu wa kwanza, Adamu, alipojiunga na mke wake, Hawa, kumwasi Muumba wao, Yehova Mungu. (Mwa. 2:16, 17; 3:1-6) Wenzi hao wa kwanza walifukuzwa kutoka katika bustani walimokuwa wakiishi “ili [Adamu] asije akanyoosha mkono wake achukue matunda kutoka pia katika mti wa uzima na kula na kuishi mpaka wakati usio na kipimo.” (Mwa. 3:22) Kwa hiyo, Adamu akiwa baba ya wanadamu wote aliiletea jamii yote ya wanadamu kifo. (Rom. 5:12) Maji ya uzima yanawakilisha maandalizi yote ya Mungu ya kuwakomboa wanadamu watiifu kutoka katika dhambi na kifo na kuwapa uzima mkamilifu wa milele katika Paradiso duniani. Maandalizi hayo yalitolewa kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo.—Mt. 20:28; Yoh. 3:16; 1 Yoh. 4:9, 10.

5. Mwaliko wa ‘kuchukua maji ya uzima bure’ unatoka kwa nani? Eleza.

5 Ni nani aliye chanzo cha mwaliko huo wa ‘kuchukua maji ya uzima bure’? Maandalizi ya kupata uzima kupitia Yesu yatakuwa kama “mto wa maji ya uzima, mwangavu kama fuwele” wakati yatakapowanufaisha kikamili wanadamu wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Mto huo unaonekana “ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo.” (Ufu. 22:1) Kwa hiyo, Yehova ambaye ni Mpaji-Uhai, ndiye Chanzo cha maji hayo ya uzima. (Zab. 36:9) Yeye ndiye anayetoa maji hayo kupitia “Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo. (Yoh. 1:29) Yehova atatumia mto huo wa mfano kuondoa madhara yote ambayo yanawapata wanadamu kwa sababu ya kutotii kwa Adamu. Ndiyo, Yehova Mungu ndiye Chanzo cha mwaliko huo.

6. “Mto wa maji ya uzima” ulianza kutiririka wakati gani?

6 Ingawa “mto wa maji ya uzima” utatiririka kikamili zaidi wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, ulianza kutiririka “katika siku ya Bwana,” ambayo ilianza wakati “Mwana-Kondoo” alipowekwa kuwa mfalme mbinguni mwaka wa 1914. (Ufu. 1:10) Hivyo, maandalizi fulani ya uzima yalianza kupatikana baada ya wakati huo. Maandalizi ya uzima yanatia ndani Neno la Mungu, Biblia, kwa kuwa ujumbe wake unalinganishwa na “maji.” (Efe. 5:26) Watu wote wanaalikwa ili waje ‘wachukue maji ya uzima’ kwa kusikia na kutii habari njema ya Ufalme. Lakini ni nani anayetoa kihalisi mwaliko huo katika siku ya Bwana?

“Bibi-Arusi” Anasema, “Njoo!”

7. Ni nani waliotoa kwanza mwaliko huo katika “siku ya Bwana,” nao waliwaalika nani?

7 Washiriki wa jamii ya bibi-arusi, wale Wakristo watiwa-mafuta, ndio wanaotoa kwanza mwaliko huo. Wanawaalika nani? Bila shaka, bibi-arusi hajiambii “Njoo!” Anawaalika watu wanaotumaini kupata uzima wa milele duniani baada ya “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.”—Soma Ufunuo 16:14, 16.

8. Ni nini kinachoonyesha kwamba kuanzia mwaka wa 1918 Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa wakitoa mwaliko unaotoka kwa Yehova?

8 Wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo wamekuwa wakiwaalika watu kuanzia mwaka wa 1918. Mwaka huo, hotuba ya watu wote yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Huenda Wasife Kamwe” ilikazia tumaini la kwamba watu wengi watapata uzima katika paradiso duniani baada ya vita vya Har–Magedoni. Hotuba iliyotolewa kwenye kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia huko Cedar Point, Ohio, Marekani, katika mwaka wa 1922 iliwahimiza wasikilizaji ‘watangaze kuhusu Mfalme na ufalme wake.’ Himizo hilo liliwasaidia mabaki ya jamii ya bibi-arusi kuwatolea watu wengi zaidi mwaliko huo. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 1929 (15/3/1929) la Kiingereza, lilikuwa na makala yenye kichwa “Mwaliko Mchangamfu,” na andiko la msingi lilikuwa Ufunuo 22:17. Makala hiyo ilisema hivi kwa sehemu: “Jamii ya mabaki waaminifu inajiunga na [Aliye Juu Zaidi] katika kutoa mwaliko mchangamfu kwa kusema, ‘Njoo.’ Ujumbe huo unapaswa kutangazwa kwa watu wanaotamani uadilifu na kweli. Ni lazima utangazwe sasa.” Jamii ya bibi-arusi inaendelea kutoa mwaliko huo mpaka leo.

“Yeyote Anayesikia na Aseme: ‘Njoo!’”

9, 10. Wale wanaosikia mwaliko huo wamealikwa jinsi gani kusema pia, “Njoo!”?

9 Namna gani wale wanaosikia mwaliko huo? Wao pia wanaalikwa kusema, “Njoo!” Kwa mfano, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1932 (1/8/1932) la Kiingereza lilisema hivi kwenye ukurasa wa 232: “Watiwa-mafuta na wawahimize wote washiriki katika kuhubiri habari njema ya ufalme. Si lazima wale wanaotangaza ujumbe wa Bwana wawe watiwa-mafuta wa Bwana. Inatia moyo kama nini kwa Mashahidi wa Yehova kujua kwamba sasa wanaruhusiwa kupeleka maji ya uzima kwa jamii ya watu ambao wataokoka Har–Magedoni na kupata uzima wa milele duniani.”

10 Kuhusu daraka la msikilizaji la kusema “Njoo!” gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1934 la Kiingereza, lilisema hivi kwenye ukurasa wa 249: “Ni lazima washiriki wa jamii ya Yonadabu washirikiane na jamii ya Yehu wa mfano, yaani, watiwa-mafuta, katika kutangaza ujumbe wa ufalme, hata ingawa wao si mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta.” Katika mwaka wa 1935, utambulisho wa ule “umati mkubwa” unaotajwa kwenye Ufunuo 7:9-17 ulifunuliwa waziwazi. Hilo lilichochea sana kazi ya kuwatolea watu mwaliko wa Mungu. Kuanzia wakati huo, hesabu inayoongezeka ya umati mkubwa wa waabudu wa kweli, ambao sasa ni zaidi ya milioni saba, wamekubali mwaliko huo. Baada ya kusikiliza na kukubali ujumbe huo, wamejiweka wakfu kwa Mungu, wakabatizwa katika maji, na kujiunga na jamii ya bibi-arusi kuwaalika wengine kwa bidii ‘waje wanywe maji ya uzima bure.’

“Roho” Inasema, “Njoo!”

11. Katika karne ya kwanza W.K., roho takatifu ilihusika jinsi gani katika kazi ya kuhubiri?

11 Yesu alipokuwa akihubiri katika sinagogi huko Nazareti, alifungua kitabu cha kukunjwa cha nabii Isaya na kusoma hivi: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema, alinituma kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka na kupata kuona tena kwa vipofu, kuacha waliopondeka waende zao wakiwa wameachiliwa huru, kuhubiri mwaka wa Yehova wenye kukubalika.” Kisha, Yesu akasema jinsi maneno hayo yanavyomhusu: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa.” (Luka 4:17-21) Kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Katika karne ya kwanza, roho takatifu ilitimiza sehemu ya maana sana katika kazi ya kuhubiri.

12. Roho ya Mungu inahusika jinsi gani katika kuwaalika watu leo?

12 Roho takatifu ya Mungu inahusika jinsi gani katika kuwaalika wanadamu leo? Yehova ndiye Chanzo cha roho takatifu. Anatumia roho hiyo kufungua mioyo na akili za washiriki wa jamii ya bibi-arusi ili waelewe Neno lake, Biblia. Roho hiyo inawachochea kutoa mwaliko huo na kuwaeleza kweli za Kimaandiko wale ambao wanatumaini kuishi milele katika Paradiso duniani. Namna gani wale wanaokubali mwaliko huo na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo, kisha kuwaalika watu wengine? Roho inawasaidia pia. Kwa kuwa wamebatizwa ‘katika jina la roho takatifu,’ wanatenda kupatana na mwongozo wa roho hiyo nao wanaitegemea ili iwasaidie. (Mt. 28:19) Pia, fikiria ujumbe ambao unahubiriwa na watiwa-mafuta na hesabu inayoongezeka ya umati mkubwa. Ujumbe huo unatoka katika Biblia, kitabu ambacho kiliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Hivyo, mwaliko huo unatolewa kupitia roho takatifu. Kwa kweli, tunaongozwa na roho hiyo. Hilo linapaswa kutuchochea kushiriki kwa kadiri gani katika kazi ya kuwaalika watu?

Wao “Huendelea Kusema: ‘Njoo!’”

13. Maneno “roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’” yanaonyesha nini?

13 “Roho na bibi-arusi” hawasemi tu, “Njoo!” Kitenzi cha lugha ya awali ambacho kinatumiwa katika andiko hilo kinaonyesha tendo linaloendelea. Kwa hiyo, andiko hilo linasema hivi katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya: “Roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’” Hilo linaonyesha kwamba wanatoa mwaliko wa Mungu kwa ukawaida. Namna gani wale ambao wanasikia na kukubali mwaliko huo? Wao pia wanasema, “Njoo!” Biblia inasema kwamba umati mkubwa wa waabudu wa kweli ‘unatoa utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu la Yehova.’ (Ufu. 7:9, 15) Umati huo ‘unatoa utumishi mchana na usiku’ jinsi gani? (Soma Luka 2:36, 37; Matendo 20:31; 2 Wathesalonike 3:8.) Mfano wa nabii Ana aliyezeeka na mfano wa mtume Paulo unaonyesha kwamba kutoa ‘utumishi mchana na usiku’ kunamaanisha kuendelea kushiriki kwa bidii nyingi katika huduma.

14, 15. Danieli alionyesha jinsi gani umuhimu wa kuabudu kwa ukawaida?

14 Nabii Danieli pia alionyesha umuhimu wa kuabudu kwa ukawaida. (Soma Danieli 6:4-10, 16.) Hakubadili desturi yake ya kiroho, hata kwa mwezi mmoja, yaani, hakubadili mazoea yake ya kusali kwa Mungu “mara tatu kwa siku, . . . kama vile alivyokuwa akifanya kwa ukawaida,” hata ingawa angetupwa katika shimo la simba. Matendo yake yaliwaonyesha watazamaji waziwazi kwamba hakuna jambo ambalo ni la maana zaidi kuliko kumwabudu Yehova kwa ukawaida!—Mt. 5:16.

15 Baada ya Danieli kukaa usiku kucha katika shimo la simba, mfalme mwenyewe alienda huko na kupaaza sauti hivi: “Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je, Mungu wako unayemtumikia daima amekuokoa kutoka kwa hao simba?” Mara moja Danieli akajibu: “Ee mfalme, uishi mpaka wakati usio na kipimo. Mungu wangu mwenyewe alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba, nao hawakuniangamiza, kwa kuwa nimeonekana kuwa mtu asiye na hatia mbele zake; na pia mbele yako, Ee mfalme, mimi sijafanya tendo lolote lenye kudhuru.” Yehova alimbariki Danieli kwa sababu alimtumikia “daima.”—Dan. 6:19-22.

16. Mfano wa Danieli unapaswa kutuchochea kujiuliza maswali gani kuhusu huduma yetu?

16 Danieli alikuwa tayari kufa badala ya kuacha desturi yake ya kiroho. Namna gani sisi? Tunajidhabihu jinsi gani au tuko tayari kujidhabihu kwa kadiri gani ili kutangaza kwa ukawaida habari njema ya Ufalme wa Mungu? Hatupaswi kamwe kuruhusu mwezi upite bila kuzungumza na wengine kumhusu Yehova! Je, hatupaswi kujitahidi kushiriki katika huduma kila juma ikiwezekana? Hata ikiwa tuna udhaifu mkubwa wa kimwili na tunaweza kuhubiri kwa dakika 15 tu kwa mwezi, tunapaswa kuripoti utumishi huo. Kwa nini? Kwa sababu tunatamani kuendelea kusema “Njoo!” pamoja na roho na bibi-arusi. Bila shaka, tunataka kufanya yote tunayoweza ili kuendelea kuwa wahubiri wa kawaida wa Ufalme.

17. Tunapaswa kutumia nafasi gani kutoa mwaliko kutoka kwa Yehova?

17 Tunapaswa kujitahidi kutoa mwaliko wa Yehova katika kila nafasi tunayopata, si wakati tu ambao tumetenga kuhubiri. Ni pendeleo kubwa kama nini kuwaalika watu wenye kiu ‘waje wachukue maji ya uzima bure’ katika nyakati mbalimbali, kama vile wakati tunaponunua vitu, tunaposafiri, tunapokuwa likizoni, tunapofanya kazi, au tunapoenda shuleni! Hata wenye mamlaka wakizuia kazi ya kuhubiri, tunaendelea kuhubiri kwa busara, labda kwa kuhubiri nyumba chache tu katika eneo fulani na kwenda eneo lingine au kwa kuhubiri zaidi kwa njia isiyo rasmi.

Endelea Kusema, “Njoo!”

18, 19. Unaonyesha jinsi gani kwamba unathamini pendeleo la kuwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu?

18 Kwa miaka zaidi ya 90 sasa, roho na bibi-arusi wamekuwa wakimwambia, “Njoo!” mtu yeyote aliye na kiu ya maji ya uzima. Je, umesikia mwaliko wao wenye kusisimua? Basi, unahimizwa uwaalike watu wengine.

19 Hatujui mwaliko huo wa upendo kutoka kwa Yehova utatolewa mpaka wakati gani, lakini tunapokubali mwaliko huo kwa kusema, “Njoo!” tunakuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu. (1 Kor. 3:6, 9) Hilo ni pendeleo kubwa kama nini! Acheni tuonyeshe kwamba tunathamini pendeleo hilo na ‘kumtolea Mungu sikuzote dhabihu ya sifa’ kwa kuhubiri kwa ukawaida. (Ebr. 13:15) Sisi ambao tuna tumaini la kuishi duniani na tujiunge na jamii ya bibi-arusi katika kuendelea kusema, “Njoo!” Na acheni watu wengi zaidi ‘wachukue maji ya uzima bure’!

Umejifunza Nini?

• Ni nani wanaoalikwa kwa kuambiwa “njoo”?

• Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ndiye chanzo cha mwaliko huo?

• Roho takatifu inatimiza sehemu gani katika kutoa mwaliko huo?

• Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuwa wa kawaida katika huduma?

[Maswali ya Funzo]

[Chati/Picha katika ukurasa wa 16]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Endelea Kusema, “Njoo!”

1914

Wahubiri 5,100

1918

Watu wengi watapata uzima katika Paradiso duniani

1922

“Tangazeni, tangazeni, tangazeni Mfalme na ufalme wake”

1929

Mabaki waaminifu wanasema, “Njoo!”

1934

Jamii ya Yonadabu yaalikwa kuhubiri

1932

Mwaliko wa kusema “Njoo!” unatolewa pia kwa watu ambao si watiwa-mafuta

1935

“Umati mkubwa” unatambulishwa

2009

Wahubiri 7,313,173