Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri’

‘Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri’

‘Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri’

“Wakajazwa roho takatifu na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri.”—MDO. 4:31.

1, 2. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuhubiri na kufundisha kwa ustadi?

SIKU tatu kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Kabla ya kupanda kwenda mbinguni, Yesu aliyefufuliwa aliwatuma wafuasi wake ‘wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo alikuwa amewaamuru.’ Aliwaahidi kwamba angekuwa pamoja nao “siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 24:14; 26:1, 2; 28:19, 20.

2 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunashiriki kwa bidii katika kazi ambayo ilianza katika karne ya kwanza. Hakuna kazi yoyote ambayo ni ya maana kuliko kazi yetu inayookoa uhai ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. Basi, ni jambo la maana kama nini kwetu kuhubiri na kufundisha kwa ustadi! Katika habari hii, tutaona jinsi kuongozwa na roho takatifu kunavyotusaidia kusema kwa ujasiri katika huduma. Makala mbili zinazofuata zitaonyesha jinsi roho ya Yehova inavyoweza kutusaidia kufundisha kwa ustadi na kuendelea kuhubiri.

Tunahitaji Ujasiri

3. Kwa nini tunahitaji ujasiri ili kuhubiri kuhusu Ufalme?

3 Mungu ametupatia pendeleo lisilo na kifani la kutangaza kuhusu Ufalme. Hata hivyo, nyakati nyingine kazi hiyo si rahisi. Ingawa watu fulani wanakubali habari njema ya Ufalme wa Mungu, wengi wanatenda kama watu walioishi katika siku za Noa. Yesu alisema hivi: “Hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” (Mt. 24:38, 39) Kisha, kuna wale wanaotudhihaki au kutupinga. (2 Pet. 3:3) Huenda tukapingwa na wenye mamlaka, wanafunzi au wafanyakazi wenzetu, au hata washiriki wa karibu wa familia yetu. Kwa kuongezea, kila mtu ana udhaifu wake, kama vile kuona haya na kuogopa kukataliwa na wengine. Kuna mambo mengi ambayo yanaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuwa na “uhuru wa kusema” na hivyo kutuzuia kusema neno la Mungu kwa “ujasiri.” (Efe. 6:19, 20) Tunahitaji ujasiri ili kuendelea kusema neno la Mungu. Ni nini kinachoweza kutusaidia kupata ujasiri?

4. (a) Ujasiri ni nini? (b) Mtume Paulo alijipa jinsi gani ujasiri wa kuwahubiria Wathesalonike?

4 Neno la Kigiriki ambalo linatafsiriwa kuwa “ujasiri” linamaanisha “kusema waziwazi, kwa unyoofu, na bila kuficha.” Neno hilo linamaanisha pia “ushujaa, uhakika, . . . hali ya kutoogopa.” Kuwa jasiri hakumaanishi kuongea bila kujali au kwa ujeuri. (Kol. 4:6) Ingawa tunahitaji kuwa wajasiri, tunapaswa pia kufanya amani na watu wote. (Rom. 12:18) Pia, tunapohubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, tunahitaji kuwa na usawaziko katika kuonyesha ujasiri na busara ili tusimkasirishe mtu yeyote bila kukusudia. Bila shaka, ili tuwe na ujasiri unaofaa ni lazima tusitawishe sifa nyingine ambazo zinahitaji jitihada nyingi. Hata hivyo, hatuwezi kusitawisha ujasiri wa aina hiyo kwa kutegemea uwezo au nguvu zetu wenyewe. Baada ya mtume Paulo na waandamani wake ‘kutendewa kwa dharau katika Filipi,’ ‘walijipa ujasiri’ jinsi gani ili kuwahubiria Wathesalonike? “Kwa njia ya Mungu wetu,” akaandika Paulo. (Soma 1 Wathesalonike 2:2.) Yehova Mungu anaweza kuondoa woga wetu na kutuwezesha kuwa na ujasiri kama huo.

5. Yehova aliwapa jinsi gani ujasiri Petro, Yohana, na wanafunzi wengine?

5 Mtume Petro na mtume Yohana walipoamuriwa waache kuhubiri na “watawala [wa watu] na wanaume wazee na waandishi,” walisema hivi: “Kama ni jambo la uadilifu mbele za macho ya Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” Badala ya kusali ili Mungu akomeshe mateso, mitume hao pamoja na waamini wenzao waliomba hivi: “Yehova, viangalie vitisho vyao, na kuwawezesha watumwa wako kuendelea kusema neno lako kwa ujasiri wote.” (Mdo. 4:5, 19, 20, 29) Yehova alijibu namna gani ombi lao? (Soma Matendo 4:31.) Yehova aliwasaidia kuwa na ujasiri kupitia roho yake. Roho ya Mungu inaweza kutusaidia vivyo hivyo leo. Basi, tunaweza kupata jinsi gani roho ya Mungu na kuongozwa nayo katika huduma yetu?

Jinsi ya Kupata Ujasiri

6, 7. Ni njia gani ya moja kwa moja ya kupata roho takatifu ya Mungu? Toa mifano.

6 Njia ya moja kwa moja ya kupata roho takatifu ya Mungu ni kumwomba akupe roho hiyo. Yesu aliwaambia hivi watu waliomsikiliza: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Kwa kweli, tunapaswa kusali sikuzote ili tupate roho takatifu. Ikiwa tunaogopa kuhubiri barabarani, kwa njia isiyo rasmi, au katika maeneo ya kibiashara, tunaweza kumwomba Yehova atupatie roho yake ili itusaidie kupata ujasiri.—1 The. 5:17.

7 Hivyo ndivyo alivyofanya mwanamke Mkristo anayeitwa Rosa. * Siku moja Rosa alipokuwa kazini, mwalimu mwenzake alikuwa akisoma ripoti iliyoonyesha jinsi watoto walivyokuwa wakiteswa katika shule nyingine. Mwalimu huyo alifadhaishwa sana na mambo aliyosoma akasema hivi kwa sauti, “Ulimwengu unaelekea wapi?” Rosa hakupoteza nafasi hiyo ya kutoa ushahidi. Alifanya nini ili apate ujasiri wa kuanzisha mazungumzo? Rosa anasema hivi: “Nilisali kwa Yehova na kuomba roho yake inisaidie.” Alitoa ushahidi mzuri, kisha akapanga kumrudia mwalimu huyo. Mfikirie pia msichana mwenye umri wa miaka mitano anayeitwa Milane, ambaye anaishi New York City. Milane anasema hivi: “Kila siku kabla ya kwenda shuleni, mimi na mama yangu tunasali kwa Yehova.” Wanasali kuhusu nini? Wanasali ili Milane awe na ujasiri wa kusimama imara na kusema waziwazi kuhusu Mungu wake! Mama yake anasema: “Kufanya hivyo kumemsaidia Milane kueleza msimamo wake kuhusu sikukuu za kuzaliwa na sikukuu nyingine na pia kutoshiriki katika sherehe hizo.” Je, mifano hiyo haionyeshi kwamba sala inaweza kutusaidia kupata ujasiri?

8. Tunajifunza nini kutokana na nabii Yeremia kuhusu kupata ujasiri?

8 Fikiria pia jambo lililomsaidia nabii Yeremia kupata ujasiri. Yehova alipomweka rasmi awe nabii kwa mataifa, Yeremia alisema hivi: “Tazama, mimi hakika sijui jinsi ya kusema, kwa sababu mimi ni mvulana tu.” (Yer. 1:4-6) Hata hivyo, baada ya muda, Yeremia alihubiri kwa bidii na kwa ujasiri sana hivi kwamba wengi walimwona kuwa mtangazaji wa msiba. (Yer. 38:4) Kwa miaka zaidi ya 65, alitangaza kwa ujasiri hukumu za Yehova. Alijulikana sana katika Israeli kwa sababu ya kuhubiri kwa ujasiri na bila woga hivi kwamba Yesu alipozungumza kwa ujasiri miaka 600 hivi baadaye, watu fulani waliamini kwamba Yesu ni Yeremia aliyefufuka. (Mt. 16:13, 14) Nabii Yeremia ambaye alisitasita mwanzoni alishinda jinsi gani woga aliokuwa nao? Anasema hivi: ‘Moyoni mwangu [neno la Mungu] likawa kama moto unaowaka ambao umefungiwa ndani ya mifupa yangu; nami nikachoka kujizuia.’ (Yer. 20:9) Ndiyo, neno la Yehova lilimtia nguvu Yeremia na kumchochea kusema.

9. Kwa nini neno la Mungu linaweza kutuchochea kama lilivyomchochea Yeremia?

9 Mtume Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Waebrania: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Ujumbe wa Mungu au neno lake linaweza kutuchochea jinsi lilivyomchochea Yeremia. Kumbuka kwamba ingawa wanadamu ndio waliotumiwa kuandika Biblia, si kitabu chenye hekima ya wanadamu, kwa kuwa kiliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Tunasoma hivi kwenye 2 Petro 1:21: “Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” Tunapotenga wakati ili kujifunza Biblia kwa undani, akili zetu zinajaa ujumbe ulioongozwa na roho takatifu. (Soma 1 Wakorintho 2:10.) Ujumbe huo unaweza kuwa “kama moto unaowaka” ndani yetu, hivi kwamba hatutaweza kujizuia kuutangaza.

10, 11. (a) Tunapaswa kujifunza Biblia kwa njia gani ikiwa tunataka kupata ujasiri wa kusema? (b) Taja hatua moja ambayo unapanga kuchukua ili kuboresha funzo lako la kibinafsi.

10 Ili tufaidike kabisa na funzo letu la Biblia, tunapaswa kujifunza na kuruhusu ujumbe wa Biblia upenye ndani kabisa ya moyo wetu na kubadili utu wetu wa ndani. Kwa mfano, nabii Ezekieli aliambiwa katika maono ale kitabu cha kukunjwa chenye ujumbe mkali ili awatangazie watu ambao hawakumsikiliza. Ezekieli alipaswa kuelewa kabisa ujumbe huo na kuishi kulingana nao. Ikiwa Ezekieli angefanya hivyo, kazi ya kutangaza ujumbe huo ingependeza na ingekuwa tamu kama asali.—Soma Ezekieli 2:8–3:4, 7-9.

11 Hali yetu ni kama ya Ezekieli. Leo, watu wengi hawataki kusikiliza ujumbe wa Biblia. Ili tuendelee kusema neno la Mungu bila kuacha, ni jambo la maana tujifunze Maandiko kwa njia inayotuwezesha kuelewa na kuamini kabisa ujumbe huo. Tunapaswa kujifunza kwa ukawaida bila kukosa. Tunapaswa kuwa na tamaa kama ya mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova Mwamba wangu na Mkombozi wangu.” (Zab. 19:14) Ni jambo la maana sana kutenga wakati wa kutafakari kuhusu mambo tunayosoma, ili kweli za Biblia zipenye ndani kabisa ya moyo wetu! Bila shaka, tunapaswa kujitahidi kuboresha funzo letu la kibinafsi. *

12. Kwa nini mikutano ya Kikristo inatusaidia kuongozwa na roho takatifu?

12 Njia nyingine ya kufaidika kutokana na roho takatifu ya Yehova ni ‘kufikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe.’ (Ebr. 10:24, 25) Kujitahidi kabisa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, kusikiliza kwa makini, na kutumia yale tunayojifunza ni njia bora za kuongozwa na roho. Kwa kweli, roho ya Yehova inatuongoza kupitia kutaniko.—Soma Ufunuo 3:6.

Faida za Kuwa Jasiri

13. Tunajifunza nini kutokana na yale ambayo Wakristo wa karne ya kwanza walitimiza katika kazi ya kuhubiri?

13 Roho takatifu ndiyo nguvu isiyo na kifani katika ulimwengu wote, na inaweza kuwapa wanadamu nguvu za kufanya mapenzi ya Yehova. Wakristo wa karne ya kwanza waliongozwa na roho takatifu kutimiza kazi kubwa ya kuhubiri. Walihubiri habari njema “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Tunapokumbuka kwamba wengi wao walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu,” tunaona wazi kwamba walichochewa na nguvu zisizo za kawaida.—Mdo. 4:13.

14. Ni nini kinachoweza kutusaidia ‘kuwaka roho’?

14 Kuishi kwa njia inayoruhusu roho takatifu iongoze maisha yetu kunaweza pia kutuchochea kutimiza huduma yetu kwa ujasiri. Kusali kwa ukawaida ili tupewe roho takatifu, kujifunza kibinafsi kwa bidii, kusali na kutafakari juu ya mambo tunayosoma, na kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo, kunaweza kutufaidi na kutusaidia ‘kuwaka roho.’ (Rom. 12:11) Kuhusu ‘Myahudi fulani anayeitwa Apolo, mzaliwa wa Aleksandria, mwanamume mfasaha, [ambaye] alifika Efeso,’ Biblia inasema hivi: “Kwa kuwa alikuwa amewaka roho, akaanza kusema na kuyafundisha kwa usahihi mambo juu ya Yesu.” (Mdo. 18:24, 25) ‘Tukiwaka moto kwa Roho,’ tunaweza kuwa na ujasiri zaidi tunapohubiri nyumba kwa nyumba na kwa njia isiyo rasmi.—Rom. 12:11, The Bible—An American Translation.

15. Tunafaidika jinsi gani tunapohubiri kwa ujasiri zaidi?

15 Tunafaidika tunapohubiri kwa ujasiri zaidi. Mtazamo wetu unakuwa bora zaidi kwa sababu tunaelewa vizuri zaidi umuhimu na faida ya kazi yetu. Furaha yetu inaongezeka kwa sababu tunapata shangwe zaidi tunapohubiri kwa ustadi. Na tunachochewa kuwa na bidii zaidi kwa sababu tunatambua uharaka wa kazi yetu ya kuhubiri.

16. Tunapaswa kufanya nini ikiwa bidii yetu katika huduma imepungua?

16 Namna gani ikiwa bidii au shauku yetu katika kazi ya kuhubiri imepungua? Basi, tunapaswa kujichunguza kwa unyoofu. Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Kor. 13:5) Jiulize hivi: ‘Je, bado ninawaka roho? Je, ninasali ili Yehova anipe roho yake? Je, sala zangu zinaonyesha kwamba ninamtegemea ninapofanya mapenzi yake? Je, ninamshukuru kwa sababu ya huduma ambayo ametukabidhi? Nina mazoea gani ya kujifunza kibinafsi? Ninatumia muda mwingi kadiri gani kutafakari yale ninayosoma na kusikia? Ninashiriki kwa kadiri gani katika mikutano ya kutaniko?’ Kutafakari maswali hayo kunaweza kukusaidia kutambua udhaifu wako na kufanya marekebisho.

Acha Roho ya Mungu Ikupe Ujasiri

17, 18. (a) Kazi ya kuhubiri inafanywa kwa kadiri gani leo? (b) Tunaweza jinsi gani kuwa na “uhuru wa kusema ulio mkubwa zaidi” tunapotangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu?

17 Yesu aliyefufuliwa aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kazi ya kuhubiri iliyoanza wakati huo, inafanywa kwa kiwango kikubwa zaidi leo. Mashahidi wa Yehova karibu milioni saba wanatangaza ujumbe wa Ufalme katika nchi zaidi ya 230, wakitumia saa bilioni 1.5 hivi kwa mwaka katika huduma. Inasisimua kama nini kushiriki kwa bidii katika kazi hiyo ambayo haitarudiwa kamwe!

18 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote inaongozwa na roho ya Mungu. Tukifuata mwongozo wa roho, tutakuwa na “uhuru wa kusema ulio mkubwa zaidi” katika huduma yetu. (Mdo. 28:31) Basi, na tuazimie kuongozwa na roho tunapotangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Ili ufaidike kabisa na usomaji wa Biblia na funzo lako la kibinafsi, ona kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, sura yenye kichwa “Jitahidi Uwe Msomaji Mzuri” na “Funzo Lina Faida,” ukurasa wa 21-32.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini tunahitaji kusema neno la Mungu kwa ujasiri?

• Ni nini kilichowasaidia wanafunzi wa mapema kuhubiri kwa ujasiri?

• Tunaweza jinsi gani kupata ujasiri?

• Tunafaidika jinsi gani tukiwa na ujasiri?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wazazi wanaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wao wawe na ujasiri?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Sala fupi inaweza kukusaidia kupata ujasiri katika huduma