Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia kwa Ustadi “Upanga wa Roho”

Tumia kwa Ustadi “Upanga wa Roho”

Tumia kwa Ustadi “Upanga wa Roho”

‘Upokeeni upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.’—EFE. 6:17.

1, 2. Tunapaswa kufanya nini kwa sababu ya uhitaji mkubwa wa watangazaji zaidi wa Ufalme?

BAADA ya kuona kwamba umati ulikuwa na uhitaji wa kiroho, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” Yesu hakuachia hapo. Baada ya kusema maneno hayo, ‘aliwaita wanafunzi wake kumi na wawili’ akawatuma kuhubiri, au ‘kuvuna.’ (Mt. 9:35-38; 10:1, 5) Baadaye, Yesu “akachagua wengine 70 na kuwatuma wawili-wawili” kufanya kazi hiyo.—Luka 10:1, 2.

2 Leo pia, kuna uhitaji mkubwa wa watangazaji zaidi wa Ufalme. Watu waliohudhuria Ukumbusho mwaka wa utumishi wa 2009 walikuwa 18,168,323. Idadi hiyo ilizidi idadi ya Mashahidi wa Yehova kwa watu zaidi ya milioni 10. Kwa kweli, mashamba ni meupe na yako tayari kuvunwa. (Yoh. 4:34, 35) Kwa hiyo, tunapaswa kusali na kuomba tupate wafanyakazi zaidi. Lakini tunaweza kutenda jinsi gani kupatana na maombi hayo? Kwa kusitawisha ustadi zaidi katika kazi ya kuhubiri kwa bidii kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20; Marko 13:10.

3. Roho ya Mungu inatusaidia jinsi gani kuwa wahubiri wenye ustadi zaidi?

3 Habari iliyotangulia ilizungumzia jinsi roho ya Mungu inavyotusaidia ‘kusema neno la Mungu kwa ujasiri.’ (Mdo. 4:31) Roho hiyo inaweza pia kutusaidia kuhubiri na kufundisha kwa ustadi. Njia moja ya kuboresha ustadi wetu katika huduma ni kutumia vizuri kifaa bora ambacho Yehova Mungu ametupatia, yaani, Neno lake lililoandikwa, Biblia. Iliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu. (2 Tim. 3:16) Ujumbe wake uliongozwa na roho ya Mungu. Kwa hiyo, tunapofundisha kweli za Kimaandiko kwa ustadi katika huduma yetu, tunaongozwa na roho takatifu. Kabla ya kuzungumzia jinsi tunavyoweza kufanya hivyo, acheni tuone jinsi Neno hilo lilivyo na nguvu.

‘Neno la Mungu Lina Nguvu’

4. Ujumbe wa Biblia unaweza kumchochea mtu afanye mabadiliko gani?

4 Ujumbe, au neno la Mungu lina nguvu nyingi sana! (Ebr. 4:12) Ujumbe wa Biblia una makali zaidi kuliko upanga wowote wa wanadamu, kwa sababu kwa njia ya mfano unachoma kufikia kugawanya mifupa na urojorojo wake. Kweli ya Kimaandiko inaingia ndani kabisa ya mtu na kupenya mawazo na hisia zake, na hivyo kufunua jinsi alivyo kikweli kwa ndani. Kweli hiyo ina nguvu za kugeuza ambazo zinaweza kumchochea mtu abadilike kikweli. (Soma Wakolosai 3:10.) Ndiyo, Neno la Mungu linaweza kubadili maisha ya watu!

5. Biblia inaweza kutuongoza katika njia gani, na matokeo yatakuwa nini?

5 Kwa kuongezea, Biblia ni kitabu chenye hekima isiyo na kifani. Ina habari za maana sana ambazo zinaweza kuwafundisha watu jinsi ya kuishi katika ulimwengu huu wenye matatizo mengi. Neno la Mungu halimuliki hatua zetu tu, bali pia barabara iliyo mbele yetu. (Zab. 119:105) Linatusaidia sana kukabiliana na matatizo au kuchagua marafiki, burudani, kazi, mavazi, na mambo mengine. (Zab. 37:25; Met. 13:20; Yoh. 15:14; 1 Tim. 2:9) Kufuata kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu kunatuwezesha kukaa na wengine kwa amani. (Mt. 7:12; Flp. 2:3, 4) Ikiwa barabara tunayotembea imemulikwa vizuri, tunaweza kutambua matokeo ya maamuzi yetu. (1 Tim. 6:9) Maandiko yanatabiri pia kuhusu kusudi la Mungu la wakati ujao, yakitusaidia kuishi kupatana na kusudi hilo. (Mt. 6:33; 1 Yoh. 2:17, 18) Mtu anaweza kuwa na maisha yenye kusudi kama nini akiruhusu kanuni za Mungu ziongoze maisha yake!

6. Biblia ni silaha yenye nguvu nyingi kadiri gani katika vita vyetu vya kiroho?

6 Pia, fikiria jinsi Biblia ilivyo silaha yenye nguvu katika vita vyetu vya kiroho. Paulo aliliita Neno la Mungu “upanga wa roho.” (Soma Waefeso 6:12, 17.) Ujumbe wa Biblia unapotolewa kwa ustadi, unaweza kuwaweka watu huru kutoka katika utumwa wa kiroho wa Shetani. Ni upanga ambao unaokoa uhai badala ya kuwaangamiza watu. Tunapaswa kuutumia kwa ustadi, sivyo?

Litumie Neno la Mungu Sawasawa

7. Kwa nini ni jambo la maana kujifunza kutumia vizuri “upanga wa roho”?

7 Askari-jeshi anaweza kutumia silaha zake kwa ustadi ikiwa tu amefanya mazoezi na amejifunza kuzitumia vizuri. Ndivyo ilivyo na kutumia “upanga wa roho” katika vita vyetu vya kiroho. Paulo aliandika hivi: “Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, ukilitumia sawasawa neno la kweli.”—2 Tim. 2:15.

8, 9. Ni nini kitakachotusaidia kuelewa Biblia? Toa mfano.

8 Ni nini kitakachotusaidia ‘kulitumia sawasawa neno la kweli’ katika huduma yetu? Kabla ya kuwasaidia wengine waelewe vizuri mafundisho ya Biblia, sisi wenyewe tunahitaji kuyaelewa vizuri. Kwa hiyo, ni lazima tuchunguze muktadha wa andiko au mistari fulani. Kamusi moja inasema kwamba “muktadha wa neno, sentensi, au andiko ni maneno, sentensi mbalimbali, au maandishi yanayotangulia na yale yanayofuata neno hilo, andiko au sentensi hiyo, ambayo yanatusaidia kuelewa waziwazi maana yake.”

9 Ili kuelewa Andiko fulani kwa usahihi tunahitaji kuchunguza mistari inayozunguka andiko hilo. Kwa mfano, tunahitaji kuchunguza muktadha ili kuelewa maneno ya Paulo kwenye Wagalatia 5:13. Aliandika hivi: “Bila shaka, ninyi mliitiwa uhuru, akina ndugu; ila msiutumie uhuru huu kuuchochea mwili, bali kupitia upendo mtumikiane.” Katika andiko hilo, Paulo alikuwa akizungumza kuhusu uhuru gani? Je, ni uhuru kutoka katika dhambi na kifo, uhuru kutoka katika dini ya uwongo, au uhuru wa aina nyingine? Mistari inayozunguka mstari huo inaonyesha kwamba Paulo alikuwa akizungumza kuhusu ‘kuachiliwa huru kutoka katika laana ya Sheria.’ (Gal. 3:13, 19-24; 4:1-5) Alikuwa akizungumza kuhusu uhuru wa Kikristo. Watu waliothamini uhuru huo walitumikiana kwa upendo. Wale ambao hawakuwa na upendo waligombana na kuwasengenya wengine.—Gal. 5:15.

10. Ili kuelewa maana ya Maandiko kwa usahihi, tunapaswa kuchunguza habari gani, na tunaweza kuzipata jinsi gani?

10 Neno “muktadha” lina maana nyingine. Linamaanisha pia ‘mazingira au hali ambamo tukio au jambo linatendeka.’ Ili kuelewa maana ya andiko kwa usahihi, tunapaswa kuchunguza mazingira ya masimulizi hayo, kwa mfano, ni nani aliyeandika kitabu hicho cha Biblia na kiliandikwa wakati gani, na katika hali gani? Ni jambo la maana pia kujua kitabu hicho kiliandikwa kwa sababu gani na ikiwezekana, hali za kijamii, kimaadili, na mazoea ya kidini yaliyokuwapo wakati kilipoandikwa. *

11. Tunapaswa kuwa waangalifu kutofanya nini tunapoeleza maana ya maandiko?

11 ‘Kulitumia sawasawa neno la kweli’ kunatia ndani mengi zaidi ya kueleza tu kwa usahihi kweli za Kimaandiko. Tunapaswa kuwa waangalifu ili tusitumie Biblia kuwatisha watu. Ingawa tunaweza kuyatumia Maandiko kuitetea kweli kama Yesu alivyofanya aliposhawishiwa na Ibilisi, hatupaswi kuitumia Biblia kama fimbo ya kuwaogopesha wasikilizaji. (Kum. 6:16; 8:3; 10:20; Mt. 4:4, 7, 10) Tunapaswa kutii shauri hili la mtume Petro: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwenu sababu ya tumaini lililo ndani yenu, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.”—1 Pet. 3:15.

12, 13. Kweli ya Neno la Mungu inaweza kupindua ‘ngome gani zenye nguvu’? Toa mfano.

12 Kweli ya Neno la Mungu inaweza kuwa na matokeo gani ikitumiwa sawasawa? (Soma 2 Wakorintho 10:4, 5.) Kweli ya Kimaandiko inaweza kupindua “ngome zenye nguvu,” yaani, inaweza kufunua mafundisho ya uwongo, mazoea yenye kudhuru, na falsafa ambazo zinategemea hekima ya wanadamu wasio wakamilifu. Tunaweza kuitumia Biblia kung’oa mawazo yoyote ambayo ‘yameinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu.’ Mafundisho ya Biblia yanaweza kutumiwa kuwasaidia wengine ili wapatanishe mawazo yao na kweli.

13 Kwa mfano, mfikirie mwanamke fulani mwenye umri wa miaka 93 anayeishi huko India. Tangu alipokuwa mtoto, alifundishwa kuamini kwamba wafu wanazaliwa katika mwili mwingine. Mwana wake anayeishi katika nchi nyingine alipoanza kumfundisha Biblia kupitia barua, mwanamke huyo alithamini sana mambo aliyokuwa akijifunza kumhusu Yehova na ahadi zake. Hata hivyo, fundisho la wafu kuzaliwa katika mwili mwingine lilikuwa limetia mizizi kabisa katika akili yake hivi kwamba alilalamika wakati mwana wake alipomwandikia kuhusu hali ya wafu. Alisema hivi: “Sielewi hata kidogo ukweli wa Maandiko hayo. Dini zote zinafundisha kwamba kuna kitu fulani ndani yetu ambacho hakiwezi kufa. Nimekuwa nikiamini kwamba mwili unakufa na sehemu fulani isiyoonekana inazaliwa tena na tena katika miili mingine mara zaidi ya 8,400,000. Sidhani kwamba huo ni uwongo! Unamaanisha kwamba dini nyingi zimekosea?” Je, “upanga wa roho” unaweza kupindua fundisho kama hilo ambalo limetia mizizi? Baada ya mazungumzo zaidi ya Kimaandiko kuhusu habari hiyo, mwanamke huyo aliandika hivi baada ya majuma machache: “Sasa nimeanza kuelewa ukweli kuhusu kifo. Ninafurahi sana kujua kwamba wakati wa ufufuo, tutakutana tena na wapendwa wetu waliokufa. Ninatumaini kwamba Ufalme wa Mungu utakuja hivi karibuni.”

Litumie Neno la Mungu kwa Ushawishi

14. Kuwashawishi wasikilizaji kunamaanisha nini?

14 Kutumia Biblia kwa ustadi katika huduma hakumaanishi kunukuu tu maandiko. Paulo alizungumza kwa “ushawishi,” na tunapaswa pia kufanya hivyo. (Soma Matendo 19:8, 9; 28:23.) Neno “shawishi” linamaanisha “sadikisha.” Yule anayeshawishiwa “anasadikishwa kabisa mpaka aamini jambo fulani.” Tunapomshawishi mtu akubali fundisho la Biblia, tunamsadikisha ili aamini fundisho hilo. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kumsadikisha msikilizaji kwamba tunasema kweli. Tunaweza kufanya hivyo kwa njia zifuatazo.

15. Unaweza kuelekeza uangalifu kwenye Biblia jinsi gani ili iheshimiwe?

15 Elekeza uangalifu kwenye Neno la Mungu kwa njia inayofanya liheshimiwe. Kabla ya kusoma andiko, kazia kwa nini ni jambo la maana kujua maoni ya Mungu kuhusu jambo mnalozungumzia. Baada ya kuuliza swali na mwenye-nyumba kujibu, unaweza kusema hivi: ‘Acha tuone maoni ya Mungu kuhusu jambo hili.’ Au unaweza kuuliza, ‘Mungu anasema nini kuhusu jambo hili?’ Unaposema hivyo kabla ya kusoma andiko unakazia kwamba Biblia iliongozwa na Mungu na hivyo unamfanya msikilizaji aiheshimu sana. Ni jambo la maana kufanya hivyo hasa tunapomhubiria mtu ambaye anamwamini Mungu lakini hajui Biblia inafundisha nini.—Zab. 19:7-10.

16. Ni nini kitakachokusaidia kueleza maana ya maandiko kwa njia inayofaa?

16 Usisome tu maandiko; eleza maana yake. Paulo alikuwa na desturi ya ‘kueleza na kuthibitisha kwa marejeo’ mambo aliyofundisha. (Mdo. 17:3) Kwa kawaida, andiko la Biblia lina masomo mbalimbali, na hivyo, huenda ukahitaji kukazia maneno makuu ambayo yanahusiana na jambo mnalozungumzia. Unaweza kufanya hivyo kwa kurudia maneno yanayokazia wazo kuu au unaweza kuuliza maswali ambayo yatamsaidia mwenye-nyumba kuyatambua. Kisha, eleza maana ya sehemu hiyo ya andiko. Baada ya kufanya hivyo, msaidie msikilizaji aone jinsi andiko hilo linavyomhusu yeye binafsi.

17. Unaweza kutumia Maandiko jinsi gani kujadiliana kwa njia yenye kusadikisha?

17 Tumia Maandiko kujadiliana kwa njia yenye kusadikisha. Paulo ‘alijadiliana na wengine kwa kutumia Maandiko’ huku akitumia hoja zenye kusadikisha na kuwasihi kutoka moyoni. (Mdo. 17:2, 4) Jitahidi kugusa moyo wa mtu anayekusikiliza kama Paulo alivyofanya. ‘Teka’ mambo yaliyo moyoni mwake kwa kutumia maswali yenye fadhili ambayo yanaonyesha kwamba unamjali kikweli mtu huyo. (Met. 20:5) Usizungumze bila kujali. Toa hoja zako kwa njia iliyo wazi na yenye kueleweka. Unapaswa kutegemeza hoja hizo kwa uthibitisho wenye kuridhisha. Mambo unayosema yanapaswa kutegemea kabisa Neno la Mungu. Ni afadhali kufafanua vizuri andiko moja na kutumia mfano kuonyesha matumizi yake, badala ya kusoma maandiko mawili au matatu haraka-haraka. Kutumia uthibitisho wa ziada kunaweza pia ‘kuongeza ushawishi kwenye midomo yetu.’ (Met. 16:23) Nyakati nyingine, huenda ikafaa kufanya utafiti na kupata habari za ziada. Yule mwanamke mwenye umri wa miaka 93 aliyetajwa mwanzoni alitaka kujua kwa nini fundisho la kutokufa kwa nafsi (au roho) limeenea sana. Ili ashawishiwe kukubali fundisho la Biblia kuhusu jambo hilo, alihitaji kuelewa chanzo cha fundisho hilo na jinsi lilivyoingizwa katika dini nyingi ulimwenguni. *

Endelea Kulitumia Neno la Mungu kwa Ustadi

18, 19. Kwa nini tunapaswa kuendelea kuutumia kwa ustadi “upanga wa roho”?

18 Biblia inasema kwamba “tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” Watu waovu wanaendelea kuwa waovu zaidi. (1 Kor. 7:31; 2 Tim. 3:13) Kwa hiyo, ni jambo la maana kwetu kuendelea kupindua “ngome zenye nguvu” kwa kutumia “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.”

19 Tunafurahi kama nini kuwa na Neno la Mungu, Biblia, na kutumia ujumbe wake wenye nguvu kung’oa mafundisho ya uwongo na kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu! Ujumbe huo una nguvu nyingi kuliko ngome yoyote ile. Basi, acheni tujitahidi kabisa kuutumia “upanga wa roho” kwa ustadi katika kazi tuliyopewa na Mungu ya kutangaza Ufalme.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Unaweza kupata habari mbalimbali kuhusu vitabu vya Biblia katika kitabu “Kila Andiko Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” mabuku ya Insight on the Scriptures (Étude perspicace des Écritures), na makala kama vile “Neno la Yehova Liko Hai,” katika Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 17 Ona broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa? ukurasa wa 5-16.

Umejifunza Nini?

• Neno la Mungu lina nguvu nyingi kadiri gani?

• Tunaweza jinsi gani ‘kulitumia sawasawa neno la kweli’?

• Ujumbe wa Biblia unaweza kuzifanya nini “ngome zenye nguvu”?

• Unaweza kuboresha jinsi gani ustadi wako wa kushawishi katika huduma?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Jinsi ya Kutumia Neno la Mungu kwa Ushawishi

▪ Itumie Biblia kwa njia inayofanya iheshimiwe

▪ Eleza maana ya Maandiko

▪ Jadiliana na watu kwa njia yenye kusadikisha ili uguse mioyo yao

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ni lazima ujifunze kuutumia kwa ustadi “upanga wa roho”