Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha “Usafi wa Moyo” Katika Nyakati Hizi za Hatari

Dumisha “Usafi wa Moyo” Katika Nyakati Hizi za Hatari

Dumisha “Usafi wa Moyo” Katika Nyakati Hizi za Hatari

“HAKUNA mtu anayeweza kupinga kwamba kuna ukosefu wa usafi wa maadili katika Kanisa leo.” Vittorio Messori, mwandishi wa habari Mkatoliki alisema maneno hayo alipozungumza kuhusu visa vya ngono ambavyo vimehusisha Kanisa hilo huko Italia hivi karibuni. “Na tatizo hilo haliwezi kusuluhishwa kwa kuondoa takwa la makasisi kuendelea kuwa waseja kwa sababu asilimia 80 ya visa hivyo vinahusu ngono kati ya watu wa jinsia moja, yaani, visa vya makasisi kuwatendea vibaya kingono wanaume na wavulana.”—La Stampa.

Bila shaka, kuenea sana kwa uovu ni ishara ya “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. (2 Tim. 3:1-5) Kama vyombo vya habari vinavyoripoti, kuharibika kwa maadili hakuwahusu tu watu kwa ujumla lakini kunahusu pia wale wanaojiita watu wa Mungu. Mioyo yao iliyopotoka na isiyo safi inawasukuma kutenda mambo maovu. (Efe. 2:2) Yesu alikuwa na sababu nzuri alipoonya kwamba “mawazo mabaya hutoka moyoni, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uwongo, makufuru.” (Mt. 15:19) Hata hivyo, Yehova Mungu anataka watumishi wake wapende “usafi wa moyo.” (Met. 22:11) Basi, Mkristo anaweza kudumisha jinsi gani usafi wa moyo katika nyakati hizi za hatari?

Inamaanisha Nini Kuwa “Safi Moyoni”?

Katika Biblia, mara nyingi “moyo” unatajwa kwa njia ya mfano. Kulingana na kitabu kimoja cha marejeo, moyo unaotajwa katika Biblia unamaanisha “sehemu ya ndani kabisa ya mwanadamu” na “ndiyo sehemu hasa ambayo Mungu anachunguza, sehemu ambayo uhusiano wa mtu pamoja na Mungu unasitawishwa, na sehemu inayoongoza mwenendo wa maadili.” Moyo unafananisha hali yetu ya ndani kabisa. Kama kitabu kilichonukuliwa hapo juu kinavyoonyesha, Yehova anachunguza moyo huo, naye anafurahi kuwachunguza watumishi wake.—1 Pet. 3:4.

Katika Biblia, maneno “takata” na “safi” yanaweza kumaanisha kitu kilicho safi kimwili. Lakini maneno hayo yanaweza pia kumaanisha kitu ambacho hakijachafuliwa, yaani, kisicho na unajisi, uchafu, au upotovu, katika maana ya kiadili na kidini. Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni.” Alikuwa akizungumza kuhusu wale ambao kwa kweli, ni safi kwa ndani. (Mt. 5:8) Mambo wanayopenda, tamaa, na nia zao ni safi. Wanachochewa na upendo na uthamini kumpenda Yehova kwa moyo wao wote, kikweli, na bila unafiki. (Luka 10:27) Bila shaka ungependa kuwa safi kwa njia hiyo, sivyo?

Si Rahisi Kuendelea Kuwa “Safi Moyoni”

Mtumishi wa Yehova hapaswi tu kuwa ‘bila hatia katika mikono yake’ bali pia anapaswa kuwa “safi moyoni.” (Zab. 24:3, 4) Hata hivyo, leo inaendelea kuwa vigumu hata zaidi kwa watumishi wa Mungu kubaki wakiwa “safi moyoni.” Shetani na ulimwengu anaotawala, pamoja na mwili wetu usio mkamilifu, unatusukuma sana tumwache Yehova. Ili tupinge uvutano huo, ni jambo la maana sana kwetu kuupenda “usafi wa moyo” na kuazimia kabisa kuushika. Hilo litatulinda na kutusaidia kuendelea kuwa marafiki wa Mungu. Tunaweza jinsi gani kudumisha moyo ulio safi?

Andiko la Waebrania 3:12 linatuonya hivi: “Jihadharini, akina ndugu, ili moyo mwovu unaokosa imani usije ukasitawi ndani ya yeyote kati yenu kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai.” Hatuwezi kuendelea kuwa “safi moyoni” tukisitawisha moyo “unaokosa imani.” Shetani Ibilisi ameeneza mawazo gani ambayo yanadhoofisha imani yetu katika Mungu? Yanatia ndani nadharia ya mageuzi, mtu kujiwekea viwango vyake mwenyewe vya maadili na dini, na kuwa na shaka kwamba Maandiko Matakatifu yameongozwa na roho ya Mungu. Hatupaswi kukubali kupotoshwa na mawazo hatari kama hayo. (Kol. 2:8) Kusoma Biblia kila siku na kutafakari kwa undani ni mambo ya maana sana yanayoweza kutulinda na mashambulizi hayo. Ujuzi sahihi wa Neno la Mungu utatia nguvu upendo wetu kwa Yehova na kutusaidia tuthamini zaidi jinsi anavyoshughulika na watu. Ni lazima tuwe na upendo na uthamini kama huo ikiwa tunataka kupinga mawazo ya uwongo na kudumisha imani yenye nguvu katika Yehova ili tuendelee kuwa na moyo safi.—1 Tim. 1:3-5.

Kukabiliana na Tamaa za Mwili

Shambulizi lingine tunaloweza kukabili tunapojaribu kudumisha “usafi wa moyo” linahusisha tamaa ya mwili na tamaa ya mali. (1 Yoh. 2:15, 16) Kupenda pesa au kutamani kujikusanyia mali na kuwa na vitu vya kimwili kunaweza kupotosha moyo, na kumfanya Mkristo afanye mambo ambayo hayapatani na mapenzi ya Mungu. Watu fulani wamekosa unyoofu kazini, wamewadanganya wengine, au hata wameiba pesa au vitu vingine.—1 Tim. 6:9, 10.

Kwa upande mwingine, tukisitawisha woga unaofaa wa kutompendeza Yehova, tukipenda haki, na kuazimia kuwa na dhamiri njema, tunaonyesha kwamba tunapenda “usafi wa moyo.” Upendo huo unatuchochea kuendelea “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Ebr. 13:18) Tunapotenda kwa unyoofu, tunaweza kupata nafasi ya kutoa ushahidi mzuri. Emilio, Shahidi anayeishi huko Italia ambaye ni dereva katika kampuni moja ya usafiri wa umma, alipata kifuko cha pesa kilichokuwa na dola za Marekani 680. Wafanyakazi wenzake walishangaa wakati alipompatia msimamizi wake kifuko hicho, naye msimamizi akampa mtu aliyekuwa amekipoteza. Baadhi ya wafanyakazi wenzi wa Emilio walifurahishwa sana na mwenendo wake hivi kwamba wakapendezwa na Biblia na wakaanza kujifunza. Matokeo ni kwamba watu saba kutoka katika familia mbili wamekubali kweli. Ndiyo, kwa kweli tunapotenda kwa unyoofu tukichochewa na moyo safi tunaweza kuwachochea wengine wamsifu Mungu.—Tito 2:10.

Jambo lingine ambalo linaweza kupotosha usafi wa moyo wa Mkristo ni maoni machafu kuhusu ngono. Watu wengi wanaona kwamba ni sawa kufanya uasherati, uzinzi, au ngono kati ya watu wa jinsia moja, na maoni hayo yanaweza kuupotosha moyo wa Mkristo. Mtu anayejihusisha na mwenendo mpotovu wa kingono anaweza kuishi maisha ya unafiki, na kuficha dhambi hiyo. Bila shaka, hilo halingeonyesha kwamba ana “usafi wa moyo.”

Gabriele alibatizwa akiwa na umri wa miaka 15 na mara moja akaanza kufanya upainia. Hata hivyo, baadaye alianza kushirikiana na marafiki wabaya na kwenda kwenye vilabu vya usiku. (Zab. 26:4) Huo ndio uliokuwa mwanzo wa maisha ya upotovu wa maadili na unafiki, na alitengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Nidhamu hiyo kutoka kwa Yehova ilimfanya afikirie kwa uzito maisha yake. Gabriele anakumbuka hivi: “Nilianza kufanya mambo yote ambayo nilipuuza mwanzoni. Nilisoma Biblia kila siku na kujaribu kuelewa mambo ambayo Yehova alikuwa anasema, na nilijifunza kwa makini vichapo vya Kikristo. Niliona jinsi funzo la kibinafsi linavyoweza kunufaisha na kuridhisha, na jinsi kusoma Biblia na kusali kwa bidii kunavyoweza kumtia mtu nguvu.” Mambo hayo yalimsaidia Gabriele aache upotovu wa maadili na kusitawisha tena uhusiano mzuri pamoja na Yehova.

Gabriele sasa anatumika tena akiwa painia, pamoja na mke wake. Mambo yaliyompata yanathibitisha kwamba kujifunza Biblia na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kunaweza kumsaidia mtu awe na moyo safi na aepuke ukosefu wa maadili.—Mt. 24:45; Zab. 143:10.

Kudumisha “Usafi wa Moyo” Tunapojaribiwa

Mkazo kutoka kwa wapinzani, matatizo ya kiuchumi, na ugonjwa mbaya umefanya watumishi fulani wa Mungu wavunjike moyo. Pindi fulani, mambo kama hayo yamekuwa pia na matokeo mabaya kwa mioyo yao. Hata Mfalme Daudi alikabili hali kama hiyo, alisema hivi: “Roho yangu inazimia ndani yangu; moyo wangu wenyewe umekufa ganzi katikati yangu.” (Zab. 143:4) Nini kilichomsaidia kukabiliana na nyakati kama hizo? Daudi alikumbuka jinsi Mungu alivyokuwa amewatendea watumishi Wake na jinsi yeye mwenyewe alivyokombolewa. Alitafakari jinsi Yehova alivyokuwa ametenda kwa ajili ya Jina lake kuu. Daudi aliendelea kuhangaikia kazi za Mungu. (Zab. 143:5) Vivyo hivyo, kutafakari kuhusu Muumba wetu na yote ambayo tayari ametufanyia na anaendelea kutufanyia, kutatusaidia hata tunapojaribiwa.

Mtu anapotukosea au tunapohisi kwamba tumekosewa, tunaweza kukasirika. Kuendelea kufikiria jambo hilo kunaweza kufanya tuwe na maoni mabaya kuhusu ndugu zetu. Huenda tukaepuka kushirikiana na wengine, kujitenga na kutopendezwa sana na wengine. Je, kutenda kwa njia hiyo kunaonyesha kwamba tunatamani kuwa na “usafi wa moyo”? Ni wazi kwamba usafi wa moyo unahusiana na jinsi tunavyowaona na kuwatendea ndugu zetu Wakristo.

Katika ulimwengu unaozidi kupotoka na uliojaa maadili mapotovu, tukiwa Wakristo wa kweli, tunakuwa tofauti kwa sababu tunapenda “usafi wa moyo.” Tunaishi maisha mazuri kwa sababu tuna amani ya moyoni ambayo inategemea kufanya mapenzi ya Mungu. Zaidi ya yote, tunafurahia urafiki wa karibu pamoja na Muumba wetu, Yehova Mungu, ambaye anapenda wale “walio safi moyoni.” (Zab. 73:1) Ndiyo, tunaweza kuwa kati ya wale ambao watakuwa na furaha kwa sababu Yesu aliahidi kwamba “watamwona Mungu,” wakati Atakapotenda kwa ajili ya wale wanaopenda “usafi wa moyo.”—Mt. 5:8.