Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, andiko la Ezekieli 18:20, ambalo linasema kwamba “mwana hatakuwa na hatia yoyote kwa sababu ya kosa la baba,” linapingana na andiko la Kutoka 20:5, ambalo linasema kwamba Yehova analeta “adhabu juu ya wana kwa sababu ya kosa la akina baba”?

Maandiko hayo mawili hayapingani. Andiko moja linakazia kwamba kila mtu ana wajibu kwa ajili ya matendo yake, nalo andiko la pili linathibitisha kwamba makosa ya mtu yanaweza kuwa na matokeo mabaya kwa wazao wake.

Mistari mingine katika Ezekieli sura ya 18 inaonyesha kwamba jambo linalokaziwa ni mtu binafsi kukubali wajibu wake. Mstari wa 4 unasema kwamba “nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” Namna gani mtu ambaye ni “mwadilifu naye ametenda haki na uadilifu”? “Hakika yeye ataendelea kuishi.” (Eze. 18:5, 9) Hivyo, baada ya mtu kufikia umri ambao anaweza kuchukua wajibu wake kwa uzito, anahukumiwa “kulingana na njia yake.”—Eze. 18:30.

Kanuni hiyo inaonekana wazi katika kisa cha Mlawi aliyeitwa Kora. Waisraeli walipokuwa wakisafiri nyikani, Kora hakutosheka na mapendeleo yake ya utumishi. Ili wapate madaraka ya ukuhani, Kora pamoja na watu wengine waliwaasi Musa na Haruni, wawakilishi wa Yehova. Yehova alimuua Kora pamoja na waasi wenzake kwa sababu walijaribu kwa kimbelembele kuchukua pendeleo hilo ambalo halikuwa lao. (Hes. 16:8-11, 31-33) Hata hivyo, wana wa Kora hawakushiriki katika uasi huo. Mungu hakuwaadhibu kwa sababu ya dhambi ya baba yao. Waliokoka kwa sababu ya ushikamanifu wao kwa Yehova.—Hes. 26:10, 11.

Lakini namna gani onyo lililo katika andiko la Kutoka 20:5, ambalo ni sehemu ya zile Amri Kumi? Fikiria tena mistari mingine katika andiko hilo. Yehova alifanya agano la Sheria pamoja na taifa la Israeli. Baada ya kusikia masharti ya agano hilo, Waisraeli walisema hivi waziwazi: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” (Kut. 19:5-8) Kwa hiyo, taifa lote likaingia katika uhusiano wa pekee pamoja na Yehova. Hivyo basi, maneno yaliyo kwenye Kutoka 20:5 yalielekezwa hasa kwa taifa hilo lote.

Waisraeli walipoendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, taifa lote lilifaidika na kufurahia baraka nyingi. (Law. 26:3-8) Walipoasi waliteseka sana. Taifa la Israeli lilipomkataa Yehova na kufuata miungu ya uwongo, aliondoa baraka na ulinzi wake; taifa hilo likapatwa na msiba. (Amu. 2:11-18) Ni kweli kwamba watu fulani waliendelea kuwa watimilifu na wakatii amri za Mungu ingawa taifa hilo lilikuwa linaabudu sanamu. (1 Fal. 19:14, 18) Inaelekea kwamba wale waliokuwa waaminifu waliteseka kwa njia fulani kwa sababu ya dhambi za taifa hilo, lakini Yehova aliwaonyesha fadhili zenye upendo.

Waisraeli walipovunja waziwazi kanuni za Yehova mpaka jina lake likadharauliwa kati ya mataifa, Yehova aliamua kuwaadhibu watu wake kwa kuruhusu wapelekwe utekwani huko Babiloni. Bila shaka, hilo lilitia ndani kuwaadhibu watu mmoja-mmoja na watu wake wakiwa kikundi. (Yer. 52:3-11, 27) Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba hatia ya taifa lote la Israeli ilikuwa kubwa sana hivi kwamba vizazi vitatu, vinne, au hata zaidi viliteseka kwa sababu ya makosa ya mababu zao, kama vile tu andiko la Kutoka 20:5 linavyosema.

Neno la Mungu pia lina masimulizi yanayoonyesha jinsi familia fulani zilivyoteseka kwa sababu ya makosa ya wazazi wao. Kuhani Mkuu Eli alimkasirisha Yehova kwa kuruhusu wanawe ambao walikuwa “watu wasiofaa kitu” na wenye maadili mapotovu waendelee kuwa makuhani. (1 Sam. 2:12-16, 22-25) Kwa kuwa Eli aliwaheshimu wanawe kuliko Yehova, Mungu aliazimia kwamba familia ya Eli ingeondolewa kwenye cheo cha kuhani mkuu, na hilo lilitendeka kuanzia kwa Abiathari, mwana wa mjukuu wake. (1 Sam. 2:29-36; 1 Fal. 2:27) Kanuni ya Kutoka 20:5 inaonekana pia katika kisa cha Gehazi. Alitumia vibaya cheo chake akiwa mtumishi wa Elisha ili kupata mali baada ya Naamani Mkuu wa Jeshi la Siria kuponywa. Yehova alitangaza hukumu kupitia Elisha, akisema: “Ukoma wa Naamani utakushika wewe na uzao wako mpaka wakati usio na kipimo.” (2 Fal. 5:20-27) Hivyo, wazao wa Gehazi walipata matokeo mabaya kwa sababu ya makosa yake.

Akiwa Muumba na Mpaji-Uhai, Yehova anastahili kabisa kuamua adhabu inayofaa na ambayo ni ya haki. Mifano iliyotajwa hapo juu inaonyesha kwamba watoto au wazao wanaweza kupatwa na matokeo mabaya ya dhambi ya wazazi wao. Hata hivyo, Yehova “hukisikia kilio cha watu wanaoteseka,” na watu wanaomgeukia kwa unyoofu wanaweza kupata kitulizo na kukubaliwa na yeye.—Ayu. 34:28.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kora na waasi wenzake waliadhibiwa kwa sababu ya matendo yao