Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tembea kwa Roho na Uishi Kulingana na Wakfu Wako

Tembea kwa Roho na Uishi Kulingana na Wakfu Wako

Tembea kwa Roho na Uishi Kulingana na Wakfu Wako

“Endeleeni kutembea kwa roho nanyi hamtatenda tamaa ya kimwili hata kidogo.”—GAL. 5:16.

1. Ni ubatizo gani wa aina mbili uliofanywa katika siku ya Pentekoste?

WAFUASI wa Yesu walisema kwa lugha mbalimbali siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. baada ya kubatizwa kwa roho takatifu. Wakafanya miujiza kupitia zawadi mbalimbali za roho. (1 Kor. 12:4-10) Zawadi hizo za roho na hotuba iliyotolewa na mtume Petro zilikuwa na matokeo gani? Wengi “walichomwa moyoni.” Baada ya kuhimizwa na Petro, walitubu na wakabatizwa. Masimulizi ya kihistoria yanasema hivi: “Wale waliokubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo wakabatizwa, na katika siku hiyo nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa.” (Mdo. 2:22, 36-41) Kama Yesu alivyoamuru, walibatizwa ndani ya maji katika jina la Baba, na la Mwana, na la roho takatifu.—Mt. 28:19.

2, 3. (a) Eleza tofauti kati ya kubatizwa kwa roho takatifu na kubatizwa katika jina la roho takatifu. (b) Kwa nini wote ambao wanakuwa Wakristo wa kweli leo wanatazamiwa kubatizwa katika maji?

2 Hata hivyo, je, kuna tofauti yoyote kati ya kubatizwa kwa roho takatifu na kubatizwa katika jina la roho takatifu? Ndiyo. Wale ambao wanabatizwa kwa roho takatifu wanazaliwa tena wakiwa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho. (Yoh. 3:3) Wanatiwa mafuta kwa roho ili wawe wafalme wakati ujao pamoja na Kristo na makuhani wa cheo cha chini katika Ufalme wa Mungu huko mbinguni, nao ni sehemu ya mwili wa kiroho wa Kristo. (1 Kor. 12:13; Gal. 3:27; Ufu. 20:6) Huo ndio ubatizo—kubatizwa kwa roho takatifu—ambao Yehova alifanya siku ya Pentekoste na baadaye, alipowachagua watu mmoja-mmoja kuwa warithi pamoja na Kristo. (Rom. 8:15-17) Lakini namna gani kuhusu kubatizwa ndani ya maji katika jina la roho takatifu, ambako kunafanywa kwa ukawaida kwenye makusanyiko ya watu wa Yehova leo?

3 Kubatizwa katika maji ni hatua ambayo Wakristo wa kweli wanachukua ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova Mungu bila masharti yoyote. Wale waliopokea mwito wa mbinguni wanabatizwa pia kwa njia hiyo. Lakini kubatizwa katika maji pia ni hatua ya lazima kwa mamilioni ya wanaume na wanawake katika nyakati zetu ambao sasa wana tumaini la kuishi milele duniani. Hata mtu akiwa na tumaini gani, kubatizwa ndani ya maji katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu ni hatua ya lazima ambayo mtu anapaswa kuchukua ili kukubaliwa na Mungu. Hivyo, Wakristo wote waliobatizwa wanatazamiwa kuendelea “kutembea kwa roho.” (Soma Wagalatia 5:16.) Je, unatembea kwa roho na hivyo kuishi kulingana na wakfu wako?

“Kutembea kwa Roho” Kunamaanisha Nini?

4. “Kutembea kwa roho” kunamaanisha nini hasa?

4 “Kutembea kwa roho” kunamaanisha kukubali utendaji wa roho takatifu katika maisha yako, na kuruhusu roho takatifu ikuongoze. Kwa maneno mengine, kunamaanisha kuongozwa na roho takatifu katika utendaji wako mbalimbali wa kila siku. Sura ya 5 ya kitabu cha Wagalatia inaonyesha tofauti kati ya kuongozwa na roho takatifu na kuongozwa na mwili.—Soma Wagalatia 5:17, 18.

5. Kuongozwa na roho takatifu kunatia ndani kuepuka matendo gani?

5 Ikiwa unaongozwa na roho takatifu, unajitahidi kuepuka matendo ya mwili. Matendo hayo yanatia ndani mambo kama vile “uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, madhehebu, husuda, vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia.” (Gal. 5:19-21) Hivyo, kwa njia fulani, ‘unayaua mazoea ya mwili kwa roho.’ (Rom. 8:5, 13) Kufanya hivyo kutakusaidia kukazia akili mambo ya roho na kuacha roho hiyo ikuongoze, badala ya kujiacha uongozwe na tamaa za mwili.

6. Toa mfano ambao unaonyesha jambo ambalo tunapaswa kufanya ili tuonyeshe matunda ya roho.

6 Roho takatifu inapokuongoza, unaonyesha sifa za kimungu, “matunda ya roho.” (Gal. 5:22, 23) Hata hivyo, unatambua kwamba unahitaji kujitahidi ili kuonyesha sifa hizo. Kwa mfano: Mkulima analima shamba. Bila shaka, mwangaza wa jua na maji ni mambo ya lazima; bila mwangaza wa jua na maji mkulima huyo hawezi kutazamia kupata mavuno yoyote. Tunaweza kulinganisha roho takatifu na mwangaza wa jua. Tunahitaji roho takatifu ili kuzaa matunda ya roho. Hata hivyo, je, mkulima anaweza kupata mazao bila kufanya kazi kwa bidii? (Met. 10:4) Ni wazi kwamba ubora na wingi wa matunda ya roho takatifu ndani yako unategemea jinsi unavyolima udongo wa moyo wako. Hivyo, jiulize hivi, ‘Je, ninaruhusu roho takatifu itokeze matunda yake ndani yangu kwa kuishi kulingana na roho hiyo?’

7. Kwa nini kujifunza na kutafakari ni mambo ya maana sana ikiwa unataka kusitawisha matunda ya roho takatifu?

7 Ili kupata mavuno mazuri, wakulima wanahitaji pia kutilia maji mimea yao. Ili kusitawisha matunda ya roho, unahitaji maji ya kweli yanayopatikana katika Biblia na kupitia kutaniko la Kikristo leo. (Isa. 55:1) Inaelekea umewaonyesha watu wengi kwamba Maandiko Matakatifu yaliongozwa na roho takatifu. (2 Tim. 3:16) Pia, jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara inatusaidia kupata uelewaji tunaohitaji sana wa maji safi ya kweli za Biblia. (Mt. 24:45-47) Basi ni wazi kwamba ili tuongozwe na roho takatifu, ni lazima tusome na kutafakari kuhusu Neno la Mungu. Ikiwa unafanya hivyo, unaiga mifano mizuri ya manabii ambao “walifanya uchunguzi kwa bidii na kutafuta kwa uangalifu” habari zilizokuwa zimetolewa. Inatia moyo kujua kwamba hata malaika wamependezwa sana na kweli za kiroho kuhusu Uzao ulioahidiwa na pia kuhusu kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta.—Soma 1 Petro 1:10-12.

Tunaweza Kuongozwa na Roho Jinsi Gani?

8. Kwa nini ni jambo la maana kumwomba Yehova roho yake?

8 Haitoshi tu kujifunza na kutafakari kuhusu Maandiko. Unahitaji kuendelea kuomba msaada na mwongozo wa Yehova. Anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” (Efe. 3:20; Luka 11:13) Hata hivyo, ungejibu jinsi gani ikiwa mtu fulani angekuuliza hivi: “Kwa nini niendelee kuomba ikiwa tayari Mungu anajua ‘ni vitu gani ninavyohitaji hata kabla sijamwomba’?” (Mt. 6:8) Sababu moja ni kwamba unaposali ili upewe roho takatifu, unaonyesha kwamba unamtegemea Yehova. Kwa mfano, mtu fulani akija kukuomba msaada, utafanya yote unayoweza ili kumsaidia, sababu moja ya kufanya hivyo ni kwamba amekuomba umsaidie, hivyo anaonyesha kwamba anakutumaini. (Linganisha na Methali 3:27.) Vivyo hivyo, Yehova anafurahi unapomwomba roho yake takatifu, naye atakupa roho hiyo.—Met. 15:8.

9. Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunaweza kukusaidia jinsi gani kuongozwa na roho ya Mungu?

9 Utafurahi kujua kwamba njia nyingine ambayo roho ya Mungu inatuongoza ni kupitia mikutano na makusanyiko yetu. Kujitahidi kuhudhuria mikutano na kusikiliza kwa makini wakati wa programu ni jambo la maana sana. Kufanya hivyo kunakusaidia uelewe “mambo mazito ya Mungu.” (1 Kor. 2:10) Pia, kuna faida nyingi za kutoa maelezo kwa ukawaida. Fikiria mikutano uliyohudhuria katika majuma manne yaliyopita. Uliinua mkono wako juu mara ngapi ili ujibu na kuonyesha imani yako? Je, unaona kwamba unahitaji kufanya marekebisho fulani katika jambo hilo? Ikiwa ni hivyo, azimia kutoa maelezo katika majuma yanayofuata. Yehova ataona nia yako nzuri ya kushiriki kutoa maelezo, naye atakupa roho yake takatifu ambayo itakusaidia kufaidika zaidi na mikutano unayohudhuria.

10. Kutembea kwa roho kunatia ndani kuwatolea wengine mwaliko gani?

10 Kutembea kwa roho kunatia ndani kukubali mwaliko ambao tunasoma katika Ufunuo 22:17: “Roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’ Na yeyote anayesikia na aseme: ‘Njoo!’ Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.” Roho, inayotenda kazi kupitia jamii ya bibi-arusi aliyetiwa mafuta, inaendelea kutoa mwaliko huo wa maji ya uzima. Ikiwa umekubali mwaliko huo, je, umeazimia kusema, “Njoo!”? Ni pendeleo kama nini kuweza kushiriki katika kazi hii ya kuokoa uhai!

11, 12. Roho takatifu inahusika jinsi gani katika kazi ya kuhubiri?

11 Kazi hii ya maana sana inatimizwa sasa chini ya mwongozo wa roho takatifu. Tunasoma kuhusu jinsi roho takatifu ilivyowaongoza wamishonari katika karne ya kwanza kuhubiri katika maeneo mapya. Mtume Paulo na wenzake “walikatazwa na roho takatifu wasiseme lile neno katika wilaya ya Asia”; wala hawakuruhusiwa kuingia Bithinia. Hatujui kabisa jinsi roho ilivyowakataza kuingia katika maeneo hayo, hata hivyo, ni wazi kwamba roho ilimwongoza Paulo kuingia katika eneo kubwa la Ulaya. Alipata maono ya mwanamume Mmakedonia aliyewasihi wamsaidie.—Mdo. 16:6-10.

12 Leo, roho ya Yehova inaongoza vivyo hivyo kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Hakuna maono ya kimuujiza yanayotumiwa ili kutoa mwongozo huo; hata hivyo, Yehova anawaongoza watiwa-mafuta kwa roho takatifu. Na roho inawachochea akina ndugu na dada kufanya yote wanayoweza katika kuhubiri na kufundisha. Bila shaka, umekuwa ukishiriki katika kazi hiyo ya maana sana. Je, unaweza kuongeza shangwe yako katika utendaji huu wenye kusisimua?

13. Unaweza kufuata mwongozo wa roho takatifu jinsi gani? Toa mfano.

13 Unaweza kufuata mwongozo wa roho takatifu kwa kutumia habari ambazo watu wa Mungu wanaandaliwa. Fikiria mfano wa dada Mihoko kutoka Japani. Akiwa painia mpya, aliona kwamba hana uwezo wa kufanya ziara za kurudia; alihisi kwamba hakujua jinsi ya kumfanya mwenye nyumba apendezwe. Wakati huo, ndipo mapendekezo mazuri yalipotolewa katika Huduma Yetu ya Ufalme kuhusu jinsi ya kufanya ziara fupi za kurudia. Kisha broshua Jinsi ya Kupata Maisha Yenye Kuridhisha ikachapishwa. Broshua hiyo ilikuwa yenye manufaa sana hasa katika eneo la lugha ya Kijapani. Mihoko alitumia mapendekezo yaliyotolewa kuhusu kutumia broshua hiyo, hasa katika kufanya ziara fupi za kurudia. Muda si muda, alianzisha mafunzo mengi ya Biblia pamoja na wale ambao huenda mwanzoni wangekataa funzo. Mihoko anasema hivi: “Nilipata mafunzo mengi sana, wakati mmoja nilikuwa na mafunzo 12, hivi kwamba niliwaweka wengine kwenye orodha ya kungojea!” Kwa kweli, unapotembea kwa roho na kufuata mwongozo unaotolewa kwa watumishi wa Yehova, unaweza kuvuna kwa wingi.

Tegemea Roho ya Mungu

14, 15. (a) Watu wasio wakamilifu wanaweza kuishi jinsi gani kulingana na wakfu wao? (b) Unaweza kupata jinsi gani marafiki wazuri zaidi?

14 Ukiwa mhudumu aliyewekwa rasmi, una huduma ya kutimiza. (Rom. 10:14) Huenda ukahisi kwamba hustahili kabisa kutimiza daraka hilo. Lakini, kama ilivyo na watiwa-mafuta, ni Mungu anayekufanya ustahili. (Soma 2 Wakorintho 3:5.) Unaweza kuishi kulingana na wakfu wako kwa kufanya yote unayoweza na kutegemea roho ya Mungu.

15 Ni kweli kwamba si rahisi kwetu sisi wanadamu wasio wakamilifu kuishi kulingana na wakfu wetu kwa Mungu mkamilifu, Yehova. Tatizo moja ni kwamba huenda watu fulani ambao walikuwa marafiki wako zamani wakashangazwa na njia yako mpya ya maisha na huenda ‘wakakutukana.’ (1 Pet. 4:4) Hata hivyo, usipuuze ukweli wa kwamba umepata marafiki wapya, na Yehova na Yesu Kristo ndio marafiki wako wa maana zaidi. (Soma Yakobo 2:21-23.) Ni jambo la maana pia kuwajua akina ndugu na dada wa kutaniko lako, ambao ni sehemu ya “ushirika mzima wa akina ndugu” ulimwenguni pote. (1 Pet. 2:17; Met. 17:17) Yehova kupitia roho yake atakusaidia kupata marafiki ambao wataendelea kuwa na uvutano mzuri juu yako.

16. Kama Paulo, kwa nini unaweza ‘kupendezwa na udhaifu’?

16 Hata ukizungukwa na marafiki wazuri katika kutaniko lako, huenda ukaona kuwa bado ni vigumu kukabiliana na matatizo ya kila siku. Nyakati nyingine, mambo ambayo unakabiliana nayo yanaweza kukufanya uhisi kwamba huna tumaini lolote, ni kana kwamba unapambana na matatizo yasiyo na mwisho. Huo ndio wakati hasa wa kusali kwa Yehova na kumwomba roho yake takatifu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.” (Soma 2 Wakorintho 4:7-10; 12:10.) Paulo alijua kwamba roho ya Mungu inaweza kutusaidia kukabiliana na udhaifu wowote ule wa kibinadamu. Hivyo, nguvu ya utendaji ya Mungu inaweza kukutia nguvu wakati wowote unapokuwa dhaifu na unapohitaji msaada. Paulo aliandika kwamba ‘alipendezwa na udhaifu.’ Alipokuwa dhaifu, ndipo alipohisi roho takatifu ikitenda kazi juu yake. Unaweza kuhisi vivyo hivyo pia!—Rom. 15:13.

17. Roho takatifu inaweza kukusaidia jinsi gani kuelekea mahali unapoenda?

17 Tunahitaji roho ya Mungu ili tuishi kulingana na wakfu wetu kwake. Tuseme kwamba wewe ni kiongozi au nahodha wa mashua. Mradi wako ni kumtumikia Yehova milele. Roho takatifu ni kama upepo ambao unataka ukufikishe kwa usalama mahali unapoenda. Hutaki kurushwa huku na huku na roho ya ulimwengu wa Shetani. (1 Kor. 2:12) Kwa njia ya mfano, unapaswa kutambua upepo unaofaa na kuuacha ukuongoze upande unaofaa. Tunaweza kulinganisha upepo huo na roho takatifu. Kupitia Neno la Mungu na tengenezo lake linaloongozwa na roho, roho takatifu itakuongoza upande unaofaa.

18. Umeazimia kufanya nini sasa, na kwa nini?

18 Ikiwa umekuwa ukijifunza na Mashahidi wa Yehova na kufurahia ushirika wao wa kiroho, lakini bado hujachukua hatua ya maana sana ya kujiweka wakfu na kubatizwa, jiulize hivi: ‘Kwa nini ninasitasita?’ Ikiwa unatambua daraka la roho takatifu katika kutimiza mapenzi ya Yehova leo na ikiwa unathamini utendaji wake, basi chukua hatua zinazofaa ambazo umejifunza. Yehova atakubariki sana. Atakupa kwa ukarimu roho yake takatifu. Ikiwa ulibatizwa miaka mingi iliyopita, bila shaka umeona uvutano wa roho takatifu katika maisha yako. Umehisi na kuona jinsi Mungu anavyoweza kukutia nguvu kwa roho yake. Anaweza kuendelea kukutia nguvu kwa umilele wote. Hivyo, azimia kuendelea kutembea kwa roho takatifu.

Je, Unakumbuka?

• “Kutembea kwa roho” kunamaanisha nini?

• Ni nini kinachoweza kukusaidia ‘kuendelea kutembea kwa roho’?

• Unaweza kuishi jinsi gani kulingana na wakfu wako?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Unahitaji kujitahidi ili kulima udongo wa moyo wako

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Je, unaongozwa na roho ya Mungu?