Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Kwa nini Masihi alipaswa kufa?

Kifo cha Yesu kilithibitisha kwamba mwanadamu mkamilifu anaweza kudumisha ujitoaji-kimungu hata akijaribiwa vikali. Pia, kifo cha Yesu kililipia adhabu ya dhambi ambayo wazao wa Adamu walirithi na kuwapa nafasi ya kupata uzima wa milele.—12/15, ukurasa wa 22-23.

• Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu awe na mtazamo unaofaa kuhusu pombe?

Kusali na kujifunza Biblia kunaweza kusaidia. Ni jambo la maana pia kusitawisha sifa ya kujizuia, mtu kushikilia azimio lake, na kuchagua marafiki wazuri. Ikiwa mtu ataamua kunywa pombe anapaswa kuweka mipaka iliyo wazi na ajifunze kukataa.—1/1, ukurasa wa 7-9.

• Mawasiliano mazuri pamoja na watoto yanatia ndani nini?

Yanatia ndani mengi zaidi ya kuongea tu na watoto. Yanatia ndani kuwauliza maswali na kusikiliza majibu yao kwa subira. Wengi wamegundua kwamba wakati wa chakula ni pindi inayofaa ya kuwa na mazungumzo.—1/15, ukurasa wa 18-19.

• Kwa nini Yehova anaweza kujuta ingawa ni mkamilifu?

Nyakati nyingine, Mungu anabadili nia yake kuelekea watu. Kwa mfano, Waisraeli wa kale walimwacha Yehova mara kwa mara na kufuata miungu mingine. Kwa hiyo, Yehova aliacha kuwalinda. Hata hivyo, watu walipojuta kwa sababu ya kosa lao na wakamlilia Mungu awasaidie, alibadili nia yake kuwaelekea, au ‘alijuta.’ (Amu. 2:18)—2/1, ukurasa wa 21.

• Ni hali gani ambazo zinaweza kufanya mtu abatizwe tena?

Inaweza kuwa hivyo ikiwa wakati wa ubatizo mtu huyo alikuwa anaishi katika hali fulani au alikuwa anazoea kutenda jambo fulani kwa siri ambalo lingefanya atengwe na ushirika ikiwa angekuwa amebatizwa kihalali.—2/15, ukurasa wa 22.

• Ni sababu gani tatu zisizofaa za kutokuwa wanyoofu ambazo watu fulani wanatoa?

Wengine wanaona kwamba ni sawa kuiba kwa sababu wao ni maskini. Wengine wanajitetea kwa kusema, “Kila mtu anaiba.” Na wengine ambao wameokota vitu vyenye thamani vilivyopotea na kukaa navyo wanaamini kwamba “kuokota si kuiba.” Biblia haiungi mkono sababu hizo tatu.—3/1, ukurasa wa 12-14.

• Katika mfano wa Yesu wa ngano na magugu, kupanda mbegu nzuri kunafananisha nini?

Mwana wa binadamu, Yesu, alitayarisha shamba wakati wa huduma yake duniani. Kuanzia Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, mbegu nzuri ilipandwa wakati Wakristo walipotiwa mafuta na kuwa wana wa Mungu, wana wa Ufalme.—3/15, ukurasa wa 20.

• Ngano ya mfano inayotajwa katika mfano wa Yesu inakusanywa jinsi gani ndani ya ghala la Yehova? (Mt. 13:30)

Kazi hiyo imeendelea kwa kipindi fulani wakati wa umalizio wa mfumo wa mambo. Wana wa Ufalme waliotiwa mafuta, yaani, ngano ya mfano, wanakusanywa katika ghala la Yehova wanapojiunga na kutaniko la Kikristo ambalo limepangwa kitengenezo au wakati wanapopata thawabu yao ya kwenda mbinguni.—3/15, ukurasa wa 22.

• Ni nani aliyeamua kwamba vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo viliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu?

Si baraza lolote la kanisa wala kiongozi yeyote wa kidini. Badala yake, Wakristo wa kweli, wakiongozwa na roho takatifu ya Mungu, walitambua maandishi ambayo kwa kweli yalikuwa yameandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu. Hilo linapatana na ukweli wa kwamba mojawapo ya zawadi za kimuujiza za roho ambazo kutaniko la Kikristo la mapema lilipewa ni “utambuzi wa maneno yaliyoongozwa na roho.” (1 Kor. 12:4, 10)—4/1, ukurasa wa 28.