Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Yehova Anavyotumia Roho Takatifu Kutimiza Kusudi Lake

Jinsi Yehova Anavyotumia Roho Takatifu Kutimiza Kusudi Lake

Jinsi Yehova Anavyotumia Roho Takatifu Kutimiza Kusudi Lake

“Neno langu linalotoka katika kinywa changu . . . hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—ISA. 55:11.

1. Toa mfano unaoonyesha tofauti kati ya mpango na kusudi.

WAZIA kwamba wanaume wawili wanajitayarisha kusafiri kwa magari. Mmoja wao anapanga kutumia njia moja tu ili kufika mahali anapoenda. Yule mwingine anajua vizuri mahali anapoenda, lakini pia anajua njia mbalimbali za kufika huko. Yuko tayari kutumia njia nyingine ikiwa tatizo litatokea. Maamuzi ya wanaume hao wawili yanaweza kutumiwa kuonyesha tofauti iliyopo kati ya mpango na kusudi. Mpango unaweza kulinganishwa na uamuzi wa kutumia njia moja tu, lakini kusudi linaweza kutia ndani kuwa na lengo fulani akilini lakini njia mbalimbali za kutimiza lengo hilo.

2, 3. (a) Kusudi la Yehova linatia ndani nini, na alishughulika jinsi gani na hali iliyotokea wakati Adamu na Hawa walipotenda dhambi? (b) Kwa nini tunapaswa kuelewa na kutenda kupatana na kutimizwa kwa kusudi la Yehova?

2 Yehova anapotaka kutimiza mapenzi yake hatumii mpango fulani usiobadilika, badala yake, anatumia kusudi ambalo linatimizwa hatua kwa hatua. (Efe. 3:11) Kusudi hilo linahusiana na jinsi alivyokusudia wanadamu na dunia iwe mwanzoni, yaani, dunia igeuzwe na kuwa makao ya paradiso ambamo wanadamu wakamilifu wanaweza kuishi kwa amani na furaha milele. (Mwa. 1:28) Adamu na Hawa walipotenda dhambi, Yehova alishughulikia hali hiyo na akajitahidi kabisa kuhakikisha kwamba kusudi lake lingetimizwa. (Soma Mwanzo 3:15.) Yehova aliamua kwamba mwanamke wake wa mfano angetokeza “uzao,” au Mwana, ambaye mwishowe angemwangamiza yule mchochezi, Shetani, na hivyo kuondoa madhara yote ambayo amesababisha.—Ebr. 2:14; 1 Yoh. 3:8.

3 Hakuna nguvu zozote mbinguni au duniani ambazo zinaweza kumzuia Mungu asitimize kusudi lake. (Isa. 46:9-11) Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Kwa sababu Yehova anatumia roho yake takatifu. Nguvu hizo ambazo haziwezi kuzuiwa zinatufanya tuwe na uhakika kwamba kusudi la Mungu “hakika litafanikiwa.” (Isa. 55:10, 11) Ni jambo la maana kwetu kuelewa vizuri kabisa jinsi Mungu anavyotimiza kusudi lake na tutende kupatana nalo. Wakati wetu ujao unategemea kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Kwa kuongezea, imani yetu inatiwa nguvu tunapoona jinsi Yehova anavyotumia roho yake takatifu. Acheni sasa tuchunguze jinsi Yehova alivyotumia roho takatifu kutimiza kusudi lake zamani, jinsi anavyoitumia leo, na jinsi atakavyoitumia wakati ujao.

Jinsi Yehova Alivyotumia Roho Takatifu Zamani

4. Yehova amefunua jinsi gani kusudi lake hatua kwa hatua?

4 Katika nyakati za Biblia, Yehova alifunua kusudi lake hatua kwa hatua. Mwanzoni, utambulisho wa Uzao ulioahidiwa ulikuwa “siri takatifu.” (1 Kor. 2:7) Baada ya miaka 2,000 hivi kupita, Yehova alizungumza tena kuhusu uzao. (Soma Mwanzo 12:7; 22:15-18.) Yehova alimpa Abrahamu ahadi ambayo ingetimizwa kwa njia kubwa zaidi. Maneno “kupitia kwa uzao wako” yalionyesha waziwazi kwamba ule Uzao ungekuwa mwanadamu, mzao wa Abrahamu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Shetani alikuwa akisikiliza kwa uangalifu sana habari hizo zilipokuwa zikifunuliwa. Bila shaka, Adui huyo alitaka tu kuharibu au kuvuruga ukoo wa uzao wa Abrahamu na hivyo kuzuia kusudi la Mungu lisitimie. Lakini hangefaulu kufanya hivyo kwa kuwa roho ya Mungu isiyoonekana ilikuwa ikifanya kazi. Jinsi gani?

5, 6. Yehova alitumia jinsi gani roho yake kuwalinda watu mmoja-mmoja wa ukoo ambao ungetokeza ule Uzao?

5 Yehova alitumia roho yake kuwalinda watu mmoja-mmoja wa ukoo ambao ungetokeza ule Uzao. Yehova alimwambia hivi Abramu (Abrahamu): “Mimi ni ngao kwako.” (Mwa. 15:1) Hiyo haikuwa ahadi ya uwongo. Kwa mfano, fikiria jambo lililotukia karibu mwaka wa 1919 K.W.K. Abrahamu na Sara walipokuwa wakaaji wa muda huko Gerari. Bila kujua kwamba Sara alikuwa mke wa Abrahamu, Abimeleki, mfalme wa Gerari alimchukua Sara akikusudia kumfanya awe mke wake. Je, Shetani alikuwa akiongoza mambo bila wao kujua ili kujaribu kumzuia Sara asizae mwana wa Abrahamu? Biblia haisemi. Inasema tu kwamba Yehova aliingilia kati. Alimwonya Abimeleki katika ndoto asimguse Sara.—Mwa. 20:1-18.

6 Yehova hakuwalinda katika pindi hiyo moja tu. Alimkomboa Abrahamu na watu wa familia yake katika pindi nyingine nyingi. (Mwa. 12:14-20; 14:13-20; 26:26-29) Ndiyo sababu mtunga-zaburi aliandika hivi kumhusu Abrahamu na wazao wake: “[Yehova] hakumruhusu binadamu yeyote awapunje, bali aliwakaripia wafalme kwa sababu yao, akisema: ‘Msiwaguse watiwa-mafuta wangu, wala msiwatendee manabii wangu lolote lililo baya.’”—Zab. 105:14, 15.

7. Yehova alilinda jinsi gani taifa la Israeli?

7 Akitumia roho yake, Yehova alilinda taifa la kale la Israeli, ambalo lingetokeza Uzao ulioahidiwa. Kupitia roho yake, Yehova aliwapa Waisraeli Sheria yake, ambayo ililinda ibada ya kweli na kuwalinda Wayahudi wasichafuliwe kiroho, kimaadili, na kimwili. (Kut. 31:18; 2 Kor. 3:3) Katika siku za Waamuzi, roho ya Yehova iliwatia nguvu wanaume fulani wawakomboe Waisraeli kutoka kwa maadui wao. (Amu. 3:9, 10) Kwa karne nyingi mpaka wakati wa kuzaliwa kwa Yesu ambaye ni sehemu ya msingi ya uzao wa Abrahamu, ni wazi kwamba roho takatifu ilitumiwa kulinda Yerusalemu, Bethlehemu, na hekalu—maeneo ambayo yangehusika katika kutimizwa kwa unabii mbalimbali kumhusu Yesu.

8. Ni nini kinachoonyesha kwamba roho takatifu ilihusika moja kwa moja katika maisha na huduma ya Mwana wa Mungu?

8 Roho takatifu ilihusika moja kwa moja katika maisha na huduma ya Yesu. Ikitenda katika tumbo la uzazi la bikira Maria, roho takatifu ilifanya jambo ambalo halijawahi kamwe kufanywa. Ilimwezesha mwanamke asiye mkamilifu abebe mimba ya Mwana mkamilifu, ambaye hakuwa chini ya hukumu ya kifo. (Luka 1:26-31, 34, 35) Baadaye, roho hiyo ilimlinda Yesu akiwa mtoto ili asiuawe kabla ya wakati kufika. (Mt. 2:7, 8, 12, 13) Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi, Mungu alimtia mafuta kwa roho takatifu, akamweka rasmi kuwa mrithi wa kiti cha ufalme cha Daudi na kumwagiza ahubiri. (Luka 1:32, 33; 4:16-21) Roho takatifu ilimwezesha Yesu kuwa na nguvu za kufanya miujiza kama vile, kuponya wagonjwa, kulisha umati wa watu, na kuwafufua wafu. Matendo hayo yenye nguvu yalionyesha baraka ambazo tunatazamia kupata wakati ambapo Yesu atatawala akiwa mfalme.

9, 10. (a) Ingeweza kuonekana wazi jinsi gani kwamba roho takatifu ilikuwa ikitenda kazi juu ya wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza? (b) Ni jambo gani jipya katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova ambalo lilifunuliwa katika karne ya kwanza W.K.?

9 Kuanzia siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Yehova alitumia roho yake kuwatia mafuta wale ambao wangekuwa sehemu ya pili ya uzao wa Abrahamu, hata ingawa wengi wao hawakuwa wazao wa Abrahamu. (Rom. 8:15-17; Gal. 3:29) Ingeweza kuonekana wazi kwamba roho takatifu ilikuwa ikitenda kazi juu ya wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza na iliwawezesha kuhubiri kwa bidii na iliwapa nguvu za kufanya matendo yenye nguvu. (Mdo. 1:8; 2:1-4; 1 Kor. 12:7-11) Kupitia zawadi hizo za kimuujiza, roho takatifu ilifunua jambo jipya katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Yehova hakuwa akitumia tena mpango wa ibada ambao ulikuwapo kwa karne nyingi katika hekalu la Yerusalemu. Sasa alikuwa akitumia kutaniko jipya la Kikristo ambalo lilikuwa limeanzishwa. Tangu wakati huo, Yehova amekuwa akitumia kutaniko hilo la watiwa-mafuta kutimiza kusudi lake.

10 Kulinda, kutia nguvu, na kutia-mafuta, ni njia chache tu ambazo Yehova alitumia roho yake takatifu katika nyakati za Biblia ili kuhakikisha kwamba kusudi lake litatimia. Namna gani katika siku zetu? Yehova anatumia jinsi gani roho yake sasa kutegemeza kusudi lake? Tunahitaji kujua hilo kwa sababu tunataka kutenda kupatana na roho hiyo. Basi, acheni tuchunguze njia nne ambazo Yehova anatumia roho yake leo.

Jinsi Roho Takatifu Inavyofanya Kazi Leo

11. Ni nini kinachoonyesha kwamba roho takatifu inawachochea watu wa Mungu kuwa safi, na unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unashirikiana na roho hiyo?

11 Kwanza, roho takatifu inawachochea watu wa Mungu kuwa safi. Ni lazima wale wanaoshiriki katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova wawe na maadili safi. (Soma 1 Wakorintho 6:9-11.) Watu fulani ambao wanakuwa Wakristo wa kweli, walikuwa na mazoea mapotovu kama vile uasherati, uzinzi, na walifanya ngono za watu wa jinsia moja. Tamaa zinazozaa matendo ya dhambi zinaweza kuwa zimetia mizizi kabisa ndani ya moyo. (Yak. 1:14, 15) Hata hivyo, watu kama hao ‘wameoshwa wakawa safi,’ kuonyesha kwamba wamefanya mabadiliko yanayohitajiwa katika maisha yao ili kumpendeza Mungu. Ni nini kinachomwezesha mtu anayempenda Mungu akatae kabisa kutenda kupatana na tamaa mbaya? Andiko la 1 Wakorintho 6:11 linasema ni “roho ya Mungu wetu.” Unapoendelea kuwa na maadili safi, unaonyesha kwamba unaruhusu roho hiyo iongoze maisha yako.

12. (a) Kulingana na maono ya Ezekieli, Yehova anaongoza jinsi gani tengenezo lake? (b) Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unatenda kupatana na roho?

12 Pili, Yehova anatumia roho yake kuongoza tengenezo lake upande anaotaka liende. Katika maono ya Ezekieli, sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova inafananishwa na gari la kimbingu ambalo haliwezi kuzuiwa na ambalo linasonga mbele ili kutimiza kusudi la Yehova. Ni nini kinachoongoza gari hilo kuelekea upande fulani? Ni roho takatifu. (Eze. 1:20, 21) Kumbuka kwamba tengenezo la Yehova lina sehemu mbili, sehemu moja iko mbinguni na sehemu nyingine iko duniani. Ikiwa sehemu ya kimbingu inaongozwa na roho takatifu, bila shaka sehemu ya kidunia inaongozwa pia na roho takatifu. Unapotii na kufuata kwa ushikamanifu mwongozo unaotolewa na sehemu ya kidunia ya tengenezo la Mungu, unaonyesha kwamba unasonga mbele pamoja na gari la Yehova la kimbingu na unatenda kupatana na roho yake takatifu.—Ebr. 13:17.

13, 14. (a) Ni nani wanaofanyiza “kizazi hiki” kilichotajwa na Yesu? (b) Toa mfano unaoonyesha kwamba Yehova anatumia roho takatifu kufunua kweli za Biblia. (Ona sanduku lenye kichwa “Je, Unaenda Sambamba na Nuru Inayoongezeka?”)

13 Tatu, Yehova anatumia roho takatifu kufunua kweli za Biblia. (Met. 4:18) Kwa miaka mingi, gazeti hili limetumiwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kuwa njia kuu ya kufunua kweli za Biblia hatua kwa hatua. (Mt. 24:45) Kwa mfano, fikiria uelewaji wetu kuhusu wale wanaofanyiza “kizazi hiki” ambacho kilitajwa na Yesu. (Soma Mathayo 24:32-34.) Yesu alikuwa akizungumzia kizazi gani? Habari yenye kichwa “Kuwapo kwa Kristo—Kunamaanisha Nini Kwako?” inaeleza kwamba Yesu hakuwa akizungumza kuhusu waovu, alikuwa akizungumza kuhusu wanafunzi wake ambao baada ya muda mfupi wangetiwa mafuta kwa roho takatifu. * Wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta, wa karne ya kwanza na wa siku zetu, ndio wangeona ishara na pia kutambua maana yake, yaani, ishara ya kwamba Yesu “yuko karibu milangoni.”

14 Maelezo hayo yana maana gani kwetu? Ingawa hatuwezi kupima kwa usahihi urefu wa “kizazi hiki,” ni vizuri kukumbuka mambo fulani kuhusu neno “kizazi”: Kwa kawaida, linamaanisha watu wenye umri mbalimbali ambao maisha yao yanapishana katika kipindi fulani hususa cha wakati; si kipindi kirefu kupita kiasi; na kina mwisho. (Kut. 1:6) Hivyo basi, tunapaswa kuelewa jinsi gani maneno ya Yesu kuhusu “kizazi hiki”? Inaonekana alimaanisha kwamba maisha ya watiwa-mafuta waliokuwapo wakati ishara ilipoanza kuonekana mwaka wa 1914 yangepishana na maisha ya watiwa-mafuta wengine ambao wangeona mwanzo wa dhiki kuu. Kizazi hicho kilikuwa na mwanzo, na bila shaka kitakuwa na mwisho. Utimizo wa sehemu mbalimbali za ile ishara unaonyesha waziwazi kwamba ni lazima ile dhiki iwe karibu. Ukidumisha mtazamo wa uharaka na kuendelea kukesha, unaonyesha kwamba unaenda sambamba na nuru inayoongezeka na unafuata mwongozo wa roho takatifu.—Marko 13:37.

15. Nini kinachoonyesha kwamba roho takatifu ndiyo inayotutia nguvu za kuhubiri habari njema?

15 Nne, roho takatifu inatutia nguvu ili tutangaze habari njema. (Mdo. 1:8) Je, kweli habari njema ingehubiriwa duniani pote bila msaada wa roho takatifu? Hebu fikiria jambo hilo. Huenda wewe ni mmoja kati ya watu waliokuwa na haya sana au wasiwasi, na labda ulisema kwamba ‘Siwezi kamwe kuhubiri nyumba kwa nyumba!’ Hata hivyo, sasa unashiriki kwa bidii katika kazi hiyo. * Mashahidi wengi wa Yehova wameendelea kuhubiri hata ingawa wanapingwa au kuteswa. Roho takatifu ya Mungu ndiyo tu inayoweza kututia nguvu za kushinda vizuizi vikubwa na kutimiza mambo ambayo hatuwezi kutimiza kwa nguvu zetu wenyewe. (Mika 3:8; Mt. 17:20) Ukishiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri, unaonyesha kwamba unashirikiana na roho takatifu.

Jinsi Yehova Atakavyotumia Roho Takatifu Wakati Ujao

16. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawalinda watu wake wakati wa dhiki kuu?

16 Wakati ujao, Yehova atatumia roho yake takatifu katika njia kubwa zaidi ili kutimiza kusudi lake. Kwanza fikiria kuhusu ulinzi. Kama tulivyoona, Yehova alitumia roho yake wakati uliopita kuwalinda watu mmoja-mmoja na vilevile taifa lote la Israeli. Hivyo, tuna kila sababu ya kuamini kwamba atatumia roho hiyohiyo yenye nguvu kuwalinda watu wake wakati wa dhiki kuu inayokuja. Hatuhitaji kukisia-kisia njia ambazo Yehova atatumia hasa kutulinda wakati huo. Badala yake tunaweza kutazamia wakati ujao tukiwa na hakika, tukijua kwamba Yehova hatakosa kamwe kuwaona wale wanaompenda na hawatakosa kamwe msaada wa roho yake takatifu.—2 Nya. 16:9; Zab. 139:7-12.

17. Yehova atatumia jinsi gani roho yake takatifu katika ulimwengu mpya?

17 Yehova atatumia jinsi gani roho yake takatifu katika ulimwengu mpya unaokuja? Ataitumia roho hiyo kuandika vitabu vipya vya kukunjwa ambavyo vitafunguliwa wakati huo. (Ufu. 20:12) Vitabu hivyo vitakuwa na habari gani? Inaonekana kwamba vitakuwa na matakwa mengi ambayo Yehova atataka tutimize katika ile miaka elfu. Je, unatamani kuchunguza habari za vitabu hivyo vya kukunjwa? Tunatazamia kwa hamu sana ulimwengu huo mpya. Hatuwezi kuwazia kamwe jinsi maisha yatakavyokuwa wakati huo uliobarikiwa ambapo Yehova atatumia roho yake takatifu kutimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia na wanadamu watakaoishi humo.

18. Umeazimia kabisa kufanya nini?

18 Acheni tusisahau kamwe kwamba bila shaka kusudi la Yehova linalotimizwa hatua kwa hatua litafanikiwa, kwa sababu anatumia roho yake takatifu, yaani, nguvu zake zisizo na kifani, ili kutimiza kusudi hilo. Kusudi hilo linakuhusu wewe. Kwa hiyo, azimia kabisa kumsihi Yehova akupe roho yake takatifu na utende kupatana na mwongozo wa roho hiyo. (Luka 11:13) Ukifanya hivyo utakuwa na tumaini la kuishi jinsi Yehova alivyokusudia wanadamu waishi, yaani, kuishi milele katika Paradiso duniani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 2008 (15/2/2008), ukurasa wa 21-25.

^ fu. 15 Unaweza kupata mfano wa mtu aliyeshinda tatizo la kuwa na haya sana na mwishowe akawa mhubiri mwenye bidii katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Septemba 15, 1993 (15/9/1993), ukurasa wa 19.

Je, Unakumbuka?

• Yehova alitumia jinsi gani roho yake takatifu katika nyakati za Biblia ili kutimiza kusudi lake?

• Yehova anatumia jinsi gani roho yake leo?

• Yehova atatumia jinsi gani roho yake wakati ujao ili kutimiza kusudi lake?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Je, Unaenda Sambamba na Nuru Inayoongezeka?

Yehova anaendelea kuwaangazia watu wake nuru. Ni marekebisho gani ambayo yamechapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi?

▪ Mfano wa Yesu wa chachu unakazia jambo gani linalofaa kuhusu ukuzi wa kiroho? (Mt. 13:33)—Julai 15, 2008 (15/7/2008), ukurasa wa 19-20.

▪ Wakristo wataacha kupata mwito wa tumaini la kimbingu wakati gani?—Mei 1, 2007 (1/5/2007), ukurasa wa 30-31.

▪ Inamaanisha nini kumwabudu Yehova “kwa roho”? (Yohana 4:24) —Julai 15, 2002, ukurasa wa 15.

▪ Umati mkubwa unatumika katika ua gani? (Ufu. 7:15)—Mei 1, 2002, ukurasa wa 30-31.

▪ Kutenganishwa kwa kondoo na mbuzi kunatukia wakati gani? (Mt. 25:31-33)—Oktoba 15, 1995 (15/10/1995), ukurasa wa 18-28.