Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiruhusu Macho Yako Yaone Mambo Yasiyofaa!

Usiruhusu Macho Yako Yaone Mambo Yasiyofaa!

Usiruhusu Macho Yako Yaone Mambo Yasiyofaa!

“Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa; unihifadhi hai katika njia yako mwenyewe.”—ZAB. 119:37.

1. Macho ni zawadi ya maana kadiri gani?

MACHO yetu ni yenye thamani sana! Kwa macho yetu tunaweza kuona vizuri sana mazingira yetu na rangi mbalimbali. Macho yanatuwezesha kuona mambo mazuri na mambo hatari tunayopaswa kuepuka. Yanatuwezesha kuona vitu vyenye kuvutia, kufurahia maajabu ya uumbaji, na kuona uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu na utukufu wake. (Zab. 8:3, 4; 19:1, 2; 104:24; Rom. 1:20) Macho ni ya maana katika kuwasiliana na ubongo, na hivyo yanatusaidia sana kupata ujuzi kumhusu Yehova na kujenga imani katika yeye.—Yos. 1:8; Zab. 1:2, 3.

2. Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mambo ambayo tunaona, na tunaweza kujifunza nini kutokana na ombi la kusihi sana la mtunga-zaburi?

2 Hata hivyo, mambo tunayoona yanaweza pia kuwa na madhara kwetu. Uhusiano kati ya macho na akili yetu ni wenye nguvu sana hivi kwamba mambo tunayoona kwa macho yetu yanaweza kusitawisha na kuchochea tamaa fulani ndani ya moyo wetu. Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu mpotovu sana unaotawaliwa na Shetani Ibilisi ambao unawachochea watu kutosheleza tamaa zao za kichoyo, tunazungukwa na propaganda na picha nyingi ambazo zinaweza kutupotosha kwa urahisi, hata tukizitazama kwa muda mfupi tu. (1 Yoh. 5:19) Basi, haishangazi kwamba mtunga-zaburi alimsihi sana Mungu hivi: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa; unihifadhi hai katika njia yako mwenyewe.”—Zab. 119:37.

Jinsi Macho Yetu Yanavyoweza Kutupotosha

3-5. Ni masimulizi gani ya Biblia yanayoonyesha hatari ya kuruhusu macho yetu yatushawishi?

3 Ona yale yaliyompata mwanamke wa kwanza, Hawa. Shetani alidai kwamba macho ya mwanamke huyo ‘yangefunguliwa’ ikiwa angekula matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Bila shaka, Hawa alivutiwa kusikia kwamba macho yake ‘yangefunguliwa.’ Tamaa yake ya kula matunda yaliyokatazwa ilichochewa zaidi ‘alipoona kwamba mti huo ulikuwa mzuri kwa chakula na kwamba ulikuwa kitu cha kutamanika kwa macho, ndiyo, mti huo ulikuwa wenye kupendeza kuutazama.’ Hawa alishawishiwa kutotii amri ya Mungu alipoutazama mti huo kwa tamaa. Mume wake, Adamu, pia hakutii, hivyo wanadamu wote wakapata madhara makubwa.—Mwa. 2:17; 3:2-6; Rom. 5:12; Yak. 1:14, 15.

4 Katika siku za Noa, malaika fulani pia walishawishiwa na mambo ambayo waliona. Andiko la Mwanzo 6:2 linasema hivi kuhusu malaika hao: “Wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.” Malaika hao waasi walipowatazama kwa tamaa nyingi mabinti wa wanadamu walichochewa kuwa na tamaa isiyo ya asili ya kufanya ngono nao, kisha wakazaa watoto wenye jeuri. Uovu wa wanadamu wakati huo ulifanya wanadamu wote waharibiwe, isipokuwa Noa na familia yake.—Mwa. 6:4-7, 11, 12.

5 Karne nyingi baadaye, macho ya Mwisraeli anayeitwa Akani yalimshawishi kuiba vitu fulani kutoka katika jiji lililotekwa la Yeriko. Mungu alikuwa ameamuru vitu vyote vya jiji hilo viharibiwe isipokuwa vitu fulani ambavyo vingewekwa katika hazina ya Yehova. Waisraeli walionywa hivi: “Mjiepushe tu na kitu kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa, msije mkawa na tamaa” na kuchukua vitu kutoka katika jiji hilo. Akani alipokosa kutii, Waisraeli walishindwa vitani katika jiji la Ai, na wachache wakauawa. Akani hakukubali kwamba aliiba mpaka alipofunuliwa. Akani alisema: “Nilipoona” vitu hivyo, ‘ndipo nikavitamani, halafu nikavichukua.’ Tamaa yake ya macho ilifanya aangamizwe pamoja na “kila kitu kilichokuwa chake.” (Yos. 6:18, 19; 7:1-26) Akani alitamani moyoni vitu ambavyo hakupaswa kuchukua.

Tunahitaji Kujitia Nidhamu

6, 7. Mara nyingi Shetani anatumia “mbinu” gani ili kutunasa, na watangazaji wa kibiashara wanaitumia jinsi gani?

6 Leo pia, wanadamu wanashawishiwa kama vile Hawa, Akani, na malaika waasi walivyoshawishiwa. Kati ya “mbinu” zote ambazo zimetumiwa na Shetani kuwapotosha wanadamu, mbinu yenye nguvu zaidi ni kuchochea “tamaa ya macho.” (2 Kor. 2:11; 1 Yoh. 2:16) Watangazaji wa kibiashara leo wanajua kwamba sikuzote watu wanavutiwa na mambo ambayo wanaona. Mtaalamu mmoja maarufu wa masoko ya Ulaya anasema hivi: “Macho ndicho kiungo cha mwili chenye kushawishi zaidi. Kwa kawaida, macho yanaongoza viungo vingine vya mwili, na yana nguvu za kutushawishi kutenda mambo ambayo tunajua hayafai.”

7 Haishangazi kwamba watangazaji wa kibiashara wanatuonyesha picha nyingi ambazo zimetungwa kwa werevu ili kuvutia kabisa macho na kuwachochea watu kuwa na tamaa ya kununua vitu au kukubali huduma zao! Mtafiti mmoja huko Marekani aliyechunguza jinsi matangazo ya kibiashara yanavyowavutia watu alisema kwamba “hayakusudiwi kutoa tu habari zinazoeleweka, lakini jambo la maana hata zaidi ni kwamba yanachochea hisia fulani na kumsukuma mtazamaji kutenda.” Picha zenye kusisimua za ngono ni kati ya picha zinazotumiwa mara nyingi katika matangazo hayo. Hivyo, ni jambo la maana sana tuwe waangalifu kuhusu mambo tunayotazama na yale ambayo tunaruhusu yaingie katika akili na moyo wetu.

8. Biblia inakazia jinsi gani uhitaji wa kulinda macho yetu?

8 Tamaa ya macho na ya mwili inaweza pia kuwa na uvutano mbaya juu ya Wakristo wa kweli. Kwa hiyo, Neno la Mungu linatutia moyo tujitie nidhamu kuhusu mambo tunayoona na kutamani. (1 Kor. 9:25, 27; soma 1 Yohana 2:15-17.) Mwanamume mwadilifu Ayubu alitambua kwamba kuna uhusiano wenye nguvu kati ya kuona na kutamani. Alisema hivi: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira?” (Ayu. 31:1) Ayubu hakukataa tu kumgusa mwanamke kwa njia potovu lakini hangeruhusu hata akili yake ifikirie jambo kama hilo. Yesu alikazia kwamba ni lazima tulinde akili zetu kutokana na mawazo mapotovu aliposema hivi: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mt. 5:28.

Mambo Yasiyofaa Ambayo Tunapaswa Kuepuka

9. (a) Kwa nini ni lazima tuwe waangalifu sana hasa tunapotumia Intaneti? (b) Ni nini kinachoweza kutukia tukiona ponografia hata kwa muda mfupi?

9 Katika ulimwengu wa leo, ni jambo la kawaida kwa watu wengi ‘kuendelea kutazama’ ponografia (picha au habari za ngono), hasa kwenye Intaneti. Hatuhitaji kutafuta vituo hivyo kwenye Intaneti, vinatutafuta sisi! Kwa njia gani? Huenda tangazo likatokea ghafula kwenye kompyuta au televisheni likiwa na picha yenye kuvutia sana. Au mara tu unapofungua barua-pepe ambayo inaonekana nzuri kwa nje, huenda picha ya ponografia ikatokea ambayo imekusudiwa kukuvutia sana hivi kwamba inakuwa vigumu kwako kuifunga. Mtu akiiangalia picha hiyo hata kwa muda mfupi tu kabla ya kuifuta, inabaki katika akili yake. Kuona ponografia hata kwa muda mfupi tu kunaweza kuwa na matokeo mabaya sana. Ponografia inaweza kumwacha mtu akiwa na dhamiri chafu na ni vigumu sana kufuta picha hizo chafu kutoka katika akili. Jambo baya hata zaidi ni kwamba mtu ‘anayeendelea kutazama’ kwa makusudi ponografia anaonyesha wazi kwamba bado hajaua tamaa mbaya ndani ya moyo wake.—Soma Waefeso 5:3, 4, 12; Kol. 3:5, 6.

10. Kwa nini ponografia ni hatari hasa kwa watoto, na huenda matokeo yakawa nini wakiitazama?

10 Watoto wanaweza kuvutiwa na ponografia kwa sababu ya udadisi wao wa kiasili. Kutazama ponografia kunaweza kubadili kabisa maoni yao kuhusu ngono. Ripoti moja inasema kwamba hilo linaweza kuwafanya wawe na maoni yaliyopotoka kuhusu ngono, “matatizo ya kuwa na mahusiano mazuri yenye upendo; maoni yasiyofaa kuhusu wanawake; na hata kuwa na zoea la kutazama ponografia ambalo linaweza kuvuruga masomo yao shuleni, na mahusiano pamoja na marafiki na pia familia.” Na baadaye jambo hilo linaweza kuharibu kabisa ndoa yao.

11. Toa mfano unaoonyesha hatari ya kuangalia ponografia.

11 Ndugu mmoja Mkristo aliandika hivi: “Kati ya mazoea yote niliyokuwa nayo kabla ya kuwa Shahidi, kutazama ponografia ndilo zoea ambalo lilikuwa gumu zaidi kwangu kuacha. Bila kutarajia, ninaona picha hizo akilini ninaponusa harufu fulani, ninaposikia muziki fulani, ninapoona jambo fulani, au hata akili yangu inapotanga-tanga. Ni pambano la kila siku ambalo halina mwisho.” Akiwa mtoto, ndugu mwingine aliangalia ponografia katika magazeti ya baba yake mlimwengu wakati ambapo wazazi wake hawakuwa nyumbani. Aliandika hivi: “Picha hizo zilichafua kabisa akili yangu nikiwa mtoto! Hata sasa baada ya miaka 25 kupita, bado ninakumbuka picha hizo. Ingawa ninajitahidi sana kuzisahau, bado ninazikumbuka. Hilo linanifanya nijihisi kuwa na hatia, hata ingawa ninaepuka kuzifikiria.” Ni jambo la hekima kama nini kuepuka hisia hizo zenye kulemea kwa kutoangalia mambo yasiyofaa! Mtu anaweza kufanya hivyo jinsi gani? Anahitaji kujitahidi kabisa ‘kuiteka kila fikira ili kuifanya imtii Kristo.’—2 Kor. 10:5.

12, 13. Ni mambo gani yasiyofaa ambayo Wakristo wanapaswa kuepuka kutazama, na kwa nini?

12 Jambo lingine ‘lisilofaa,’ ambalo tunapaswa kuepuka ni vipindi vya kujifurahisha au burudani ambazo zinawachochea watu kupenda vitu vya kimwili, mambo ya uchawi, jeuri, umwagaji wa damu, na kuua. (Soma Zaburi 101:3.) Yehova amewapa wazazi daraka la kuchagua mambo ambayo yanaweza kutazamwa nyumbani mwao. Bila shaka, hakuna Mkristo wa kweli ambaye anaweza kujihusisha kimakusudi na zoea la kuwasiliana na roho waovu. Hata hivyo, wazazi wanahitaji kujua sinema, vipindi vya mfululizo vya televisheni, michezo ya video, na hata vitabu vyenye vichekesho na vitabu vingine vya watoto ambavyo vinahusu mazoea ya kuwasiliana na roho waovu.—Met. 22:5.

13 Iwe sisi ni vijana au wazee, macho yetu hayapaswi kufurahia michezo ya video yenye jeuri inayoonyesha mauaji ya kikatili. (Soma Zaburi 11:5.) Hatupaswi kukazia akili zetu juu ya jambo lolote ambalo Yehova anakataza. Kumbuka kwamba Shetani analenga fikira zetu. (2 Kor. 11:3) Vilevile, kutumia wakati mwingi sana kufurahia burudani ambazo huenda zikaonekana ni nzuri kunaweza kupoteza wakati wetu wa kuwa na ibada ya familia, kusoma Biblia kila siku, na kutayarisha mikutano.—Flp. 1:9, 10.

Fuata Mfano wa Yesu

14, 15. Tunajifunza jambo gani kutokana na jaribu la tatu ambalo Shetani alimletea Kristo, na Yesu alilishinda jinsi gani?

14 Inasikitisha kwamba katika ulimwengu huu mwovu, hatuwezi kuepuka kutazama mambo fulani yasiyofaa. Hata Yesu alionyeshwa mambo kama hayo. Katika jaribu la tatu la Shetani la kumzuia Yesu asifanye mapenzi ya Mungu, ‘Ibilisi alimchukua, akaenda pamoja naye kwenye mlima mrefu isivyo kawaida, na kumwonyesha falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.’ (Mt. 4:8) Kwa nini Shetani alifanya hivyo? Bila shaka, alitaka kutumia uvutano wenye nguvu wa macho. Kutazama utukufu wa falme zote za ulimwengu kungemchochea Yesu atamani kupata umashuhuri wa ulimwengu. Yesu alifanya nini?

15 Yesu hakukazia akili jaribu hilo lenye kushawishi. Hakuruhusu tamaa mbaya iingie katika moyo wake. Naye hakuhitaji wakati wa kutafakari kuhusu jaribu hilo kutoka kwa Ibilisi ili alikatae. Yesu alimpinga papo hapo. Alimwamuru hivi: “Nenda zako, Shetani!” (Mt. 4:10) Yesu aliendelea kukazia akili uhusiano wake pamoja na Yehova na alijibu kupatana na kusudi lake maishani, yaani, kufanya mapenzi ya Mungu. (Ebr. 10:7) Hivyo, Yesu alifanikiwa kushinda mbinu za werevu za Shetani.

16. Ni mambo gani tunayojifunza kutokana na mfano ambao Yesu aliweka katika kupinga majaribu ya Shetani?

16 Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wa Yesu. Kwanza, tunajifunza kwamba Shetani anaweza kutumia mbinu zake kumnasa mtu yeyote. (Mt. 24:24) Pili, mambo ambayo tunatazama yanaweza kuchochea tamaa za moyo wetu, kwa njia nzuri au mbaya. Tatu, Shetani atatumia “tamaa ya macho” kadiri anavyoweza ili kujaribu kutupotosha. (1 Pet. 5:8) Na nne, sisi pia tunaweza kumpinga Shetani, hasa ikiwa tunachukua hatua ya haraka.—Yak. 4:7; 1 Pet. 2:21.

Endelea Kuwa na Jicho “Rahisi”

17. Kwa nini si jambo la hekima kungoja mpaka tunapokabili jambo fulani lisilofaa ili tuamue hatua ambayo tutachukua?

17 Wakfu wetu kwa Yehova unatia ndani ahadi nzito ya kuepuka mambo yasiyofaa. Tunapoweka nadhiri ya kufanya mapenzi ya Mungu, tunajiunga na mtunga-zaburi aliyesema hivi: “Nimeizuilia mbali miguu yangu kutoka katika kila pito baya, kusudi nipate kulishika neno lako.” (Zab. 119:101) Si jambo la hekima kungoja mpaka tukabili jambo fulani lisilofaa ili tuamue hatua ambayo tutachukua. Tunajua wazi mambo ambayo Maandiko yanakataza. Hatukosi kujua mbinu za Shetani. Yesu alishawishiwa wakati gani abadili mawe yawe mikate? Ilikuwa baada ya kufunga siku 40 mchana na usiku na ‘kuona njaa.’ (Mt. 4:1-4) Shetani anaweza kutambua wakati tunapokuwa dhaifu na tunapoweza kushawishiwa kwa urahisi zaidi. Kwa hiyo, huu ndio wakati wa kufikiria kwa uangalifu mambo hayo. Usikawie kufanya hivyo! Tukikumbuka siku baada ya siku nadhiri yetu ya kujiweka wakfu kwa Yehova, tutaazimia kabisa kuepuka mambo yasiyofaa.—Met. 1:5; 19:20.

18, 19. (a) Eleza tofauti iliyopo kati ya jicho “rahisi” na jicho “bovu.” (b) Kwa nini ni jambo la maana tuendelee kufikiria mambo yaliyo muhimu, na andiko la Wafilipi 4:8 linatoa shauri gani kuhusu hilo?

18 Kila siku, tunakabili mambo mengi zaidi na zaidi yenye kuvutia ambayo yanakengeusha fikira. Basi, ni jambo la maana sana leo kutii shauri la Yesu la kuwa na jicho “rahisi.” (Mt. 6:22, 23) Jicho “rahisi” linakazia kabisa kusudi moja, yaani, kufanya mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, jicho “bovu” ni lenye udanganyifu, tamaa, na linavutiwa na mambo yasiyofaa.

19 Kumbuka kwamba macho yetu yanalisha akili yetu nayo akili yetu inalisha moyo wetu. Kwa hiyo, ni jambo la maana sana kwetu kuendelea kufikiria mambo yaliyo muhimu. (Soma Wafilipi 4:8.) Kwa kweli, na tuendelee kusali kama mtunga-zaburi: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.” Halafu, tunapojitahidi kutenda kulingana na sala hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ‘atatuhifadhi hai katika njia yake mwenyewe.’—Zab. 119:37; Ebr. 10:36.

Tunapaswa Kukumbuka Nini Kuhusu . . .

• uhusiano kati ya macho, akili, na moyo wetu?

• hatari za kutazama ponografia?

• umuhimu wa kuendelea kuwa na jicho “rahisi”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ni mambo gani yasiyofaa ambayo ni lazima Wakristo waepuke kutazama?