Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana—Imarisheni Tamaa Yenu ya Kumtumikia Yehova

Vijana—Imarisheni Tamaa Yenu ya Kumtumikia Yehova

Vijana—Imarisheni Tamaa Yenu ya Kumtumikia Yehova

“Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.”—MHU. 12:1.

1. Katika Israeli watoto walialikwa kufanya nini?

MIAKA 3,500 hivi iliyopita, Musa, nabii wa Yehova aliwaamuru hivi makuhani na wanaume wazee wa Israeli: “Wakutanishe watu, wanaume na wanawake na watoto wadogo . . . , ili wasikilize na ili wajifunze, kwa maana ni lazima wamwogope Yehova Mungu wenu na kuwa waangalifu kuyatimiza maneno yote ya sheria hii.” (Kum. 31:12) Ona kwamba wanaume, wanawake, na watoto waliagizwa wahudhurie mikutano ya ibada. Ndiyo, hata watoto walikuwa kati ya wale walioambiwa wasikilize, wajifunze, na kufuata mwongozo wa Yehova.

2. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba aliwajali vijana katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?

2 Katika karne ya kwanza, Yehova aliendelea kuonyesha kwamba anawajali vijana wanaomwabudu. Kwa mfano, alimwongoza mtume Paulo aandike mashauri ya moja kwa moja kwa vijana katika barua fulani ambazo alituma kwa makutaniko. (Soma Waefeso 6:1; Wakolosai 3:20.) Vijana Wakristo ambao walifuata mashauri hayo walimthamini zaidi Baba yao wa mbinguni mwenye upendo na wakapata baraka zake.

3. Vijana wanaonyesha jinsi gani leo kwamba wanatamani kumtumikia Mungu?

3 Je, leo vijana wanaalikwa kukusanyika ili wamwabudu Yehova? Ndiyo! Kwa hiyo, watu wa Mungu wanafurahi sana kuona watumishi wengi wa Yehova ambao ni vijana ulimwenguni pote wakitii kutoka moyoni himizo hili la Paulo: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Kwa kuongezea, watoto wengi wanashiriki pamoja na wazazi wao katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Na ili kuonyesha kwamba wanampenda sana Yehova kutoka moyoni, kila mwaka maelfu ya vijana wanajitoa ili kubatizwa na hivyo wanafurahia baraka ambazo wanafunzi wa Kristo wanapata.—Mt. 16:24; Marko 10:29, 30.

Kubali Mwaliko Sasa

4. Vijana wanaweza kukubali mwaliko wa kumtumikia Mungu wakiwa na umri gani?

4 Andiko la Mhubiri 12:1 linasema hivi: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” Vijana, mnapaswa kuwa na umri gani ili mkubali mwaliko huo mchangamfu wa kumwabudu na kumtumikia Yehova? Maandiko hayataji umri fulani. Kwa hiyo, usisitesite na kufikiri kwamba umri wako ni mdogo sana hivi kwamba huwezi kumsikiliza na kumtumikia Yehova. Hata uwe una umri gani, unatiwa moyo kuchukua hatua bila kukawia.

5. Wazazi wanaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wao wafanye maendeleo ya kiroho?

5 Wengi wenu mnasaidiwa kufanya maendeleo ya kiroho na mzazi mmoja au wazazi wote wawili. Hivyo, ninyi ni kama Timotheo anayetajwa katika Biblia. Alipokuwa mtoto mchanga, mama yake Eunike, na nyanya yake Loisi walimfundisha maandiko matakatifu. (2 Tim. 3:14, 15) Inaelekea kwamba wazazi wako wanakuzoeza kwa njia kama hiyo kwa kujifunza Biblia pamoja nawe, kusali pamoja nawe, kwenda nawe kwenye mikutano na makusanyiko ya watu wa Mungu, na kushiriki pamoja nawe katika utumishi wa shambani. Kwa kweli, wazazi wako wamepewa daraka la maana sana na Yehova mwenyewe la kukufundisha njia zake. Je, unathamini jinsi wanavyokupenda na kukujali?—Met. 23:22.

6. (a) Kulingana na andiko la Zaburi 110:3, Yehova anapendezwa na ibada ya aina gani? (b) Tutachunguza nini sasa?

6 Hata hivyo, mnapoendelea kukua, Yehova anataka ninyi vijana “mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu,” kama Timotheo alivyofanya. (Rom. 12:2) Mkifanya hivyo, mtashiriki katika utendaji mbalimbali wa kutaniko, si kwa sababu wazazi wenu wanataka mfanye hivyo, bali kwa sababu mnataka kufanya mapenzi ya Mungu. Yehova atafurahi ikiwa mtamtumikia kwa moyo wa kupenda. (Zab. 110:3) Basi, mnaweza kuonyesha jinsi gani kwamba mnataka kuimarisha tamaa yenu ya kumsikiliza Yehova na kufuata mwongozo wake? Tutachunguza njia tatu kuu za kufanya hivyo. Njia hizo ni kujifunza, kusali, na mwenendo. Acheni tuchunguze kila moja ya njia hizo.

Jifunze Kumwona Yehova Kuwa Halisi

7. Yesu aliweka mfano jinsi gani katika kujifunza Maandiko, na ni nini kilichomsaidia kufanya hivyo?

7 Njia ya kwanza ambayo unaonyesha kwamba unataka kuimarisha tamaa yako ya kumtumikia Yehova ni kusoma Biblia kila siku. Unaweza kutosheleza uhitaji wako wa kiroho na kupata ujuzi wa Biblia wenye thamani kwa kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida. (Mt. 5:3) Yesu alituwekea mfano. Pindi moja alipokuwa na umri wa miaka 12, wazazi wake walimpata hekaluni akiwa “ameketi katikati ya walimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” (Luka 2:44-46) Akiwa mtoto, tayari Yesu alikuwa amesitawisha tamaa ya kujua na kuelewa Maandiko. Ni nini kilichomsaidia kufanya hivyo? Bila shaka, mama yake, Maria, na baba yake mlezi, Yosefu, walimsaidia sana. Walikuwa watumishi wa Mungu na walimfundisha Yesu tangu akiwa mtoto mchanga kumhusu Mungu.—Mt. 1:18-20; Luka 2:41, 51.

8. (a) Wazazi wanapaswa kuanza wakati gani kukazia kupenda Neno la Mungu katika mioyo ya watoto wao? (b) Simulia jambo lililoonwa ambalo linathibitisha kwamba ni jambo la maana kuwazoeza watoto tangu wakiwa wachanga.

8 Vivyo hivyo, wazazi wanaomwogopa Mungu leo wanatambua kwamba ni jambo la maana sana kukazia au kusitawisha katika mioyo ya watoto wao tamaa ya kujua kweli za Biblia tangu wakiwa wachanga. (Kum. 6:6-9) Hivyo ndivyo alivyofanya dada mmoja Mkristo anayeitwa Rubi, baada tu ya kumzaa mwana wake wa kwanza, Joseph. Kila siku, alimsomea Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Alipoendelea kukua, alimfundisha kushika akilini maandiko fulani. Je, mazoezi hayo yalimsaidia Joseph? Mara tu alipojua kuzungumza, alianza kusimulia hadithi nyingi za Biblia kwa maneno yake mwenyewe. Na alipokuwa na umri wa miaka mitano, alitoa hotuba yake ya kwanza kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

9. Kwa nini ni jambo la maana kusoma Biblia na kutafakari mambo unayosoma?

9 Enyi vijana, ikiwa mnataka kufanya maendeleo ya kiroho, mnapaswa kuwa na zoea la kusoma Biblia miaka yenu yote ya ujana na hata mnapokuwa watu wazima. (Zab. 71:17) Kwa nini kusoma Biblia kutawasaidia kufanya maendeleo? Ona jambo ambalo Yesu alisema katika sala kwa Baba yake: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli.” (Yoh. 17:3) Bila shaka, kadiri unavyoendelea kupata ujuzi zaidi kumhusu Yehova, ndivyo atakavyokuwa halisi zaidi kwako na hilo litakuchochea umpende zaidi. (Ebr. 11:27) Hivyo basi, kila mara unaposoma sehemu fulani katika Biblia, tumia nafasi hiyo kujifunza mengi kumhusu Yehova. Jiulize hivi: ‘Simulizi hili linanifundisha nini kumhusu Yehova akiwa halisi? Andiko hili la Biblia linanionyesha jinsi gani kwamba Yehova ananipenda na kunijali?’ Ukitenga wakati wa kutafakari maswali kama hayo, utajifunza jinsi Yehova anavyofikiri na kuhisi, na utajua mambo anayotaka ufanye. (Soma Methali 2:1-5.) Kama kijana Timotheo, ‘utashawishiwa kuamini’ mambo unayojifunza katika Maandiko, na utachochewa kumwabudu Yehova kwa moyo wa kupenda.—2 Tim. 3:14.

Jinsi Sala Inavyokusaidia Kumpenda Yehova Zaidi

10, 11. Sala inakusaidia jinsi gani kuimarisha tamaa yako ya kumtumikia Mungu?

10 Njia ya pili ambayo unaweza kuimarisha tamaa yako ya kumtumikia Yehova kwa moyo wote ni kupitia sala zako. Tunasoma hivi katika Zaburi 65:2: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.” Hata wakati ambapo Waisraeli walikuwa katika agano pamoja na Mungu, watu wa mataifa mengine ambao walikuja kwenye hekalu la Yehova wangeweza kusali kwake. (1 Fal. 8:41, 42) Mungu hana ubaguzi. Wale wanaotii amri zake wana hakika kwamba atawasikiliza. (Met. 15:8) Bila shaka, “watu wote wenye mwili” wanatia ndani ninyi vijana.

11 Unajua kwamba msingi wa urafiki wa kweli ni mawasiliano mazuri. Inaelekea kwamba unafurahia kuwaambia marafiki wa karibu mawazo, mahangaiko, na hisia zako. Vivyo hivyo, unawasiliana na Muumba wako Mkuu unaposali kutoka moyoni. (Flp. 4:6, 7) Mweleze Yehova hisia zako za moyoni kana kwamba unazungumza na mzazi mwenye upendo au rafiki wa karibu. Kwa kweli, kuna uhusiano mkubwa kati ya jinsi unavyosali na jinsi unavyohisi kumhusu Yehova. Utaona kwamba kadiri urafiki wako pamoja na Yehova unavyokuwa wa karibu zaidi, ndivyo sala zako zitakavyokuwa na maana zaidi.

12. (a) Kwa nini sala inayotoka moyoni inahusisha mengi zaidi ya maneno tu? (b) Ni nini kitakachokusaidia kutambua kwamba Yehova yuko karibu nawe?

12 Hata hivyo, kumbuka kwamba sala inayotoka moyoni inahusisha mengi zaidi ya maneno tu. Inatia ndani hisia zako za ndani kabisa. Unaposali, mwambie Yehova jinsi unavyompenda kikweli, jinsi unavyomheshimu sana, na jinsi unavyomtegemea kabisa. Unapoona jinsi Yehova anavyojibu sala zako, utatambua waziwazi kwamba “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia.” (Zab. 145:18) Ndiyo, Yehova atakukaribia, atakutia nguvu ili umpinge Ibilisi na kufanya maamuzi yanayofaa maishani.—Soma Yakobo 4:7, 8.

13. (a) Dada mmoja alifaidika jinsi gani kwa sababu ya kuwa rafiki ya Mungu? (b) Urafiki pamoja na Mungu unakusaidia jinsi gani unaposhinikizwa na marafiki?

13 Fikiria jinsi Cherie alivyotiwa nguvu kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Alipokuwa katika shule ya sekondari, alipewa zawadi nyingi kwa sababu alifanya vizuri katika masomo na michezo. Alipomaliza shule, alipewa nafasi ya kulipiwa masomo ya chuo kikuu. Cherie anasema hivi: “Nafasi hiyo ilikuwa yenye kushawishi sana, na walimu wa michezo na wanafunzi wenzangu walinishinikiza sana niikubali.” Hata hivyo, alitambua kwamba ikiwa angeendelea na elimu ya juu angelazimika kutumia wakati mwingi zaidi akisoma na kujitayarisha kwa ajili ya mashindano ya michezo na hangekuwa na wakati wa kutosha wa kumtumikia Yehova. Cherie alifanya nini? Anasema hivi: “Baada ya kusali kwa Yehova, nilikataa nafasi hiyo ya kulipiwa masomo na nikaanza kutumika nikiwa painia wa kawaida.” Kufikia sasa, amekuwa painia kwa miaka mitano. Anasema hivi: “Sijuti kamwe. Ninafurahi kujua kwamba nilifanya uamuzi ambao unampendeza Yehova. Kwa kweli, ukitanguliza Ufalme wa Mungu, utaongezewa vitu vingine vyote.”—Mt. 6:33.

Mwenendo Mzuri Unaonyesha Kwamba Uko “Safi Moyoni”

14. Kwa nini mwenendo wako mzuri ni jambo la maana machoni pa Yehova?

14 Njia ya tatu ya kuonyesha kwamba unamtumikia Yehova kwa moyo wa kupenda ni kupitia mwenendo wako. Yehova anawabariki vijana wanaoendelea kuwa na maadili safi. (Soma Zaburi 24:3-5.) Kijana Samweli alikataa kuiga mwenendo mpotovu wa wana wa Kuhani Mkuu Eli. Wengine waliona mwenendo mzuri wa Samweli. Simulizi hilo la Biblia linasema: “Na wakati huo wote mvulana Samweli alikuwa akiendelea kukua na kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.”—1 Sam. 2:26.

15. Ni sababu gani zinazofanya udumishe mwenendo mzuri?

15 Tunaishi katika ulimwengu ambao umejaa watu wanaojipenda wenyewe, wenye majivuno, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wakali, wenye kujivuna kwa kiburi, na wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu. Hizo ni kati ya sifa mbaya ambazo Paulo alitaja. (2 Tim. 3:1-5) Kwa hiyo, inaweza kuwa vigumu sana kwako kuendelea kudumisha mwenendo mzuri unapozungukwa na mazingira hayo maovu. Hata hivyo, kila mara unapofanya yaliyo sawa na kuepuka mwenendo usiompendeza Mungu, unathibitisha kwamba unamuunga mkono Yehova katika lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. (Ayu. 2:3, 4) Pia, unaridhika moyoni unapojua kwamba unakubali mwaliko huu wenye upendo wa Yehova: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Met. 27:11) Zaidi ya hayo, kujua kwamba una kibali cha Yehova kutaimarisha tamaa yako ya kumtumikia.

16. Dada mmoja alifanya nini na kuufanya moyo wa Yehova ushangilie?

16 Dada mmoja Mkristo anayeitwa Carol alishikamana na viwango vya Biblia shuleni alipokuwa kijana, na wengine waliona mwenendo wake mzuri. Ni nini kilichotukia? Carol alidhihakiwa na wanafunzi wenzake kwa sababu dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia haikumruhusu kushiriki katika sherehe za sikukuu na kuadhimisha sikukuu za uzalendo. Katika pindi hizo, nyakati nyingine alipata nafasi ya kuwaeleza wengine kuhusu imani yake. Baada ya miaka mingi kupita, Carol alipokea kadi kutoka kwa mwanafunzi mwenzake wa zamani ambaye aliandika hivi: “Sikuzote nimetamani kuwasiliana nawe ili nikushukuru. Wengine waliona mwenendo wako mzuri, mfano wako ukiwa kijana Mkristo, na msimamo wako thabiti kuhusu sikukuu. Wewe ndiye Shahidi wa kwanza wa Yehova ambaye nilikutana naye.” Mfano mzuri wa Carol ulimchochea sana mwanafunzi mwenzake hivi kwamba baadaye alianza kujifunza Biblia. Katika kadi aliyomtumia Carol, aliandika kwamba sasa yeye ni Shahidi aliyebatizwa kwa miaka zaidi ya 40! Kama Carol, ninyi vijana ambao mnashikamana na kanuni za Biblia leo mnaweza kuwachochea watu wenye mioyo minyoofu wamjue Yehova.

Vijana Wanaomsifu Yehova

17, 18. (a) Unahisi namna gani kuhusu vijana walio katika kutaniko lenu? (b) Vijana wanaomwogopa Yehova watapata nini wakati ujao?

17 Sisi sote tulio katika tengenezo la Yehova la ulimwenguni pote tunasisimuka kuona maelfu ya vijana wenye bidii ambao wanashiriki katika ibada ya kweli! Vijana hao wanaimarisha tamaa yao ya kumwabudu Yehova kwa kusoma Biblia kila siku, kusali, na kujiendesha kulingana na mapenzi ya Mungu. Vijana hao wanaoweka mfano mzuri wanafanya wazazi wao wafurahi na pia wanawafurahisha watu wote wa Yehova.—Met. 23:24, 25.

18 Wakati ujao, vijana waaminifu watakuwa kati ya watu ambao wataokoka na kuingia katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. (Ufu. 7:9, 14) Wakati huo, watapata baraka nyingi sana na kuendelea kumthamini Yehova, nao watapata nafasi ya kumsifu mpaka wakati usio na kipimo.—Zab. 148:12, 13.

Je, Unaweza Kueleza?

• Vijana wanaweza kushiriki jinsi gani katika ibada ya kweli leo?

• Ili ufaidike na usomaji wa Biblia, kwa nini ni jambo la maana kutafakari?

• Sala inakusaidia jinsi gani kumkaribia Yehova?

• Mwenendo mzuri wa Mkristo unaweza kuwa na matokeo gani mazuri?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Je, una zoea la kusoma Biblia kila siku?