Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anataka Uwe “Salama Salimini”

Yehova Anataka Uwe “Salama Salimini”

Yehova Anataka Uwe “Salama Salimini”

TUKIO hatari zaidi katika historia litakapotokea, Mungu Mweza-Yote atahakikisha kwamba watu wote wenye kibali chake ‘wataokoka.’ (Yoe. 2:32) Lakini kwa kweli Yehova amekuwa akiwalinda watu wasipate madhara. Kwa kuwa ‘kwake yeye iko chemchemi ya uzima,’ anawaona wanadamu wote kuwa wenye thamani na wanastahili kulindwa.—Zab. 36:9.

Watumishi waaminifu wa zamani wa Mungu walithamini pia uhai kama yeye. Andiko la Mwanzo 33:18 linasema kwamba Yakobo na familia yake walimaliza safari hatari wakiwa “salama salimini.” Yakobo alimtegemea Yehova amlinde, lakini pia alichukua hatua zinazofaa ili kuwalinda wote waliokuwa wakisafiri pamoja naye. (Mwa. 32:7, 8; 33:14, 15) Ukitumia kanuni za Biblia, unaweza kuongeza usalama wako na wa wengine. Acheni tuone jinsi kweli hii inavyowahusu wale wanaojenga Majumba ya Ufalme na miradi mingine kama hiyo na wale wanaotoa misaada wakati wa misiba.

Usalama Chini ya Sheria ya Musa

Sheria ya Musa ilikuwa na matakwa ya usalama ambayo watu wa Mungu walipaswa kufuata. Kwa mfano, Mwisraeli aliyejenga nyumba alipaswa kujenga ukuta mfupi katika ukingo wa dari. Kwa sababu mara nyingi watu walikaa juu ya dari zilizo tambarare za nyumba zao, ukuta huo wa ukingoni uliwazuia kuanguka chini. (1 Sam. 9:26; Mt. 24:17) Ikiwa mtu angeanguka kwa sababu mjenzi hakufuata sheria hiyo ya usalama, Yehova aliona kwamba mwenye nyumba hiyo alikuwa na hatia ya damu.—Kum. 22:8.

Sheria ilitoa pia adhabu kwa wanyama wa kufugwa ambao waliwaumiza watu. Ikiwa ng’ombe-dume alimpiga mtu kwa pembe na kumuua, mwenye ng’ombe-dume huyo alihitaji kumuua ili kuwalinda watu wengine. Alipata hasara kubwa kwa kumuua mnyama huyo kwa sababu hangeweza kula nyama yake wala kuwauzia wengine ili wale. Lakini namna gani ikiwa baada ya ng’ombe-dume kumuumiza mtu, mwenyewe hakumfunga mnyama huyo? Ni nini kingetukia? Ikiwa ng’ombe-dume huyo baadaye alimuua mtu mwingine, basi ng’ombe huyo pamoja na mwenyewe wangeuawa. Sheria hiyo ilimchochea mtu yeyote mwenye tabia ya kutoangalia wanyama wake awe mwangalifu.—Kut. 21:28, 29.

Sheria pia iliwatia watu moyo watumie vizuri vifaa vya kazi. Waisraeli wengi walitumia shoka kupasua kuni. Ikiwa kichwa cha shoka kingechomoka ghafula kutoka kwenye mpini wake na kumuua mtu aliyesimama kando, mtu aliyekuwa akikata kuni alihitaji kukimbilia jiji la makimbilio. Alipaswa kukaa katika jiji hilo mpaka kifo cha kuhani mkuu, hilo lingemaanisha kwamba muuaji ambaye si wa kukusudia angekaa mbali na familia yake na nyumba yake kwa miaka mingi. Mpango huo ulifundisha taifa hilo kwamba Yehova anaona uhai kuwa mtakatifu. Mtu aliyekuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu uhai aliweka vifaa vyake katika hali nzuri na kuvitumia kwa njia salama.—Hes. 35:25; Kum. 19:4-6.

Kupitia sheria kama hizo, Yehova alionyesha wazi kwamba aliwataka watu wake wadumishe viwango vya usalama ndani na nje ya nyumba zao. Watu waliowaua au kuwaumiza wengine, hata bila kukusudia, walihitaji kutoa hesabu kwake. Maoni ya Yehova kuhusu usalama hayajabadilika. (Mal. 3:6) Bado anataka watu waepuke kujiumiza wenyewe na kuwaumiza wengine. Ndivyo anavyotaka hasa wakati tunapojenga na kutunza majengo yaliyowekwa wakfu kwa ajili ya ibada yake ya kweli.

Usalama Kwenye Miradi ya Ujenzi

Tunaona kujenga na kutunza Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya ofisi za tawi kuwa pendeleo kubwa. Ndivyo ilivyo na kazi tunayofanya ya kutoa misaada wakati wa misiba. Nyakati zote, tunataka kufanya kazi yetu kwa ustadi kwa sababu tusipokuwa waangalifu, hata tunapofanya kazi ndogo, tunaweza kujiumiza wenyewe na kuwaumiza wengine. (Mhu. 10:9) Kwa kweli, tukisitawisha mazoea ya kufanya kazi kwa njia salama, tunaweza kuepuka madhara.

Biblia inasema hivi: “Uzuri wa vijana ni nguvu zao, na utukufu wa wazee ni kichwa chao chenye mvi.” (Met. 20:29) Nguvu za ujana zinahitajiwa ili kufanya kazi inayohitaji nguvu nyingi. Lakini wafanyakazi waliozeeka, ambao wana uzoefu mkubwa katika kazi za ufundi, wanafanya kazi nzuri zaidi ya kurembesha majengo wakitumia mikono na vifaa vyao. Wakati fulani, wale ambao sasa wamezeeka walitumia nguvu zao za ujana kufanya kazi iliyohitaji nguvu nyingi. Ikiwa umejitolea hivi karibuni, tazama jinsi wafanyakazi wenye uzoefu wanavyofanya kazi, na ufuate maagizo yao. Ikiwa unataka kujifunza, ndugu wenye uzoefu katika ujenzi watakufundisha mambo mengi. Watakufundisha mambo kama vile njia salama ya kushughulikia vitu hatari na jinsi ya kuinua mizigo mizito. Hivyo utafanya kazi vizuri zaidi, kwa njia salama, na kwa furaha.

Ni lazima sikuzote wale wanaofanya kazi mahali pa ujenzi wawe macho. Hali zinabadilika kwa ghafula. Mahali ambapo hapakuwa na shimo, huenda sasa pamechimbwa shimo. Huenda wafanyakazi wenzako wakawa wamehamisha ngazi, ubao wa kukanyagia, au ndoo ya rangi. Ukikengeushwa fikira, unaweza kuumia kwa urahisi. Kwa kawaida, sheria za usalama zinasema kwamba wafanyakazi walio mahali pa ujenzi wanapaswa kutumia vifaa vya kujilinda. Miwani ya usalama, kofia ngumu, na viatu vinavyofaa vinaweza kukulinda na hatari nyingi mahali pa ujenzi. Lakini vitu hivyo vitakulinda tu ikiwa utavitunza na kuvivaa.

Ingawa inaonekana kwamba ni rahisi kutumia vifaa vingi vya kazi, ili mtu avitumie kwa njia salama na kwa ustadi anahitaji kufundishwa na kuzoezwa kuvitumia. Ikiwa huna uzoefu wa kutumia kifaa fulani unachohitaji, mwambie ndugu anayesimamia kazi akufundishe. Atapanga ili upewe mazoezi yanayofaa. Ni jambo la maana kuwa na sifa ya kiasi, yaani, kutambua mambo unayoweza kufanya na yale usiyoweza kufanya. Kwa kweli, ili uepuke kujiumiza mwenyewe na kuwaumiza wengine katika ujenzi ni lazima uwe na sifa hiyo.—Met. 11:2.

Watu wengi ambao wanaumia kwenye ujenzi ni wale wanaoanguka. Kabla ya kupanda juu ya ngazi, hakikisha kwamba ngazi hiyo ina vifaa vyote vya usalama na viko katika hali nzuri. Ikiwa mnafanya kazi mkiwa juu ya jukwaa au juu ya paa, huenda mkahitaji kujifunga mishipi ya usalama au kujenga vyuma vya ukingoni vya kuwazuia msianguke. Muulize msimamizi wa kazi maswali yoyote kuhusu kufanya kazi sehemu za juu. *

Kadiri idadi ya wale wanaomtumikia Yehova inavyoongezeka ulimwenguni pote, ndivyo kunavyokuwa na uhitaji zaidi wa kujenga Majumba ya Ufalme na majengo mengine yanayotumiwa kuendeleza ibada ya kweli. Wale wanaosimamia kazi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme na miradi mingine kama hiyo wamepewa daraka la kuwalinda kondoo wenye thamani wa Yehova ambao wanafanya kazi chini ya mwongozo wao. (Isa. 32:1, 2) Ikiwa una pendeleo la kuwaongoza akina ndugu na dada katika mradi wa ujenzi, usisahau kamwe kwamba usalama ni jambo la maana sana. Hakikisha kwamba eneo la ujenzi liko safi na vitu visivyohitajiwa vimeondolewa. Waeleze kwa fadhili lakini kwa uthabiti wale wanaohitaji kukumbushwa kuhusu jinsi ya kufanya kazi kwa usalama. Usiruhusu wafanyakazi wenye umri mdogo au wasio na uzoefu kufanya kazi katika sehemu hatari. Tambua hatari ambazo wafanyakazi watakabili, na uwatayarishe kufanya kazi kwa njia salama. Kumbuka kwamba kusudi letu ni kumaliza mradi huo bila mtu yeyote kuumia.

Daraka Linalotimizwa na Upendo

Kujenga Majumba ya Ufalme na majengo mengine yanayotumiwa katika ibada ya kweli kunatia ndani kufanya kazi ambazo zinaweza kuwa hatari. Kwa hiyo, ni lazima wale wanaoshiriki katika miradi hiyo wawe waangalifu. Lakini ukiheshimu kanuni za Biblia, ukitii sheria za kazi, na kutumia busara, unaweza kuepuka hatari na kuwalinda wafanyakazi wenzako kutokana na madhara.

Ni nini kinachotuchochea tukazie sana mambo ya usalama? Ni upendo. Ndiyo, upendo kwa ajili ya Yehova unatuchochea kuthamini uhai, kama anavyouthamini. Na kuwapenda watu kunatuzuia tusiwe watu wasiojali na kutofanya jambo lolote linaloweza kuwaumiza. (Mt. 22:37-39) Kwa hiyo, acheni tufanye yote tunayoweza ili kuhakikisha kwamba wale wanaoshiriki katika miradi yetu ya ujenzi wako “salama salimini.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Ona sanduku lenye kichwa “Kutumia Ngazi kwa Njia Salama,” kwenye ukurasa wa 30.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 30]

Kutumia Ngazi kwa Njia Salama

Katika mwaka fulani hivi karibuni, wafanyakazi zaidi ya 160,000 walianguka kutoka kwenye ngazi na kuumia nchini Marekani. Kwa kuongezea, wafanyakazi 150 hivi walianguka na kufa. Miongozo ifuatayo inaweza kukusaidia kuepuka kuanguka kutoka kwenye ngazi popote pale unapoishi na kufanya kazi.

◇ Usitumie ngazi ambayo si thabiti au iliyoharibika, na usiirekebishe ngazi kama hiyo. Iharibu.

◇ Ngazi zote zina kiwango cha uzito ambao zinaweza kustahimili. Hakikisha kwamba uzito wako pamoja na wa vifaa vyako vya kazi hauzidi uzito ambao ngazi unayotumia inaweza kustahimili.

◇ Iweke ngazi yako mahali tambarare ambapo ni pagumu. Usiiweke juu ya sehemu ambayo si thabiti, kama vile kwenye jukwaa la kufanyia kazi au juu ya ndoo na masanduku.

◇ Sikuzote shuka uso wako ukiwa umeelekeana na ngazi.

◇ Usisimame au kuketi juu ya vipandio viwili vya juu kabisa vya ngazi ya aina yoyote.

◇ Ngazi inapotumiwa kupanda au kushuka kutoka kwenye paa, inapaswa kupita urefu wa ukuta huo kwa mita moja hivi. Izuie miguu ya ngazi kuteleza kwa kuifunga kwa kamba au kupigilia ubao mbele yake. Ikiwa huwezi kuifunga ngazi kwa njia hizo, mwombe mtu fulani aishikilie unapofanya kazi ukiwa umeipanda. Funga vizuri sehemu ya juu ya ngazi ili isiteleze na kuanguka upande wa kulia au wa kushoto.

◇ Usiweke mbao kwenye vipandio vya ngazi kama jukwaa la kufanyia kazi.

◇ Ngazi inaweza kuanguka ikiwa utanyoosha sana mikono na miguu yako wakati unapofanya kazi sehemu iliyo juu. Usijinyooshe kupita kiasi kwa njia hiyo kwa kuwa ni hatari. Isogeze ngazi mara kwa mara inapohitajika ili iwe karibu na mahali unapofanyia kazi.

◇ Ikiwa ni lazima ufanye kazi ukiwa umepanda juu ya ngazi ambayo iko mbele ya mlango uliofungwa, weka ishara ya kuonya kwenye mlango huo na uufunge kabisa. Ikiwa huwezi kuufunga kabisa mlango huo, weka mtu ambaye atawazuia watu kupitia kwenye mlango huo.

◇ Mtu mmoja tu ndiye anayepaswa kupanda juu ya ngazi isipokuwa iwe ngazi hiyo imekusudiwa kutumiwa na wafanyakazi wawili. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 33 Orodha yenye mambo zaidi ya kukumbuka unapofanya kazi kwa kutumia ngazi iko katika gazeti la Amkeni! la Agosti 8, 1999 (8/8/1999), ukurasa wa 22-24.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Sheria ya Musa iliamuru kwamba kuta fupi zijengwe kwenye kingo za dari zilizo tambarare