Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Akina Ndugu—Pandeni kwa Roho na Mjitahidi Kufikia Mapendeleo!

Akina Ndugu—Pandeni kwa Roho na Mjitahidi Kufikia Mapendeleo!

Akina Ndugu—Pandeni kwa Roho na Mjitahidi Kufikia Mapendeleo!

“Yeye anayepanda kwa roho atavuna uzima wa milele.”—GAL. 6:8.

1, 2. Andiko la Mathayo 9:37, 38 linaendelea kutimizwa jinsi gani, na hilo linatokeza uhitaji gani katika makutaniko?

UNASHUHUDIA sasa matukio ambayo yatakumbukwa kwa umilele wote! Kazi iliyotabiriwa na Yesu Kristo sasa inatimizwa kikamili. Yesu alisema hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Leo, Yehova Mungu anajibu sala hizo kwa njia ya pekee sana. Katika mwaka wa utumishi wa 2009, hesabu ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote iliongezeka kwa 2,031, na hivyo kufikia 105,298. Kwa wastani, watu 757 walibatizwa kila siku!

2 Kwa sababu ya ongezeko hilo, ndugu wengi wenye sifa za kustahili wanahitajiwa ili kuongoza katika kufundisha na kufanya uchungaji katika makutaniko. (Efe. 4:11) Kwa makumi ya miaka, Yehova ametokeza wanaume wenye sifa za kustahili ili watosheleze mahitaji ya kondoo wake, na tuna hakika kwamba ataendelea kufanya hivyo. Unabii ulioandikwa katika Mika 5:5 unatuhakikishia kwamba katika siku za mwisho, watu wa Yehova watakuwa na “wachungaji saba” na “watawala wadogo wanane,” ambao wanafananisha hesabu kubwa ya wanaume wenye uwezo wanaoongoza kati yao.

3. Eleza maana ya ‘kupanda kwa roho.’

3 Ikiwa wewe ni ndugu aliyebatizwa ambaye ni Shahidi wa Yehova, ni nini kinachoweza kukusaidia kutaka kufikia mapendeleo ya utumishi? Jambo kuu ni kwamba unapaswa ‘kupanda kwa roho.’ (Gal. 6:8) Kufanya hivyo kunatia ndani kuishi kwa njia ambayo inaruhusu roho takatifu ya Mungu itende kazi kwa uhuru katika maisha yako. Azimia ‘kutopanda kwa mwili.’ Epuka kuruhusu mambo kama vile anasa, starehe, na tafrija yapunguze tamaa yako ya kujitolea kumtumikia Mungu. Wakristo wote wanapaswa ‘kupanda kwa roho,’ na baada ya muda, wanaume wanaofanya hivyo huenda wakatimiza sifa za kustahili kupata mapendeleo katika kutaniko. Kwa sababu leo kuna uhitaji mkubwa wa watumishi wa huduma na wazee, habari hii inaelekezwa hasa kwa wanaume Wakristo. Kwa hiyo, akina ndugu, tunawatia moyo msali na mfikirie kwa uzito habari hii.

Jitahidi Kufikia Kazi Njema

4, 5. (a) Wanaume waliobatizwa wanahimizwa wajitahidi kufikia mapendeleo gani katika kutaniko? (b) Ndugu anajitahidi kufikia mapendeleo jinsi gani?

4 Mwanamume Mkristo hawezi kuwa mwangalizi bila kufanya bidii. Ni lazima ajitahidi kufikia ‘kazi hiyo njema.’ (1 Tim. 3:1) Hilo linatia ndani kuwatumikia waamini wenzetu kwa kuwatimizia kwa unyoofu mahitaji yao. (Soma Isaya 32:1, 2.) Mwanamume anayejitahidi kufikia mapendeleo akiwa na nia nzuri hajitakii makuu. Badala yake, ana tamaa kubwa isiyo ya kichoyo ya kuwasaidia wengine.

5 Ndugu anatimiza sifa za kustahili kuwa mtumishi wa huduma na kufikia cheo cha mwangalizi kwa kujitahidi kutimiza sifa zinazoonyeshwa katika Maandiko. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9) Ikiwa wewe ni ndugu aliyejiweka wakfu, jiulize hivi: ‘Je, ninashiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri, na ninawasaidia wengine kufanya hivyo? Je, ninawajenga waabudu wenzangu kwa kupendezwa kwa unyoofu na hali yao njema? Je, ninajulikana kuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu? Je, ninaboresha zaidi maelezo yangu? Je, ninashughulikia kwa bidii migawo ninayopewa na wazee?’ (2 Tim. 4:5) Maswali au maulizo kama hayo yanastahili kufikiriwa kwa uzito.

6. Ni jambo gani kuu linalohitajiwa ili kutimiza sifa za kustahili mapendeleo katika kutaniko?

6 Njia nyingine ya kutimiza sifa za kustahili kupata mapendeleo katika kutaniko ni ‘kufanywa kuwa na uwezo katika mtu tuliye kwa ndani tukiwa na nguvu kupitia roho ya Mungu.’ (Efe. 3:16) Kuwa mtumishi wa huduma au mzee katika kutaniko la Kikristo hakumaanishi kuchaguliwa tu kwa ajili ya cheo fulani. Mtu anaweza kufikia pendeleo hilo kupitia tu ukuzi wa kiroho. Mtu anakua kiroho jinsi gani? Njia moja ambayo unaweza kufanya hivyo ni ‘kuendelea kutembea kwa roho’ na kusitawisha tunda lake. (Gal. 5:16, 22, 23) Unapoonyesha kwamba una sifa za kiroho zinazohitajiwa ili kushughulikia mapendeleo zaidi na ukifuata mashauri unayopewa kuhusu jinsi unavyoweza kufanya vizuri zaidi, ‘maendeleo yako yatakuwa wazi kwa watu wote.’—1 Tim. 4:15.

Roho ya Kujidhabihu Inahitajiwa

7. Kuwatumikia wengine kunatia ndani nini?

7 Kuwatumikia wengine kunatia ndani kujitahidi kwa bidii na kunahitaji roho ya kujidhabihu. Kwa sababu waangalizi Wakristo ni wachungaji wa kiroho, wanapaswa kuhangaikia sana matatizo ya kundi. Ona jinsi madaraka ya kazi ya uchungaji yalivyokuwa na uvutano juu ya mtume Paulo. Aliwaambia hivi waamini wenzake huko Korintho: “Kutokana na dhiki nyingi na maumivu makali ya moyo niliwaandikia ninyi kwa machozi mengi, si ili mhuzunishwe, bali ili muujue upendo nilio nao hasa zaidi kwa ajili yenu.” (2 Kor. 2:4) Ni wazi kwamba Paulo alijitoa kwa moyo wake wote katika kazi yake.

8, 9. Toa mifano inayoonyesha jinsi wanaume katika Biblia walivyotimiza mahitaji ya wengine.

8 Sikuzote roho ya kujidhabihu imekuwa alama inayowatambulisha wanaume wanaowatumikia watumishi wa Yehova. Kwa mfano, hatuwezi kamwe kuwazia Noa akiwaambia wengine katika familia yake: ‘Mnijulishe kazi ya kujenga safina itakapokwisha ili nijiunge nanyi.’ Musa hakuwaambia Waisraeli huko Misri hivi: ‘Nitakutana nanyi kwenye Bahari Nyekundu. Mjitahidi kadiri mnavyoweza kufika huko.’ Yoshua hakusema kamwe hivi: ‘Mnijulishe wakati kuta za Yeriko zitakapoanguka.’ Naye Isaya hakumwelekezea kidole mtu mwingine na kusema: ‘Yule pale! Mtume yeye.’—Isa. 6:8.

9 Yesu Kristo ndiye kielelezo chetu kikuu zaidi cha mwanamume ambaye aliruhusu roho ya Mungu imchochee. Alikubali kwa kupenda mgawo wake wa kutumikia akiwa Mkombozi wa wanadamu. (Yoh. 3:16) Je, upendo wa Yesu wa kujidhabihu haupaswi kutuchochea kufanya vivyo hivyo? Alipoeleza hisia zake kwa ajili ya kundi, mzee mmoja ambaye ametumikia kwa muda mrefu alisema hivi: “Maneno ya Yesu kwa Petro—chunga kondoo wangu wadogo—yananichochea sana. Kwa miaka mingi, nimethamini jinsi maneno machache tu ya upendo au tendo moja la fadhili linavyoweza kumtia moyo mtu mwingine. Ninafurahia sana kazi ya uchungaji.”—Yoh. 21:16.

10. Ni nini kinachoweza kuwachochea wanaume Wakristo waige mfano wa Yesu katika kuwatumikia wengine?

10 Inapohusu kundi la Mungu, bila shaka wanaume waliojiweka wakfu ambao wako katika kutaniko wanapaswa kuiga mtazamo wa Yesu, ambaye alisema hivi: “Nitawaburudisha ninyi.” (Mt. 11:28) Imani katika Mungu na kulipenda kutaniko kunawachochea wanaume Wakristo wajitahidi sana kufikia kazi hiyo njema, na kutofikiri kwamba wanajidhabihu sana kwa kufanya kazi hiyo au ni kazi yenye kulemea sana. Hata hivyo, namna gani ikiwa mtu hana mwelekeo wa kujitahidi kufikia mapendeleo? Je, ndugu anaweza kusitawisha tamaa ya kulitumikia kutaniko?

Sitawisha Tamaa ya Kuwatumikia Wengine

11. Mtu anaweza kusitawisha jinsi gani tamaa ya kuwatumikia wengine?

11 Ikiwa hujitahidi kufikia mapendeleo kwa sababu unahisi kwamba hustahili, ni vizuri kusali ili upate roho takatifu. (Luka 11:13) Roho ya Yehova itakusaidia kushinda wasiwasi wowote ambao huenda ukawa nao. Mungu ndiye anayetupatia tamaa ya kutaka kuwatumikia wengine, kwa kuwa roho ya Yehova ndiyo inayomchochea ndugu kufikia mapendeleo na kisha inamtia nguvu ili atoe utumishi mtakatifu. (Flp. 2:13; 4:13) Kwa hiyo, ni jambo linalofaa kumwomba Yehova akusaidie kusitawisha tamaa ya kukubali mapendeleo ya utumishi.—Soma Zaburi 25:4, 5.

12. Mtu anaweza kupata jinsi gani hekima ya kutosha ili kushughulikia madaraka aliyopewa?

12 Mkristo anaweza kuamua kutojitahidi kufikia mapendeleo kwa sababu anaona kwamba ni kazi ngumu kutimiza mahitaji ya kundi. Au huenda akafikiri kwamba hana hekima ya kutosha kushughulikia madaraka. Ikiwa anafikiri hivyo, Mkristo huyo anaweza kupata hekima kwa kujifunza kwa bidii zaidi Neno la Mungu na vichapo vinavyotegemea Biblia. Anaweza kujiuliza, ‘Je, ninatenga wakati wa kujifunza Neno la Mungu, na ninasali ili nipate hekima?’ Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yak. 1:5) Je, unaamini maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu? Mungu alijibu sala ya Sulemani kwa kumpa “moyo wenye hekima na wenye uelewaji” ambao ulimwezesha kutofautisha kati ya lililo jema na lililo baya wakati wa kutoa hukumu. (1 Fal. 3:7-14) Ni kweli kwamba kisa cha Sulemani kilikuwa cha pekee. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atawapa hekima wanaume ambao wamepewa madaraka katika kutaniko ili waweze kuwatunza vizuri kondoo wake.—Met. 2:6.

13, 14. (a) Eleza jinsi Paulo alivyochochewa na “upendo alio nao Kristo.” (b) “Upendo alio nao Kristo” unapaswa kutuchochea jinsi gani?

13 Jambo lingine linaloweza kutusaidia kusitawisha tamaa ya kuwatumikia wengine ni kufikiria kwa uzito mambo yote ambayo Yehova na Mwana wake wametufanyia. Kwa mfano, fikiria 2 Wakorintho 5:14, 15. (Soma.) “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha” katika njia gani? Upendo ambao Kristo alionyesha kwa kufa kwa ajili yetu kulingana na mapenzi ya Mungu ni wa pekee sana hivi kwamba tunapouthamini zaidi upendo huo, moyo wetu unachochewa sana. Upendo wa Kristo uliongoza matendo ya Paulo. Upendo huo ulimzuia Paulo kutenda kwa uchoyo na ulimsaidia akazie fikira kumtumikia Mungu na wanadamu wenzake ndani na nje ya kutaniko.

14 Kutafakari kuhusu upendo ambao Kristo alikuwa nao kuelekea watu kunatuchochea kuwa wenye shukrani. Kwa sababu hiyo, tunatambua kwamba ni jambo lisilofaa kabisa kwetu kuendelea ‘kupanda kwa mwili’ kwa kufuatia miradi ya kichoyo na kuishi tu kwa ajili ya kutosheleza tamaa zetu wenyewe. Badala yake, tunafanya marekebisho katika maisha yetu ili kutanguliza kazi ambayo Mungu ametupatia tufanye. Tunachochewa na upendo ‘kuwatumikia’ ndugu zetu. (Soma Wagalatia 5:13.) Ikiwa tunajiona sisi wenyewe kuwa watumwa ambao wanawatumikia kwa unyenyekevu watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu, tutawatendea kwa heshima. Bila shaka, hatupaswi kuiga roho inayoenezwa na Shetani ya kuwachambua-chambua watu na kuwahukumu.—Ufu. 12:10.

Jitihada ya Familia

15, 16. Washiriki wa familia wanatimiza daraka gani ili mtu astahili kuwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma au mzee?

15 Ikiwa ndugu ameoa na ana watoto, hali ya familia yake inafikiriwa wazee wanapochunguza ikiwa anatimiza sifa za kustahili kuwa mtumishi wa huduma au mzee. Kwa kweli, kuwekwa kwake rasmi kunahusiana moja kwa moja na hali ya kiroho na sifa ya familia yake. Hilo linaonyesha wazi kwamba familia ina daraka muhimu la kumuunga mkono mume na baba anapotaka kulitumikia kutaniko akiwa mtumishi wa huduma au mzee.—Soma 1 Timotheo 3:4, 5, 12.

16 Yehova anafurahi sana washiriki wa familia ambao ni Wakristo wanaposhirikiana. (Efe. 3:14, 15) Kichwa cha familia anahitaji kuwa na usawaziko ili kushughulikia madaraka ya kutaniko na kusimamia nyumba yake “kwa njia nzuri.” Hivyo, ni jambo la maana sana kwa mzee au mtumishi wa huduma kujifunza Biblia pamoja na mke na watoto wake ili wote waweze kufaidika na Ibada ya Familia ya kila juma. Anapaswa kushiriki kwa ukawaida pamoja nao katika kazi ya kuhubiri. Vivyo hivyo, ni jambo la maana kwa washiriki wa familia kuunga mkono jitihada za kichwa cha familia.

Je, Utatumikia Tena?

17, 18. (a) Ikiwa ndugu hastahili tena kutumikia, huenda anahitaji kufanya nini? (b) Ndugu aliyetumika zamani akiwa mzee au mtumishi wa huduma anaweza kuwa na mtazamo gani?

17 Labda wakati fulani ulikuwa mzee au mtumishi wa huduma lakini kwa sasa hutumikii tena katika daraka hilo. Unampenda Yehova na unaweza kuwa na hakika kwamba bado anakujali. (1 Pet. 5:6, 7) Je, uliambiwa kwamba unahitaji kufanya marekebisho fulani? Uwe tayari kukubali kosa lako na ulirekebishe kwa msaada wa Mungu. Epuka kuwa mwenye uchungu. Uwe mwenye hekima, na uonyeshe mtazamo mzuri. Mzee mmoja aliyetumika kwa miaka mingi lakini akapoteza mapendeleo yake ya utumishi alisema hivi: “Niliazimia kuendelea kuhudhuria mikutano kama kawaida, kushiriki katika utumishi wa shambani, na kusoma Biblia kama nilivyofanya nilipokuwa nikitumika nikiwa mzee, na niliweza kutimiza mradi huo. Nilijifunza kuwa mwenye subira kwa sababu nilifikiri kwamba ningepata tena mapendeleo yangu baada ya mwaka mmoja au miwili, lakini miaka saba hivi ilipita kabla ya mimi kutumika tena nikiwa mzee. Wakati wote huo nilisaidiwa sana na kitia-moyo kinachosema tusichoke lakini tuendelee kujitahidi kufikia mapendeleo.”

18 Ikiwa wewe ni ndugu aliye katika hali inayoelezwa hapo juu, usivunjike moyo. Fikiria jinsi Yehova anavyobariki huduma yako na familia yako. Jenga hali ya kiroho ya familia yako, tembelea wagonjwa, na uwatie moyo watu walio dhaifu. Zaidi ya yote, thamini sana pendeleo lako la kumsifu Mungu na kutangaza habari njema ya Ufalme ukiwa Shahidi wa Yehova. *Zab. 145:1, 2; Isa. 43:10-12.

Chunguza Upya Hali Zako

19, 20. (a) Ndugu wote waliobatizwa wanatiwa moyo wafanye nini? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika habari inayofuata?

19 Kuna uhitaji mkubwa zaidi wa waangalizi na watumishi wa huduma leo kuliko wakati mwingine wowote ule. Kwa hiyo, tunawatia moyo ndugu wote waliobatizwa wachunguze upya hali zao na kujiuliza hivi: ‘Ikiwa mimi si mtumishi wa huduma au mzee, je, ninapaswa kuchunguza sababu zinazonizuia nisitumikie?’ Acha roho ya Mungu ikusaidie kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu jambo hilo la maana sana.

20 Washiriki wote wa kutaniko watafaidika kutokana na jitihada za waamini wenzao ambao wanajidhabihu kwa ajili ya Mungu. Tunapoendelea kutenda kwa fadhili na bila uchoyo, tunavuna shangwe inayotokana na kuwatumikia wengine na kupanda kwa roho. Hata hivyo, kama habari inayofuata itakavyoonyesha, hatupaswi kuihuzunisha roho takatifu ya Mungu. Tunaweza kuepuka kufanya hivyo jinsi gani?

[Maelezo ya Chini]

Ungesema Nini?

• Unabii ulio katika Mika 5:5 unatuhakikishia nini?

• Eleza roho ya kujidhabihu inatia ndani nini.

• Mtu anaweza kusitawisha jinsi gani tamaa ya kuwatumikia wengine?

• Ushirikiano katika familia ni wa maana kadiri gani ili mtu astahili kutumika akiwa mtumishi wa huduma au mzee?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Unaweza kufanya nini ili ufikie mapendeleo?