Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kuwa na Nguvu Kiroho Unapomtunza Mshiriki wa Familia Aliye Mgonjwa

Endelea Kuwa na Nguvu Kiroho Unapomtunza Mshiriki wa Familia Aliye Mgonjwa

Endelea Kuwa na Nguvu Kiroho Unapomtunza Mshiriki wa Familia Aliye Mgonjwa

BAADA ya uvimbe kupatikana karibu na uti wa mgongo wa Kim, ambaye ni Shahidi, uchunguzi ulionyesha kwamba alikuwa na kansa. * Mume wake Steve anasema hivi: “Baada ya kufanyiwa upasuaji wa kuondoa uvimbe huo, Kim alipokea matibabu ya kutumia miale (radiotherapy) na kemikali (chemotherapy). Baada ya kupokea matibabu hayo alidhoofika sana. Hangeweza kutembea kwa urahisi.”

Unaweza kuwazia uchungu ambao Steve alihisi alipokuwa akimtazama mwenzi wake mpendwa akipambana na ugonjwa huo wenye kudhoofisha? Labda una mshiriki wa familia ambaye ana ugonjwa wenye kudhoofisha au aliye na matatizo ya uzee. (Mhu. 12:1-7) Ikiwa ndivyo, unajua kwamba ili uwatunze wapendwa wako vizuri, ni lazima ujitunze mwenyewe. Ikiwa hali yako ya kiroho itadhoofika, hisia zako na afya yako ya kimwili inaweza pia kuanza kudhoofika na huenda ukashindwa kutoa msaada ambao mshiriki wa familia yako anahitaji. Unaweza kuendelea jinsi gani kuwa na usawaziko wa kiroho unapomtunza mshiriki wa familia aliye mgonjwa au aliyezeeka? Je, kuna jambo ambalo washiriki wengine wa kutaniko la Kikristo wanaweza kufanya ili kuonyesha kwamba wanamjali mgonjwa huyo?

Unaweza Jinsi Gani Kuendelea Kuwa na Usawaziko?

Ili uendelee kuwa na usawaziko wa kiroho na afya nzuri ya kimwili unapomtunza mtu wa familia aliye mgonjwa, unahitaji kubadilikana kulingana na hali na kutumia vizuri wakati na nguvu zako. Andiko la Methali 11:2 linasema: “Wenye kiasi wana hekima.” Katika andiko hilo, neno “kiasi” linamaanisha kutambua mambo unayoweza kutimiza. Ili kuhakikisha kwamba hufanyi mambo yanayozidi uwezo wako, huenda ukahitaji kuchunguza ratiba na madaraka yako.

Steve alitenda kwa hekima na kiasi kwa kuchunguza tena madaraka yake. Alikuwa na kazi ya kimwili, na pia alitumika akiwa mratibu wa baraza la wazee na mwangalizi wa utumishi katika kutaniko la kwao la Mashahidi wa Yehova huko Ireland. Alikuwa pia Mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali katika eneo lao. Steve anasema: “Kim hakuwahi kamwe kulalamika kwamba nilikuwa nikimpuuza na kushughulikia sana madaraka hayo. Lakini nilijua kwamba nilikuwa nikifanya mambo ambayo yanazidi uwezo wangu.” Steve alishughulikia hali hiyo jinsi gani? Anasema hivi: “Baada ya kusali na kutafakari, niliamua kuacha kutumika nikiwa mratibu. Niliendelea kutumika nikiwa mzee, lakini niliwapa wengine madaraka fulani niliyokuwa nayo katika kutaniko na hivyo nikapata wakati wa kuwa pamoja na Kim na kumtunza.”

Baada ya muda, afya ya Kim ilikuwa nzuri kiasi. Steve na Kim walichunguza upya hali yao, na kwa msaada wa mke wake, Steve alianza tena kushughulikia madaraka aliyokuwa nayo katika kutaniko hapo awali. Steve anaeleza hivi: “Sote wawili tumejifunza kufanya mambo kulingana na uwezo wetu kwa kadiri ugonjwa wa Kim unavyoruhusu. Ninamshukuru sana Yehova kwa sababu ya msaada wake na pia mke wangu kwa sababu ananiunga mkono bila kulalamika ingawa afya yake si nzuri.”

Fikiria pia kisa cha Jerry, mwangalizi anayesafiri, na mke wake, Maria. Walilazimika kubadili miradi yao ili wawatunze wazazi wao waliozeeka. Maria anasema: “Mimi na mume wangu tulikuwa na mradi wa kutumika tukiwa wamishonari katika nchi ya kigeni. Hata hivyo, Jerry hana ndugu wala dada wa kimwili, na wazazi wake walihitaji kutunzwa. Hivyo, tuliamua kubaki Ireland ili tuwatunze. Kwa kufanya hivyo, tulipata wakati wa kumtunza baba ya Jerry alipolazwa katika hospitali kabla ya kufa. Sasa tunazungumza na mama ya Jerry kila siku, na tunaweza kumtembelea kwa urahisi anapohitaji kusaidiwa. Kutaniko ambalo mama ya Jerry anashirikiana nalo limetusaidia sana na kututegemeza, na hilo limetuwezesha kuendelea na kazi ya kusafiri.”

Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia

Alipokuwa akizungumza kuhusu msaada wa kimwili ambao wajane waliozeeka katika kutaniko walipaswa kupewa, mtume Paulo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” Paulo aliwakumbusha Wakristo wenzake kwamba ili mwenendo wao ‘ukubalike machoni pa Mungu,’ ni lazima wawatunze kifedha wazazi, nyanya, na babu zao. (1 Tim. 5:4, 8) Hata hivyo, wengine katika kutaniko wanaweza na wanapaswa kusaidia.

Fikiria kisa cha Hakan na Inger, wenzi wa ndoa waliozeeka wanaoishi huko Sweden. Hakan anasema: “Sote wawili tulishtuka tulipojua kwamba mke wangu ana kansa. Sikuzote Inger alikuwa na afya nzuri na alikuwa mwenye nguvu. Sasa tulilazimika kwenda hospitali kila siku ili kupata matibabu, na dawa alizopewa zilimdhoofisha kimwili. Wakati huo, Inger alikaa nyumbani, na nilihitaji kukaa na yeye ili nimtunze.” Washiriki wa kutaniko waliwasaidia jinsi gani Hakan na Inger?

Wazee wa kutaniko lao walifanya mpango ili wenzi hao wa ndoa wasikilize mikutano ya Kikristo kupitia simu. Kwa kuongezea, ndugu na dada waliendelea kuwasiliana nao kwa kuwatembelea na kuwapigia simu. Vilevile, walituma barua na kadi. Hakan anasema: “Tulihisi kwamba ndugu wote walitutegemeza na pia tuliona jinsi Yehova alivyotusaidia. Msaada huo ulikuwa wa maana sana ili tuendelee kuwa na nguvu kiroho. Sasa Inger amepona, na sasa tunaweza tena kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme.” Washiriki wa kutaniko wanapofanya yote wanayoweza ili kuwasaidia wagonjwa na waliozeeka kati yao, wanathibitisha kwamba wao ni ‘marafiki wa kweli wanaopenda nyakati zote, nao ni ndugu waliozaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.’—Met. 17:17.

Yehova Anathamini Jitihada Zako

Bila shaka, kumtunza mshiriki wa familia aliye mgonjwa kunaweza kuchosha sana. Hata hivyo, Mfalme Daudi aliandika hivi: “Mwenye furaha ni mtu yeyote anayetenda kwa kumfikiria mtu wa hali ya chini,” kama vile mtu anayehitaji kusaidiwa kwa sababu ya ugonjwa.—Zab. 41:1.

Kwa nini wale wanaowatunza wagonjwa au watu wanaoteseka wana furaha? Andiko la Methali 19:17 linasema: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” Mungu wa kweli anapendezwa kwa njia ya pekee na watumishi wake washikamanifu ambao ni wagonjwa, na anambariki yule anayewaonyesha kibali. Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Yehova mwenyewe atamtegemeza [mtu kama huyo] katika kitanda cha ugonjwa; kitanda chake chote hakika utakibadilisha wakati wa ugonjwa wake.” (Zab. 41:3) Tunaweza kuwa na hakika kwamba ikiwa yule anayetoa msaada kwa upendo atapatwa na hali ngumu au msiba, Yehova atamsaidia.

Tunafurahi kama nini kujua kwamba Yehova Mungu anaona na kuthamini yale tunayofanya katika kumtunza mshiriki wa familia aliye mgonjwa! Ingawa tunahitaji kujitahidi sana ili kutoa msaada huo, Maandiko yanatuhakikishia kwamba “Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.”—Ebr. 13:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Endelea kuwa na usawaziko wa kiroho na ukubali kusaidiwa na wengine