Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kuzoeza Nguvu Zako za Ufahamu

Endelea Kuzoeza Nguvu Zako za Ufahamu

Endelea Kuzoeza Nguvu Zako za Ufahamu

INAFURAHISHA kama nini kumwona mwanasarakasi (gymnaste) hodari akifanya sarakasi kwa ustadi sana! Biblia inawatia moyo Wakristo wazoeze uwezo wao wa kufikiri kama vile tu mwanasarakasi anavyojizoeza.

Mtume Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Waebrania: “Chakula kigumu ni cha watu wakomavu, cha wale ambao kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu [Kihalisi, “viungo vya kuhisi”] zimezoezwa [kama mwanasarakasi] kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Ebr. 5:14) Kwa nini Paulo aliwahimiza Wakristo Waebrania wazoeze uwezo wao wa kufikiri kama vile mwanasarakasi anavyozoeza misuli yake? Tunaweza kuzoeza jinsi gani nguvu zetu za ufahamu?

“Mnapaswa Kuwa Walimu”

Alipokuwa akieleza kuhusu cheo cha Yesu akiwa “kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki,” Paulo aliandika hivi: “Kumhusu yeye [Yesu] sisi tuna mengi ya kusema na yaliyo magumu kufafanuliwa, kwa kuwa mmekuwa wazito katika kusikia kwenu. Kwa maana, kwa kweli, ijapokuwa mnapaswa kuwa walimu kwa sababu ya wakati, ninyi mnahitaji tena mtu awafundishe tangu mwanzo mambo ya msingi ya maneno matakatifu ya Mungu; nanyi mmekuwa kama wanaohitaji maziwa, si chakula kigumu.”—Ebr. 5:10-12.

Inaonekana kwamba Wakristo fulani Wayahudi wa karne ya kwanza hawakupanua uelewaji wao na hawakufanya maendeleo ya kiroho. Kwa mfano, ilikuwa vigumu kwao kukubali nuru iliyoongezeka kuhusu Sheria na kutahiriwa. (Mdo. 15:1, 2, 27-29; Gal. 2:11-14; 6:12, 13) Wengine waliona kuwa jambo gumu kuacha mazoea ya kidesturi yaliyohusianishwa na Sabato ya kila juma na Siku ya Upatanisho ya kila mwaka. (Kol. 2:16, 17; Ebr. 9:1-14) Hivyo basi, Paulo aliwatia moyo wazoeze nguvu zao za ufahamu ili waweze kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia na akawaambia ‘wasonge mbele kuelekea ukomavu.’ (Ebr. 6:1, 2) Bila shaka, himizo lake liliwachochea watu fulani wafikirie jinsi walivyokuwa wakitumia uwezo wao wa kufikiri na huenda himizo hilo liliwasaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Namna gani sisi?

Zoeza Nguvu Zako za Ufahamu

Tunaweza jinsi gani kuzoeza uwezo wetu wa kufikiri ili tuwe wakomavu kiroho? Paulo alisema ni “kwa kutumia.” Kama wanasarakasi, ambao wanazoeza misuli na miili yao kufanya sarakasi ngumu zenye kuvutia, sisi pia tunapaswa kuzoeza uwezo wetu wa kufikiri ili tutofautishe yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.

John Ratey, profesa wa magonjwa ya akili katika Chuo cha Kitiba cha Harvard anasema kwamba “mazoezi ndilo jambo bora zaidi ambalo unaweza kuufanyia ubongo wako.” Gene Cohen, msimamizi wa Kituo Kinachochunguza Hali ya Kuzeeka, Afya na Elimu ya Jamii, katika Chuo Kikuu cha George Washington anasema: “Tunapoulazimisha ubongo wetu kufanya kazi ngumu, chembe za ubongo zinatokeza misuli mipya, na hilo linaongeza njia za kupitishia habari katika ubongo.”

Basi, ni jambo la hekima kuzoeza uwezo wetu wa kufikiri na kuongeza ujuzi wetu juu ya Neno la Mungu. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa tayari zaidi kutimiza ‘mapenzi ya Mungu yaliyo makamilifu.’—Rom. 12:1, 2.

Sitawisha Hamu ya Kula “Chakula Kigumu”

Ikiwa tunatamani ‘kusonga mbele kuelekea ukomavu,’ tunahitaji kujiuliza hivi: ‘Je, ninafanya maendeleo katika kuelewa kweli ya Biblia? Je, wengine wananiona kuwa mtu mkomavu kiroho?’ Mama anafurahia kumnyonyesha mtoto wake mchanga maziwa na kumlisha vyakula vya watoto. Lakini, wazia jinsi ambavyo angehisi ikiwa miaka ingepita na mtoto hali chakula kigumu. Vivyo hivyo, tunafurahi kuona mtu ambaye tumejifunza naye Biblia akifanya maendeleo kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Namna gani ikiwa baada ya hapo mtu huyo hafanyi maendeleo ya kiroho? Je, hilo halingevunja moyo? (1 Kor. 3:1-4) Mwalimu anatumaini kwamba baada ya muda mwanafunzi huyo mpya atakuwa mwalimu pia.

Tunahitaji kutafakari ili tutumie nguvu zetu za ufahamu kuelewa mambo mbalimbali, na hilo linahitaji jitihada. (Zab. 1:1-3) Hatupaswi kuruhusu mambo kama vile kutazama televisheni au mambo tunayopenda ambayo hayahitaji kutumia sana akili yatukengeushe na kutuzuia kutafakari kuhusu mambo ya maana. Ili tusitawishe uwezo wa kufikiri, ni lazima tuwe na hamu na kutosheleza tamaa yetu ya kujifunza Biblia na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Zaidi ya kuwa na ratiba ya kawaida ya kusoma Biblia kibinafsi, ni jambo la maana kwetu kutenga wakati kwa ajili ya Ibada ya Familia na kujifunza kwa undani habari mbalimbali za Biblia.

Jerónimo, ambaye ni mwangalizi anayesafiri huko Mexico, anasema kwamba anajifunza kila gazeti la Mnara wa Mlinzi mara tu anapolipokea. Pia, anatenga wakati wa kujifunza pamoja na mke wake. Jerónimo anasema, “Tukiwa wenzi wa ndoa tuna zoea la kusoma Biblia pamoja kila siku, na tunatumia vichapo vingine kama vile broshua ‘Nchi Nzuri.’” Mkristo anayeitwa Ronald anasema kwamba sikuzote anafuata ratiba ya kutaniko ya usomaji wa Biblia. Pia, ana mradi mmoja au miradi miwili ya muda mrefu ya kufanya utafiti wakati wa funzo la Biblia la kibinafsi. Ronald anasema hivi: “Miradi hiyo inafanya nitazamie kwa hamu kipindi kinachofuata cha funzo.”

Namna gani sisi? Je, tunatenga wakati wa kutosha ili kujifunza Biblia na kutafakari kuhusu Neno la Mungu? Je, tunazoeza uwezo wetu wa kufikiri na kupata uzoefu wa kufanya maamuzi kupatana na kanuni za Kimaandiko? (Met. 2:1-7) Na tuazimie kuwa watu wakomavu kiroho, ambao wamebarikiwa kuwa na ujuzi na hekima na ambao wamezoeza nguvu zao za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia!

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tunazoeza uwezo wetu wa kufikiri ‘kwa kuutumia’