Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uwaheshimu Waliozeeka?

Kwa Nini Uwaheshimu Waliozeeka?

Kwa Nini Uwaheshimu Waliozeeka?

MTI mmoja ulio kando ya pwani ya California, huko Marekani ni kati ya miti inayopigwa picha nyingi zaidi duniani. Mti huo wa mvinje unaitwa Lone Cypress. Inaripotiwa kwamba mti huo umekuwapo kwa miaka zaidi ya 250. Mti huo wenye kuvutia sana unajulikana kwa sababu ya ustahimilivu wake na unatunzwa kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, umeshikiliwa kwa nyaya na mawe yaliyowekwa kuzunguka shina lake.

Mti huo unaweza kutukumbusha kuhusu Wakristo waliozeeka walio kati yetu ambao wanaonyesha uvumilivu mkubwa. Njia moja kuu ambayo wanafanya hivyo ni kwa kutangaza habari njema. Nabii Yoeli alitabiri kwamba “wazee” wangetangaza ujumbe wa Biblia. (Yoe. 2:28-32; Mdo. 2:16-21) Hebu fikiria saa nyingi ambazo waliozeeka wanatumia wakiwasaidia wengine kwa bidii kujifunza kuhusu “habari njema ya ufalme”! (Mt. 24:14) Wengine kati ya watangazaji hao wa Ufalme waliozeeka wamevumilia mateso au matatizo mengine kwa miaka mingi. Ikiwa mti tu wa mvinje unaheshimiwa kwa sababu ya kustahimili na unashikiliwa kwa mawe na nyaya, je, watu waliozeeka ambao wako kati yetu hawastahili kutegemezwa na kutendewa kwa heshima zaidi?

Yehova Mungu aliwaamuru hivi watu wake wa kale: “Unapaswa kusimama mbele ya mtu mwenye mvi, nawe umwonyeshe ufikirio mtu mzee.” (Law. 19:32) Leo, kuna mifano mizuri sana ya watumishi waaminifu wa Yehova ambao wamekuwa ‘wakitembea na Mungu’ kwa miaka mingi. (Mika 6:8) Kwa kweli, kichwa chao chenye mvi ni “taji la uzuri” wanapoendelea kufuata kanuni za Kimaandiko.—Met. 16:31.

Mtume Paulo alimwagiza hivi kijana Timotheo: “Usimkemee kwa ukali mwanamume mzee.” Badala yake, Timotheo alipaswa ‘kumsihi kama baba’ na kuwatendea “wanawake wazee kama mama.” (1 Tim. 5:1, 2) Kwa kweli, Timotheo alipaswa “kusimama” mbele ya mtu mwenye mvi. Basi, ni wazi kwamba Yehova anatazamia tuwaheshimu watu waliozeeka kwa maneno yetu.

Andiko la Waroma 12:10 linasema: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” Bila shaka, waangalizi katika kutaniko wanawaheshimu Wakristo waliozeeka. Ingawa hivyo, sisi sote tunapaswa kuwa wa kwanza katika kuonyeshana heshima.

Bila shaka, washiriki wa familia wana daraka la pekee la kuwatunza wazazi, nyanya (bibi), na babu zao. Watu wametafuta njia za kuutunza mti wa Lone Cypress, na wanaendelea kufanya hivyo. Kwa hakika basi, tunapaswa kutafuta njia za kuendelea kuwaheshimu wazazi, nyanya, na babu zetu wanaozeeka. Kwa mfano, kuwa wasikilizaji wazuri kutatuzuia tusisisitize kufanya mambo kwa njia yetu bila kujali hisia zao.—Met. 23:22; 1 Tim. 5:4.

Yehova anawathamini sana watu ambao wamezeeka kati yetu. Yeye hawaachi. (Zab. 71:18) Kwa kweli, Mungu wa kweli anawatia nguvu ili waendelee kumtumikia kwa uaminifu. Sisi pia na tuendelee kuwategemeza na kuwaheshimu waliozeeka.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kama vile mti wa “Lone Cypress” unavyohitaji kushikiliwa, waliozeeka wanahitaji kutendewa kwa heshima sana

[Hisani]

American Spirit Images/age fotostock