Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa kuwa Yehova anakataza ibada ya sanamu, kwa nini hakumwadhibu Haruni alipotengeneza ndama wa dhahabu?

Haruni alipotengeneza ndama wa dhahabu kama ilivyoandikwa kwenye Kutoka sura ya 32, alivunja sheria ya Yehova kuhusu ibada ya sanamu. (Kut. 20:3-5) Matokeo ni kwamba ‘Yehova alimkasirikia sana Haruni kufikia hatua ya kumwangamiza; lakini Musa aliomba dua pia kwa ajili ya Haruni wakati huo.’ (Kum. 9:19, 20) Je, dua ya mwanamume mwadilifu Musa ilikuwa na “nguvu nyingi” katika kisa cha Haruni? (Yak. 5:16) Ndiyo, inaonekana kwamba Yehova alijibu sala ya Musa na hakumwadhibu Haruni kwa sababu ya dua hiyo na angalau kwa sababu nyingine mbili.

Inaonekana kwamba sababu moja ilihusiana na miaka mingi ambayo Haruni alitumikia kwa uaminifu. Musa alipoagizwa aende mbele ya Farao na kuwatoa Waisraeli huko Misri, Yehova alimchagua Haruni aende pamoja na Musa na kuzungumza kwa niaba yake. (Kut. 4:10-16) Wanaume hao wawili walitii na kwenda mara nyingi mbele ya mfalme wa Misri, wakivumilia ukali wa Farao aliyekuwa na moyo mgumu. Kwa hiyo, walipokuwa bado Misri, Haruni alitumikia kwa ushikamanifu kwa muda mrefu, na alimtumikia Yehova bila kuyumbayumba.—Kut. 4:21.

Fikiria pia hali zilizomsukuma Haruni atengeneze yule ndama wa dhahabu. Musa alipanda Mlima Sinai na kukaa huko kwa siku 40. ‘Watu walipoona kwamba Musa alikuwa akichukua muda mrefu kushuka kutoka mlimani,’ wakamshawishi Haruni awatengenezee sanamu. Haruni alishirikiana nao na akatengeneza sanamu ya ndama wa dhahabu. (Kut. 32:1-6) Hata hivyo, baadaye Haruni alitenda kwa njia iliyoonyesha kwamba kwa kweli hakukubali ibada hiyo ya sanamu. Inaonekana kwamba alisukumwa na umati. Kwa mfano, Musa alipokomesha ibada hiyo ya sanamu kwa njia ya kustaajabisha, wana wote wa Lawi, kutia ndani Haruni, walisimama imara upande wa Yehova. Waabudu 3,000 wa sanamu ambao waliongoza katika ibada hiyo ya sanamu waliuawa.—Kut. 32:25-29.

Baada ya hapo Musa aliwaambia watu hivi: “Mmetenda dhambi kubwa.” (Kut. 32:30) Hivyo, si Haruni tu aliyekuwa na hatia kwa sababu ya kosa hilo. Yeye pamoja na watu wengine walifaidika kwa kuonyeshwa rehema nyingi na Yehova.

Baada ya kisa hicho cha ndama wa dhahabu, Yehova aliamuru kwamba Haruni awekwe rasmi kuwa kuhani mkuu. Mungu alimwambia Musa hivi: “Nawe utamvisha Haruni mavazi matakatifu na kumtia mafuta na kumtakasa, naye atatenda akiwa kuhani kwangu.” (Kut. 40:12, 13) Inaonekana kwamba Yehova alimsamehe Haruni udhaifu wake. Moyoni, Haruni alikuwa mfuasi mshikamanifu wa ibada ya kweli, hakuwa mwabudu mwasi wa sanamu.