Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukristo wa Mapema na Miungu ya Roma

Ukristo wa Mapema na Miungu ya Roma

Ukristo wa Mapema na Miungu ya Roma

KATIKA barua ambayo gavana wa Bithinia, Plini Mdogo alimwandikia Mtawala Mroma aliyeitwa Trajani, alisema hivi: “Hii ndiyo hatua ambayo nimewachukulia wale ambao wanashtakiwa mbele yangu kuwa Wakristo. Niliwauliza ikiwa walikuwa Wakristo, na ikiwa walikubali, niliwauliza tena mara ya pili na mara ya tatu huku nikiwatisha kwamba wangeadhibiwa. Ikiwa waliendelea kusema kwamba wao ni Wakristo niliamuru wauawe.” Plini aliandika hivi kuhusu wale ambao walikana Ukristo kwa kumlaani Kristo na kuabudu sanamu ya mtawala huyo na sanamu za miungu ambayo alikuwa ameleta mahakamani: “Niliona kwamba inafaa kuwaacha huru.”

Wakristo wa mapema waliteswa kwa sababu walikataa kumwabudu mtawala wa Roma na sanamu za miungu mbalimbali. Namna gani kuhusu dini nyingine katika Milki yote ya Roma? Ni miungu gani iliyoabudiwa, na Waroma walikuwa na maoni gani kuihusu? Kwa nini Wakristo waliteswa walipokataa kutoa dhabihu kwa miungu ya Roma? Majibu ya maswali au maulizo hayo yatatusaidia kujua jinsi ambavyo leo tunaweza kushughulika na mambo kama hayo yanayohusu ushikamanifu wetu kwa Yehova.

Dini za Milki

Kulikuwa na miungu tofauti-tofauti iliyoabudiwa katika Milki ya Roma sawa tu na jinsi kulivyokuwa na lugha na tamaduni mbalimbali. Hata hivyo, ingawa huenda Waroma waliiona Dini ya Kiyahudi kuwa ya ajabu, waliiona pia kuwa religio licita, au dini inayotambuliwa, na waliilinda. Katika hekalu la Yerusalemu, mara mbili kwa siku, wana-kondoo wawili na ng’ombe-dume mmoja walitolewa dhabihu kwa ajili ya Kaisari na taifa la Roma. Waroma hawakujali ikiwa dhabihu hizo zilimpendeza mungu mmoja au miungu mingi. Jambo ambalo waliona kuwa la maana ni kwamba tendo hilo lilitoa uthibitisho wa kutosha kwamba Wayahudi walikuwa washikamanifu kwa taifa la Roma.

Desturi mbalimbali za kipagani zilienea katika madhehebu mengi. Hadithi za Wagiriki zilikuwa zimekubaliwa na watu wengi, na uaguzi ulikuwa jambo la kawaida. Dini za Mashariki zenye mambo ya mafumbo-mafumbo ziliwaahidi wafuasi wake kwamba wangepata nafsi isiyoweza kufa, wangefunuliwa mambo moja kwa moja, na wangefikia miungu kupitia desturi za mafumbo. Dini hizo zilienea kotekote katika milki hiyo. Madhehebu yaliyojulikana sana katika karne za mapema W.K., ni kama vile madhehebu ya mungu Serapisi na mungu wa kike Isisi wa Misri, madhehebu ya Atargatisi, mungu wa kike wa samaki wa Wasiria, na madhehebu ya Mithra, mungu wa jua wa Waajemi.

Kitabu cha Biblia cha Matendo kinaonyesha waziwazi mazingira ya kipagani yaliyowazunguka Wakristo wa mapema. Kwa mfano, liwali Mroma wa Kipro alishirikiana na mwanamume Myahudi aliyekuwa mlozi. (Mdo. 13:6, 7) Huko Listra, watu walifikiria kimakosa kwamba Paulo na Barnaba walikuwa Herme na Zeu, miungu ya Wagiriki. (Mdo. 14:11-13) Paulo alipokuwa huko Filipi, alikutana na kijakazi aliyekuwa akifanya uaguzi. (Mdo. 16:16-18) Mtume Paulo alisema kwamba wakaaji wa Athene ‘walionekana kuwa wenye mwelekeo zaidi wa kuogopa miungu kuliko wengine.’ Katika jiji hilo alikuwa ameona pia madhabahu ambayo ilikuwa imeandikwa “Kwa Mungu Asiyejulikana.” (Mdo. 17:22, 23) Wakaaji wa Efeso waliabudu mungu wa kike, Artemi. (Mdo. 19:1, 23, 24, 34) Kwenye kisiwa cha Malta, watu walisema kwamba Paulo alikuwa mungu kwa sababu hakupatwa na madhara baada ya kuumwa na nyoka. (Mdo. 28:3-6) Katika mazingira kama hayo, Wakristo walihitaji kuwa waangalifu ili kuepuka mielekeo ambayo ingechafua ibada yao safi.

Dini ya Waroma

Milki ya Roma ilipoendelea kupanuka, Waroma walikubali miungu mipya wakiamini kwamba ilikuwa miungu ileile waliyoijua lakini yenye umbo lingine. Badala ya kuharibu kabisa madhehebu ya kigeni, washindi Waroma walikubali madhehebu hayo na kuyafanya kuwa ya Kiroma. Hivyo, dini ya Waroma ikawa na madhehebu mbalimbali kama vile tu raia wake walivyokuwa na utamaduni mbalimbali. Dini ya Waroma haikudai watu wajitoe kikamili. Watu wangeweza kuabudu miungu tofauti-tofauti wakati uleule.

Kati ya miungu ya Waroma wenyewe, Sumbula (Jupiter) ndiye aliyekuwa mungu mkuu na walimpa jina Optimus Maximus, yaani, aliye bora kabisa na mkuu zaidi. Ilidhaniwa kwamba alijionyesha kupitia upepo, mvua, radi, na ngurumo. Juno, dada ya Sumbula ambaye pia alikuwa mke wake, alihusianishwa na mwezi. Vilevile ilisemekana kwamba alisimamia mambo yote katika maisha ya wanawake. Binti yake, Minerva, alikuwa mungu wa kike wa kazi za mikono, ujuzi wa kazi mbalimbali, sanaa, na vita.

Waroma walikuwa na miungu mingi sana. Lares na Penates walikuwa miungu ya familia. Vesta alikuwa mungu wa kike wa jiko la kuotea moto. Janus, aliyekuwa na nyuso mbili, alikuwa mungu wa mwanzo wa kila kitu. Kila kazi ya ufundi ilikuwa na mungu wake. Waroma waliamini pia miungu ya vitu visivyoonekana. Pax alikuwa mungu wa kudumisha amani, Salus mungu wa afya, Pudicitia mungu wa kiasi na usafi wa maadili, Fides mungu wa uaminifu, Virtus mungu wa ujasiri, na Voluptas, mungu wa raha. Walifikiri kwamba kila tendo lililofanywa na Waroma waziwazi na faraghani lilihusiana na mapenzi ya miungu. Kwa hiyo, ili kufanikiwa katika jambo lolote, mungu aliyehusika alipaswa kufurahishwa kupitia sala, dhabihu, na sherehe za kidesturi.

Njia moja iliyotumiwa kujua mapenzi ya miungu ilikuwa kutafuta ishara za bahati. Njia kuu waliyotumia kutafuta ishara za bahati ni kuchunguza viungo vya ndani vya wanyama waliotolewa dhabihu. Walifikiri kwamba hali ya viungo hivyo ilionyesha ikiwa miungu ilikubali au kukataa tendo fulani.

Kufikia mwisho wa karne ya pili K.W.K., taifa la Roma lilikuwa limeamua kwamba miungu yao mikuu ilifanana na miungu fulani ya Wagiriki. Sumbula alifanana na Zeu, Juno alifanana na Hera, na kadhalika. Waroma walikuwa pia wamekubali hadithi ambazo zilihusianishwa na miungu ya Wagiriki. Hadithi hizo zilisema mambo mabaya kuhusu miungu hiyo, ambayo ilifanya makosa na ilikuwa na udhaifu kama wa wanadamu. Kwa mfano, ilisemekana kwamba Zeu aliwalala wanawake kinguvu na alifanya ngono na watoto, watu walio hai, na pia wafu. Matendo mapotovu ya miungu hiyo—ambayo mara nyingi yalishangiliwa kwa kelele katika majumba ya maonyesho—yaliwachochea waabudu wa miungu hiyo wafanye matendo mapotovu kabisa.

Inaelekea kwamba ni watu wachache wenye elimu waliokubali kwamba hadithi hizo zilikuwa za kweli. Wengine walisema kwamba zilikuwa hadithi za kuwaziwa tu. Inaonekana kwamba hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Pontio Pilato aulize swali hili linalojulikana sana, “Kweli ni nini?” (Yoh. 18:38) Swali hilo linaonyesha “maoni ya watu waliokuwa na elimu, kwamba haingewezekana hata kidogo kuthibitisha ukweli wa mambo hayo.”

Kumwabudu Mtawala

Ibada ya watawala ilianza wakati wa utawala wa Augusto (27 K.W.K. mpaka 14 W.K.). Hasa katika majimbo ya Mashariki ambako lugha ya Kigiriki ilizungumzwa, wengi walitaka kumshukuru sana Augusto, ambaye alikuwa ameleta maendeleo na amani baada ya vita vya muda mrefu. Watu walitaka kuendelea kulindwa na kiongozi ambaye walimwona. Walitamani kuanzisha serikali ambayo ingeondoa tofauti za kidini, kutetea uzalendo, na kuunganisha ulimwengu chini ya “mwokozi” wake. Matokeo ni kwamba mtawala alionwa kuwa mungu.

Ingawa Augusto hakuruhusu watu wamwite mungu alipokuwa hai, alisisitiza kwamba nchi ya Roma iabudiwe kama mungu wa kike—Roma Dea. Augusto aliwekwa rasmi kuwa mungu baada ya kufa. Hivyo, ibada na uzalendo katika majimbo ilielekezwa kwa kitovu cha milki na watawala wake. Ibada hiyo mpya ya mtawala, ambayo baada ya muda mfupi ilienea katika majimbo yote, ilionwa kuwa njia ya kuonyesha heshima na uaminifu kwa Taifa.

Domitiani, ambaye alitawala kuanzia mwaka wa 81 mpaka 96 W.K., ndiye mtawala wa kwanza wa Roma aliyetaka aabudiwe kama mungu. Kufikia wakati huo, Waroma walikuwa wametambua tofauti kati ya Wakristo na Wayahudi na walipinga yale ambayo yalionwa kuwa madhehebu mapya. Inaelekea kwamba mtume Yohana alipelekwa uhamishoni kwenye kisiwa cha Patmo wakati wa utawala wa Domitiani kwa sababu ya “kutoa ushahidi kumhusu Yesu.”—Ufu. 1:9.

Yohana aliandika kitabu cha Ufunuo akiwa utekwani. Katika kitabu hicho, anamtaja Antipa, Mkristo aliyeuawa huko Pergamamu, kituo kikuu cha ibada ya mtawala. (Ufu. 2:12, 13) Kufikia wakati huo, huenda serikali iliyoongozwa na mfalme ilikuwa imeanza kudai kwamba Wakristo washiriki katika desturi za ibada ya Taifa. Iwe hali ilikuwa hivyo au la, kufikia mwaka wa 112 W.K., kama inavyoonyeshwa na barua ambayo Trajani aliandikiwa ambayo ilitajwa mwanzoni mwa habari hii, Plini alikuwa akidai kwamba Wakristo huko Bithinia washiriki katika desturi hizo.

Trajani alimsifu Plini kwa sababu ya vile alivyoshughulikia kesi zilizoletwa mbele yake na akaagiza kwamba Wakristo waliokataa kuabudu miungu ya Waroma wauawe. Trajani aliandika hivi: “Hata hivyo, ikiwa mtu atakana kwamba yeye si Mkristo, na ikiwa ataonyesha wazi kwamba yeye si Mkristo, kwa kuapa kwa miungu yetu, msamehe ikiwa ametubu (bila kujali mashtaka yoyote yaliyotolewa kumhusu).”

Waroma hawangekubali dini ambayo ilitaka wafuasi wake wajitoe kikamili. Miungu ya Waroma haikutaka watu wajitoe kikamili, basi, kwa nini Mungu wa Wakristo alitaka wajitoe kikamili? Waliamini kwamba kuabudu miungu ya Taifa kulionyesha kuwa mtu anatambua mfumo huo wa kisiasa. Hivyo, kukataa kuabudu miungu hiyo kulionwa kuwa kosa la uhaini. Plini alitambua kwamba haingewezekana kuwalazimisha Wakristo wengi kushiriki katika ibada hiyo. Waliona kwamba kushiriki katika ibada hiyo kungeonyesha kuwa wao si waaminifu kwa Yehova, na Wakristo wengi wa mapema walichagua kufa badala ya kushiriki katika ibada ya sanamu ya kumwabudu mtawala.

Kwa nini tunapaswa kupendezwa na jambo hilo leo? Katika nchi fulani, raia wanatazamiwa kuabudu nembo au ishara za taifa. Tukiwa Wakristo, bila shaka tunaheshimu mamlaka za serikali. (Rom. 13:1) Hata hivyo, katika sherehe ambazo zinahusisha bendera ya taifa, tunamtii Yehova Mungu kwa kujitoa kwake kikamili na kufuata shauri la Neno lake kwamba ‘tukimbie ibada ya sanamu’ na ‘tujilinde na sanamu.’ (1 Kor. 10:14; 1 Yoh. 5:21; Nah. 1:2) Yesu alisema hivi: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Luka 4:8) Hivyo basi, na tuendelee kuwa washikamanifu kwa Mungu tunayemwabudu.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Wakristo wa kweli wanajitoa kikamili kwa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 3]

Wakristo wa mapema walikataa kuabudu mtawala au sanamu za miungu

Mtawala Domitiani

Zeu

[Hisani]

Emperor Domitian: Todd Bolen/Bible Places.com; Zeus: Photograph by Todd Bolen/Bible Places.com, taken at Archaeological Museum of Istanbul

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wakristo huko Efeso walikataa kumwabudu Artemi, mungu wa kike aliyejulikana sana.—Matendo 19:23-41