Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiihuzunishe Roho Takatifu ya Yehova

Usiihuzunishe Roho Takatifu ya Yehova

Usiihuzunishe Roho Takatifu ya Yehova

“Msiwe mkiihuzunisha roho takatifu ya Mungu, ambayo kupitia hiyo mmetiwa muhuri.”—EFE. 4:30.

1. Yehova amewafanyia nini mamilioni ya watu, na wana wajibu gani?

YEHOVA amewafanyia jambo la pekee mamilioni ya watu wanaoishi katika ulimwengu huu wenye misukosuko. Amewapa watu hao nafasi ya kumkaribia kupitia Mwana wake mzaliwa-pekee, Yesu Kristo. (Yoh. 6:44) Ikiwa umejiweka wakfu kwa Mungu na unaishi kulingana na wakfu huo, basi wewe ni mmoja wao. Kwa kuwa ulibatizwa katika jina la roho takatifu, una wajibu wa kujiendesha kulingana na roho hiyo.—Mt. 28:19.

2. Tutazungumzia maswali au maulizo gani?

2 Sisi ambao ‘tunapanda kwa roho’ tunavaa utu mpya. (Gal. 6:8; Efe. 4:17-24) Lakini mtume Paulo anatushauri na kutuonya kwamba tusiihuzunishe roho takatifu ya Mungu. (Soma Waefeso 4:25-32.) Tutachunguza sasa kwa makini shauri hilo la mtume Paulo. Paulo alimaanisha nini aliposema kuhusu kuihuzunisha roho ya Mungu? Mtu yeyote aliyejiweka wakfu kwa Yehova anaweza jinsi gani kufanya jambo kama hilo? Na tunaweza kuepuka jinsi gani kuihuzunisha roho ya Yehova?

Paulo Alimaanisha Nini?

3. Eleza maana ya maneno yaliyo katika Waefeso 4:30?

3 Kwanza kabisa, ona maneno ya Paulo katika Waefeso 4:30. Aliandika hivi: “Msiwe mkiihuzunisha roho takatifu ya Mungu, ambayo kupitia hiyo mmetiwa muhuri kwa ajili ya siku ya kuachiliwa huru kupitia fidia.” Paulo hakutaka waamini wenzake wapendwa wahatarishe hali yao ya kiroho. Walikuwa ‘wametiwa muhuri kupitia roho ya Yehova kwa ajili ya siku ya kuachiliwa huru kupitia fidia.’ Roho takatifu ya Mungu ilikuwa muhuri na bado ni muhuri, au ‘rehani ya kile kitakachokuja’ baadaye kwa ajili ya watiwa-mafuta wanaoshika utimilifu. (2 Kor. 1:22) Muhuri huo unaonyesha kwamba wao ni mali ya Mungu na kwamba watapata uhai wa kimbingu. Hesabu ya wale watakaotiwa muhuri mwishowe itakuwa 144,000.—Ufu. 7:2-4.

4. Kwa nini ni jambo la maana kuepuka kuihuzunisha roho ya Mungu?

4 Kuihuzunisha roho kunaweza kuwa hatua ya kwanza inayomwongoza Mkristo kupoteza kabisa uvutano wa nguvu ya utendaji ya Mungu katika maisha yake. Yale ambayo Daudi alisema baada ya kutenda dhambi na Bath-sheba yanaonyesha kwamba mtu anaweza kupoteza roho ya Mungu. Daudi alipokuwa akitubu alimsihi Yehova hivi: “Usinitupilie mbali na uso wako; wala usiniondolee roho yako takatifu.” (Zab. 51:11) Watiwa-mafuta ambao wanathibitika kuwa ‘waaminifu hata kufikia kifo’ ndio tu watakaopokea “taji” la uhai usioweza kufa mbinguni. (Ufu. 2:10; 1 Kor. 15:53) Wakristo walio na tumaini la kuishi duniani wanahitaji pia roho takatifu ili waendelee kuwa watimilifu kwa Mungu na kupokea zawadi yake ya uzima kwa msingi wa imani katika fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo. (Yoh. 3:36; Rom. 5:8; 6:23) Hivyo, sisi sote tunapaswa kuwa waangalifu sana ili tusiihuzunishe roho takatifu ya Yehova.

Mkristo Anaweza Kuihuzunisha Roho Jinsi Gani?

5, 6. Mkristo anaweza kuihuzunisha roho ya Yehova jinsi gani?

5 Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, tunaweza kuepuka kuihuzunisha roho. Hilo linawezekana ikiwa ‘tunaendelea kutembea na kuishi kwa roho,’ na hivyo hatutashindwa na tamaa mbaya za mwili wala kuonyesha sifa mbaya. (Gal. 5:16, 25, 26) Lakini hali inaweza kubadilika. Tunaweza kuihuzunisha roho ya Mungu kwa kadiri fulani kwa kujiruhusu tupeperuke pole kwa pole, labda bila sisi kutambua, na kutumbukia katika mwenendo ambao unakatazwa na Neno la Mungu lililoongozwa na roho.

6 Tukiendelea kutenda kinyume na mwongozo wa roho takatifu, tutakuwa tukiihuzunisha roho na pia Yehova, ambaye ndiye Chanzo cha roho hiyo. Tukichunguza Waefeso 4:25-32 tutaona jinsi tunavyopaswa kujiendesha, na hilo linaweza kutusaidia kuepuka kuihuzunisha roho ya Mungu.

Jinsi ya Kuepuka Kuihuzunisha Roho

7, 8. Eleza kwa nini ni lazima tuwe na zoea la kusema kweli.

7 Ni lazima tuwe na zoea la kusema kweli. Kulingana na Waefeso 4:25, Paulo aliandika hivi: “Sasa kwa kuwa mmeuondolea mbali uwongo, semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake, kwa sababu sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.” Kwa kuwa tumeunganishwa tukiwa “viungo vya mtu na mwenzake,” bila shaka hatupaswi kuwatendea kwa hila au kujaribu kuwapotosha kimakusudi waabudu wenzetu, kwa kuwa kufanya hivyo ni kama tu kuwadanganya. Yeyote ambaye anaendelea kufanya hivyo mwishowe ataharibu uhusiano wake pamoja na Mungu.—Soma Methali 3:32.

8 Maneno na matendo ya udanganyifu yanaweza kuvuruga umoja wa kutaniko. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa kama nabii Danieli aliyekuwa mwenye kutegemeka, ambaye ndani yake wengine hawakupata jambo lolote lenye ufisadi au baya. (Dan. 6:4) Na tunapaswa kukumbuka shauri la Paulo kwa Wakristo walio na tumaini la kimbingu kwamba kila mshiriki wa “mwili wa Kristo” ni sehemu ya wale wengine wote na anahitaji kuendelea kuwa na umoja na wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta ambao wana zoea la kusema kweli. (Efe. 4:11, 12) Ikiwa tunatumaini kuishi milele katika Paradiso duniani, ni lazima sisi pia tuwe na zoea la kusema kweli, na hivyo kuchangia umoja wa undugu wetu wa ulimwenguni pote.

9. Kwa nini ni jambo la maana kutii shauri la Waefeso 4:26, 27?

9 Ni lazima tumpinge Ibilisi, na kutompa nafasi ya kutuumiza kiroho. (Yak. 4:7) Roho takatifu inatusaidia kumpinga Shetani. Kwa mfano, tunaweza kufanya hivyo kwa kuepuka hasira kali isiyozuilika. Paulo aliandika hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Ikiwa tuna sababu yoyote ya kukasirika, kusali papo hapo kimyakimya kunaweza kutusaidia kuwa na “roho ya utulivu,” na kuonyesha sifa ya kujizuia badala ya kutenda kwa njia ambayo inaweza kuihuzunisha roho ya Mungu. (Met. 17:27) Basi acheni tusiendelee kuwa katika hali ya kuchokozeka na hivyo kumpa Shetani nafasi ya kutushawishi tutende jambo ovu. (Zab. 37:8, 9) Njia moja ya kumpinga ni kutatua ugomvi haraka iwezekanavyo kulingana na shauri la Yesu.—Mt. 5:23, 24; 18:15-17.

10, 11. Kwa nini hatupaswi kuiba au kufanya jambo ambalo si la unyoofu?

10 Hatupaswi kushindwa na kishawishi chochote cha kuiba au cha kukosa unyoofu. Kuhusu kuiba, Paulo aliandika hivi: “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (Efe. 4:28) Ikiwa Mkristo aliyejiweka wakfu angeiba, bila shaka angekuwa ‘amelishambulia jina la Mungu’ kwa kuliletea suto. (Met. 30:7-9) Umaskini haumfanyi mtu awe na haki ya kuiba. Wale wanaompenda Mungu na jirani wanatambua kwamba hawana sababu yoyote ya kuiba.—Marko 12:28-31.

11 Paulo hataji tu kile ambacho hatupaswi kufanya; anaonyesha pia kile ambacho tunapaswa kufanya. Ikiwa tunaishi na kutembea kwa roho takatifu, tutafanya kazi kwa bidii ili tuweze kuitunza familia yetu na pia kuwa na “kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (1 Tim. 5:8) Yesu na mitume wake walikuwa na hazina ya kuwasaidia maskini, lakini yule msaliti Yuda Iskariote alikuwa akiiba pesa kutoka katika hazina hiyo. (Yoh. 12:4-6) Bila shaka, Yuda Iskariote hakuwa akiongozwa na roho takatifu. Sisi ambao tunaongozwa na roho ya Mungu ‘tunajiendesha kwa unyoofu katika mambo yote,’ kama Paulo. (Ebr. 13:18) Kwa kufanya hivyo, tunaepuka kuihuzunisha roho takatifu ya Yehova.

Njia Nyingine za Kuepuka Kuihuzunisha Roho

12, 13. (a) Kama inavyoonyeshwa katika Waefeso 4:29, ni usemi wa aina gani tunaopaswa kuepuka? (b) Usemi wetu unapaswa kuwa wa aina gani?

12 Ni lazima tulinde usemi wetu. Paulo alisema hivi: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.” (Efe. 4:29) Kwa mara nyingine tena, mtume huyo hasemi tu yale ambayo hatupaswi kufanya; anatuambia pia yale ambayo tunapaswa kufanya. Chini ya uvutano wa roho ya Mungu, tutachochewa ‘kusema jambo lililo jema kwa ajili ya kujenga ili liwape wasikiaji lile linalofaa.’ Zaidi ya hayo, hatupaswi kuruhusu “neno lililooza” litoke katika kinywa chetu. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “lililooza” limetumiwa kuhusiana na tunda, samaki, au nyama iliyooza. Kama vile tunavyochukizwa na chakula kama hicho, ndivyo tunavyochukia usemi ambao Yehova anauona kuwa mbaya.

13 Usemi wetu unapaswa kuwa wenye heshima, fadhili, na ‘wenye kukolezwa chumvi.’ (Kol. 3:8-10; 4:6) Watu wanapaswa kutambua kwamba sisi tuko tofauti wanaposikia yale ambayo tunasema. Basi acheni tuwasaidie wengine kwa kusema mambo ambayo ni ‘mema kwa ajili ya kujenga.’ Na tuhisi kama mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova Mwamba wangu na Mkombozi wangu.”—Zab. 19:14.

14. Kulingana na Waefeso 4:30, 31, tunapaswa kuondolea mbali nini?

14 Ni lazima tuondolee mbali uchungu, ghadhabu, matukano, na ubaya wote. Baada ya kuonya kuhusu kuihuzunisha roho ya Mungu, Paulo aliandika hivi: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Efe. 4:30, 31) Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, sisi sote tunahitaji kufanya bidii ili kudhibiti au kuzuia mawazo na matendo yetu. Tukimwaga ‘uchungu wenye uovu na hasira na ghadhabu,’ tutakuwa tukiihuzunisha roho ya Mungu. Vivyo hivyo tutaihuzunisha roho ya Mungu ikiwa tunaendelea kuhesabu makosa ambayo tunatendewa, kuwa na kinyongo, na kukataa kupatana na mtu aliyetukosea. Tukianza tu kupuuza shauri la Biblia, huenda tukasitawisha tabia ambazo zitatuongoza kutenda dhambi juu ya roho na tunaweza kupata matokeo mabaya.

15. Ikiwa tumekosewa, tunapaswa kufanya nini?

15 Tunahitaji kuwa wenye fadhili, wenye huruma, na wenye kusamehe. Paulo aliandika hivi: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Efe. 4:32) Hata tukiumia sana moyoni kwa sababu ya kutendewa jambo fulani baya, acheni tusamehe, kama Mungu anavyosamehe. (Luka 11:4) Tuseme mwamini mwenzetu amesema jambo fulani baya kutuhusu. Tunaenda kuzungumza naye ili kujaribu kutatua tatizo hilo. Anaonyesha huzuni ya kweli na anaomba msamaha. Tunamsamehe, lakini tunahitaji kufanya mengi zaidi. Andiko la Mambo ya Walawi 19:18 linasema hivi: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako; nawe mpende mwenzako kama wewe mwenyewe. Mimi ni Yehova.”

Tunahitaji Kuwa Macho

16. Toa mfano unaoonyesha kwamba huenda tukahitaji kufanya marekebisho ili tusiihuzunishe roho ya Yehova.

16 Hata faraghani au mahali pa siri, tunaweza kushawishiwa kufanya jambo fulani lisilompendeza Mungu. Kwa mfano, huenda ndugu fulani amekuwa akisikiliza muziki usiowafaa Wakristo. Mwishowe, dhamiri yake inamsumbua kwa sababu ya kupuuza mashauri ya Biblia yanayotolewa katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Huenda akasali kuhusu tatizo hilo na anaweza kukumbuka maneno ya Paulo yaliyo katika Waefeso 4:30. Akiwa ameazimia kutofanya jambo lolote linaloweza kuihuzunisha roho ya Mungu, anaamua tangu sasa na kuendelea kuepuka kusikiliza muziki usiowafaa Wakristo. Yehova atabariki roho ambayo ndugu huyo anaonyesha. Kwa hiyo, acheni tuendelee daima kuepuka kuihuzunisha roho ya Mungu.

17. Ni jambo gani linaloweza kutukia tusipokuwa macho na kudumu katika sala?

17 Tusipokuwa macho na kudumu katika sala, tunaweza kuanguka katika tendo lisilo safi au zoea baya ambalo linaweza kuihuzunisha roho ya Mungu. Kwa kuwa roho takatifu inatokeza sifa za Baba yetu wa mbinguni, tunaweza kuihuzunisha roho hiyo, jambo ambalo kwa kweli hatutaki kamwe kufanya. (Efe. 4:30) Waandishi Wayahudi wa karne ya kwanza walitenda dhambi kwa kudai kwamba Yesu alifanya miujiza kwa nguvu za Shetani. (Soma Marko 3:22-30.) Maadui hao wa Kristo ‘walikufuru roho takatifu’ na hivyo wakatenda dhambi isiyoweza kusamehewa. Tusifanye hivyo kamwe!

18. Tunaweza kujua jinsi gani kwamba hatujatenda dhambi isiyoweza kusamehewa?

18 Kwa kuwa hatutaki hata kukaribia kutenda dhambi isiyoweza kusamehewa, tunahitaji kukumbuka yale ambayo Paulo alisema kuhusu kutoihuzunisha roho. Lakini namna gani ikiwa tumetenda kosa zito? Ikiwa tumetubu na tumesaidiwa na wazee, tunaweza kukata kauli kwamba Mungu ametusamehe na hatujaitendea dhambi roho takatifu. Kwa msaada wa Mungu, tunaweza pia kuepuka kuihuzunisha roho kwa njia yoyote ile.

19, 20. (a) Taja mambo fulani ambayo tunahitaji kuepuka. (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Mungu anatumia roho yake takatifu ili kusitawisha upendo, shangwe, na umoja kati ya watu wake. (Zab. 133:1-3) Kwa hiyo, tunapaswa kuepuka kuihuzunisha roho kwa kushiriki katika porojo zenye kuumiza au kwa kusema mambo ambayo yangewapunguzia heshima wachungaji waliowekwa rasmi na roho takatifu. (Mdo. 20:28; Yuda 8) Badala yake, tunapaswa kuendeleza umoja na kuheshimiana katika kutaniko. Kwa kweli, hatupaswi kuanzisha vikundi-vikundi vya “marafiki” kati ya watu wa Mungu. Paulo aliandika hivi: “Nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko katikati yenu, bali kwamba muunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.”—1 Kor. 1:10.

20 Yehova yuko tayari na anaweza kutusaidia kuepuka kuihuzunisha roho yake. Acheni basi tuendelee kusali ili tupewe roho takatifu na tuazimie kutoihuzunisha. Na tuendelee ‘kupanda kwa roho,’ kwa kutafuta kwa bidii mwongozo wake sasa na kwa umilele wote.

Ungesema Nini?

• Inamaanisha nini kuihuzunisha roho ya Mungu?

• Mtu aliyejiweka wakfu kwa Yehova anaweza kuihuzunisha roho yake jinsi gani?

• Tunaweza kuepuka jinsi gani kuihuzunisha roho takatifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 30]

Tatua ugomvi haraka

[Picha katika ukurasa wa 31]

Usemi wako unaonyesha unazaa tunda gani?