Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanawake—Kwa Nini Mjitiishe Chini ya Ukichwa?

Wanawake—Kwa Nini Mjitiishe Chini ya Ukichwa?

Wanawake—Kwa Nini Mjitiishe Chini ya Ukichwa?

“Kichwa cha mwanamke ni mwanamume.”—1 KOR. 11:3.

1, 2. (a) Mtume Paulo aliandika nini kuhusu mpango wa Yehova wa ukichwa na kujitiisha? (b) Ni maswali au maulizo gani ambayo yatazungumziwa katika habari hii?

YEHOVA ameweka utaratibu ambao mtume Paulo alitaja alipoandika kwamba “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo” nacho “kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Kor. 11:3) Habari iliyotangulia ilionyesha kwamba Yesu aliona ni pendeleo na shangwe kujitiisha chini ya Kichwa chake, Yehova Mungu, na pia ilionyesha kwamba Kristo ndiye kichwa cha wanaume Wakristo. Kristo alikuwa mwenye fadhili, mpole, mwenye huruma, naye hakuwa mwenye uchoyo aliposhughulika na watu. Wanaume walio katika kutaniko wanahitaji kuwatendea wengine kwa njia hiyo, hasa wake zao.

2 Hata hivyo, namna gani wanawake? Kichwa chao ni nani? Paulo aliandika: “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” Wanawake wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu? Je, bado wanapaswa kufuata kanuni hiyo ikiwa mume si mwamini? Je, kujitiisha chini ya ukichwa wa wanaume kunamaanisha kwamba mke anapaswa kunyamaza tu katika ndoa, na hapaswi kusema lolote maamuzi yanapofanywa? Mwanamke anajiletea sifa jinsi gani?

“Nitamfanyia Msaidizi”

3, 4. Kwa nini kufuata mpango wa ukichwa katika ndoa kuna faida?

3 Mungu ndiye aliyeanzisha mpango wa ukichwa. Baada ya kumuumba Adamu, Yehova Mungu alisema: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.” Baada ya Hawa kuumbwa, Adamu alifurahi sana kupata mwenzi na msaidizi na akasema hivi: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.” (Mwa. 2:18-24) Adamu na Hawa walikuwa na tarajio zuri ajabu la kuwa baba na mama wa jamii yote ya wanadamu wakamilifu, ambao wangeishi milele kwa furaha katika paradiso duniani.

4 Kwa sababu ya uasi wa wazazi wetu wa kwanza, hali kamilifu katika bustani ya Edeni ilipotea. (Soma Waroma 5:12.) Lakini bado Mungu alimwona mume kuwa kichwa cha mke wake. Mume na mke wakifuata mpango huo kwa njia inayofaa, wanapata faida kubwa na furaha katika ndoa yao. Wanahisi kama Yesu alivyohisi kuhusu kujitiisha chini ya Kichwa chake, Yehova. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu ‘alifurahi mbele za Yehova wakati wote.’ (Met. 8:30) Kwa sababu ya hali ya kutokamilika, wanaume hawawezi tena kutumia ukichwa wao kwa njia kamilifu, nao wake hawawezi kujitiisha kwa ukamilifu. Hata hivyo, waume na wake wanapoendelea kujitahidi kadiri wanavyoweza, mpango wa ukichwa unaleta furaha kubwa zaidi katika ndoa wakati huu.

5. Kwa nini wenzi wa ndoa wanapaswa kuchukua kwa uzito shauri la Waroma 12:10?

5 Ili ndoa ifanikiwe ni lazima wenzi wa ndoa watumie shauri hili la Kimaandiko ambalo linawahusu Wakristo wote: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Rom. 12:10) Pia, mume na mke wanapaswa kujitahidi kabisa ‘kuwa wenye fadhili wao kwa wao, wenye huruma nyororo, wakisameheana kwa hiari.’—Efe. 4:32.

Wakati Mwenzi wa Ndoa Si Mwamini

6, 7. Matokeo yanaweza kuwa nini ikiwa mke Mkristo anajitiisha chini ya mume ambaye si mwamini?

6 Namna gani ikiwa mwenzi wako wa ndoa si mtumishi wa Yehova? Katika visa vingi, mume ndiye asiye mwamini. Mke anapaswa kumtendea jinsi gani mume asiyemwamini? Biblia inajibu hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”—1 Pet. 3:1, 2.

7 Neno la Mungu linamwambia mke aendelee kujitiisha chini ya mume ambaye si mwamini. Mwenendo wake mzuri unaweza kumchochea mume achunguze kile kinachomfanya mke wake ajiendeshe kwa njia nzuri hivyo. Na hilo linaweza kumfanya mume achunguze mafundisho ya mke wake Mkristo na mwishowe anaweza kukubali kweli.

8, 9. Mke Mkristo anaweza kufanya nini ikiwa mume wake ambaye si mwamini hathamini mwenendo wake mzuri?

8 Namna gani ikiwa mume ambaye si mwamini hathamini mwenendo mzuri wa mke wake? Maandiko yanamtia moyo mke Mkristo aonyeshe sifa za Kikristo nyakati zote, hata inapokuwa vigumu sana kufanya hivyo. Kwa mfano, tunasoma hivi kwenye 1 Wakorintho 13:4: “Upendo ni wenye ustahimilivu.” Hivyo basi, ni vizuri mke Mkristo aendelee kujiendesha kwa ‘unyenyekevu kamili wa akili na upole, na ustahimilivu,’ huku akivumilia hali hiyo kwa upendo. (Efe. 4:2) Kwa msaada wa nguvu ya utendaji ya Mungu, yaani, roho takatifu, tunaweza kuendelea kuonyesha sifa za Kikristo hata chini ya hali ngumu.

9 Paulo aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Flp. 4:13) Roho ya Mungu inamwezesha mwenzi wa ndoa Mkristo kufanya mambo mengi ambayo hangeweza kufanya. Kwa mfano, akitendewa vibaya na mwenzi wake wa ndoa anaweza kushawishiwa kulipiza kisasi. Hata hivyo, Biblia inawaambia hivi Wakristo wote: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Rom. 12:17-19) Pia, andiko la 1 Wathesalonike 5:15 linatushauri hivi: “Angalieni kwamba mtu asimlipe mwingine yeyote ubaya kwa ubaya, bali sikuzote fuatilieni yaliyo mema kuelekea mtu na mwenzake na kwa wengine wote.” Kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova, tunaweza kufanya mambo ambayo hatuwezi kufanya kwa uwezo wetu. Inafaa kama nini kwetu kusali ili roho takatifu ya Mungu itupe nguvu tunazohitaji!

10. Yesu alitenda jinsi gani watu waliposema au kumtendea kwa njia isiyo ya fadhili?

10 Yesu aliweka mfano mzuri sana katika kushughulika na watu ambao walisema au kumtendea mambo mabaya. Andiko la 1 Petro 2:23 linasema: “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.” Tunahimizwa tufuate mfano wake mzuri. Usikasirishwe na matendo mabaya ya wengine. Kama Wakristo wote wanavyoshauriwa, uwe ‘mwenye huruma nyororo, mnyenyekevu katika akili, usilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano.’—1 Pet. 3:8, 9.

Je, Mke Anapaswa Kunyamaza Tu Katika Ndoa?

11. Wanawake fulani Wakristo watashiriki katika pendeleo gani kubwa?

11 Je, kujitiisha kwa ukichwa wa mume kunamaanisha kwamba wanawake wanapaswa kunyamaza tu katika ndoa, na hawapaswi kusema jambo lolote kuhusu mambo ya familia au mambo mengine? Hapana. Yehova amewapa wanawake na pia wanaume mapendeleo mengi. Hebu fikiria pendeleo kubwa ambalo wale 144,000 wamepewa la kuwa wafalme na makuhani mbinguni chini ya Kristo atakapotawala juu ya dunia! Hesabu hiyo inatia ndani wanawake. (Gal. 3:26-29) Bila shaka, Yehova amewapa wanawake daraka la maana katika mpango wake wa mambo.

12, 13. Toa mfano unaoonyesha kwamba wanawake walitoa unabii.

12 Kwa mfano, katika nyakati za Biblia, wanawake fulani walitoa unabii. Andiko la Yoeli 2:28, 29 lilitabiri hivi: “Nitaimimina roho yangu juu ya kila namna ya mwili, na wana wenu na binti zenu watatoa unabii. . . . Na hata juu ya watumishi wa kiume na juu ya wajakazi katika siku hizo nitaimimina roho yangu.”

13 Wanafunzi 120 hivi wa Yesu ambao walikusanyika katika chumba cha juu huko Yerusalemu katika siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., walitia ndani wanawake na wanaume pia. Roho ya Mungu ilimiminwa juu ya kikundi hicho chote. Ndiyo sababu Petro alitaja maneno yaliyotabiriwa na nabii Yoeli kuwahusu wanaume na wanawake pia. Petro alisema hivi: “Hili ndilo lililosemwa kupitia nabii Yoeli, ‘Na katika siku za mwisho,’ Mungu asema, ‘Nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila namna ya mwili, nao wana wenu na binti zenu watatoa unabii . . . ; na hata juu ya watumwa wangu na juu ya wajakazi wangu nitaimimina sehemu ya roho yangu katika siku hizo, nao watatoa unabii.’”—Mdo. 2:16-18.

14. Wanawake walitimiza sehemu gani katika kueneza Ukristo katika karne ya kwanza?

14 Katika karne ya kwanza, wanawake walitimiza sehemu ya maana sana katika kueneza Ukristo. Waliwahubiria wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na walifanya mambo mengine yaliyohusiana na kazi ya kuhubiri. (Luka 8:1-3) Kwa mfano, mtume Paulo alimtaja Fibi kuwa “mhudumu wa kutaniko lililo katika Kenkrea.” Na alipotuma salamu kwa wafanyakazi wenzake, Paulo aliwataja wanawake fulani waaminifu kutia ndani “Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana.” Pia alimtaja “Persisi mpendwa wetu, kwa maana mwanamke huyo alifanya kazi nyingi katika Bwana.”—Rom. 16:1, 12.

15. Wanawake wanatimiza sehemu gani katika kueneza Ukristo siku zetu?

15 Katika siku zetu, kati ya watu milioni saba wanaohubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote, wengi wao ni wanawake wenye umri mbalimbali. (Mt. 24:14) Wengi kati ya wanawake hao ni wahudumu wa wakati wote, wamishonari, na Wanabetheli. Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.” (Zab. 68:11) Maneno hayo yamethibitika kuwa ya kweli! Yehova anathamini sehemu ambayo wanawake wanatimiza katika kutangaza habari njema na kutimiza makusudi yake. Bila shaka, takwa lake la kwamba wanawake wanapaswa kujitiisha halimaanishi kuwa wanapaswa kujitiisha kwa kunyamaza tu.

Wanawake Wawili Ambao Hawakunyamaza Tu

16, 17. Mfano wa Sara unaonyesha jinsi gani kwamba wanawake hawapaswi kunyamaza tu katika ndoa?

16 Ikiwa Yehova anawapa wanawake mapendeleo mengi, je, waume hawapaswi kuzungumza na wake zao kabla ya kufanya maamuzi mazito? Ni jambo la hekima kwa waume kufanya hivyo. Maandiko yanataja wake fulani ambao walitoa maoni yao au walichukua hatua hata bila kuombwa maoni na waume zao. Fikiria mifano miwili.

17 Sara, mke wa mzee wa ukoo Abrahamu, alizidi kumwambia amfukuze mke wake wa pili na mwana wake kwa sababu walikosa heshima. ‘Jambo hilo halikumpendeza Abrahamu hata kidogo,’ lakini si Mungu. Yehova alimwambia Abrahamu hivi: “Usiruhusu jambo lolote ambalo Sara anazidi kukuambia liwe lisilokupendeza juu ya huyo mvulana na juu ya kijakazi wako. Sikiliza sauti yake.” (Mwa. 21:8-12) Abrahamu alimtii Yehova, akamsikiliza Sara, naye akafanya jambo ambalo Sara aliomba.

18. Abigaili alichukua hatua gani?

18 Mfikirie pia Abigaili, mke wa Nabali. Daudi alipokuwa akimkimbia Mfalme Sauli mwenye wivu, alipiga kambi kwa muda karibu na makundi ya Nabali. Badala ya kuchukua kitu chochote kutoka katika vitu vingi vya mwanamume huyo tajiri, Daudi na wanaume wake walilinda mali yake. Hata hivyo, Nabali “alikuwa mkali na mwenye matendo mabaya,” naye ‘aliwakemea wanaume wa Daudi kwa sauti kali.’ Alikuwa “mtu asiyefaa kitu,” na ‘ukosefu wa akili ulikuwa pamoja naye.’ Wanaume wa Daudi walipoomba kwa heshima chakula kidogo, Nabali alikataa kuwapa. Abigaili alifanya nini aliposikia jambo lililotukia? Bila kumwambia Nabali, ‘alifanya haraka, akachukua mikate mia mbili na mitungi miwili mikubwa ya divai na kondoo watano na vipimo vitano vya sea vya nafaka iliyochomwa na keki mia moja za zabibu kavu na keki mia mbili za tini zilizoshinikizwa’ na kumpa Daudi na wanaume wake. Je, Abigaili alifanya jambo linalofaa? Biblia inasema: “Yehova akampiga Nabali, naye akafa.” Baadaye, Daudi alimwoa Abigaili.—1 Sam. 25:3, 14-19, 23-25, 38-42.

‘Mwanamke Anayejiletea Sifa’

19, 20. Kwa kweli ni nini kinachomfanya mwanamke astahili kusifiwa?

19 Maandiko yanampongeza mke anayefanya mambo kwa njia ya Yehova. Kitabu cha Biblia cha Methali kinamsifu “mke mwenye uwezo,” na kinasema hivi kumhusu: “Thamani yake inapita sana ile ya marijani. Moyo wa mume wake umemtegemea, wala hakuna faida inayokosekana. Amemthawabisha mume wake kwa mema, wala si kwa mabaya, siku zote za maisha yake.” Zaidi ya hayo, yeye “hufungua kinywa chake kwa hekima, na sheria ya fadhili zenye upendo ziko katika ulimi wake. Anaangalia shughuli za nyumba yake, wala hali mkate wa uvivu. Wanawe wamesimama na kumtangaza kuwa mwenye furaha, mume wake husimama, naye humsifu.”—Met. 31:10-12, 26-28.

20 Kwa kweli ni nini kinachomfanya mwanamke astahili sifa? Methali 31:30 inasema: “Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.” Kumwogopa Yehova kunatia ndani kujitiisha kwa kupenda chini ya mpango wa ukichwa ulioanzishwa na Mungu. “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume,” kama vile tu “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo,” na “kichwa cha Kristo ni Mungu.”—1 Kor. 11:3.

Mshukuru Mungu kwa Ajili ya Zawadi Ambayo Amekupa

21, 22. (a) Wakristo waliofunga ndoa wana sababu gani za kumshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi ya ndoa? (b) Kwa nini tunapaswa kuheshimu mipango ya Yehova ya mamlaka na ukichwa? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.)

21 Wakristo waliofunga ndoa wana sababu nyingi sana za kumshukuru Mungu! Wanaweza kutembea bega kwa bega wakiwa wenzi wa ndoa wenye furaha. Wanapaswa hasa kumshukuru Mungu kwa kuwapa zawadi yenye baraka ya ndoa kwa sababu inawapa nafasi ya kuungana katika maisha na kutembea pamoja na Yehova. (Rut. 1:9; Mika 6:8) Akiwa ndiye Mwanzilishi wa ndoa, Yehova anajua kile tunachohitaji hasa ili tupate furaha katika ndoa. Sikuzote fanyeni mambo kwa njia yake, na ‘shangwe ya Yehova itakuwa ngome yenu,’ hata katika ulimwengu huu wenye misukosuko.—Neh. 8:10.

22 Mume Mkristo ambaye anampenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe atatumia ukichwa wake kwa njia ya upole na fadhili. Atampenda kikweli mke wake, kwa kuwa mke huyo anayemwogopa Mungu atamuunga mkono na kumheshimu sana. Na jambo la maana hata zaidi ni kwamba ndoa yao ambayo ni mfano mzuri itamletea heshima Mungu wetu anayestahili kusifiwa, Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Yehova ameweka mpango gani wa ukichwa na kujitiisha?

• Kwa nini wenzi wa ndoa wanapaswa kuonyeshana heshima?

• Mke ambaye ni mwamini anapaswa kumtendea namna gani mume wake ambaye si mwamini?

• Kwa nini waume wanapaswa kuzungumza na wake zao kabla ya kufanya maamuzi mazito?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Kwa Nini Unapaswa Kuheshimu Mamlaka?

Yehova ameweka mipango ya mamlaka na ukichwa kati ya viumbe wake wenye akili. Amefanya mipango hiyo kwa faida ya wanadamu na viumbe wake wa roho. Mipango hiyo inawapa nafasi ya kutumia uhuru wao wa kuchagua na kumheshimu Mungu kwa kumtumikia kwa umoja na upatano.—Zab. 133:1.

Kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta linatambua mamlaka na ukichwa wa Yesu Kristo. (Efe. 1:22, 23) Ili kuonyesha kwamba anatambua mamlaka ya Yehova, mwishowe ‘Mwana mwenyewe atajitiisha pia kwa Yeye aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.’ (1 Kor. 15:27, 28) Basi, inafaa kama nini kwamba wanadamu waliojiweka wakfu kwa Mungu waunge mkono mpango wa ukichwa katika kutaniko na katika familia! (1 Kor. 11:3; Ebr. 13:17) Tunapofanya hivyo, tunafaidika kwa sababu Yehova anatukubali na kutubariki.—Isa. 48:17.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Sala inaweza kumsaidia mke Mkristo kuonyesha sifa zinazompendeza Mungu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova anathamini daraka ambalo wanawake wanatimiza katika kuendeleza kazi ya Ufalme