Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Kulijenga Kutaniko

Endeleeni Kulijenga Kutaniko

Endeleeni Kulijenga Kutaniko

“Endeleeni kufarijiana na kujengana.”—1 THE. 5:11.

1. Tunapata baraka gani tunaposhirikiana na kutaniko la Kikristo, lakini ni matatizo gani ambayo tunaendelea kupambana nayo?

KWA kweli, kuwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo ni baraka kubwa sana. Una uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Unapotegemea Neno lake ili likuongoze unalindwa kutokana na matokeo mabaya ya mtindo wa maisha usio wa Kikristo. Una marafiki wengi wa kweli ambao wanataka ufanikiwe. Ndiyo, baraka ni nyingi. Hata hivyo, Wakristo wengi wanapambana na matatizo ya aina mbalimbali. Huenda wengine wao wanahitaji msaada ili kuelewa mambo mazito zaidi ya Neno la Mungu. Wengine ni wagonjwa au wameshuka moyo, au huenda wanapatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kufanya maamuzi yasiyo ya hekima. Na sote tunalazimika kuishi katika ulimwengu huu usiomwogopa Mungu.

2. Tunapaswa kufanya nini ndugu zetu wanapopatwa na matatizo, na kwa nini?

2 Hakuna yeyote kati yetu anayetaka kuona Wakristo wenzetu wakiteseka au kupambana na hali ngumu. Mtume Paulo alilinganisha kutaniko na mwili na akasema kwamba “kiungo kimoja kikiumia, vile viungo vingine vyote huumia pamoja nacho.” (1 Kor. 12:12, 26) Katika hali kama hizo, tunapaswa kujitahidi kuwasaidia ndugu na dada zetu. Kuna masimulizi mengi ya Biblia yanayoonyesha jinsi washiriki wa kutaniko walivyowasaidia wengine kupambana na matatizo fulani na kuyashinda. Tunapochunguza masimulizi hayo, fikiria jinsi unavyoweza kusaidia katika njia kama zile zinazoelezwa katika masimulizi hayo. Unaweza kuwasaidia jinsi gani kiroho ndugu zako na hivyo kulijenga kutaniko la Yehova?

“Wakamchukua”

3, 4. Akila na Prisila walimsaidia Apolo katika njia gani?

3 Apolo alipohamia Efeso, tayari alikuwa mweneza-injili mwenye bidii. Simulizi la kitabu cha Matendo linasema hivi: “Kwa kuwa alikuwa amewaka roho, akaanza kusema na kuyafundisha kwa usahihi mambo juu ya Yesu, lakini akiwa anaufahamu ubatizo wa Yohana tu.” Kwa kuwa Apolo hakujua mtu anapaswa kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu” inaelekea hilo lilimaanisha kwamba huenda alihubiriwa na wanafunzi wa Yohana Mbatizaji au na wafuasi wa Yesu kabla ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Ingawa Apolo alikuwa mwenye bidii, hakuelewa mambo fulani. Kushirikiana na waamini wenzake kulimsaidia jinsi gani?—Mdo. 1:4, 5; 18:25; Mt. 28:19.

4 Wenzi wa ndoa Wakristo, Akila na Prisila walimsikia Apolo akisema kwa ujasiri katika sinagogi, wakamchukua, na kumfundisha mambo mengi zaidi. (Soma Matendo 18:24-26.) Walimtendea kwa njia ya upendo. Bila shaka, Akila na Prisila walizungumza na Apolo kwa njia ya busara na kumsaidia. Hawakumfanya ahisi kwamba anachambuliwa. Tatizo ni kwamba hakujua tu historia ya kutaniko la Kikristo la mapema. Na bila shaka Apolo aliwashukuru sana marafiki wake wapya kwa kumweleza habari hizo za maana sana. Baada ya kujua habari hizo, Apolo ‘aliwasaidia sana’ ndugu zake huko Akaya naye akatoa ushahidi wenye nguvu.—Mdo. 18:27, 28.

5. Maelfu ya wahubiri wa Ufalme wanatoa msaada gani wenye upendo, na wanapata matokeo gani?

5 Watu wengi walio katika kutaniko la Kikristo leo wanawathamini sana wale ambao waliwasaidia kuielewa Biblia. Wanafunzi wengi wameanzisha urafiki wenye kudumu pamoja na walimu wao wa Biblia. Mara nyingi, ili kuwasaidia watu waielewe kweli tunahitaji kupanga mambo ili kuwa na mazungumzo ya kawaida pamoja nao kwa miezi mingi. Hata hivyo, wahubiri wa Ufalme wako tayari kujidhabihu kwa sababu wanatambua kwamba uhai wa watu unahusika. (Yoh. 17:3) Na tunashangilia kama nini kuona watu wakielewa kweli, wakiishi kulingana na kweli hiyo, na kutumia maisha yao kufanya mapenzi ya Yehova!

“Alishuhudiwa Vema”

6, 7. (a) Kwa nini Paulo alimchagua Timotheo ili asafiri pamoja naye? (b) Timotheo alisaidiwa kufanya maendeleo gani?

6 Mtume Paulo na mtume Sila walipotembelea Listra wakati wa safari yao ya pili ya umishonari, walimpata kijana mmoja aliyeitwa Timotheo, ambaye labda alikuwa katika miaka ya mwisho ya utineja au alikuwa na umri wa miaka 20 hivi. “Alishuhudiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikoniamu.” Mama ya Timotheo, Eunike, na nyanya yake Loisi, walikuwa Wakristo waliojiweka wakfu kwa Mungu, lakini baba yake hakuwa mwamini. (2 Tim. 1:5) Huenda Paulo alifahamiana na familia hiyo katika safari yake ya kwanza katika eneo hilo miaka fulani mapema. Lakini sasa mtume huyo alipendezwa kwa njia ya pekee na Timotheo kwa sababu alionekana kuwa kijana wa pekee. Hivyo, baada ya kukubaliwa na baraza la wazee la kwao, Timotheo akawa msaidizi wa Paulo katika kazi ya umishonari.—Soma Matendo 16:1-3.

7 Timotheo alikuwa na mambo mengi ya kujifunza kutoka kwa huyo rafiki yake mwenye umri mkubwa. Na alifanya maendeleo makubwa hivi kwamba baada ya muda, Paulo akiwa na uhakika, alimtuma Timotheo kutembelea makutaniko na kuwa mwakilishi wake. Katika muda wa miaka 15 au zaidi ambayo Timotheo alifurahia kushirikiana na Paulo, kijana huyo ambaye hakuwa na uzoefu na ambaye labda alikuwa mwenye haya alifanya maendeleo kufikia kuwa mwangalizi mzuri sana.—Flp. 2:19-22; 1 Tim. 1:3.

8, 9. Washiriki wa kutaniko wanaweza kufanya nini ili kuwatia moyo vijana? Toa mfano.

8 Vijana wengi wanaume na wanawake katika kutaniko la Kikristo leo wana uwezo mkubwa. Ikiwa watatiwa moyo na kusaidiwa na waabudu wenzao ambao wanathamini mambo ya kiroho, vijana hao wanaweza kufikia na kukubali mapendeleo makubwa zaidi kati ya watu wa Yehova. Chunguza katika kutaniko lenu! Je, unaona vijana wowote ambao wanaweza kujitolea kutumika, kama alivyofanya Timotheo? Ukiwasaidia na kuwatia moyo, wanaweza kuwa mapainia, Wanabetheli, wamishonari, au waangalizi wanaosafiri. Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia wafikie miradi kama hiyo?

9 Martin, ambaye amekuwa mshiriki wa familia ya Betheli kwa miaka 20, anakumbuka kwa shukrani jinsi mwangalizi mmoja wa mzunguko alivyopendezwa naye miaka 30 iliyopita walipokuwa pamoja katika utumishi wa shambani. Mwangalizi huyo alizungumza kwa shauku kuhusu utumishi wake mwenyewe wa Betheli alipokuwa kijana. Alimtia moyo Martin afikirie uwezekano wa kuwa tayari kujitoa ili kutumiwa na tengenezo la Yehova katika njia hiyohiyo. Martin anahisi kwamba mazungumzo hayo ambayo hawezi kuyasahau yalikuwa na uvutano mkubwa sana juu ya maamuzi aliyofanya baadaye. Ni nani anayejua mambo mazuri ambayo unaweza kuwachochea marafiki wako vijana watimize ukizungumza nao kuhusu miradi ya kiroho?

“Semeni kwa Kuzifariji Nafsi Zilizohuzunika”

10. Epafrodito alihisi namna gani, na kwa nini?

10 Epafrodito alifunga safari ndefu na yenye kuchosha kutoka Filipi mpaka Roma ili kumtembelea mtume Paulo, aliyekuwa amefungwa kwa sababu ya imani yake. Msafiri huyo alikuwa mjumbe wa Wafilipi. Alipeleka zawadi zao kwa mtume Paulo na pia alipanga kubaki naye ili afanye jambo lolote ambalo lingemsaidia mtume huyo katika hali yake ngumu. Hata hivyo, akiwa huko Roma, Epafrodito alikuwa mgonjwa “karibu kufa.” Akihisi kwamba alikuwa ameshindwa kutimiza kazi iliyompeleka huko, Epafrodito alishuka moyo.—Flp. 2:25-27.

11. (a) Kwa nini hatupaswi kushangaa ikiwa watu fulani katika kutaniko wameshuka moyo? (b) Katika kisa cha Epafrodito, Paulo alipendekeza nini?

11 Mikazo mbalimbali inafanya watu washuke moyo leo. Idadi zinazotolewa na Shirika la Afya Ulimwenguni zinaonyesha kwamba mtu 1 kati ya watu 5 huenda akapatwa na ugonjwa wa kushuka moyo pindi fulani katika maisha yake. Watu wa Yehova pia wanashuka moyo. Matatizo ya kutimiza mahitaji ya familia, magonjwa, kuvunjika moyo kwa sababu ya makosa ya kibinafsi, au mambo mengine huenda yakachangia hali ya kushuka moyo. Wafilipi wangemsaidia Epafrodito jinsi gani? Paulo aliandika hivi: “Mkaribisheni kama ilivyo desturi katika Bwana kwa shangwe yote; nanyi mwendelee kuwaheshimu sana watu wa namna hiyo, kwa sababu alikaribia sana kufa kwa ajili ya kazi ya Bwana, akiihatarisha nafsi yake, ili ajazie kikamilifu kutokuwapo kwenu hapa ili kunitolea mimi utumishi wa kibinafsi.”—Flp. 2:29, 30.

12. Ni nini kinachoweza kumfariji mtu aliyeshuka moyo?

12 Sisi pia tunapaswa kuwatia moyo ndugu ambao wamevunjika moyo au kushuka moyo. Bila shaka, tunaweza kuwatajia mambo mazuri ambayo wanatimiza katika utumishi wa Yehova. Labda wamefanya mabadiliko makubwa katika maisha yao ili kuwa Wakristo au kutumika katika utumishi wa wakati wote. Tunathamini jitihada hizo, na tunaweza kuwahakikishia kwamba Yehova pia anathamini jitihada zao. Ingawa umri mkubwa au magonjwa yanawazuia waaminifu fulani kutofanya mambo ambayo walikuwa wakifanya zamani, bado wanastahili kuheshimiwa sana kwa sababu ya miaka yao mingi ya utumishi. Hata wakikabili hali gani, Yehova anawapa waaminifu wake wote shauri hili: “Semeni kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika, tegemezeni walio dhaifu, iweni wenye ustahimilivu kuelekea wote.”—1 The. 5:14.

“Mnapaswa Kumsamehe kwa Fadhili na Kumfariji”

13, 14. (a) Ni hatua gani nzito ambayo kutaniko la Korintho lilichukua, na kwa nini? (b) Hatua ya kumtenga na ushirika mtu huyo ilikuwa na matokeo gani?

13 Katika kutaniko la Korintho la karne ya kwanza kulikuwa na mwanamume mmoja aliyezoea kufanya uasherati bila kutubu. Mwenendo wake ulitishia usafi wa kutaniko na ulileta aibu kubwa hata kati ya watu wasio waamini. Hivyo, kwa kufaa Paulo aliamuru kwamba mwanamume huyo aondolewe katika kutaniko.—1 Kor. 5:1, 7, 11-13.

14 Nidhamu hiyo ilikuwa na matokeo mazuri. Kutaniko hilo lililindwa kutokana na uvutano mbaya, na mtenda-dhambi huyo alisaidiwa kurudiwa na akili zake na kutubu kikweli. Kwa kuwa matendo ya mwanamume huyo yalionyesha kwamba ametubu, Paulo alisema katika barua yake ya pili kwa kutaniko hilo kwamba mwanamume huyo alistahili kurudishwa. Hata hivyo, mengi zaidi yalihitajiwa. Paulo aliamuru pia kwamba kutaniko ‘limsamehe kwa fadhili na kumfariji mtenda-dhambi huyo aliyetubu, ili kwa njia fulani mtu huyo asimezwe na huzuni yake ya kupita kiasi.’—Soma 2 Wakorintho 2:5-8.

15. Tunapaswa kuwaona jinsi gani wakosaji wanaotubu ambao wanarudishwa katika kutaniko?

15 Tunajifunza nini kutokana na simulizi hilo? Tunahuzunika tunapoona watu wakitengwa na ushirika. Huenda wameleta suto juu ya jina la Mungu na kuliaibisha kutaniko. Huenda hata wametutendea dhambi sisi binafsi. Hata hivyo, wazee waliowekwa rasmi kuchunguza kisa hicho wanapoamua kulingana na mwongozo wa Yehova kwamba mtenda-dhambi aliyetubu anapaswa kurudishwa katika kutaniko, hilo linaonyesha kwamba mtu huyo amesamehewa na Yehova. (Mt. 18:17-20) Je, hatupaswi kujitahidi kumwiga Yehova? Kwa kweli, kuwa wagumu na wasiosamehe kungemaanisha kwamba tunampinga Yehova. Ili kuchangia amani na umoja wa kutaniko la Mungu na hivyo kukubaliwa na Yehova, je, hatupaswi ‘kuwahakikishia upendo wetu’ watenda-dhambi wanaotubu kikweli na kurudishwa?—Mt. 6:14, 15; Luka 15:7.

“Yeye Ni Mwenye Faida Kwangu”

16. Kwa nini Paulo alivunjwa moyo na Marko?

16 Simulizi lingine la Biblia linaonyesha kwamba hatupaswi kuwawekea kinyongo wale ambao wametuvunja moyo. Kwa mfano, Yohana Marko, alimvunja moyo sana mtume Paulo. Jinsi gani? Paulo na Barnaba walipoanza safari yao ya kwanza ya umishonari, Marko alienda pamoja nao ili kuwasaidia. Lakini walipokuwa katika safari hiyo, Yohana Marko aliwaacha wenzake na kurudi nyumbani kwa sababu ambayo haitajwi. Paulo alivunjwa moyo sana na uamuzi huo hivi kwamba walipokuwa wakipanga safari yao ya pili, alikosana na Barnaba kuhusu uamuzi wa kwenda na Marko tena. Kwa sababu ya yale yaliyotukia katika safari ya kwanza, Paulo hakutaka Marko asafiri nao.—Soma Matendo 13:1-5, 13; 15:37, 38.

17, 18. Tunajua jinsi gani kwamba tatizo kati ya Paulo na Marko lilitatuliwa, na tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo hilo?

17 Ni wazi kwamba Marko hakujiruhusu avunjike moyo kupita kiasi kwa sababu ya kukataliwa na Paulo, kwa kuwa aliendelea na kazi yake ya umishonari katika eneo lingine akiwa pamoja na Barnaba. (Mdo. 15:39) Yale ambayo Paulo aliandika kuhusu Marko miaka fulani baadaye yanaonyesha kwamba Marko alithibitika kuwa mwaminifu na mwenye kutegemeka. Paulo, akiwa sasa mfungwa huko Roma, aliandika barua akimwomba Timotheo aje kumtembelea. Katika barua hiyohiyo, Paulo alisema hivi: “Umchukue Marko na uje pamoja naye, kwa maana yeye ni mwenye faida kwangu kwa ajili ya huduma.” (2 Tim. 4:11) Ndiyo, sasa Paulo aliamini kwamba Marko alikuwa amefanya maendeleo makubwa.

18 Tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na simulizi hilo. Marko alisitawisha sifa za kuwa mmishonari mzuri. Hakukwazika kwa sababu alikataliwa na Paulo mwanzoni. Marko na Paulo walikuwa wanaume wa kiroho, na hawakuwa na uadui wa kudumu kati yao. Badala yake, Paulo alitambua baadaye kwamba Marko alikuwa msaidizi mwenye faida. Hivyo, ndugu wanapotatua matatizo kati yao, jambo zuri la kufanya ni kusonga mbele na kuendelea kuwasaidia wengine wafanye maendeleo ya kiroho. Kutambua sifa nzuri za wengine kunajenga kutaniko.

Uhusiano Wako na Kutaniko

19. Ni nini kinachoweza kuwasaidia washiriki wote wa kutaniko la Kikristo kusaidiana?

19 Katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” unahitaji msaada wa ndugu na dada zako katika kutaniko, nao wanahitaji msaada wako. (2 Tim. 3:1) Huenda Wakristo fulani wasijue sikuzote hatua ya kuchukua ili kufaulu kushughulikia hali wanazokabiliana nazo, lakini Yehova anajua. Naye anaweza kutumia washiriki mbalimbali wa kutaniko, kutia ndani wewe, ili kuwasaidia wengine wafuate njia iliyo sawa. (Isa. 30:20, 21; 32:1, 2) Hivyo basi, fuata himizo hili la mtume Paulo! Endeleeni “kufarijiana na kujengana, kama vile mnavyofanya.”—1 The. 5:11.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunahitaji kuwajenga wengine katika kutaniko la Kikristo?

• Unaweza kuwasaidia wengine kushinda matatizo ya aina gani?

• Kwa nini tunahitaji msaada wa wengine katika kutaniko letu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

Mkristo mwenzetu anapopambana na hali ngumu, tunaweza kumsaidia

[Picha katika ukurasa wa 12]

Vijana wengi wanaume na wanawake katika kutaniko la Kikristo leo wana uwezo mkubwa