Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Endeleeni Kuushinda Uovu’ kwa Kuizuia Hasira

‘Endeleeni Kuushinda Uovu’ kwa Kuizuia Hasira

‘Endeleeni Kuushinda Uovu’ kwa Kuizuia Hasira

‘Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe, bali endeleeni kuushinda uovu kwa wema.’—ROM. 12:19, 21.

1, 2. Mashahidi fulani waliokuwa wakisafiri walionyesha mfano gani mzuri?

MASHAHIDI WA YEHOVA 34 walikuwa wakisafiri ili kuhudhuria programu ya kuweka wakfu ofisi moja ya tawi lakini ndege ikachelewa kwa sababu ya matatizo ya kiufundi. Ndege hiyo ilitazamiwa kutua kwa muda wa saa moja ili iongezwe mafuta, hata hivyo, ilikaa kwa muda wa saa 44 kwenye uwanja huo ulio mbali sana ambao hauna chakula, maji, wala vyoo vya kutosha. Wasafiri wengi walikasirika na kuwatisha wafanyakazi wa uwanja wa ndege. Lakini akina ndugu na dada walikuwa watulivu.

2 Mwishowe, Mashahidi hao walifika mahali walipokuwa wakienda na kupata sehemu ya mwisho ya programu ya wakfu. Ingawa walikuwa wamechoka, hawakuondoka baada ya programu, walifurahia kuzungumza na ndugu wa nchi hiyo. Baadaye, walipata habari kwamba kuna watu ambao waliona jinsi walivyoonyesha subira na kujizuia. Msafiri mmoja aliwaambia hivi wafanyakazi wa kampuni hiyo ya ndege: “Kama si hao Wakristo 34 waliokuwa katika ndege hiyo, kungekuwa na fujo kwenye uwanja wa ndege.”

Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Hasira

3, 4. (a) Hasira yenye jeuri ilianza jinsi gani katika jamii ya wanadamu na imekuwapo kwa muda mrefu kadiri gani? (b) Je, Kaini angeweza kuizuia hasira yake? Eleza.

3 Mikazo ya maisha katika mfumo huu mwovu wa mambo inaweza kuwafanya watu wakasirike. (Mhu. 7:7) Mara nyingi, hasira hiyo inatokeza chuki na hata jeuri. Kuna vita vikali ndani ya nchi nyingi na kati ya nchi mbalimbali, na mikazo katika familia inasababisha ugomvi katika nyumba nyingi. Hasira na jeuri kama hiyo ilianza zamani sana. Kaini, mwana wa kwanza wa Adamu na Hawa, alimuua ndugu yake mdogo Abeli kwa sababu ya hasira iliyochochewa na wivu. Kaini alitenda tendo hilo ovu hata ingawa Yehova alikuwa amemsihi azuie hasira yake na kumwahidi kwamba angembariki ikiwa angefanya hivyo.—Soma Mwanzo 4:6-8.

4 Hata ingawa alirithi hali ya kutokamilika, Kaini angeweza kuchagua jambo la kufanya. Angeweza kuzuia hasira yake. Kwa hiyo, alikuwa na hatia kwa sababu ya tendo lake la jeuri. Vivyo hivyo, hali yetu ya kutokuwa wakamilifu inafanya iwe vigumu zaidi kwetu kuepuka hasira na matendo ya hasira. Pia, matatizo mengine mazito yanaweza kuzidisha mikazo katika ‘nyakati hizi za hatari.’ (2 Tim. 3:1) Kwa mfano, tunaweza kupata mikazo ya kihisia kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi. Polisi na mashirika ya kusaidia familia yanasema kwamba misukosuko ya kiuchumi inasababisha kuongezeka kwa milipuko ya hasira na jeuri nyumbani.

5, 6. Ni mtazamo gani wa ulimwengu kuhusu hasira unaoweza kuwa na uvutano juu yetu?

5 Zaidi ya hayo, watu wengi tunaokutana nao ni “wenye kujipenda wenyewe,” “wenye majivuno,” na hata ni “wakali.” Ni rahisi sana kwetu kuiga sifa mbaya kama hizo na zinaweza hata kutufanya tuwe na hasira. (2 Tim. 3:2-5) Kwa kweli, mara nyingi sinema na programu za televisheni zinaonyesha kwamba kulipiza kisasi ni jambo zuri na kutenda kijeuri ni njia ya kawaida na inayokubalika ya kusuluhisha matatizo. Kwa kawaida, sinema zinazopendwa zinawafanya watazamaji wangoje kwa hamu kumwona adui “akipata kile anachostahili,” kwa kawaida anaangamizwa kwa jeuri na shujaa wa sinema hiyo.

6 Propaganda kama hizo hazifundishi njia za Mungu, badala yake zinasitawisha “roho ya ulimwengu” na ya mtawala wake mwenye hasira, Shetani. (1 Kor. 2:12; Efe. 2:2; Ufu. 12:12) Roho hiyo inawachochea watu kutosheleza tamaa za mwili wenye dhambi na inapingana kabisa na roho takatifu ya Mungu na tunda lake. Kwa kweli, fundisho la msingi la Ukristo ni kutolipiza kisasi unapochokozwa. (Soma Mathayo 5:39, 44, 45.) Basi, tunaweza jinsi gani kufuata kikamili zaidi mafundisho ya Yesu?

Mifano Mizuri na Mibaya

7. Ni nini kilichotukia Simeoni na Lawi walipokosa kuzuia hasira yao?

7 Biblia ina mashauri mengi kuhusu kuzuia hasira na pia ina mifano halisi inayoonyesha matokeo ya kufanya hivyo na kutofanya hivyo. Fikiria kilichotukia wakati Simeoni na Lawi, wana wa Yakobo, walipolipiza kisasi juu ya Shekemu kwa sababu ya kumnajisi dada yao Dina. ‘Waliumia hisia zao, wakakasirika sana.’ (Mwa. 34:7) Kisha, wale wana wengine wa Yakobo wakashambulia mji wa Shekemu, wakapora vitu, na wakawateka nyara wanawake na watoto. Hawakufanya mambo yote hayo kwa sababu tu ya Dina bali pia inaelekea ni kwa sababu ya kiburi, yaani, hawakutaka kudharauliwa na wengine. Walihisi kwamba Shekemu alikuwa amewakosea na kumkosea baba yao, Yakobo. Lakini Yakobo alikuwa na maoni gani kuhusu mwenendo wao?

8. Simulizi la Simeoni na Lawi linaonyesha nini kuhusu kulipiza kisasi?

8 Bila shaka, msiba uliompata Dina ulimhuzunisha sana Yakobo; hata hivyo, alishutumu hatua ya watoto wake ya kulipiza kisasi. Bado Simeoni na Lawi walijaribu kutetea matendo yao, kwa kusema hivi: “Je, yeyote anapaswa kumtendea dada yetu kama kahaba?” (Mwa. 34:31) Lakini huo haukuwa mwisho wa mambo, kwa kuwa Yehova hakufurahi. Baada ya miaka mingi kupita, Yakobo alitabiri kwamba kwa sababu ya matendo ya jeuri na hasira ya Simeoni na Lawi, wazao wao wangetawanyika kati ya makabila ya Israeli. (Soma Mwanzo 49:5-7.) Ndiyo, walipoteza kibali cha Mungu na cha baba yao kwa sababu ya kutozuia hasira yao.

9. Ni wakati gani ambapo Daudi alikuwa karibu kushindwa kuzuia hasira yake?

9 Mfalme Daudi alitenda kwa njia tofauti kabisa. Alipata nafasi nyingi za kulipiza kisasi, lakini hakufanya hivyo. (1 Sam. 24:3-7) Hata hivyo, pindi moja alikuwa karibu kushindwa kuzuia hasira yake. Mwanamume fulani tajiri aliyeitwa Nabali aliwatukana kwa ukali wanaume wa Daudi, ingawa walikuwa wamelinda makundi ya Nabali na wachungaji wake. Akiwa amekasirika labda kwa sababu ya jinsi wanaume wake walivyotendewa, Daudi alikuwa karibu kulipiza kiasi kwa ukali. Daudi na wanaume wake walipokuwa wakienda kumshambulia Nabali na familia yake, kijana mmoja alimjulisha Abigaili, mke mwenye busara wa Nabali, kuhusu jambo lililotukia naye akamsihi achukue hatua. Papo hapo, Abigaili alichukua zawadi kubwa na kwenda kukutana na Daudi. Kwa unyenyekevu, aliomba msamaha kwa sababu ya ukaidi wa Nabali naye akamsihi Daudi kwa msingi wa kwamba Daudi alimwogopa Yehova. Daudi alirudiwa na fahamu zake naye akasema hivi: “Nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu.”—1 Sam. 25:2-35.

Mtazamo wa Kikristo

10. Wakristo wanapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu kulipiza kisasi?

10 Kisa cha Simeoni na Lawi na kisa cha Daudi na Abigaili kinaonyesha waziwazi kwamba Yehova anapinga hasira inayopita mipaka na jeuri na kwamba anawabariki wale wanaojitahidi kufanya amani. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’ Lakini, ‘ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe; kwa maana kwa kufanya hivyo utakusanya makaa yenye moto juu ya kichwa chake.’ Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.”—Rom. 12:18-21. *

11. Dada mmoja alijifunza jinsi gani kuzuia hasira yake?

11 Tunaweza kutumia shauri hilo. Kwa mfano, dada mmoja alilalamika kwa mzee wa kutaniko lao kuhusu msimamizi wake mpya kazini ambaye ni mwanamke. Dada huyo alisema kwamba msimamizi huyo alimwonea na hakumtendea kwa fadhili. Dada huyo alimkasirikia sana mwanamke huyo na alitaka kuacha kazi. Mzee huyo alimshauri asifanye uamuzi wa haraka-haraka. Mzee alitambua kwamba mambo yalizidi kuwa mabaya wakati dada huyo alipokasirika kwa sababu ya kutendewa vibaya na msimamizi wake. (Tito 3:1-3) Mzee alimwambia dada huyo kwamba hata ikiwa mwishowe angepata kazi nyingine, bado angehitaji kubadili njia yake ya kukabiliana na matendo yasiyo ya fadhili. Alimshauri dada huyo amtendee msimamizi wake jinsi ambavyo angependa kutendewa, kama Yesu alivyotufundisha tufanye. (Soma Luka 6:31.) Dada huyo alikubali kwamba angejaribu kufanya hivyo. Matokeo yakawa nini? Baada ya muda, yule msimamizi alibadili mtazamo wake akawa mwenye fadhili, na hata alimshukuru dada huyo kwa sababu ya kazi yake.

12. Kwa nini kutoelewana kati ya Wakristo kunaweza kutokeza maumivu zaidi?

12 Huenda tusishangae tukitendewa hivyo na mtu ambaye si mshiriki wa kutaniko la Kikristo. Tunajua kwamba mara nyingi tunatendewa kwa njia isiyo ya haki kwa kuwa tunaishi katika mfumo huu wa Shetani na hivyo tunahitaji kujitahidi ili watenda-dhambi wasitukasirishe. (Zab. 37:1-11; Mhu. 8:12, 13; 12:13, 14) Hata hivyo, matatizo yanapotokea kati yetu na ndugu na dada yetu wa kiroho tunaumia sana moyoni. Shahidi mmoja alikumbuka hivi: “Tatizo kubwa zaidi ambalo nilikabili nilipoingia katika kweli lilikuwa kukubali uhakika wa kwamba watu wa Yehova si wakamilifu.” Tulitoka katika ulimwengu usio na upendo na usiojali, tukitumaini kwamba watu wote katika kutaniko wangetendeana kwa fadhili ya Kikristo. Hivyo, Mkristo mwenzetu, hasa yule aliye na mapendeleo katika kutaniko, akitutendea bila kufikiri au kwa njia isiyo ya Kikristo, tunaweza kuumia au kukasirika. Huenda tukajiuliza: ‘Mambo kama hayo yanaweza kutokea jinsi gani kati ya watu wa Yehova?’ Kwa kweli, mambo kama hayo yalitokea hata kati ya Wakristo watiwa-mafuta katika siku za mitume. (Gal. 2:11-14; 5:15; Yak. 3:14, 15) Tunapaswa kufanya nini tukitendewa hivyo?

13. Tunapaswa kushirikiana kusuluhisha tofauti zetu jinsi gani na kwa nini?

13 Dada aliyetajwa hapo juu alisema hivi: “Nilijifunza kusali kwa ajili ya mtu yeyote anayeniumiza moyoni. Sikuzote kufanya hivyo kunanisaidia.” Kama vile ambavyo tayari tumesoma, Yesu alitufundisha kusali kwa ajili ya wale wanaotutesa. (Mt. 5:44) Basi, je, hatupaswi kusali hata zaidi kwa ajili ya ndugu na dada zetu wa kiroho? Kama vile baba anavyotaka watoto wake wapendane, ndivyo Yehova anavyotaka watumishi wake duniani wawe na uhusiano mzuri kati yao. Tunatazamia kwa hamu kuishi pamoja kwa amani na furaha milele, na Yehova anatufundisha kufanya hivyo sasa. Anataka tushirikiane katika kufanya kazi yake kuu. Kwa hiyo, acheni tusuluhishe matatizo au ‘tupite’ tu makosa na kusonga mbele kwa umoja. (Soma Methali 19:11.) Badala ya kujitenga na ndugu zetu tunapokosana, tunapaswa kusaidiana kubaki kati ya watu wa Mungu, na kukaa kwa usalama katika “mikono ya milele” ya Yehova.—Kum. 33:27, American Standard Version.

Kuwa Wapole kwa Wote Kunaleta Matokeo Mazuri

14. Tunaweza kupambana jinsi gani na uvutano wa Shetani unaotokeza migawanyiko?

14 Ili kutuzuia tusieneze habari njema, Shetani na roho wake waovu wanajaribu sana kuvuruga familia na makutaniko yenye furaha. Wanajaribu kuleta migawanyiko, kwa kuwa wanajua kwamba migawanyiko ya ndani inaweza kusababisha uharibifu. (Mt. 12:25) Ili tushinde uvutano wao mwovu, tunapaswa kufuata shauri hili la Paulo: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.” (2 Tim. 2:24) Kumbuka kwamba vita vyetu si, “juu ya damu na mwili, bali . . . juu ya majeshi ya roho waovu.” Ili tufanikiwe katika vita hivi, tunahitaji kuvaa mavazi ya silaha za kiroho, ambayo yanatia ndani “viatu vya habari njema ya amani.”—Efe. 6:12-18.

15. Tunapaswa kutenda namna gani tukishambuliwa kutoka nje ya kutaniko?

15 Maadui wa Yehova wanawashambulia vikali watu wake wenye amani kutoka nje ya kutaniko. Wengine kati ya maadui hao wanawashambulia kimwili Mashahidi wa Yehova. Wengine wanaeneza uwongo kutuhusu katika vyombo vya habari na mahakamani. Yesu aliwaambia wafuasi wake watazamie mambo hayo. (Mt. 5:11, 12) Tunapaswa kutenda namna gani? Hatupaswi kamwe ‘kulipa uovu kwa uovu,’ kwa maneno au kwa matendo.—Rom. 12:17; soma 1 Petro 3:16.

16, 17. Kutaniko moja lilikabili hali gani yenye kujaribu?

16 Hata Ibilisi akituletea majaribu gani, tunaweza kutoa ushahidi mzuri kwa “kuushinda uovu kwa wema.” Kwa mfano, kutaniko moja kwenye kisiwa kimoja cha Pasifiki lilikodi jumba fulani kwa ajili ya Ukumbusho. Wakuu wa kanisa moja walipopata habari hizo, waliwaambia wafuasi wa kanisa lao wakusanyike katika jumba hilo kwa ajili ya ibada ya kanisa siku yetu ya kuadhimisha Ukumbusho. Hata hivyo, mkuu wa polisi aliwaamuru wakuu wa kanisa hilo waondoke kwenye jumba hilo wakati huo ili Mashahidi walitumie. Lakini, wakati ulipofika, wafuasi wa kanisa hilo walijaa ndani ya jumba hilo na wakaanza ibada yao.

17 Polisi walipokuwa wakijitayarisha kuwafukuza kwa nguvu kutoka katika jumba hilo, msimamizi wa kanisa hilo alimfikia mzee wetu mmoja na kumuuliza hivi: “Je, mmepanga kufanya jambo lolote la pekee leo jioni?” Ndugu huyo alimwambia kuhusu Ukumbusho, na mwanamume huyo akamjibu hivi: “Oh, sikujua!” Papo hapo, polisi mmoja akasema hivi: “Lakini tuliwaambia leo asubuhi!” Kiongozi huyo wa kanisa alimgeukia yule mzee huku akitabasamu kwa dhihaka na kumuuliza hivi: “Sasa mtafanya nini? Watu wetu wamejaa katika jumba hili. Je, mtawaambia polisi watufukuze?” Alibadili mambo kwa ujanja ili ionekane kwamba Mashahidi ndio waliokuwa wakiwatesa! Ndugu zetu wangefanya nini?

18. Ndugu zetu walifanya nini walipokasirishwa, na matokeo yakawa nini?

18 Mashahidi waliamua kuruhusu kanisa hilo lifanye ibada ya dakika 30, na baadaye akina ndugu waadhimishe Ukumbusho. Ibada ya kanisa hilo ilipita wakati, lakini baada ya wafuasi wa kanisa hilo kuondoka, ndugu waliadhimisha Ukumbusho. Siku iliyofuata, serikali iliunda halmashauri rasmi ya kuchunguza jambo hilo. Baada ya kuchunguza ukweli wa mambo, halmashauri hiyo iliagiza kanisa hilo litangaze kwamba kiongozi wa kanisa hilo ndiye aliyesababisha tatizo hilo bali si Mashahidi. Halmashauri hiyo pia iliwashukuru Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya kushughulikia hali hiyo ngumu kwa subira. Jitihada za Mashahidi za “kufanya amani na watu wote” zilikuwa na matokeo mazuri.

19. Ni nini kingine kinachoweza kudumisha mahusiano yenye amani?

19 Jambo lingine la maana katika kudumisha mahusiano yenye amani pamoja na wengine ni kutumia maneno yenye neema. Habari inayofuata itazungumzia maana ya kutumia maneno yenye neema na jinsi tunavyoweza kusitawisha na kutumia maneno hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 “Makaa yenye moto” yalitumiwa zamani kuyeyusha mawe yenye madini ya chuma kwa kuchoma mawe hayo kwa moto juu na chini ili kupata chuma. Tunapowaonyesha fadhili watu wanaotenda bila fadhili tunaweza kuwafanya wabadili mtazamo wao na kuonyesha sifa zao nzuri.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini watu katika ulimwengu leo wana hasira sana?

• Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha matokeo ya kuzuia au kutozuia hasira?

• Tunapaswa kutenda jinsi gani Mkristo mwenzetu anapotuumiza?

• Tunapaswa kutenda jinsi gani tukishambuliwa na watu walio nje ya kutaniko?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Simeoni na Lawi walirudi—lakini baada ya kutenda kwa hasira

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuonyesha fadhili kunaweza kubadili mtazamo wa wengine