Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushughulika na Hali Mwenzi wa Ndoa Anapokusaliti

Kushughulika na Hali Mwenzi wa Ndoa Anapokusaliti

Kushughulika na Hali Mwenzi wa Ndoa Anapokusaliti

MARGARITA na mume wake Raúl, walikuwa wamemtumikia Yehova pamoja katika utumishi wa wakati wote kwa miaka mingi. * Lakini muda mfupi baada ya mtoto wao wa kwanza kuzaliwa, Raúl aliruhusu uhusiano wake na Yehova uharibike. Mwishowe, Raúl alianza kuishi maisha mapotovu kiadili na akatengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Margarita anasema hivi: “Mambo hayo yote yalipotendeka, nilihisi kwamba nitakufa. Nilivunjika moyo na sikujua jambo la kufanya.”

Mara tu baada ya kufunga ndoa, mume wa Jane alianza kukosa uaminifu na upendo kwa njia tofauti. Alianza kumpiga. Jane anasema hivi: “Mara ya kwanza aliponipiga ngumi, nilishtuka, nikaaibika, na kufedheheka. Alizoea kunipiga mara kwa mara na kuniomba msamaha. Nilifikiri kwamba nikiwa Mkristo nilikuwa na wajibu wa kumsamehe na kusahau. Nilifikiria pia kwamba ningekosa ushikamanifu ikiwa ningemwambia mtu yeyote tatizo hilo—hata wazee wa kutaniko. Zoea hilo la kupigwa na kusamehe liliendelea kwa miaka mingi. Muda huo wote, nilifikiri kwamba kuna jambo ambalo ningeweza kufanya ili mume wangu anipende. Mwishowe aliponiacha pamoja na binti yetu, nilihisi kwamba nilikuwa nimekosea, na kwamba ningejitahidi zaidi ili ndoa yetu isivunjike.”

Kama Margarita na Jane, huenda unateseka kihisia, kifedha, na kiroho kwa sababu mume wako amekusaliti. Au huenda wewe ni mume ambaye anaumia moyoni na kuteseka kwa sababu mke wako amekusaliti. Bila shaka, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” kama Biblia ilivyotabiri. Unabii huo unaonyesha kwamba katika “siku za mwisho,” familia zingekuwa na matatizo, na familia nyingi hazingekuwa kamwe na upendo wa asili. Wengine hawangeishi kulingana na dai lao la kumtumikia Mungu. (2 Tim. 3:1-5) Wakristo wa kweli pia wanapatwa na matatizo hayo; hivyo basi, ni nini kinachoweza kukusaidia kushughulika na hali mwenzi wako anapokusaliti?

Uwe na Maoni Kama ya Yehova Kujielekea

Mwanzoni, huenda ikawa vigumu kuamini kwamba mtu unayempenda amekuumiza vibaya sana. Unaweza hata kuanza kujilaumu kwa sababu ya mwenendo wake wa dhambi.

Hata hivyo, kumbuka kwamba hata mwanamume mkamilifu Yesu alisalitiwa na mtu ambaye alimwamini na kumpenda. Yesu aliwachagua washiriki wake wa karibu zaidi, yaani, mitume, baada ya kusali na kutafakari sana kuhusu jambo hilo. Wakati huo, mitume wote 12 walikuwa watumishi waaminifu wa Yehova. Kwa hiyo, bila shaka Yesu alihuzunika sana wakati ambapo Yuda ‘aligeuka na kuwa msaliti.’ (Luka 6:12-16) Hata hivyo, Yehova hakuona kwamba Yesu alikuwa na hatia kwa sababu ya matendo ya Yuda.

Ni kweli kwamba leo hakuna mwenzi wa ndoa ambaye ni mkamilifu. Wenzi wote wawili watafanya makosa. Mtunga-zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu aliandika maneno haya ya kweli: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zab. 130:3) Wenzi wote wawili wanapaswa kumwiga Yehova kwa kuwa tayari kusameheana udhaifu wao.—1 Pet. 4:8.

Hata hivyo, “kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Rom. 14:12) Ikiwa mwenzi wa ndoa amezoea kumtukana au kumtendea vibaya mwenzi wake, mwenzi huyo mwenye hatia ndiye atakayetoa hesabu mbele za Yehova. Yehova anakataza jeuri na matukano, kwa hiyo, hakuna sababu yoyote nzuri ya kumtendea mwenzi wa ndoa kwa njia hiyo inayoonyesha kwamba humpendi wala humheshimu hata kidogo. (Zab. 11:5; Efe. 5:33; Kol. 3:6-8) Kwa kweli, ikiwa Mkristo anazoea kulipuka kwa hasira bila kutubu na habadiliki, ni lazima atengwe na ushirika wa kutaniko la Kikristo. (Gal. 5:19-21; 2 Yoh. 9, 10) Mwenzi wa ndoa hapaswi kuhisi kwamba ana hatia kwa kuwa amewaambia wazee kuhusu mwenendo kama huo usio wa Kikristo. Kwa kweli, Yehova anawahurumia watu kama hao wanaotendewa vibaya.

Mwenzi wa ndoa anapofanya uzinzi, anamtendea dhambi mwenzi asiye na hatia na vilevile anamtendea dhambi Yehova. (Mt. 19:4-9; Ebr. 13:4) Ikiwa mwenzi asiye na hatia amekuwa akijitahidi kuishi kulingana na kanuni za Biblia, hana sababu ya kuhisi kwamba ana hatia kwa sababu ya dhambi ya usaliti ya mwenzi wake mzinzi.

Kumbuka kwamba Yehova anaelewa jinsi unavyohisi. Anasema kwamba yeye ni mume wa taifa la Israeli, na Neno lake lina masimulizi mengi yenye kugusa moyo yanayoonyesha jinsi alivyohuzunika kwa sababu ya matendo ya uzinzi wa kiroho ya taifa hilo. (Isa. 54:5, 6; Yer. 3:1, 6-10) Uwe na hakika kwamba Yehova anaona vizuri machozi yako ikiwa mwenzi wako anakusaliti kwa njia fulani. (Mal. 2:13, 14) Anajua kwamba unahitaji kufarijiwa na kutiwa moyo.

Jinsi Yehova Anavyotoa Faraja

Njia moja ambayo Yehova anatumia kutufariji ni kupitia kutaniko la Kikristo. Jane alisaidiwa kwa njia hiyo. Jane anasema hivi: “Mwangalizi wa mzunguko alikuja wakati ambapo nilikuwa nimeshuka moyo kabisa. Alijua jinsi nilivyokuwa nimeshuka moyo kwa sababu mume wangu alikuwa ameenda mahakamani kuomba talaka. Alitumia muda kunisaidia kutafakari kuhusu maandiko kama vile 1 Wakorintho 7:15. Maandiko hayo ya Biblia na maelezo yake yenye fadhili yalinisaidia kushinda hisia za hatia na kupata amani ya akili kwa kadiri fulani.” *

Margarita aliyetajwa mwanzoni, alijifunza pia kwamba Yehova anatoa msaada unaofaa kupitia kutaniko la Kikristo. Margarita anasema hivi: “Ilipoonekana wazi kwamba mume wangu hakuwa tayari kutubu, nilichukua watoto wangu na kuhamia mji mwingine. Nilipofika huko nilipata vyumba viwili vya kukodi. Siku iliyofuata, nilikuwa nikitoa vitu ndani ya mifuko yetu huku nikiwa nimelemewa na huzuni wakati niliposikia mtu akigonga mlango. Nilifikiria kwamba ni mwanamke mwenye nyumba hiyo, ambaye alikuwa anaishi katika nyumba iliyo karibu. Jambo la kushangaza ni kwamba dada aliyejifunza Biblia na mama yangu na kuisaidia familia yetu kujifunza kweli ndiye aliyekuwa mlangoni. Hakutazamia kunikuta katika nyumba hiyo kwa sababu alikuwa akijifunza Biblia na mwenye nyumba. Nilifurahi sana, nikashindwa kuzuia machozi yangu. Nilimwelezea hali yangu, na tukalia pamoja. Mara moja alifanya mpango ili tuhudhurie mkutano siku hiyo. Kutaniko lilitukaribisha, na wazee wakafanya mipango ya kunisaidia kushughulikia mahitaji ya kiroho ya familia yangu.”

Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia

Kwa kweli, washiriki wa kutaniko la Kikristo wanaweza kutoa msaada unaohitajiwa kwa njia nyingi. Kwa mfano, Margarita alihitaji sasa kutafuta kazi. Familia moja kutanikoni ilijitolea kuwatunza watoto wake wanapotoka shuleni.

Margarita anasema hivi: “Jambo ninalothamini sana ni wakati ndugu na dada wanapojitolea kwenda pamoja nami na watoto wangu kwenye utumishi wa shambani.” Washiriki wa kutaniko wanapotoa msaada huo unaofaa wanasaidiana ‘kubeba mizigo mizito,’ na hivyo wanatimiza “sheria ya Kristo.”—Gal. 6:2.

Wale wanaoteseka kwa sababu ya dhambi za wengine wanathamini kikweli msaada kama huo unaofaa. Monique, ambaye mume wake alimwacha na deni la dola 15,000 za Marekani na daraka la kuwalea watoto wanne, anasema hivi: “Ndugu na dada zangu wa kiroho walinionyesha upendo sana. Sifikiri kwamba ningefaulu bila msaada wao. Ninahisi kwamba Yehova alinipa ndugu wazuri kabisa, ambao walijitolea kuwasaidia watoto wangu. Nimefurahi kuwaona watoto wangu wakikomaa kiroho kwa sababu ya msaada huo. Wazee walinisaidia nilipohitaji mashauri. Walinisikiliza nilipohitaji mtu wa kuzungumza naye.”—Marko 10:29, 30.

Bila shaka, rafiki mwenye upendo atatambua wakati usiofaa wa kuzungumzia hali ya mwingine yenye kuhuzunisha. (Mhu. 3:7) Margarita anasema hivi: “Wakati mwingi, nilifurahia kuzungumza na akina dada katika kutaniko langu jipya kuhusu kazi ya kuhubiri, mafunzo yetu ya Biblia, na watoto wetu, lakini sikufurahia kuzungumza kuhusu matatizo yangu. Nilithamini kwamba walinisaidia kusahau yaliyopita na kuanza maisha mapya.”

Kataa Kishawishi cha Kulipiza Kisasi

Nyakati nyingine, badala ya kuhisi kwamba kwa njia fulani ulichangia dhambi za mwenzi wako, huenda ukakasirika kwa kuwa unateseka vibaya sana kwa sababu ya makosa yake. Usipozuia hasira hiyo, huenda ikakufanya uache azimio lako la kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova. Kwa mfano, huenda ukashawishiwa kutafuta njia za kulipiza kisasi juu ya mwenzi wako asiye mwaminifu.

Ukitambua kwamba hisia hizo zinatia mizizi ndani yako, unaweza kukumbuka mfano wa Yoshua na Kalebu. Wanaume hao waaminifu walihatarisha uhai wao ili waipeleleze Nchi ya Ahadi. Wale wapelelezi wengine walikosa imani na wakawachochea watu wasimtii Yehova. Hata Waisraeli fulani walitaka kuwapiga Yoshua na Kalebu kwa mawe walipojaribu kutia moyo taifa liendelee kuonyesha uaminifu. (Hes. 13:25–14:10) Kwa sababu ya matendo ya Waisraeli, Yoshua na Kalebu walilazimika kutembea nyikani kwa miaka 40 kwa sababu ya makosa ya wengine, bali si kwa sababu ya makosa yao.

Ingawa inaelekea kwamba Yoshua na Kalebu walivunjika moyo, hawakuruhusu dhambi za ndugu zao ziwafanye wakasirike. Walikazia fikira kudumisha hali yao nzuri ya kiroho. Mwishoni mwa ile miaka 40 katika nyika, ni wao pamoja na Walawi, katika kizazi chao ambao waliendelea kuishi na kuruhusiwa kuingia katika Nchi ya Ahadi.—Hes. 14:28-30; Yos. 14:6-12.

Matendo ya mwenzi wako asiye mwaminifu yanaweza kufanya uteseke kwa muda fulani. Huenda ndoa ikavunjika, hata hivyo, baadaye huenda ukapata matatizo ya kihisia na ya kifedha. Lakini, badala ya kuacha ulemewe na hisia za kuvunjika moyo, kumbuka kwamba Yehova anajua njia nzuri zaidi ya kushughulika na wale wanaopuuza kimakusudi viwango vyake, kama vile tu alivyoshughulika na Waisraeli waliokosa imani nyikani.—Ebr. 10:30, 31; 13:4.

Unaweza Kufanikiwa!

Badala ya kuruhusu mawazo yasiyofaa yakulemee, jaza mawazo ya Yehova katika akili yako. Jane anasema hivi: “Niliona kwamba kusikiliza kanda zilizorekodiwa za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kulinisaidia kufanikiwa. Mikutano pia ilinitia nguvu sana. Kushiriki kwa bidii katika mikutano kulinisaidia kusahau matatizo yangu. Kazi ya kuhubiri ilinisaidia pia. Kwa kuwasaidia wengine wawe na imani katika Yehova, niliitia nguvu imani yangu mwenyewe. Na kuwahangaikia wanafunzi wangu wa Biblia kulinisaidia kukazia fikira mambo ya maana zaidi.”

Monique aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Nimeweza kuvumilia kwa sababu ya kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na kushiriki katika utumishi wa shambani kadiri ninavyoweza. Tumekuwa na uhusiano wa karibu zaidi katika familia na pamoja na kutaniko. Hali yangu imenisaidia kutambua udhaifu wangu. Nimejaribiwa, lakini nimefaulu kukabiliana na hali hiyo kwa msaada wa Yehova.”

Wewe pia unaweza kuvumilia majaribu kama hayo. Ingawa unaumia moyoni kwa sababu ya kusalitiwa na mwenzi wako wa ndoa, jitahidi kufuata shauri hili la Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu: “Tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Gal. 6:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 13 Ili upate habari zaidi kuhusu maoni ya Biblia kuhusu kutengana na talaka, ona kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 125-130, 219-221.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wenzi wa ndoa walioachwa wanathamini wale wanaowasaidia katika utumishi wa shambani