Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuunganishwa Katika Upendo—Ripoti ya Mkutano wa Kila Mwaka

Kuunganishwa Katika Upendo—Ripoti ya Mkutano wa Kila Mwaka

Kuunganishwa Katika Upendo—Ripoti ya Mkutano wa Kila Mwaka

KULIKUWA na msisimuko katika Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Jersey City, New Jersey, Marekani. Asubuhi ya Oktoba 3, 2009 (3/10/2009), watu zaidi ya 5,000 walikuwa wamehudhuria mkutano wa 125 wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Maelfu ya watu wengine walisikiliza au kutazama programu hiyo kupitia video katika majengo matatu ya Betheli nchini Marekani na Betheli ya Kanada. Kwa ujumla, watu 13,235, waliounganishwa na upendo wao kwa Yehova, walifurahia mkutano huo uliofanywa kwa muda wa saa tatu.

Geoffrey Jackson, ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, ndiye aliyekuwa mwenyekiti. Alianzisha programu kwa kukaribisha kikundi cha waimbaji kutoka Betheli ambao waliimba nyimbo kutoka katika kitabu kipya cha nyimbo. Waimbaji hao walielekezwa na David Splane, mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, ambaye alieleza kwa ufupi kwa nini muziki ni wa maana katika ibada safi. Wahudhuriaji walikaribishwa kuimba nyimbo tatu mpya katika mkutano huo; kikundi hicho cha waimbaji kiliimba kwanza nyimbo hizo, kisha baadaye kikaimba nyimbo hizo pamoja na wahudhuriaji. Kikundi hicho cha waimbaji kilitumiwa kuimba katika mkutano huo wa pekee tu; makutaniko, mizunguko, au makusanyiko ya wilaya hayapaswi kuwa na vikundi vya waimbaji.

Ripoti Kutoka Kwenye Ofisi za Tawi

Washiriki wa Halmashauri za Tawi walitoa ripoti kutoka kwenye ofisi tano za tawi. Kenneth Little alisema kwamba hivi karibuni ofisi ya tawi ya Kanada itaanza kuchapisha magazeti mengi kwa ajili ya nchi ya Marekani na Kanada, na hivyo idadi ya magazeti yanayochapishwa katika ofisi hiyo ya tawi itaongezeka mara kumi. Ili kutosheleza uhitaji huo, mashini ya kuchapisha ambayo ilinunuliwa hivi karibuni itafanya kazi mchana na usiku kwa saa 16 kwa siku.

Reiner Thompson alitoa ripoti kuhusu kazi ya Ufalme katika Jamhuri ya Dominika, naye Albert Olih akaeleza kuhusu kazi yetu huko Nigeria. Emile Kritzinger, kutoka Msumbiji alieleza kwamba Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo waliandikishwa rasmi mwaka wa 1992, baada ya kuteswa kwa miaka mingi. Hivi karibuni, nchi hizo tatu zimekuwa na ongezeko kubwa la wahubiri. Viv Mouritz kutoka ofisi ya tawi ya Australia alieleza jinsi kazi inavyoendelea katika nchi ya Timor Mashariki, ambayo inasimamiwa na ofisi ya Australia.

Halmashauri za Baraza Linaloongoza

Mwaka wa 1976, utendaji wote wa Mashahidi wa Yehova ulianza kusimamiwa na halmashauri sita za Baraza Linaloongoza. Baadaye, washiriki wa jamii ya kondoo wengine waliwekwa rasmi kuwa wasaidizi. Sasa kuna wasaidizi 23 ambao wanasaidia kufanya kazi hiyo. Wasaidizi sita walihojiwa. Kwa ujumla, wasaidizi hao sita wametumikia kwa miaka 341 katika utumishi wa wakati wote, yaani, kwa wastani, kila mmoja ametumikia kwa miaka 57.

Don Adams, ambaye alianza kutumika Betheli mwaka wa 1943, alieleza kwamba Halmashauri ya Mratibu ina waratibu wa halmashauri zile nyingine tano, na hilo linahakikisha kwamba halmashauri zote tano zinafanya kazi pamoja kwa njia nzuri. Halmashauri hiyo inashughulikia hali za dharura, mateso, kesi za mahakamani, misiba, na mambo mengine ya dharura yanayowahusu Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.

Dan Molchan alieleza kuhusu kazi ya Halmashauri ya Wafanyakazi, ambayo inasimamia hali ya kimwili na ya kiroho ya Wanabetheli 19,851 ulimwenguni pote. David Sinclair alizungumzia jinsi Halmashauri ya Utangazaji inavyosimamia ununuzi wa vitu mbalimbali kwa ajili ya ofisi za tawi. Kisha, Robert Wallen, ambaye ametumika Betheli kwa karibu miaka 60, alieleza jinsi Halmashauri ya Utumishi inavyosimamia utendaji wa watu wa Yehova shambani na katika makutaniko. William Malenfant alieleza kuhusu kazi ngumu ambayo Halmashauri ya Ufundishaji inafanya katika kutayarisha programu ya kusanyiko la wilaya. Mwishowe, John Wischuk akaeleza jinsi Halmashauri ya Uandikaji inavyosimamia kwa uangalifu kazi ya kutayarisha na kukusanya habari zinazochapishwa katika vichapo vyetu. *

Andiko la Mwaka wa 2010 Linakazia Upendo

Hotuba tatu zilizofuata zilitolewa na washiriki wa Baraza Linaloongoza. Gerrit Lösch alianza kwa kuuliza, “Je, unataka kupendwa na wengine?” Alieleza kwamba upendo ni uhitaji wa msingi wa wanadamu, na sote tunachangamka tunapoonyeshwa upendo. Tuko hai kwa sababu ya upendo wa Yehova. Alituumba kwa sababu alichochewa na upendo usio na uchoyo. Jambo kuu linalotuchochea kuhubiri na kufundisha ni upendo wetu kwa Yehova.

Hatuwaonyeshi majirani wetu tu upendo unaoongozwa na kanuni bali pia maadui wetu. (Mt. 5:43-45) Wahudhuriaji waliombwa wafikirie mateso ambayo Yesu alivumilia kwa ajili yetu, kama vile, kupigwa viboko, kudhihakiwa, kutemewa mate, na kudungwa. Hata hivyo, Yesu alisali kwa ajili ya askari-jeshi waliomtundika. Je, hilo halitufanyi tumpende hata zaidi? Kisha, Ndugu Lösch akatangaza andiko la mwaka wa 2010: 1 Wakorintho 13:7, 8, ‘Upendo huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.’ Hatutumaini tu kuishi milele, bali tunatumaini pia kupenda na kupendwa milele.

Je, Wewe Ni Kama Gari Lisilo na Mafuta?

Samuel Herd alianza hotuba yake kwa kutoa mfano. Tuseme rafiki yako angependa usafiri naye umbali wa kilomita 50 kwa gari. Ukiwa umeketi kwenye kiti cha abiria, unaona kwamba kifaa cha kupima kiasi cha mafuta katika tangi kinaonyesha mafuta yanakaribia kwisha. Unamwambia rafiki yako kwamba mafuta yanakaribia kwisha. Anakwambia usiwe na wasiwasi; bado kuna lita nne za mafuta katika tangi. Hata hivyo, baada ya muda mfupi mafuta yanakwisha. Je, ni jambo linalofaa ‘kuendesha gari ambalo halina mafuta’ na kukabili hatari ya kukwama barabarani? Lingekuwa jambo bora kama nini kujaza tangi mafuta! Kwa njia ya mfano, tunapaswa kujaza tangi letu mafuta, mafuta yakiwa ni ujuzi wetu juu ya Yehova.

Kwa hiyo, tunapaswa kujaza tangi letu mafuta na kufanya hivyo kwa ukawaida. Kuna njia nne za kufanya hivyo. Njia ya kwanza ni funzo la kibinafsi, yaani, kuifahamu Biblia kwa kuisoma kila siku. Zaidi ya kusoma tu maneno, ni lazima tuelewe mambo tunayosoma. Pili, tunapaswa kutumia vizuri jioni yetu ya Ibada ya Familia. Je, tunasimamisha gari letu la mfano kila juma ili kujaza tangi au tunaweka kiasi kidogo tu katika tangi letu? Njia ya tatu ni funzo la kutaniko na kuhudhuria mikutano. Njia ya nne ni kutafakari kimyakimya, kwa utulivu, tukifikiria njia za Yehova. Zaburi 143:5 inasema hivi: “Nimezikumbuka siku za zamani za kale; nimetafakari juu ya utendaji wako wote.”

“Waadilifu Watang’aa”

John Barr alitoa hotuba ya tatu na ya mwisho, ambayo ilieleza kuhusu mfano wa Yesu wa ngano na magugu. (Mt. 13:24-30, 38, 43) Mfano huo unazungumzia “wakati wa mavuno” ambapo “wana wa Ufalme” wanakusanywa na magugu yanatenganishwa ili yateketezwe kwa moto.

Ndugu Barr alieleza waziwazi kwamba kazi ya kukusanya haitaendelea milele. Alitaja andiko la Mathayo 24:34 ambalo linasema: “Kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote hayo yatukie.” Alisoma mara mbili maneno haya: “Inaonekana Yesu alimaanisha kwamba maisha ya watiwa-mafuta waliokuwapo ishara ilipoanza kuonekana mwaka wa 1914 yangepishana na maisha ya watiwa-mafuta wengine ambao wangeona mwanzo wa dhiki kuu.” Hatujui urefu kamili wa “kizazi hiki,” lakini kinahusisha vikundi hivyo viwili ambavyo maisha yao yanapishana. Ingawa watiwa-mafuta wana umri mbalimbali, wale walio katika vikundi hivyo viwili ambavyo vinafanyiza kizazi hicho wanaishi pamoja katika kipindi fulani cha siku za mwisho. Inatia moyo kama nini kujua kwamba watiwa-mafuta wenye umri mdogo ambao waliishi pamoja na watiwa-mafuta wenye umri mkubwa ambao walitambua ishara ilipoonekana kuanzia mwaka wa 1914, hawatakufa wote kabla ya dhiki kuu kuanza.

“Wana wa ufalme” wanangoja kwa hamu kupokea thawabu yao ya kimbingu, lakini ni lazima sote tuendelee kuwa waaminifu, na kung’aa kwa uangavu mpaka mwisho. Tuna pendeleo kubwa sana la kuona “ngano” ikikusanywa katika wakati wetu.

Baada ya wimbo wa mwisho, sala ya kumalizia ilitolewa na Theodore Jaracz mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Programu ya mkutano wa kila mwaka ilikuwa yenye kujenga kama nini!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kwa maelezo kuhusu kazi zinazofanywa na halmashauri sita za Baraza Linaloongoza, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2008 (15/5/2008), ukurasa wa 29.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

SHULE YA WAZEE

Katika mkutano wa kila mwaka, Anthony Morris, ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kwamba kutakuwa na mazoezi yanayoendelea ya wazee wa kutaniko. Shule ya wazee nchini Marekani ilianza mwanzoni mwa mwaka wa 2008 katika kituo cha elimu cha Patterson, New York. Darasa la 72 lilikuwa limetoka tu kumalizika, na kufikia wakati huo wazee 6,720 walikuwa wamezoezwa. Bado kuna kazi nyingi. Nchini Marekani peke yake, kuna wazee zaidi ya 86,000. Hivyo, Baraza Linaloongoza lilikubali shule nyingine ifanywe huko Brooklyn, New York, kuanzia Desemba 7, 2009 (7/12/2009).

Kwa miezi miwili, waangalizi wanne wanaosafiri wangezoezwa kuwa walimu huko Patterson. Kisha, wangepelekwa Brooklyn ili kufundisha, na waangalizi wengine wanne wanaosafiri wangezoezwa. Waangalizi hao wangeenda kufundisha katika shule ya wazee huko Brooklyn, halafu waangalizi wanne waliozoezwa kwanza wangeenda kufundisha shule za wazee katika Majumba ya Kusanyiko na Majumba ya Ufalme. Mazoezi hayo yangeendelea mpaka kuwe na walimu 12 wanaofundisha katika shule sita za wazee kila juma katika lugha ya Kiingereza nchini Marekani. Kisha walimu wanne wangezoezwa kufundisha katika Kihispania. Shule hiyo haitachukua mahali pa Shule ya Huduma ya Ufalme; kusudi la shule hiyo ni kuwasaidia wazee waendelee kukomaa kiroho. Ofisi za tawi ulimwenguni pote zitaanza kufanya shule hizo kwenye Majumba ya Kusanyiko na Majumba ya Ufalme katika mwaka wa utumishi wa 2011.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Mkutano wa kila mwaka ulianza kwa nyimbo zilizoimbwa kutoka katika kitabu chetu kipya cha nyimbo kinachoitwa, “Mwimbieni Yehova”