Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maneno Yenye Neema Yanadumisha Mahusiano Mazuri

Maneno Yenye Neema Yanadumisha Mahusiano Mazuri

Maneno Yenye Neema Yanadumisha Mahusiano Mazuri

“Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote.”—KOL. 4:6.

1, 2. Ndugu mmoja alipata matokeo gani mazuri alipotumia maneno yenye neema?

NDUGU mmoja anaripoti hivi: “Nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba, nilikutana na mwanamume fulani ambaye alikasirika sana hivi kwamba midomo yake na mwili wake wote ulitetemeka. Nilijaribu kuzungumza naye kwa utulivu kwa kutumia Maandiko, lakini hasira yake iliendelea tu kupanda. Mke na watoto wake walijiunga naye kunishambulia kwa maneno, hivyo nikaona kwamba ni wakati wa kuondoka. Niliihakikishia familia hiyo kwamba nilikuja kwa amani na ningependa kwenda kwa amani. Niliwaonyesha andiko la Wagalatia 5:22 na 23, ambalo linataja upendo, upole, kujizuia, na amani. Kisha nikaondoka.

2 “Baadaye, nilipotembelea nyumba zilizokuwa upande wa pili wa barabara, niliona familia hiyo ikiwa imeketi mbele ya mlango wa nyumba yao. Waliniita. Nikajiuliza, ‘Sasa kuna nini?’ Mwanamume huyo alikuwa na kopo la maji baridi akaniuliza ikiwa nilitaka maji ya kunywa. Aliniomba msamaha kwa sababu ya kunishambulia kwa maneno kisha akanipongeza kwa sababu ya imani yangu yenye nguvu. Tuliachana kwa amani.”

3. Kwa nini hatupaswi kuwaruhusu wengine watukasirishe?

3 Katika ulimwengu wa leo uliojaa mikazo, kwa kawaida hatuwezi kuepuka kukutana na watu wenye hasira, hata katika huduma yetu. Tunapokutana nao, ni jambo la maana kwetu kuonyesha “tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:15) Kama ndugu aliyetajwa hapo juu angeruhusu hasira na ukosefu wa fadhili wa wenye nyumba umchochee kukasirika, inaelekea kwamba mtazamo wa yule mwanamume haungebadilika; huenda angekasirika hata zaidi. Lakini kwa sababu ndugu huyo alijizuia na kusema maneno yenye neema, matokeo yalikuwa mazuri.

Ni Nini Kinachofanya Maneno Yawe Yenye Neema?

4. Kwa nini ni jambo la maana kutumia maneno yenye neema?

4 Iwe tunashughulika na watu walio nje au ndani ya kutaniko, hata na washiriki wa familia yetu, ni jambo la maana sana kufuata shauri hili la mtume Paulo: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi.” (Kol. 4:6) Maneno hayo yenye kupendeza na yanayofaa yanadumisha amani na mahusiano mazuri.

5. Kuzungumza waziwazi hakumaanishi nini? Toa mfano.

5 Kuzungumza waziwazi hakumaanishi kusema jambo lolote ambalo unafikiria na kuhisi wakati wowote ule, hasa unapokasirika. Maandiko yanasema kwamba mtu anayeonyesha hasira bila kujizuia anathibitisha kwamba ana udhaifu bali si nguvu. (Soma Methali 25:28; 29:11.) Musa ambaye alikuwa “mpole zaidi” kuliko watu wote walioishi siku zake, pindi moja aliruhusu uasi wa taifa la Israeli umfanye akasirike na kukosa kumpa Mungu utukufu. Musa alisema waziwazi jinsi alivyohisi, lakini Yehova hakufurahi. Baada ya kuwaongoza Waisraeli kwa miaka 40, Musa alipoteza pendeleo la kuwaingiza katika Nchi ya Ahadi.—Hes. 12:3; 20:10, 12; Zab. 106:32.

6. Kuzungumza kwa busara kunamaanisha nini?

6 Maandiko yanawapongeza watu ambao wanajizuia na kuzungumza kwa busara au hekima. “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa, lakini anayezuia midomo yake anatenda kwa busara.” (Met. 10:19; 17:27) Hata hivyo, kutumia busara hakumaanishi kwamba mtu hapaswi kamwe kutoa maoni yake. Kunamaanisha kuongea kwa “neema,” na kutumia ulimi kuponya badala ya kuumiza.—Soma Methali 12:18; 18:21.

“Wakati wa Kukaa Kimya na Wakati wa Kusema”

7. Ni maneno ya aina gani ambayo hatupaswi kusema, na kwa nini?

7 Kama vile tu tunavyohitaji kutumia maneno yenye neema na kujizuia tunapozungumza na wafanyakazi wenzetu au watu tusiowajua katika huduma, tunahitaji pia kufanya hivyo kutanikoni na nyumbani. Tunapomwaga hasira bila kujali matokeo ya kufanya hivyo tunaweza kujiumiza na kuwaletea wengine madhara makubwa sana ya kiroho, kihisia, na kimwili. (Met. 18:6, 7) Ni lazima tuzuie hisia mbaya ambazo zinasababishwa na hali yetu ya kutokamilika. Maneno ya matukano, dhihaka, dharau, na maneno ya hasira yenye chuki hayafai kamwe. (Kol. 3:8; Yak. 1:20) Yanaweza kuharibu mahusiano yenye thamani sana na watu wengine na pamoja na Yehova. Yesu alifundisha hivi: “Kila mtu anayeendelea kuwa na ghadhabu na ndugu yake atatoa hesabu mahakamani; lakini yeyote yule anayemwambia ndugu yake neno la dharau lisilosemeka atatoa hesabu katika Mahakama Kuu Zaidi; na yeyote yule anayesema, ‘Wewe mpumbavu wa kudharauliwa!’ atastahili Gehena ya moto.”—Mt. 5:22.

8. Ni wakati gani tunapopaswa kusema jinsi tunavyohisi, lakini kwa njia gani?

8 Hata hivyo, kuna mambo fulani ambayo tunaweza kuona kwamba ni vizuri kuyasema. Ikiwa ndugu fulani amesema au kufanya jambo fulani ambalo limekuumiza sana hivi kwamba huwezi kuliachilia tu, usiruhusu hisia za chuki zisitawi katika moyo wako. (Met. 19:11) Mtu akikukasirisha, zuia hisia zako kisha uchukue hatua zinazofaa ili kutatua tatizo hilo. Paulo aliandika hivi: “Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” Kwa kuwa tatizo hilo linaendelea kukuumiza, lishughulikie kwa fadhili wakati unaofaa. (Soma Waefeso 4:26, 27, 31, 32.) Zungumza na ndugu yako kuhusu jambo hilo waziwazi lakini ukitumia maneno yenye neema, ukiwa na kusudi la kupatana naye.—Law. 19:17; Mt. 18:15.

9. Kwa nini tunapaswa kuzuia hisia zetu kabla ya kuzungumza na wengine?

9 Bila shaka, unapaswa kuchagua kwa uangalifu wakati unaofaa. Kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhu. 3:1, 7) Zaidi ya hayo, “moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” (Met. 15:28) Huenda ukahitaji kungoja ili mzungumze na kusuluhisha matatizo hayo. Mambo yanaweza kuharibika zaidi mkizungumza wakati bado mmekasirika sana; lakini pia si jambo la hekima kungoja kwa muda mrefu sana.

Matendo ya Fadhili Yanadumisha Mahusiano Mazuri

10. Kuwatendea wengine kwa fadhili kunaweza kuboresha mahusiano jinsi gani?

10 Kusema maneno yenye neema na kuzungumza kwa njia nzuri kunaweza kusitawisha na kudumisha mahusiano yenye amani. Kwa kweli, kufanya yote tunayoweza ili kuboresha mahusiano yetu na wengine kunaweza kuboresha mazungumzo yetu pamoja nao. Kuchukua hatua ya kuwatendea wengine mambo ya fadhili kutoka moyoni, na kutafuta nafasi za kuwasaidia, kuwapa zawadi kwa nia nzuri, na kuwakaribisha, kunaweza kuchangia mazungumzo mazuri. Hata kunaweza ‘kukusanya makaa yenye moto’ juu ya mtu na kumfanya aonyeshe sifa nzuri, na hivyo inakuwa rahisi zaidi kuzungumza waziwazi na kusuluhisha matatizo.—Rom. 12:20, 21.

11. Yakobo alichukua hatua gani ili kuboresha uhusiano wake na Esau, na matokeo yalikuwa nini?

11 Mzee wa ukoo Yakobo alielewa jambo hilo. Esau, ndugu yake pacha, alimkasirikia sana hivi kwamba Yakobo akakimbia kwa sababu aliogopa kuwa Esau angemuua. Baada ya miaka mingi kupita, Yakobo alirudi. Esau alienda na wanaume 400 ili akutane naye. Yakobo alisali ili Yehova amsaidie. Kisha, kabla ya kukutana na Esau, akapeleka zawadi kubwa ya wanyama wa kufugwa. Zawadi hiyo ilitimiza kusudi lake. Walipokutana, moyo wa Esau ulikuwa umebadilika, akakimbia na kumkumbatia Yakobo.—Mwa. 27:41-44; 32:6, 11, 13-15; 33:4, 10.

Watie Moyo Wengine kwa Maneno Yenye Neema

12. Kwa nini tunapaswa kutumia maneno yenye neema tunapozungumza na ndugu zetu?

12 Wakristo wanamtumikia Mungu, bali si wanadamu wenzao. Hata hivyo, tuna tamaa ya asili ya kukubaliwa na wengine. Maneno yetu yenye neema yanaweza kupunguza mizigo ya ndugu na dada zetu. Hata hivyo, kuwachambua kwa ukali kunaweza kufanya mizigo hiyo iwe mizito zaidi na hata kuwafanya wengine wafikiri kwamba wamepoteza kibali cha Yehova. Kwa hiyo, acheni tuwaambie wengine kwa unyoofu mambo yenye kutia moyo, “neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.”—Efe. 4:29.

13. Wazee wanapaswa kukumbuka nini (a) wanapotoa shauri? (b) wanapoandika barua?

13 Wazee, hasa, wanapaswa kuwa “wapole” na kulitendea kundi kwa wororo. (1 The. 2:7, 8) Wazee wanapohitajika kutoa shauri, kusudi lao ni kufanya hivyo kwa “upole,” hata wanapoongea na wale “wasio na mwelekeo unaofaa.” (2 Tim. 2:24, 25) Wazee wanapaswa pia kutumia maneno yenye neema wanapoandikia baraza lingine la wazee au ofisi ya tawi. Wanapaswa kuwa wenye fadhili na busara, kama tunavyosoma katika andiko la Mathayo 7:12.

Kutumia Maneno Yenye Neema Katika Familia

14. Paulo anawapa waume shauri gani, na kwa nini?

14 Ni rahisi kufikiri kwamba maneno yetu, ishara zetu za uso na za mwili hazina matokeo yoyote juu ya watu wengine. Kwa mfano, huenda wanaume fulani wasijue kikamili jinsi maneno yao yanavyowaumiza sana wanawake. Dada mmoja alisema hivi: “Ninashtuka wakati mume wangu anaponifokea kwa hasira.” Maneno makali yanaweza kumuumiza sana mwanamke kuliko mwanamume na huenda akayakumbuka kwa muda mrefu. (Luka 2:19) Na jambo hilo ni la kweli hasa inapohusu maneno yanayosemwa na mtu fulani ambaye mwanamke anampenda na anataka kumheshimu. Paulo aliwashauri hivi waume: “Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.”—Kol. 3:19.

15. Toa mfano ambao unaonyesha kwa nini mume anapaswa kumtendea mke wake kwa upole.

15 Kuhusu jambo hilo, ndugu mmoja mwenye uzoefu ambaye ameoa alitoa mfano unaoonyesha kwa nini mume anapaswa kumtendea mke wake kwa upole, kama “chombo dhaifu zaidi.” Alisema hivi: “Unapobeba chombo chenye thamani kinachoweza kuvunjika kwa urahisi, hupaswi kukishika kwa nguvu sana, kinaweza kuvunjika. Hata kikirekebishwa, huenda alama hiyo bado itaonekana. Mume akimwambia mke wake maneno makali sana, anaweza kumuumiza. Hilo linaweza kusababisha madhara yenye kudumu katika uhusiano wao.”—Soma 1 Petro 3:7.

16. Mke anaweza kujenga familia yake jinsi gani?

16 Wanaume pia wanaweza kutiwa moyo au kuvunjwa moyo na maneno ya watu wengine, kutia ndani na wake zao. “Mke mwenye busara,” ambaye mume wake anaweza kwa kweli ‘kumtegemea,’ anajali hisia za mume, kama vile anavyotaka mume ajali hisia zake. (Met. 19:14; 31:11) Kwa kweli, mke anaweza kuwa na uvutano mkubwa katika familia, kwa njia nzuri au mbaya. “Mwanamke mwenye hekima kwelikweli amejenga nyumba yake, lakini aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.”—Met. 14:1.

17. (a) Watoto wanapaswa kuzungumza jinsi gani na wazazi wao? (b) Watu wazima wanapaswa kuzungumza jinsi gani na watoto, na kwa nini?

17 Wazazi na pia watoto wanapaswa kutumia maneno yenye neema wanapozungumza pamoja. (Mt. 15:4) Ufikirio utatusaidia kuepuka ‘kuwakasirisha’ au kuwachokoza watoto tunapozungumza nao. (Kol. 3:21; Efe. 6:4) Hata ikiwa ni lazima watoto watiwe nidhamu, wazazi na wazee wanapaswa kuzungumza nao kwa heshima. Kwa njia hiyo, watu wazima wanafanya iwe rahisi zaidi kwa vijana kurekebisha mwenendo wao na kudumisha urafiki wao pamoja na Mungu. Kufanya hivyo ni bora zaidi kuliko kuonyesha kwamba tumechoka nao, jambo ambalo linaweza kuwavunja moyo. Huenda watoto wasikumbuke mashauri yote waliyopewa, lakini watakumbuka jinsi wengine walivyozungumza nao.

Kusema Mambo Mazuri Kutoka Moyoni

18. Tunaweza kuondoa jinsi gani mawazo na hisia zenye kuumiza?

18 Kuzuia hasira hakumaanishi tu kuonekana kwa nje kuwa mtulivu. Kusudi letu halipaswi kuwa tu kutuliza hasira yetu kali. Tunapata mkazo tunapojifanya kuwa watulivu kwa nje huku tukichemka kwa hasira moyoni. Ni kama kujaribu kukanyaga breki ya gari na wakati huohuo kujaribu kuliendesha gari hilo. Kufanya hivyo kunaweza kuliharibu gari. Kwa hiyo, usifungie hasira moyoni na kuiacha ilipuke baadaye. Sali ili Yehova akusaidie kuondoa hisia zenye kuumiza moyoni mwako. Acha roho ya Yehova igeuze akili na moyo wako kupatana na mapenzi yake.—Soma Waroma 12:2; Waefeso 4:23, 24.

19. Ni hatua gani zinazoweza kutusaidia kuepuka ugomvi wenye hasira?

19 Chukua hatua zinazofaa. Ukikabili hali yenye kufadhaisha ambayo inakuchochea kukasirika, huenda ikafaa uondoke mahali hapo, ili upate wakati wa kutuliza hasira yako. (Met. 17:14) Ikiwa mtu unayeongea naye anaanza kukasirika, jitahidi sana kutumia maneno yenye neema. Kumbuka: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Met. 15:1) Maneno makali au yenye kuumiza yataongeza kuni kwenye moto hata ikiwa yatasemwa kwa sauti ya upole. (Met. 26:21) Kwa hiyo, hali fulani inapojaribu sifa yako ya kujizuia, uwe “mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” Sali ili roho ya Yehova ikusaidie kusema mambo mazuri, wala si mabaya.—Yak. 1:19.

Kusamehe Kutoka Moyoni

20, 21. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwasamehe wengine, na kwa nini ni lazima tufanye hivyo?

20 Inahuzunisha kwamba hakuna yeyote kati yetu anayeweza kuuzuia kikamili ulimi wake. (Yak. 3:2) Hata wakijitahidi kadiri gani, nyakati nyingine washiriki wa familia yetu na ndugu na dada zetu wa kiroho wapendwa wanaweza kusema bila kufikiri maneno ambayo yanatuumiza hisia. Badala ya kukasirika haraka, fikiria kwa subira sababu zilizowafanya waseme mambo hayo. (Soma Mhubiri 7:8, 9.) Je, walikuwa na mkazo, woga, hawakuwa wakijisikia vizuri, au walikuwa wakipambana na tatizo fulani mwilini mwao au kutoka chanzo kingine?

21 Mambo kama hayo si kisingizio cha kumwaga hasira. Lakini tukitambua mambo hayo, tunaweza kuelewa kwa nini nyakati nyingine watu wanasema na kufanya mambo ambayo hayafai na hilo linaweza kutuchochea kuwasamehe. Sote tunasema au kufanya mambo ambayo yanawaumiza wengine, na tunatumaini kwamba watatusamehe kwa fadhili. (Mhu. 7:21, 22) Yesu alisema kwamba ili Mungu atusamehe, ni lazima tuwasamehe wengine. (Mt. 6:14, 15; 18:21, 22, 35) Kwa hiyo, tunapaswa kuomba haraka msamaha na kuwasamehe wengine haraka, na hivyo kudumisha upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano,” katika familia na katika kutaniko.—Kol. 3:14.

22. Kwa nini jitihada zetu za kutumia maneno yenye neema si za bure?

22 Inaelekea kwamba itakuwa vigumu zaidi kudumisha shangwe na umoja wetu kadiri mfumo huu wa mambo uliojaa watu wenye hasira unavyokaribia mwisho wake. Kufuata kanuni bora za Neno la Mungu kutatusaidia kutumia ulimi wetu kusema mambo mazuri, bali si mabaya. Tutafurahia mahusiano mazuri katika kutaniko na katika familia, na mfano wetu utawatolea wengine ushahidi mzuri sana kumhusu ‘Mungu wetu mwenye furaha,’ Yehova.—1 Tim. 1:11.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini ni jambo la maana kuchagua wakati unaofaa ili kuzungumzia matatizo?

• Kwa nini washiriki wa familia wanapaswa sikuzote kutumia maneno “yenye neema” wanapozungumza?

• Tunaweza kuepuka jinsi gani kusema mambo yenye kuumiza?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa wenye kusamehe?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Acha hisia zako zitulie, kisha utafute wakati unaofaa wa kuzungumza

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mwanamume anapaswa sikuzote kuzungumza na mke wake kwa upole