Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pata Burudisho Katika Mambo ya Kiroho

Pata Burudisho Katika Mambo ya Kiroho

Pata Burudisho Katika Mambo ya Kiroho

“Chukueni nira yangu . . . , nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—MT. 11:29.

1. Mungu alifanya mpango gani katika Mlima Sinai, na kwa nini?

WAKATI agano la Sheria lilipoanzishwa katika Mlima Sinai, lilitia ndani mpango wa Sabato ya kila juma. Yehova aliliamuru hivi taifa la Israeli kupitia msemaji wake Musa: “Siku sita utafanya kazi yako; lakini siku ya saba utaacha, ili ng’ombe-dume wako na punda wako wapate kupumzika na mwana wa kijakazi wako na mkaaji mgeni wapate kujiburudisha.” (Kut. 23:12) Ndiyo, Yehova aliwajali wale ambao walikuwa chini ya Sheria hivi kwamba kwa upendo alifanya mpango kuwe na siku moja ya kupumzika ili watu wake waweze “kujiburudisha.”

2. Waisraeli walifaidika jinsi gani kwa sababu ya kushika Sabato?

2 Je, Sabato ilikuwa siku ya watu kustarehe tu? Hapana, Sabato ilikuwa sehemu ya maana sana katika ibada ambayo Waisraeli walimtolea Yehova. Kushika Sabato kuliwezesha vichwa vya familia kupata wakati wa kufundisha familia zao ‘kushika njia ya Yehova ili kutenda uadilifu.’ (Mwa. 18:19) Pia, kushika Sabato kuliwezesha marafiki na familia kuwa pamoja na kutafakari kuhusu matendo ya Yehova na kushirikiana pamoja kwa furaha. (Isa. 58:13, 14) Jambo ambalo ni la maana zaidi ni kwamba Sabato ilionyesha kwa njia ya unabii wakati ujao ambapo Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo utaleta burudisho la kweli. (Rom. 8:21) Lakini namna gani katika siku zetu? Wakristo wa kweli ambao wanapendezwa na njia za Yehova wanaweza kupata wapi na jinsi gani burudisho kama hilo?

Pata Burudisho Kupitia Ushirika wa Kikristo

3. Wakristo wa karne ya kwanza walitegemezana jinsi gani, na matokeo yalikuwa nini?

3 Mtume Paulo alisema kwamba kutaniko la Kikristo ni “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Tim. 3:15) Wakristo wa karne ya kwanza walitegemezana sana kwa kutiana moyo na kujengana katika upendo. (Efe. 4:11, 12, 16) Paulo alipokuwa Efeso, washiriki wa kutaniko la Korintho walimtembelea na kumtia moyo. Ona jinsi alivyohisi baada ya kutembelewa: “Nashangilia kuwapo kwa Stefana na Fortunato na Akaiko,” akasema Paulo, “kwa maana wameiburudisha roho yangu.” (1 Kor. 16:17, 18) Vivyo hivyo, Tito alipoenda Korintho kuwahudumia akina ndugu huko, Paulo aliliandikia kutaniko hilo na kusema hivi: “Roho yake imeburudishwa na ninyi nyote.” (2 Kor. 7:13) Leo pia, Mashahidi wa Yehova wanapata burudisho la kweli kupitia ushirika wa Kikristo wenye kujenga.

4. Mikutano ya kutaniko inatuburudisha jinsi gani?

4 Umejionea mwenyewe kwamba mikutano ya kutaniko inaleta shangwe kubwa. Katika mikutano hiyo tunapata “ubadilishanaji wa kitia-moyo . . . kila mmoja kupitia imani ya mwingine.” (Rom. 1:12) Ndugu na dada zetu Wakristo si watu tunaowafahamu tu, si marafiki wa kijuu-juu ambao tunakutana nao mara kwa mara. Ni marafiki wa kweli, watu ambao tunawapenda na kuwaheshimu. Tunapata shangwe nyingi na faraja kwa kukusanyika kwa ukawaida pamoja nao katika mikutano yetu.—Flm. 7.

5. Tunaweza kuburudishana jinsi gani katika makusanyiko yetu?

5 Tunapata pia burudisho kupitia makusanyiko yetu ya kila mwaka. Makusanyiko hayo makubwa yanatuandalia maji ya kweli ya uhai kutoka katika Neno la Mungu, Biblia, na pia tunapata nafasi ya ‘kupanuka’ katika mashirika yetu. (2 Kor. 6:12, 13) Lakini namna gani ikiwa sisi ni wenye haya na tunaogopa kukutana na watu? Njia moja ya kuwafahamu ndugu na dada zetu ni kujitolea katika kusanyiko. Baada ya kujitolea kusaidia katika kusanyiko la kimataifa, dada mmoja alisema hivi: “Mwanzoni, sikujua watu wengi katika kusanyiko, isipokuwa familia yangu na marafiki fulani wachache. Lakini niliposaidia katika kufanya usafi, nilikutana na ndugu na dada wengi sana! Nilifurahi sana!”

6. Taja njia moja ya kupata burudisho wakati wa likizo.

6 Waisraeli walikuwa wakisafiri kwenda Yerusalemu kuabudu wakati wa sherehe tatu za kila mwaka. (Kut. 34:23) Mara nyingi hilo lilimaanisha kuacha mashamba na maduka na kutembea kwa miguu kwa siku nyingi kwenye barabara zenye vumbi. Hata hivyo, walipoenda hekaluni walipata “shangwe kubwa” kwa kuwa wale waliokuwapo walikuwa “wakimtolea Yehova sifa.” (2 Nya. 30:21) Watumishi wengi wa Yehova leo, wanapata pia shangwe kubwa wanapoenda pamoja na familia zao kutembelea Betheli, yaani, ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova zilizo karibu nao. Je, mnaweza kupanga kutembelea Betheli wakati wa likizo inayofuata ya familia yenu?

7. (a) Tafrija zinaweza kutunufaisha jinsi gani? (b) Ni nini kinachoweza kufanya tafrija iwe nzuri na yenye kujenga?

7 Tunaweza pia kutiwa moyo tukikusanyika pamoja tukiwa familia na marafiki kwa ajili ya tafrija. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.” (Mhu. 2:24) Tafrija zinaburudisha nafsi na vilevile zinatia nguvu kifungo cha upendo kati yetu na Wakristo wenzetu tunapowajua vizuri zaidi. Ili tafrija iwe nzuri sana na yenye kujenga, ni vizuri kupanga tafrija yenye watu wachache na kuhakikisha kwamba wanasimamiwa vizuri, hasa ikiwa kutakuwa na pombe.

Huduma Inaburudisha

8, 9. (a) Eleza tofauti kati ya ujumbe wa Yesu na ule wa waandishi na Mafarisayo. (b) Tunafaidika jinsi gani tunapowahubiria wengine kweli za Biblia?

8 Yesu alikuwa na bidii katika huduma, na aliwatia moyo wanafunzi wake wafanye vivyo hivyo. Maneno yake yanaonyesha hivyo: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Ujumbe ambao Yesu alifundisha ulikuwa wenye kuburudisha kwelikweli; ulikuwa “habari njema.” (Mt. 4:23; 24:14) Ulikuwa tofauti kabisa na sheria zenye kulemea ambazo Mafarisayo waliwawekea watu.—Soma Mathayo 23:4, 23, 24.

9 Tunapowahubiria wengine ujumbe wa Ufalme, tunawaburudisha kiroho na, wakati huohuo, kweli hizo zenye thamani kutoka katika Biblia zinatia mizizi katika akili na mioyo yetu. Mtunga-zaburi alisema hivi kwa kufaa: “Msifuni Yah, kwa maana ni vema kumpigia Mungu wetu muziki; kwa maana inapendeza.” (Zab. 147:1) Je, unaweza kuongeza shangwe unayopata unapomsifu Yehova mbele ya majirani wako?

10. Je, mafanikio yetu katika huduma yanategemea jinsi watu wanavyoitikia vizuri ujumbe wetu? Eleza.

10 Ni kweli kwamba katika maeneo fulani watu wanasikiliza sana habari njema kuliko katika maeneo mengine. (Soma Matendo 18:1, 5-8.) Ikiwa unaishi katika eneo ambalo wengi hawakubali ujumbe wa Ufalme, jaribu kukazia fikira mambo mazuri unayotimiza katika huduma. Kumbuka kwamba jitihada zako za kuendelea kutangaza jina la Yehova si za bure. (1 Kor. 15:58) Zaidi ya hayo, mafanikio yetu katika huduma hayategemei jinsi watu wanavyoitikia habari njema. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atahakikisha kuwa watu wenye mioyo minyoofu watapata nafasi ya kusikiliza ujumbe wa Ufalme.—Yoh. 6:44.

Ibada ya Familia Inaburudisha

11. Yehova amewapa wazazi daraka gani, na wanaweza kulitimiza jinsi gani?

11 Wazazi wanaomwogopa Mungu wana daraka la kuwafundisha watoto wao kumhusu Yehova na njia zake. (Kum. 11:18, 19) Ikiwa wewe ni mzazi, je, umetenga wakati wa kuwafundisha watoto wako kumhusu Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo? Ili kukusaidia utimize daraka hilo zito na kutosheleza mahitaji ya familia yako, Yehova ametoa chakula kingi cha kiroho chenye kujenga kupitia vitabu, magazeti, video, na rekodi za kusikiliza.

12, 13. (a) Familia zinaweza kufaidika jinsi gani kupitia jioni ya Ibada ya Familia? (b) Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba ibada yao ya familia inaburudisha?

12 Zaidi ya hayo, jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara imefanya mipango ili tuwe na jioni ya Ibada ya Familia. Hiyo ni jioni ambayo imetengwa kila juma kwa ajili ya funzo la Biblia la familia. Wengi wameona kwamba mpango huo umewasaidia kuwa na uhusiano wa karibu zaidi wenye upendo katika familia na umetia nguvu uhusiano wao pamoja na Yehova. Lakini wazazi wanaweza kuhakikisha jinsi gani kwamba ibada yao ya familia inaburudisha kiroho?

13 Jioni ya Ibada ya Familia haipaswi kuwa pindi inayochosha ambayo haifurahishi. Kwa kweli, tunamwabudu “Mungu mwenye furaha,” ambaye anataka tupate shangwe katika ibada yetu. (1 Tim. 1:11; Flp. 4:4) Ni baraka kubwa sana kuwa na jioni ya ziada ya kuzungumzia kweli za kiroho zenye thamani kutoka katika Biblia. Wazazi wanaweza kubadili-badili njia za kufundisha, wakitumia mbinu mbalimbali na maarifa. Kwa mfano, familia moja ilimwomba mwana wao mwenye umri wa miaka 10, anayeitwa Brandon, atoe ripoti yenye kichwa “Kwa Nini Yehova Alitumia Nyoka Kumfananisha Shetani?” Jambo hilo lilikuwa limemsumbua Brandon kwa sababu anapenda nyoka, naye hakufurahi kuona nyoka wakitumiwa ili kumfananisha Shetani. Mara kwa mara, familia fulani zimeigiza drama za Biblia, huku kila mshiriki wa familia akiigiza sehemu ya mtu fulani, na kusoma sehemu yake katika Biblia, au kuigiza tukio fulani. Njia hizo za kufundisha hazifurahishi tu bali pia zinawafanya watoto washiriki, na hivyo kanuni za Biblia zinagusa mioyo yao. *

Epuka Mambo Yanayoweza Kukulemea

14, 15. (a) Ukosefu wa usalama na mikazo imeongezeka jinsi gani katika siku za mwisho? (b) Huenda tukapata mkazo gani zaidi?

14 Ukosefu wa usalama na mikazo imeongezeka katika siku hizi za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo. Mamilioni ya watu hawana kazi na wanahangaishwa na matatizo mengine ya kiuchumi. Hata wale ambao wana kazi mara nyingi wanaona kwamba pesa ambazo wanapata hazisaidii sana familia yao kwa sababu ni kana kwamba wanazibeba kwa mfuko uliojaa matundu. (Linganisha na Hagai 1:4-6.) Inaonekana kwamba wanasiasa na viongozi wengine hawajui jinsi ya kupambana na ugaidi na hali nyingine zinazosababisha uovu. Watu wengi wanavunjika moyo kwa sababu ya makosa yao wenyewe.—Zab. 38:4.

15 Wakristo wa kweli wanapatwa pia na matatizo na mikazo inayosababishwa na mfumo wa mambo wa Shetani. (1 Yoh. 5:19) Nyakati nyingine, huenda wanafunzi wa Kristo wakapata mkazo zaidi wanapojitahidi kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova. Yesu alisema hivi: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Lakini, hata ‘tunapoteswa,’ “hatuachwi kabisa bila msaada.” (2 Kor. 4:9) Kwa nini?

16. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kuwa na shangwe?

16 Yesu alisema hivi: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi.” (Mt. 11:28) Tunapoonyesha kwamba tuna imani kamili katika fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo, ni kana kwamba tunajiweka mikononi mwa Yehova. Kwa njia hiyo, tunapata “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7) Roho takatifu ya Mungu ni “msaidizi,” na inatia nguvu sana imani yetu hivi kwamba tunavumilia majaribu na mateso au dhiki tunazokabili na kuendelea kuwa na shangwe.—Yoh. 14:26; Yak. 1:2-4.

17, 18. (a) Tunahitaji kujilinda na roho gani? (b) Matokeo yanaweza kuwa nini tukifuatia sana raha za maisha?

17 Wakristo wa kweli leo wanahitaji kujilinda ili wasishawishiwe na roho ya ulimwengu huu ambayo inawachochea watu kufuatia raha kupita kiasi. (Soma Waefeso 2:2-5.) Tusipofanya hivyo, tunaweza kunaswa na “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani.” (1 Yoh. 2:16) Au huenda tukaamini kimakosa kwamba tutapata burudisho tukifuata tamaa za mwili. (Rom. 8:6) Kwa mfano, watu fulani wanatumia vibaya dawa za kulevya na pombe, wanatazama ponografia (picha au habari za ngono), wanacheza michezo hatari, au kufanya mambo mbalimbali yasiyofaa ili kupata msisimuko. “Hila” za Shetani zinakusudiwa kutupotosha kwa kutuletea burudisho la uwongo.—Efe. 6:11.

18 Ni kweli kwamba si vibaya kula, kunywa, na kufurahia burudani nzuri kwa kiasi. Hata hivyo, hatupaswi kuruhusu mambo kama hayo yawe mambo makuu katika maisha yetu. Ni jambo la maana sana kuwa na usawaziko na kujizuia, hasa tukifikiria nyakati tunamoishi. Kufuatia mambo ya kibinafsi kunaweza kutulemea na kutufanya tuwe “wasiotenda au wasiozaa matunda kuhusiana na ujuzi sahihi juu ya Bwana wetu Yesu Kristo.”—2 Pet. 1:8.

19, 20. Tunaweza jinsi gani kupata burudisho la kweli?

19 Tunapoelewa maagizo ya Yehova, tunatambua kwamba raha yoyote inayotolewa na ulimwengu huu ni ya muda tu. Musa alitambua hilo, hata sisi tunatambua hilo. (Ebr. 11:25) Ukweli ni kwamba burudisho la kweli, ambalo linatufanya tutosheke na kupata shangwe nyingi inayodumu, linatokana na kufanya mapenzi ya Baba yetu aliye mbinguni.—Mt. 5:6.

20 Na tuendelee kupata burudisho katika mambo ya kiroho. Tunapofanya hivyo, ‘tunakataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu huku tukilingojea tumaini la furaha na kufunuliwa kwenye utukufu kwa Mungu mkuu na kwa Mwokozi wetu, Kristo Yesu.’ (Tito 2:12, 13) Kwa hiyo, acheni tuazimie kukaa chini ya nira ya Yesu kwa kujitiisha chini ya mamlaka na mwongozo wake. Tukifanya hivyo, tutapata furaha na burudisho la kweli!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Kwa habari zaidi kuhusu njia za kufanya funzo la familia lipendeze na kuelimisha, ona Huduma ya Ufalme Yetu ya Desemba 1990, ukurasa wa 1-2.

Ungesema Nini?

• Watu wa Yehova wanapata burudisho leo jinsi gani?

• Ni katika njia gani huduma inatuburudisha pamoja na wale tunaowahubiria?

• Vichwa vya familia wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba ibada yao ya familia inaburudisha?

• Ni mambo gani yanayotulemea kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tukiichukua nira ya Yesu, tunapata burudisho kwa njia mbalimbali