Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pata Usalama Kati ya Watu wa Mungu

Pata Usalama Kati ya Watu wa Mungu

Pata Usalama Kati ya Watu wa Mungu

“Nitakusifu katika kutaniko kubwa.”—ZAB. 35:18.

1-3. (a) Ni nini kinachoweza kuwaingiza Wakristo fulani katika hali hatari ya kiroho? (b) Watu wa Mungu wanaweza kupata wapi ulinzi?

WAKIWA katika likizo, Joe na mke wake walikuwa wakipiga mbizi baharini wakiwa wamevaa vifaa vya kupumua huku wakiogelea karibu na mwamba wa baharini uliojaa samaki wenye rangi na ukubwa mbalimbali. Waliogelea mbali kidogo na ufuo ili kutazama miamba ya bahari. Walipofika katika sehemu yenye kina kirefu cha maji, mke wa Joe akasema, “Ninafikiri tunaenda mbali sana.” Joe akamjibu: “Tulia, ninajua kile ninachofanya.” Joe anakumbuka jinsi alivyoshangaa muda mfupi baadaye na kujiuliza hivi: ‘Wale samaki wote wameenda wapi?’ Alishtuka kwa woga alipotambua sababu. Katika maji hayo ya bahari yenye kina kirefu, samaki mkubwa anayeitwa papa alikuwa akija kumshambulia. Maisha ya Joe yalikuwa hatarini kabisa. Lakini alipokuwa umbali wa mita chache tu kutoka mahali ambapo Joe alikuwa, samaki huyo mkubwa aligeuka kwa ghafula na kwenda zake.

2 Mkristo anaweza kuvutiwa sana na mambo yenye kuvutia ya mfumo huu wa mambo wa Shetani, kama vile, burudani, kazi, na mali hivi kwamba asitambue kuwa anaelekea katika maji yenye kina kirefu zaidi yenye hatari. Joe, ambaye ni mzee Mkristo, anasema hivi: “Mambo ambayo nimejionea katika maisha yalinifanya nifikirie watu ambao tunashirikiana nao. Ogelea mahali pazuri na penye usalama, yaani, katika kutaniko!” Usiogelee mahali penye maji mengi sana ambapo unaweza kujikuta umejitenga kiroho na uko katika hatari. Ikiwa utajikuta mahali kama hapo, rudi haraka sana mahali penye ‘maji salama.’ Usipofanya hivyo, huenda ukajikuta katika hatari ya kumezwa kiroho.

3 Leo, ulimwengu ni mahali hatari kwa Wakristo. (2 Tim. 3:1-5) Shetani anajua kwamba siku zake zimehesabiwa, na ameazimia kummeza mtu yeyote asiyekuwa macho. (1 Pet. 5:8; Ufu. 12:12, 17) Hata hivyo, sisi tuna ulinzi. Yehova amewaandalia watu wake mahali salama pa kukimbilia kiroho, yaani, kutaniko la Kikristo.

4, 5. Watu wengi wanahisi jinsi gani kuhusu wakati wao ujao, na kwa nini?

4 Jamii ya kibinadamu inatoa usalama wa kiasi tu, iwe ni wa kimwili au wa kihisia. Watu wengi wanahisi kwamba usalama wao wa kimwili unatishwa na uhalifu, jeuri, gharama ya juu ya maisha, na hata hali ya mazingira. Wote wanapambana na matatizo ya uzee na ya afya. Halafu wengine walio na kazi, nyumba, pesa, na afya nzuri kwa kadiri fulani, huenda wakajiuliza vitu hivyo vitadumu kwa muda gani.

5 Wengi wameshindwa kupata usalama wa kihisia. Inasikitisha kwamba watu wengi ambao walitumaini kupata amani na furaha katika ndoa na kuwa na familia wamegundua kwamba matarajio yao hayajatimia. Kwa upande wa kiroho, watu wengi wanaoenda kanisani wamevurugika na kuchanganyikiwa, huku wakitilia shaka ubora wa mwongozo ambao wamepata. Watu hao wanahisi hivyo hasa wanapofikiria mwenendo mbaya na mafundisho yasiyopatana na Maandiko ya viongozi wao wa kidini. Hivyo, watu wengi wanahisi kwamba hawana la kufanya isipokuwa kuitumaini tu sayansi au hekima na nia njema ya wanadamu wenzao. Hivyo, haishangazi kuona kwamba majirani wetu wanahisi kuwa hawana usalama hata kidogo au hawapendi kufikiria sana kuhusu wakati wao ujao.

6, 7. (a) Kwa nini watu wanaomtumikia Mungu wana mtazamo tofauti na wale ambao hawamtumikii? (b) Tutachunguza nini?

6 Wale ambao wako katika kutaniko la Kikristo wana mtazamo tofauti kama nini na wale ambao hawako katika kutaniko hilo! Hata ingawa sisi tukiwa watu wa Yehova tunapambana na mambo na matatizo yaleyale kama majirani wetu, tunatenda kwa njia tofauti kabisa. (Soma Isaya 65:13, 14; Malaki 3:18.) Kwa nini? Kwa sababu tunapata katika Biblia maelezo yenye kuridhisha kuhusu hali ambazo zinawapata wanadamu leo, na tunatayarishwa vizuri ili kupambana na hali ngumu na matatizo ya maisha. Kwa sababu hiyo, hatuhangaiki kupita kiasi kuhusu wakati ujao. Kuwa waabudu wa Yehova kunatulinda na mawazo yasiyofaa ambayo hayapatani na Maandiko, na kunatulinda pia na mazoea mapotovu kiadili, na matokeo yake. Hivyo, washiriki wa kutaniko la Kikristo wana utulivu ambao wengine hawana.—Isa. 48:17, 18; Flp. 4:6, 7.

7 Huenda mifano fulani ikatusaidia kufikiria usalama ambao wale wanaomtumikia Yehova wanafurahia tofauti na wale ambao hawamtumikii. Mifano hiyo inaweza kutuchochea kuchunguza njia yetu ya kufikiri na mazoea yetu na kuona ikiwa tunaweza kufuata kikamili zaidi mashauri ya Mungu, ambayo yanakusudiwa kutulinda.—Isa. 30:21.

“Karibu Miguu Yangu Igeuke Kando”

8. Sikuzote watumishi wa Yehova wamelazimika kufanya nini?

8 Tangu mwanzo wa historia ya wanadamu, wale waliochagua kumtumikia na kumtii Yehova walijitahidi kuepuka kushirikiana na wale ambao hawakumtumikia. Kwa kweli, Yehova alionyesha kwamba kungekuwa na uadui kati ya waabudu wake na wale ambao walimfuata Shetani. (Mwa. 3:15) Kwa sababu ya kushikamana kabisa na kanuni zilizoongozwa na roho ya Mungu, watu wa Mungu wametenda kwa njia tofauti na majirani wao. (Yoh. 17:15, 16; 1 Yoh. 2:15-17) Si rahisi kuwa na msimamo huo sikuzote. Kwa kweli, wakati mwingine watumishi fulani wa Yehova wametilia shaka hekima ya kuishi maisha ya kujidhabihu.

9. Eleza hisia ambazo mwandikaji wa Zaburi ya 73 alipambana nazo.

9 Mmoja wa watumishi wa Yehova ambaye alianza kujiuliza ikiwa alifanya maamuzi ya hekima ni mwandikaji wa Zaburi ya 73, ambaye inaelekea alikuwa mzao wa Asafu. Mtunga-zaburi huyo alijiuliza kwa nini mara nyingi waovu wanaonekana wanafanikiwa, wana furaha, na wanasitawi, huku watu wengine wanaojitahidi kumtumikia Mungu wakipata majaribu na matatizo.—Soma Zaburi 73:1-13.

10. Kwa nini maswali au maulizo ambayo mtunga-zaburi aliuliza ni ya maana sana kwako?

10 Je, umewahi kujiuliza maswali kama yale ambayo mtunga-zaburi huyo aliandika? Ikiwa ndivyo, hakuna haja ya kujihisi kuwa mwenye hatia sana au kufikiri kwamba imani yako inadhoofika. Ni kweli kwamba watumishi wengi wa Yehova, kutia ndani watu fulani ambao Yehova alitumia kuandika Biblia, walikuwa na mawazo kama hayo. (Ayu. 21:7-13; Zab. 37:1; Yer. 12:1; Hab. 1:1-4, 13) Kwa kweli, ni lazima wote ambao wanataka kumtumikia Yehova watafakari kwa uzito kuhusu jambo hilo na kukubali jibu la swali hili: Je, kumtumikia na kumtii Mungu ndilo jambo bora zaidi ambalo mtu anapaswa kufanya? Swali hilo linahusiana na suala ambalo Shetani alitokeza katika bustani ya Edeni. Ni suala la maana sana ambalo linahusu enzi kuu ya Mungu ya ulimwenguni pote. (Mwa. 3:4, 5) Hivyo, ni vizuri sote tuchunguze jambo hilo ambalo mtunga-zaburi alitokeza. Je, tunapaswa kuwaonea wivu waovu wenye kujivuna ambao wanaonekana hawana matatizo ya maisha? Je, tunapaswa ‘kugeuka kando’ kwa kuacha kumtumikia Yehova na kuwaiga watu hao? Bila shaka, hilo ndilo jambo ambalo Shetani angetaka hasa tufanye.

11, 12. (a) Mtunga-zaburi alishinda mashaka yake jinsi gani, na hilo linatufundisha nini? (b) Ni nini ambacho kimekusaidia kukata kauli kama ile ya mtunga-zaburi?

11 Ni nini kilichomsaidia mtunga-zaburi kushinda mashaka yake? Ingawa alikubali kwamba alikuwa karibu kugeuka kando na kuacha uadilifu, maoni yake yalibadilika alipoingia katika “patakatifu pakuu pa Mungu,” yaani, aliposhirikiana na watu wa kiroho katika maskani ya Mungu au hekalu lake na kutafakari juu ya kusudi la Mungu. Ndipo mtunga-zaburi alipotambua waziwazi kwamba hakutaka kupatwa na matokeo mabaya kama watenda-maovu. Sasa angeweza kuona kwamba maisha yao na maamuzi yao maishani yaliwaweka kwenye “udongo unaoteleza.” Mtunga-zaburi alitambua kwamba wale wote wanaomwacha Yehova na kufuata upotovu wa maadili, bila shaka watafikia mwisho wao katika “matisho ya ghafula,” lakini Yehova atawategemeza wale wanaomtumikia. (Soma Zaburi 73:16-19, 27, 28.) Ni wazi kwamba umejionea ukweli wa maneno hayo. Huenda watu wengi wakavutiwa na maisha ya kujitegemea na kutojali sheria za Mungu, lakini matokeo mabaya ya mwenendo huo hayawezi kuepukika.—Gal. 6:7-9.

12 Ni nini kingine tunachojifunza kutokana na mambo ambayo mtunga-zaburi alijionea maishani? Alipata usalama na hekima kati ya watu wa Mungu. Alianza tena kufikiri vizuri na waziwazi alipoenda mahali ambapo Yehova aliabudiwa. Vivyo hivyo leo, tunaweza kupata washauri wenye hekima na kufurahia chakula kizuri cha kiroho katika mikutano ya kutaniko. Kwa hiyo, Yehova ana sababu nzuri ya kuwaambia watumishi wake wahudhurie mikutano ya Kikristo. Katika mikutano hiyo, watajihisi wametiwa moyo nao watachochewa kutenda kwa hekima.—Isa. 32:1, 2; Ebr. 10:24, 25.

Chagua Marafiki Wako kwa Hekima

13-15. (a) Dina alipatwa na nini, na hilo linaonyesha nini? (b) Kwa nini kushirikiana na Wakristo wenzetu ni ulinzi?

13 Dina, binti ya Yakobo ni mfano wa mtu ambaye alijiingiza katika matatizo mazito kwa sababu ya kushirikiana na marafiki wa ulimwengu. Simulizi la kitabu cha Mwanzo kumhusu linatuambia kwamba Dina alikuwa na zoea la kushirikiana na wasichana Wakanaani katika eneo ambalo familia yake iliishi. Wakanaani hawakuwa na viwango vya juu vya maadili kama waabudu wa Yehova. Kinyume na hilo, vitu ambavyo wataalamu wa vitu vya kale wamegundua vinaonyesha kwamba maisha ya Wakanaani yalifanya nchi yao ijae ibada ya sanamu, upotovu wa maadili, ibada chafu sana ya ngono, na jeuri. (Kut. 23:23; Law. 18:2-25; Kum. 18:9-12) Kumbuka matokeo mabaya yaliyompata Dina kwa sababu ya kushirikiana na watu hao.

14 Mwanamume mmoja mwenyeji, Shekemu, ambaye inasemekana alikuwa “mwenye kuheshimika zaidi katika nyumba nzima ya baba yake,” alimwona Dina na “kisha akamchukua, akalala naye, akamnajisi.” (Mwa. 34:1, 2, 19) Ulikuwa msiba mkubwa kama nini! Je, unafikiri Dina aliwazia kwamba jambo hilo lingeweza kumpata? Labda alikuwa akitaka tu kufanya urafiki pamoja na vijana wa eneo hilo, ambao alifikiri kwamba hawakuwa hatari. Hata hivyo, Dina alidanganyika kabisa.

15 Simulizi hilo linatufundisha nini? Kwamba hatuwezi kushirikiana na watu ambao si waamini huku tukifikiri kwamba hatuwezi kupatwa na matokeo mabaya. Maandiko yanasema kwamba “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Kor. 15:33) Kwa upande mwingine, ni ulinzi kushirikiana na watu ambao wana imani kama yako, viwango vya juu vya maadili kama vyako, na upendo kama wako kwa Yehova. Marafiki hao wazuri watakutia moyo kutenda kwa hekima.—Met. 13:20.

“Mmeoshwa Mkawa Safi”

16. Mtume Paulo alisema nini kuhusu watu fulani katika kutaniko la Korintho?

16 Kutaniko la Kikristo limewasaidia watu wengi kusafisha maisha yao kwa kuacha mazoea machafu. Mtume Paulo alipoandika barua yake ya kwanza kwa kutaniko la Korintho, alizungumza kuhusu mabadiliko ambayo Wakristo wa huko walifanya ili kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Zamani, wengine wao walikuwa waasherati, waabudu-sanamu, wazinzi, walawiti, wezi, walevi, na kadhalika. Paulo aliwaambia hivi: “Lakini mmeoshwa mkawa safi.”—Soma 1 Wakorintho 6:9-11.

17. Kuishi kulingana na viwango vya Biblia kumebadili jinsi gani maisha ya watu wengi?

17 Watu wasio na imani hawana kanuni nzuri za kuwaongoza. Wanajiwekea wenyewe viwango vyao ya maisha au huenda wakawa wanaiga mwenendo mpotovu wa majirani wao, kama walivyofanya Wakorintho fulani wa zamani kabla ya kuwa waamini. (Efe. 4:14) Hata hivyo, ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na makusudi yake, una nguvu za kubadili kwa njia nzuri zaidi maisha ya wote ambao wanafuata Maandiko. (Kol. 3:5-10; Ebr. 4:12) Watu wengi ambao leo ni washiriki wa kutaniko la Kikristo wanaweza kukwambia kwamba kabla ya kujifunza na kukubali viwango vya uadilifu vya Yehova, waliishi maisha mapotovu kabisa kiadili. Hata hivyo, hawakuridhika na hawakuwa na furaha. Walipata amani walipoanza tu kushirikiana na watu wa Mungu na kuishi kulingana na kanuni za Biblia.

18. Dada mmoja kijana alipatwa na nini, na hilo linathibitisha nini?

18 Kinyume na hilo, wengine ambao zamani waliamua kutoka katika eneo la ‘maji salama’ ya kutaniko la Kikristo sasa wanajuta kwa uchungu kwa sababu ya uamuzi waliofanya. Dada mmoja, ambaye tutamwita Tanya, anaeleza kwamba “alilelewa katika familia ya Kikristo,” lakini alipokuwa na umri wa miaka 16, aliacha kutaniko ili “atafute raha za ulimwengu.” Alikabili matatizo kama vile kupata mimba isiyotakiwa na kisha akaitoa. Sasa anasema hivi: “Miaka mitatu niliyokuwa nje ya kutaniko iliacha makovu mabaya sana moyoni mwangu ambayo hayatapona. Jambo ambalo linaendelea kunisumbua ni kwamba nilimuua mtoto wangu ambaye hakuwa amezaliwa. . . . Ningependa kuwaambia hivi vijana wote ambao wanatamani ‘kuonja’ ulimwengu hata kwa muda mfupi tu: ‘Msijaribu!’ Mwanzoni huenda ulimwengu ukaonekana kuwa wenye kuvutia, lakini unaacha maumivu makali sana moyoni. Ulimwengu hauna chochote cha kutoa isipokuwa maumivu. Ninajua. Nilionja maumivu hayo. Kaeni katika tengenezo la Yehova! Ndiyo njia pekee ya maisha inayoleta furaha.”

19, 20. Kutaniko la Kikristo linatoa ulinzi gani, na jinsi gani?

19 Wazia jinsi ambavyo maisha yako yangekuwa ikiwa ungeacha mazingira yenye ulinzi ya kutaniko la Kikristo. Wengi wanaogopa wanapofikiria maisha ya ubatili waliyokuwa nayo kabla ya kujifunza kweli. (Yoh. 6:68, 69) Unaweza kuendelea kupata usalama na ulinzi na kuepuka taabu na maumivu ambayo ni ya kawaida katika ulimwengu huu wa Shetani ukishirikiana kwa ukaribu sana na ndugu na dada zako Wakristo. Ukishirikiana nao na kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya kutaniko utakumbuka sikuzote kwamba ni jambo la hekima kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova na utatiwa moyo kuishi kulingana na viwango hivyo. Una kila sababu ya ‘kumsifu Yehova katika kutaniko kubwa,’ kama tu alivyofanya mtunga-zaburi.—Zab. 35:18.

20 Bila shaka, kwa sababu mbalimbali, Wakristo wote wanapambana na nyakati ngumu inapoonekana kuwa vigumu kwao kuendelea kudumisha utimilifu wao wa Kikristo. Huenda wakahitaji tu mtu fulani awaonyeshe njia nzuri ya kufuata. Wewe na wengine wote katika kutaniko, mnaweza kufanya nini ili kuwasaidia waamini wenzetu katika nyakati hizo? Habari inayofuata itachunguza jinsi unavyoweza ‘kuendelea kuwafariji na kuwajenga’ ndugu zako.—1 The. 5:11.

Ungesema Nini?

• Tunajifunza nini kutokana na mambo yaliyompata mwandikaji wa Zaburi ya 73?

• Mambo yaliyompata Dina yanatufundisha nini?

• Kwa nini unaweza kupata usalama katika kutaniko la Kikristo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ogelea mahali salama; kaa katika kutaniko!