Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Endelea Kufanya Bidii . . . Katika Kufundisha”

“Endelea Kufanya Bidii . . . Katika Kufundisha”

“Endelea Kufanya Bidii . . . Katika Kufundisha”

“NINYI huniita, ‘Mwalimu,’ na, ‘Bwana,’ nanyi mnasema sawasawa, kwa maana ndivyo nilivyo.” (Yoh. 13:13) Yesu alipowaambia wanafunzi wake maneno hayo alikazia daraka lake akiwa mwalimu. Kisha, muda mfupi kabla ya Yesu kupanda mbinguni, aliwaamuru hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, 20) Baadaye, mtume Paulo pia alikazia umuhimu wa kuwa walimu wa Neno la Mungu. Alimhimiza hivi mzee Mkristo Timotheo: “Endelea kufanya bidii katika kusoma mbele ya watu wote, katika kuhimiza, katika kufundisha. . . . Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yawe wazi kwa watu wote.”—1 Tim. 4:13-15.

Leo, kama ilivyokuwa wakati huo, kufundisha ni sehemu ya maana sana ya huduma yetu ya shambani na mikutano yetu ya Kikristo. Tunaweza kuendelea jinsi gani kufanya bidii katika kufundisha, na hilo litatusaidia katika njia gani kufanya maendeleo tukiwa walimu wa Neno la Mungu?

Mwige Yule Mwalimu Mkuu

Watu wengi waliomsikiliza Yesu walivutiwa na njia yake ya kufundisha. Angalia jinsi maneno yake yalivyowavutia watu walioenda katika sinagogi huko Nazareti. Luka, mwandikaji wa Injili, aliandika hivi: “Wote wakaanza kutoa ushahidi mwema juu yake wakistaajabia maneno yenye kuvutia sana yaliyokuwa yakitoka kinywani mwake.” (Luka 4:22) Wanafunzi wa Yesu waliiga mfano wa Bwana wao katika mahubiri yao. Kwa kweli, mtume Paulo aliwatia moyo hivi Wakristo wenzake: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Kor. 11:1) Kwa sababu ya kuiga njia za Yesu za kufundisha, Paulo alikuja kuwa mwenye ustadi sana katika ‘kufundisha hadharani na nyumba kwa nyumba.’—Mdo. 20:20.

Kufundisha “Sokoni”

Kitabu cha Matendo sura ya 17 kina mfano mzuri sana ambao unaonyesha uwezo wa Paulo wa kufundisha hadharani. Katika kitabu hicho tunasoma kuhusu safari yake huko Athene, Ugiriki. Paulo aliona sanamu kila mahali katika jiji hilo, yaani, barabarani na katika sehemu za watu wote. Haishangazi kwamba Paulo aliudhika sana. Hata hivyo, hakuruhusu hisia hizo zimzuie kuhubiri. Badala yake, ‘alianza kujadiliana katika sinagogi na kila siku sokoni pamoja na wale waliokuwapo.’ (Mdo. 17:16, 17) Alituwekea mfano mzuri kama nini! Tunapozungumza na watu wa malezi mbalimbali, bila kuwahukumu-hukumu, lakini kwa njia ya heshima, tunafungua njia ili wengine wao wasikilize na mwishowe watoke katika utumwa wa dini ya uwongo.—Mdo. 10:34, 35; Ufu. 18:4.

Watu wengi ambao Paulo aliwahubiria sokoni hawakukubali ujumbe wake. Kati ya watu waliomsikiliza ni wanafalsafa ambao walikuwa na maoni yasiyopatana na kweli ambazo alikuwa akihubiri. Paulo alipokutana na watu wenye ubishi, bila shaka alisikiliza maelezo yao. Wengine wao walimwita “mpiga-domo” (yaani, kihalisi, “mtu anayeokota mbegu”). Wengine wakasema: “Anaonekana kuwa mtangazaji wa miungu migeni.”—Mdo. 17:18.

Hata hivyo, Paulo hakuvunjwa moyo na maelezo hayo yenye kuumiza ya wasikilizaji wake. Badala yake, alipoombwa aeleze mafundisho yake, Paulo alitumia nafasi hiyo kutoa hotuba yenye kuelimisha ambayo ilionyesha vizuri ustadi wake wa kufundisha. (Mdo. 17:19-22; 1 Pet. 3:15) Acheni tupitie hotuba hiyo kwa undani na kujifunza masomo ambayo yanaweza kutusaidia kuboresha ustadi wetu wa kufundisha.

Weka Msingi wa Makubaliano

Paulo alisema hivi: ‘Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa wenye mwelekeo zaidi wa kuogopa miungu kuliko wengine. Kwa mfano, nilipokuwa nikitazama kwa uangalifu vitu vyenu vya ibada, niliona pia madhabahu ambayo ilikuwa imeandikwa “Kwa Mungu Asiyejulikana.” Kwa hiyo kile mnachokipa ujitoaji-kimungu bila kujua, hicho ninawatangazia ninyi.’—Mdo. 17:22, 23.

Paulo aliangalia kwa uangalifu sana mazingira yake. Kutokana na vitu ambavyo alikuwa ameangalia kwa uangalifu, alijifunza mengi kuhusu wasikilizaji wake. Sisi pia tunaweza kujifunza jambo fulani kuhusu mwenye nyumba kwa kutazama mambo kwa uangalifu. Kwa mfano, tunaweza kujifunza mengi tukiona vitu vya watoto vya kuchezea au ikiwa kuna ishara mbalimbali kwenye mlango. Ikiwa tunajua kwa kiasi fulani hali za mwenye nyumba, tunaweza kuchagua kwa uangalifu jambo la kusema na pia jinsi ya kulisema.—Kol. 4:6.

Paulo hakuwahukumu-hukumu wengine katika mazungumzo yake. Hata hivyo, aligundua kwamba “ujitoaji-kimungu” wa Waathene haukutegemea ujuzi sahihi. Paulo alieleza waziwazi jinsi ambavyo wangemwabudu Mungu wa kweli. (1 Kor. 14:8) Ni jambo la maana kama nini kwetu kuzungumza kwa njia iliyo wazi na yenye kujenga tunapotangaza habari njema ya Ufalme!

Tumia Busara na Usiwe na Ubaguzi

Paulo aliendelea kusema hivi: “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama Huyu alivyo, Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono, wala hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote, kwa sababu yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.”—Mdo. 17:24, 25.

Katika andiko hilo Paulo alimwelekezea fikira Yehova akiwa Mpaji-Uhai wetu, na alitumia busara kwa kumwita “Bwana wa mbingu na dunia.” Ni pendeleo kama nini kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu kutoka katika dini na malezi mbalimbali kujifunza kwamba Yehova Mungu ndiye aliyeumba vitu vyote vilivyo hai!—Zab. 36:9.

Kisha, Paulo anasema hivi: “Naye alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, . . . naye aliamuru nyakati na mipaka ya makao ya watu, ili wao wamtafute Mungu, ikiwa wangeweza kupapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ijapokuwa, kweli, hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Mdo. 17:26, 27.

Kupitia njia yetu ya kufundisha, tunaweza kuwasaidia wengine wajue tunamwabudu Mungu wa aina gani. Bila ubaguzi, Yehova anawaruhusu watu wa mataifa yote ‘wapapase-papase wakimtafuta na kwa kweli wampate.’ Vivyo hivyo, tunazungumza bila ubaguzi na watu wote tunaokutana nao. Tunajaribu kuwasaidia wale ambao wanamwamini Muumba ili wasitawishe uhusiano wa karibu pamoja naye ambao unaweza kuwawezesha kupata baraka za milele. (Yak. 4:8) Lakini tunawasaidia jinsi gani wale ambao wana shaka kwamba kuna Mungu? Tunafuata mfano wa Paulo. Ona jambo ambalo alisema baadaye.

“Kupitia kwake tuna uhai na tunaenda na kuwako, hata kama vile ambavyo watu fulani ambao ni washairi kati yenu wamesema, ‘Kwa maana sisi pia ni uzao wake.’ Kwa hiyo, kwa kuwa sisi ni uzao wa Mungu, hatupaswi kuwazia kwamba Mungu ni kama dhahabu au fedha au jiwe.”—Mdo. 17:28, 29.

Katika andiko hilo Paulo alijaribu kuwashawishi wamsikilize kwa kutaja washairi ambao Waathene waliwajua na kuwakubali. Sisi pia tunajitahidi kuweka msingi wa makubaliano kwa kuzungumzia mambo ambayo tunajua kwamba wasikilizaji wetu watakubali. Kwa mfano, katika barua yake kwa Waebrania, Paulo anatoa mfano ambao unasadikisha leo pia: “Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Ebr. 3:4) Kuwatia moyo wenye nyumba wafikirie mfano huo rahisi kunaweza kuwasaidia wakubali ukweli wa yale tunayosema. Ona jambo lingine linaloonyesha ustadi wa kufundisha katika hotuba ya Paulo, yaani, kuwachochea watu.

Kazia Kwamba Tunapaswa Kuchukua Hatua Haraka

Paulo alisema hivi: “Ni kweli, Mungu ameachilia mbali nyakati hizo za kutojua, lakini sasa anawaambia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu. Kwa sababu ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi.”—Mdo. 17:30, 31.

Hatua ya Mungu ya kuruhusu uovu kwa muda imetupatia sisi sote nafasi ya kumwonyesha mambo ambayo kwa kweli yako ndani ya mioyo wetu. Ni jambo la maana tukazie kwamba leo tunapaswa kuchukua hatua haraka na tuzungumze kwa usadikisho kuhusu baraka za utawala wa Ufalme ambao utakuja hivi karibuni.—2 Tim. 3:1-5.

Watu Wanaitikia kwa Njia Tofauti-Tofauti

“Basi, waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine kati yao wakaanza kudhihaki, huku wengine wakisema: ‘Tutakusikiliza tena juu ya jambo hili wakati mwingine.’ Hivyo Paulo akatoka katikati yao, lakini wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini.”—Mdo. 17:32-34.

Watu fulani wanakubali papo hapo mafundisho yetu; huenda wengine wakahitaji wakati zaidi ili wasadikishwe na njia yetu ya kufikiri. Lakini tunapoeleza kweli kwa njia rahisi na iliyo wazi na kumsaidia angalau mtu mmoja kupata ujuzi sahihi kumhusu Yehova, tunashukuru kama nini kutumiwa na Mungu kuwavuta watu kwa Mwana wake!—Yoh. 6:44.

Mambo Tunayojifunza

Tukifikiria hotuba ya Paulo, tunaweza kujifunza mengi kuhusu jinsi ya kuwaeleza wengine kweli za Biblia. Ikiwa tuna pendeleo la kutoa hotuba za watu wote katika kutaniko, tunaweza kujitahidi kumwiga Paulo kwa kutumia maneno ya busara ambayo yatamsaidia mtu asiye mwamini aelewe na kukubali kweli za Biblia. Tunapaswa kufundisha kweli hizo kwa njia iliyo wazi, lakini tutakuwa waangalifu ili tusidharau imani ya mtu yeyote asiye mwamini ambaye huenda akawa amehudhuria mikutano. Wakati huohuo, tunapohubiri hadharani, tunajitahidi kuhubiri kwa ushawishi na busara. Kwa njia hiyo, tutakuwa kwa kweli tukifuata shauri la Paulo la ‘kufanya bidii katika kufundisha.’

[Picha katika ukurasa wa 30]

Paulo alifundisha kwa njia iliyo wazi, rahisi, na kwa busara

[Picha katika ukurasa wa 31]

Tunamwiga Paulo kwa kufikiria hisia za watu tunaowahubiria