Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shiriki Kikamili Katika Mavuno Makubwa ya Kiroho

Shiriki Kikamili Katika Mavuno Makubwa ya Kiroho

Shiriki Kikamili Katika Mavuno Makubwa ya Kiroho

‘Uwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’—1 KOR. 15:58.

1. Ni mwaliko gani ambao Yesu aliwatolea wanafunzi wake?

ALIPOKUWA akisafiri kupitia eneo la Samaria mwishoni mwa mwaka wa 30 W.K., Yesu alipumzika kwenye kisima kimoja karibu na mji wa Sikari. Akiwa hapo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35) Yesu hakuwa akizungumza kuhusu mavuno halisi, bali kuhusu kukusanywa kiroho kwa watu wenye mioyo minyoofu ambao wangekuwa wafuasi wake. Kwa maneno hayo, Yesu alikuwa akiwaomba wafuasi wake washiriki katika mavuno hayo. Kulikuwa na kazi nyingi ya kufanya ambayo ilipaswa kutimizwa kwa muda mfupi tu!

2, 3. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba tunaishi wakati wa mavuno? (b) Habari hii itazungumzia nini?

2 Maneno ya Yesu kuhusu mavuno yana maana ya pekee katika siku zetu. Tunaishi wakati ambapo shamba la ulimwengu wa wanadamu ni ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’ Kila mwaka, mamilioni ya watu wanapewa mwaliko wa kujifunza kweli zinazotoa uhai, na maelfu mengi ya wanafunzi wapya wanabatizwa. Tuna pendeleo la kushiriki katika mavuno hayo makubwa zaidi yasiyo na kifani, chini ya usimamizi wa Bwana wa mavuno, Yehova Mungu. Je, una “mengi ya kufanya” katika kazi hii ya mavuno?—1 Kor. 15:58.

3 Wakati wa huduma yake ya miaka mitatu na nusu duniani, Yesu aliwatayarisha wanafunzi wake ili kutimiza daraka lao la kuwa wafanyakazi katika mavuno. Habari hii itazungumzia masomo matatu ya maana kati ya mengine mengi ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake. Kila somo linakazia sifa moja yenye thamani kubwa kwetu tunapojitahidi kufanya yote tunayoweza katika kazi ya kukusanya wanafunzi leo. Acheni tuchunguze sifa hizo moja baada ya nyingine.

Unyenyekevu Ni wa Maana

4. Akitumia mfano, Yesu alionyesha jinsi gani umuhimu wa unyenyekevu?

4 Wazia hali hii: Wanafunzi wametoka tu kubishana kuhusu ni nani aliye mkuu zaidi kati yao. Inaelekea kwamba nyuso zao bado zinaonyesha hisia za kutoaminiana na za uadui. Hivyo, Yesu anamwita mtoto mchanga asimame katikati yao. Akikazia uangalifu mtoto huyo mchanga, Yesu anasema hivi: “Yeyote atakayejinyenyekeza mwenyewe [au “yeyote atakayejifanya mwenyewe kuwa mdogo,” Byington] kama mtoto huyu mchanga ndiye aliye mkuu zaidi katika ufalme wa mbinguni.” (Soma Mathayo 18:1-4.) Badala ya kufikiri kama watu wa ulimwengu, ambao wanapima ubora wa mtu kwa kutegemea mamlaka, mali, na cheo chake, wanafunzi walihitaji kuelewa kwamba ukuu wao ulitegemea ‘kujifanya wenyewe kuwa wadogo’ machoni pa wengine. Yehova angewabariki na kuwatumia ikiwa tu wangeonyesha unyenyekevu wa kweli.

5, 6. Kwa nini unapaswa kuwa mnyenyekevu ili ushiriki kikamili katika kazi ya mavuno? Toa mfano.

5 Leo pia, watu wengi ulimwenguni wamejitoa maishani kufuatia mamlaka, mali, na vyeo. Kwa sababu hiyo, wana wakati mdogo au hata hawana wakati kwa ajili ya mambo ya kiroho. (Mt. 13:22) Kinyume na hilo, watu wa Yehova wana furaha kwa kuwa ‘wanajifanya wenyewe kuwa wadogo’ machoni pa wengine ili wapate baraka na kibali cha Bwana wa mavuno.—Mt. 6:24; 2 Kor. 11:7; Flp. 3:8.

6 Fikiria mfano wa Francisco, anayetumikia akiwa mzee wa kutaniko huko Amerika Kusini. Akiwa kijana, aliacha chuo kikuu ili kuwa painia. Anakumbuka hivi: “Baadaye nilipopata mchumba, ningepata kazi ambayo ingeniletea mimi na mke wangu usalama mkubwa zaidi wa kifedha. Badala yake, tuliamua kurahisisha maisha yetu na kuendelea pamoja katika utumishi wa wakati wote. Baadaye, tulizaa watoto, na matatizo yakaongezeka. Lakini Yehova alitusaidia kushikamana na uamuzi wetu.” Francisco anamalizia hivi: “Kwa zaidi ya miaka 30, nimefurahia pendeleo la kutumikia nikiwa mzee, na pia mapendeleo mengine mengi ya pekee. Hatujawahi kamwe kujuta kwa sababu ya kuishi maisha rahisi.”

7. Umejaribu jinsi gani kufuata shauri la Waroma 12:16?

7 Ikiwa unakataa “mambo makuu” ya ulimwengu huu na kujiacha mwenyewe ‘uongozwe na mambo ya hali ya chini,’ wewe pia unaweza kutazamia kufurahia baraka na mapendeleo mengi zaidi katika kazi hii ya mavuno.—Rom. 12:16; Mt. 4:19, 20; Luka 18:28-30.

Bidii Inathawabisha

8, 9. (a) Eleza kwa ufupi mfano wa Yesu wa talanta. (b) Ni nani hasa wanaoweza kutiwa moyo na mfano huo?

8 Sifa nyingine ambayo tunahitaji ili kushiriki kikamili katika kazi hii ya mavuno ni bidii. Yesu alionyesha hilo katika mfano wa talanta. * Mfano huo unahusu mwanamume ambaye, kabla ya kusafiri kwenda ng’ambo, aliwakabidhi watumwa watatu mali zake. Mtumwa wa kwanza alipokea talanta tano na wa pili akapokea talanta mbili; na wa tatu, talanta moja. Baada ya bwana wao kuondoka, watumwa wawili wa kwanza walitenda kwa bidii na papo hapo ‘wakafanya biashara’ na talanta zao. Tofauti na watumwa hao wawili wa kwanza, mtumwa wa tatu alikuwa “goigoi.” Aliizika talanta yake ndani ya udongo. Aliporudi kutoka safarini, bwana huyo aliwathawabisha watumwa wawili wa kwanza kwa kuwaweka rasmi “juu ya mambo mengi.” Aliichukua talanta ambayo alikuwa amempa yule mtumwa wa tatu na kumfukuza mtumwa huyo kutoka nyumbani kwake.—Mt. 25:14-30.

9 Bila shaka, unatamani moyoni mwako kuiga watumwa wenye bidii katika mfano wa Yesu na hivyo kushiriki kikamili kadiri iwezekanavyo katika kazi ya kufanya wanafunzi. Lakini namna gani ikiwa hali hazikuruhusu kutimiza mengi sasa? Labda hali ngumu za kiuchumi zinakulazimisha kufanya kazi kwa saa nyingi ili kupata riziki kwa ajili ya familia yako. Au labda kwa sababu ya umri mkubwa huna tena nguvu na afya nzuri kama zamani. Ikiwa ndivyo ilivyo, mfano wa talanta una ujumbe ambao utakutia moyo.

10. Bwana anayetajwa katika mfano wa talanta alijionyesha jinsi gani kuwa mwenye usawaziko, na kwa nini hilo linakutia moyo?

10 Ona kwamba bwana katika mfano huo anatambua kuwa kila mmoja wa watumwa wake ana uwezo tofauti. Alionyesha hilo alipowapa talanta “kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.” (Mt. 25:15) Kama ilivyotazamiwa, mtumwa wa kwanza alipata talanta zaidi kuliko mtumwa wa pili. Hata hivyo, bwana alitambua jitihada zenye bidii za watumwa hao wawili kwa kuwatangaza kuwa watumwa ‘wema na waaminifu’ na kuwapa thawabu zinazofanana. (Mt. 25:21, 23) Vivyo hivyo, Bwana wa mavuno, Yehova Mungu, anajua kwamba yale unayoweza kufanya katika utumishi wake yanategemea hali zako. Hatakosa kutambua jitihada zako za kumtumikia kwa nafsi yako yote naye atakuthawabisha.—Marko 14:3-9; soma Luka 21:1-4.

11. Toa mfano unaoonyesha jinsi bidii inavyoweza kutokeza baraka nyingi katika hali ngumu.

11 Mfano wa Selmira, dada Mkristo anayeishi huko Brazili, unaonyesha kwamba kuwa mwenye bidii katika utumishi wa Mungu hakutegemei mtu kuwa na hali nzuri katika maisha. Miaka 20 iliyopita, mume wa Selmira alipigwa risasi na wezi, hivyo akamwacha na watoto wachanga watatu wa kulea. Kazi ya dada huyo akiwa mtumishi wa nyumbani ilitia ndani kufanya kazi kwa muda wa saa nyingi na alichoka sana kwa kuwa alisafiri kwa mabasi ya mjini yanayojaa watu wengi. Ingawa alikabili matatizo yote hayo, alipanga vizuri mambo yake ili aweze kutumika akiwa painia wa kawaida. Baadaye, wawili kati ya watoto wake watatu walijiunga naye katika utumishi wa painia. Anaeleza hivi: “Katika miaka ambayo imepita, nimejifunza Biblia na watu zaidi ya 20, nao wamekuwa washiriki wa ‘familia’ yangu. Kufikia sasa, ninafurahia upendo na urafiki wao. Ni hazina ambayo pesa haziwezi kununua.” Bila shaka, Bwana wa mavuno amemthawabisha Selmira kwa sababu ya jitihada zake zenye bidii!

12. Tunaweza kuonyesha jinsi gani bidii katika kazi ya kuhubiri?

12 Ikiwa hali zako za sasa za maisha zinapunguza wakati ambao unatumia katika huduma, bado unaweza kujaribu kuongeza jitihada zako katika kazi ya mavuno kwa kufanya huduma yako iwe yenye matokeo zaidi. Ukifuata kwa uangalifu sana mapendekezo mazuri yanayotolewa katika Mkutano wa Utumishi wa kila juma, utaboresha ustadi wako wa kuhubiri na kujaribu njia mpya za kuhubiri. (2 Tim. 2:15) Pia, ikiwezekana, unaweza kubadili ratiba yako au kuacha mambo yasiyo ya lazima ili uweze kuunga mkono kwa ukawaida mipango ya kutaniko ya kuhubiri.—Kol. 4:5.

13. Ni jambo gani la maana zaidi linaloweza kutusaidia kusitawisha na kudumisha bidii?

13 Kumbuka kwamba bidii inatokana na moyo wenye kuthamini. (Zab. 40:8) Mtumwa wa tatu anayetajwa katika mfano wa Yesu alimwogopa bwana wake, na kumwona kuwa mwenye kudai sana na mtu asiyekuwa na usawaziko. Kwa sababu hiyo, mtumwa huyo alizika talanta yake moja badala ya kuitumia ili kuongeza mali za bwana wake. Ili kuepuka mtazamo kama huo wa uzembe, tunahitaji kusitawisha na kudumisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Bwana wa mavuno, Yehova. Tenga wakati ili kujifunza na kutafakari juu ya sifa zake zenye kuvutia, kama vile, upendo, subira, na huruma yake. Ukifanya hivyo, utachochewa kutoka moyoni kufanya yote unayoweza katika utumishi wake.—Luka 6:45; Flp. 1:9-11.

“Muwe Watakatifu”

14. Ni takwa gani la maana ambalo ni lazima litimizwe na wale ambao wanataka kuwa wafanyakazi wa mavuno?

14 Akinukuu Maandiko ya Kiebrania, mtume Petro anataja mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa kwa ajili ya watumishi wake walio duniani, akisema: “Kwa kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Pet. 1:15, 16; Law. 19:2; Kum. 18:13) Maneno hayo yanakazia kwamba wafanyakazi wa mavuno wanahitaji kuwa safi kiadili na kiroho. Tunaweza kutimiza takwa hilo la maana kwa kuchukua hatua za kusafishwa kwa njia ya mfano ili tuwe safi. Hilo linawezekana jinsi gani? Kwa msaada wa neno la Mungu la kweli.

15. Kweli ya neno la Mungu ina nguvu za kutufanyia nini?

15 Neno la Mungu la kweli linafananishwa na maji ambayo yanasafisha. Kwa mfano, mtume Paulo aliandika kwamba kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta ni safi machoni pa Mungu, kama bibi-arusi aliye safi kwa ajili ya Kristo, ambaye alilisafisha “na kuliosha kwa maji kwa njia ya neno . . . , ili liwe takatifu na bila dosari.” (Efe. 5:25-27) Mapema, Yesu pia alikuwa amezungumza kuhusu nguvu za kusafisha za neno la Mungu, ambalo alitangaza. Akizungumza na wanafunzi wake, Yesu alisema hivi: “Tayari ninyi ni safi kwa sababu ya neno ambalo nimewaambia.” (Yoh. 15:3) Hivyo, neno la Mungu lina nguvu za kusafisha kiadili na kiroho. Mungu atakubali ibada yetu ikiwa tu tutaruhusu kweli yake itusafishe kwa njia hiyo.

16. Tunaweza kulinda jinsi gani usafi wetu wa kiroho na kiadili?

16 Kwa hiyo, ili tuwe wafanyakazi katika kazi ya Mungu ya mavuno, tunapaswa kwanza kuondoa kabisa mazoea yote yenye kuchafua kiadili na kiroho katika maisha yetu. Ndiyo, ili tuendelee kustahili kuwa na pendeleo la kuwa wafanyakazi wa mavuno, ni lazima tuweke mfano mzuri katika kufuata viwango vya juu vya Yehova vya maadili na vya kiroho. (Soma 1 Petro 1:14-16.) Kama vile tu tunavyohangaikia sana usafi wetu wa kimwili, vivyo hivyo ni lazima tukubali kuongozwa kwa ukawaida na uvutano wenye kusafisha wa neno la Mungu la kweli. Hilo linatia ndani kusoma Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hilo pia linamaanisha kujitahidi kwa unyoofu kufuata vikumbusho vya Mungu katika maisha yetu. Tukifanya hivyo tutaweza kupambana na mielekeo yetu yenye dhambi na kushinda uvutano mbalimbali wenye kuchafua wa ulimwengu huu. (Zab. 119:9; Yak. 1:21-25) Ndiyo, inafariji kama nini kujua kwamba kwa msaada wa neno la Mungu la kweli, tunaweza ‘kusafishwa na kuwa safi’ kutokana na hata dhambi nzito!—1 Kor. 6:9-11.

17. Ili kubaki safi, ni lazima tutii shauri gani la Biblia?

17 Je, unakubali uongozwe na uvutano wenye kusafisha wa neno la kweli la Mungu katika maisha yako? Kwa mfano, unaitikia jinsi gani unapoonywa kuhusu hatari za burudani potovu za ulimwengu huu? (Zab. 101:3) Je, unaepuka kushirikiana isivyo lazima na wanafunzi na wafanyakazi wenzako ambao hawana imani kama yako? (1 Kor. 15:33) Je, unajitahidi kikweli kushinda udhaifu wako ambao unaweza kukufanya uwe mchafu machoni pa Yehova? (Kol. 3:5) Je, unajitenga na mizozo ya kisiasa na roho ya uzalendo ya ulimwengu huu ambayo inaonekana katika mashindano mengi ya michezo?—Yak. 4:4.

18. Kuwa safi kiadili na kiroho kutatusaidia jinsi gani kuwa wafanyakazi wenye matokeo katika mavuno?

18 Ukionyesha utii kwa uaminifu katika mambo kama hayo matokeo yatakuwa mazuri sana. Akiwalinganisha wanafunzi wake watiwa-mafuta na matawi ya mzabibu, Yesu alisema hivi: “Kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda [Baba yangu] huliondolea mbali, na kila tawi linalozaa matunda yeye hulisafisha, lipate kuzaa matunda zaidi.” (Yoh. 15:2) Unaporuhusu maji ya kweli ya Biblia yakusafishe, utazaa matunda mengi hata zaidi.

Baraka Sasa na Wakati Ujao

19. Wanafunzi wa Yesu walibarikiwa jinsi gani katika jitihada zao wakiwa wafanyakazi katika mavuno?

19 Wanafunzi waaminifu ambao walikubali mazoezi waliyopewa na Yesu baadaye walitiwa nguvu na roho takatifu siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. ili kuwa mashahidi “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Baadaye walitumika wakiwa washiriki wa baraza linaloongoza, wamishonari, na wazee wanaosafiri, na walitimiza daraka kubwa katika kuhubiri habari njema “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Walipokea baraka nyingi na kuwaletea wengine shangwe kama nini!

20. (a) Ni baraka gani ambazo umepata kwa kushiriki kikamili katika mavuno ya kiroho? (b) Umeazimia kufanya nini?

20 Ndiyo, tukionyesha unyenyekevu, bidii, na kufuata viwango vya juu vya Neno la Mungu, tutaendelea kufurahia kushiriki kikamili katika mavuno makubwa ya kiroho yanayoendelea sasa. Watu wengi wanapopata maumivu na kukata tamaa kwa sababu ya kufuatia vitu vya kimwili vya ulimwengu huu na maisha ya kupenda raha, sisi tunapata shangwe na uradhi wa kweli. (Zab. 126:6) Jambo la maana zaidi ni kwamba ‘kazi yetu si ya bure kuhusiana na Bwana.’ (1 Kor. 15:58) Bwana wa mavuno, Yehova Mungu, atatuthawabisha milele kwa sababu ya ‘kazi yetu na upendo ambao tunaonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Ebr. 6:10-12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kwanza kabisa, mfano wa talanta unaonyesha jinsi Yesu anavyoshughulika na wanafunzi wake watiwa-mafuta, lakini mfano huo una kanuni ambazo zinawahusu Wakristo wote.

Je, Unakumbuka?

Unapojitahidi kushiriki kikamili katika kazi hii ya mavuno . . .

• kwa nini ni jambo la maana kuonyesha unyenyekevu?

• unaweza kusitawisha na kudumisha bidii jinsi gani?

• kwa nini ni jambo la maana kuendelea kuwa safi kiadili na kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Unyenyekevu unaweza kutusaidia kuishi maisha rahisi ambayo yanakazia mambo ya Ufalme