Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Ndani ya Watoto Wako Tamaa ya Kupenda Kusoma na Kujifunza

Sitawisha Ndani ya Watoto Wako Tamaa ya Kupenda Kusoma na Kujifunza

Sitawisha Ndani ya Watoto Wako Tamaa ya Kupenda Kusoma na Kujifunza

KUJITAHIDI kabisa kuwafundisha watoto wako kusoma na kujifunza ni kati ya mambo ya maana zaidi ambayo yanaweza kuboresha wakati wao ujao. Pia kusoma na kujifunza kunaweza kuleta furaha nyingi kama nini! Watu fulani wanafurahi sana wanapokumbuka jinsi wazazi wao walivyokuwa wakiwasomea vitabu wakiwa watoto. Kusoma kunaweza kuwa jambo la kupendeza, na ndivyo ilivyo pia na matokeo yake. Jambo hilo ni la kweli hasa kuhusiana na watumishi wa Mungu, kwa kuwa wanapojifunza Biblia wanafanya maendeleo makubwa katika ukuzi wa kiroho. Mzazi mmoja Mkristo alisema hivi: “Mambo ambayo tunathamini zaidi yanahusiana na kusoma na kujifunza.”

Mazoea mazuri ya kujifunza yanaweza kuwasaidia watoto wako kujenga uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Mungu. (Zab. 1:1-3, 6) Ingawa kujua kusoma si takwa la kupata wokovu, Biblia inaonyesha kwamba kusoma kunaleta faida kubwa za kiroho. Kwa mfano, andiko la Ufunuo 1:3 linasema hivi: “Mwenye furaha ni yeye anayesoma kwa sauti na wale wanaosikia maneno ya unabii huu.” Zaidi ya hayo, shauri lililoongozwa na roho ya Mungu ambalo mtume Paulo alimwandikia Timotheo linaonyesha waziwazi faida ya kukaza fikira, jambo ambalo ni la maana sana katika kujifunza: “Tafakari mambo haya; zama katika hayo.” Kwa nini? “Ili maendeleo yako yawe wazi kwa watu wote.”—1 Tim. 4:15.

Bila shaka, kujua tu kusoma na kujifunza hakumpi mtu uhakikisho wa kwamba uwezo huo utamletea faida. Watu wengi ambao wana ustadi huo hawautumii; badala yake, wanafuatia mambo mengine ambayo hayana faida sana. Basi, wazazi wanaweza jinsi gani kusitawisha ndani ya watoto wao tamaa ya kupata ujuzi wenye faida?

Upendo Wako na Mfano Wako

Watoto wanafurahia vipindi vya funzo wanapoonyeshwa upendo. Owen na Claudia, wenzi wa ndoa Wakristo, wanakumbuka hivi kuhusu watoto wao wawili: “Walitazamia kwa hamu wakati wa funzo kwa sababu ulikuwa wakati wa pekee ambao walijihisi kwamba wamestarehe na kulindwa. Walianza kuona kwamba mazingira ya kujifunza ni yenye upendo.” Hata watoto wanapokua na kufikia miaka ya utineja ambayo ina mikazo mingi, mazingira yenye upendo katika funzo la familia yataendelea kuwa na uvutano mzuri juu ya mtazamo wao. Sasa watoto wa Owen na Claudia ni mapainia na wanaendelea kufaidika kwa sababu wazazi wao walisitawisha ndani yao tamaa ya kupenda kusoma na kujifunza.

Njia bora zaidi ya kuwafundisha kupenda kusoma ni kuwawekea mfano. Inaelekea kwamba watoto ambao mara nyingi wanawaona wazazi wao wakisoma na kujifunza wataona mambo hayo kuwa sehemu ya kawaida ya maisha yao wenyewe. Lakini ukiwa mzazi unaweza jinsi gani kuwawekea watoto wako mfano kama huo ikiwa hupendi kusoma? Huenda ukahitaji kubadili mambo unayotanguliza au mtazamo wako kuhusu kusoma. (Rom. 2:21) Ikiwa una zoea la kusoma kila siku, utachochea sana mioyo ya watoto wako. Bidii yako, hasa katika kusoma Biblia, kutayarisha mikutano, na kuongoza funzo la familia, kutaonyesha wazi kwamba mambo hayo ni ya maana sana.

Hivyo, upendo wako na mfano wako ni mambo ya maana katika kusitawisha ndani ya watoto wako tamaa ya kusoma. Lakini ni hatua gani zinazofaa ambazo unaweza kuchukua ili kuwatia moyo?

Upendo Ambao Unaanza kwa Kusoma

Ni hatua gani za maana ambazo unaweza kuchukua ili usitawishe ndani ya watoto wako tamaa ya kupenda kusoma? Wape vitabu vingi wakiwa wachanga. Mzee mmoja Mkristo ambaye wazazi wake walisitawisha ndani yake tamaa ya kupenda kusoma anapendekeza hivi: “Acha watoto wako wazoee kushika na kutumia vitabu. Kwa njia hiyo, watapenda vitabu na vitakuwa sehemu ya maisha yao.” Hivyo, watoto wengi wanapenda sana kuwa na vitabu vinavyotegemea Biblia, kama vile Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, hata kabla hawajajua kusoma. Unaposoma vitabu hivyo ukiwa pamoja na watoto wako, huwasaidii tu wajifunze lugha bali pia “mambo ya kiroho” na “maneno ya kiroho.”—1 Kor. 2:13.

Soma kwa sauti kwa ukawaida. Sitawisha zoea la kusoma pamoja na watoto wako kila siku. Kufanya hivyo kunawafundisha kutamka maneno kwa usahihi na kunafanya zoea hilo litie mizizi katika maisha yao. Njia yako ya kusoma ni ya maana pia. Soma kwa uchangamfu, nao pia watafanya hivyo. Kwa kweli, huenda ukaona kwamba watoto wako watakuomba usome hadithi hiyo tena na tena. Kubali ombi lao na uwasomee tena hadithi hiyo! Baada ya muda, watataka kuchunguza habari mpya. Lakini uwe mwangalifu ili usiwalazimishe kusoma. Yesu aliweka mfano kwa kuwafundisha wasikilizaji wake ‘kwa kadiri tu walivyoweza kusikiliza.’ (Marko 4:33) Ikiwa huwalazimishi watoto wako kusoma, watangojea kwa hamu kipindi kinachofuata cha kusoma, na itakuwa rahisi kwako kutimiza mradi wako wa kusitawisha ndani yao tamaa ya kupenda kusoma.

Watie moyo washiriki, na mzungumzie mambo mnayosoma. Muda si muda, utafurahi sana kuona watoto wako wachanga wakiwa na uwezo wa kufahamu, kutamka, na kuelewa maana ya maneno mengi. Kuzungumzia mambo mnayosoma kunaweza kuwachochea sana kufanya maendeleo. Mazungumzo yanawasaidia watoto “kujifunza maneno ambayo watahitaji kufahamu na kuelewa wanaposoma,” kinasema kitabu kimoja kinachozungumza kuhusu jinsi ya kuwasaidia watoto kuwa wasomaji wazuri. Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Ili kuwasaidia watoto wachanga ambao akili zao zinazokua zinajifunza kusoma na kuandika, ni jambo la maana kuzungumza nao, na ukizungumzia mambo yenye maana zaidi . . . utapata matokeo bora zaidi.”

Waombe watoto wako wasome huku ukisikiliza, na uwatie moyo waulize maswali. Unaweza kuamua kuuliza maswali na kupendekeza majibu ambayo huenda yakafaa. Ukifanya hivyo, watoto watajifunza kwamba vitabu vina habari nyingi na kwamba maneno ambayo wanasoma yana maana. Njia hiyo inasaidia hasa ikiwa mnasoma habari ambazo zinategemea Neno la Mungu, kitabu chenye maana zaidi kuliko vitabu vyote.—Ebr. 4:12.

Hata hivyo, usisahau kamwe kwamba kusoma kunahitaji ustadi mwingi. Ili mtu awe msomaji mwenye ustadi anahitaji kutumia wakati mwingi na kufanya mazoezi. * Kwa hiyo, hakikisha kwamba unawapongeza sana watoto ili uwachochee waendelee kupenda kusoma. Ukiwapongeza watoto wako utawatia moyo wapende sana kusoma.

Kusoma Ni Jambo Lenye Faida na Linalofurahisha

Kuwafundisha watoto wako jinsi ya kujifunza kunawasaidia waone kwamba kusoma ni jambo la maana. Kujifunza kunatia ndani kuelewa mambo ya hakika na kuona jinsi yanavyohusiana. Kunatia ndani uwezo wa kupanga, kukumbuka, na kutumia habari. Mtoto anapojua jinsi ya kujifunza na kuona thamani ya mambo anayojifunza, anapata faida na kufurahia kujifunza.—Mhu. 10:10.

Wafundishe ustadi mbalimbali wa kujifunza. Jioni za Ibada ya Familia, mazungumzo ya andiko la siku, na pindi nyingine kama hizo zinatoa nafasi nzuri sana za kuwafundisha watoto wako ustadi wa kujifunza. Wakiketi kimya na kukazia habari fulani kwa vipindi vifupi vya wakati watajifunza kukaza fikira, jambo ambalo ni la maana sana katika kujifunza. Zaidi ya hayo, unaweza kumtia moyo mwana wako akuambie jinsi mambo ambayo ametoka kujifunza yanavyohusiana na yale ambayo tayari anajua. Hilo linamfundisha kulinganisha mambo. Namna gani ukimwomba binti yako aeleze kwa ufupi kwa maneno yake mwenyewe habari ambayo amesoma? Kufanya hivyo kutamsaidia aelewe maana ya habari hiyo na kuikumbuka. Kuwafundisha watoto kurudia, yaani, kueleza kwa maneno yao mambo makuu baada ya kusoma habari fulani, ni njia nyingine ya kuwasaidia kukumbuka. Hata watoto wachanga wanaweza kufundishwa kuandika mambo machache wakati wa kujifunza au katika mikutano ya kutaniko. Hilo linaweza kuwasaidia sana kukaza fikira! Mbinu hizo rahisi sana zinafanya kusoma kuwe jambo linalofurahisha na linalokunufaisha wewe na watoto wako.

Fanya kuwe na mazingira mazuri ya kujifunza. Ni rahisi zaidi kukaza fikira mahali penye hewa na mwangaza wa kutosha, na katika hali yenye utulivu na yenye kustarehesha. Bila shaka, maoni ya wazazi kuhusu kujifunza ni ya maana sana. Mama mmoja anasema hivi: “Ni jambo la maana sana kwako kupanga kwa ukawaida wakati wa kusoma na kujifunza. Jambo hilo linawasaidia watoto wako kufanya mambo kwa utaratibu. Wanajifunza kupanga mambo yanayohitaji kutimizwa wakati fulani hususa.” Wazazi wengi wanahakikisha kwamba hakuna jambo lingine linalofanywa wakati wa kujifunza. Kulingana na mtaalamu mmoja, mtazamo huo unasaidia kuwafundisha watoto wawe na mazoea mazuri ya kujifunza.

Kazia thamani ya kujifunza. Mwishowe, wasaidie watoto wako waone faida za kujifunza. Kusudi kuu la kujifunza ni kutumia mambo wanayojifunza. Ndugu mmoja kijana anakubali hivi: “Nisipoona faida yoyote ya jambo ninalojifunza, inakuwa vigumu sana kuwa na hamu ya kutaka kujifunza jambo hilo. Lakini ikiwa ninaweza kutumia jambo hilo katika maisha yangu, ninakuwa na hamu ya kutaka kulielewa.” Vijana wanapoona kwamba kujifunza ni jambo linalowasaidia kufikia kusudi fulani la maana, watajitahidi kabisa kujifunza. Wataanza kutazamia kwa hamu wakati wa kujifunza, kama walivyokuwa wakitazamia wakati wa kusoma.

Thawabu Bora Zaidi

Kuna faida nyingi sana za kusitawisha ndani ya watoto wako tamaa ya kupenda kusoma hivi kwamba faida hizo haziwezi kutoshea katika makala hii moja. Faida hizo zinatia ndani kufanya vizuri shuleni, kazini, katika mahusiano na wanadamu wengine, kuelewa ulimwengu wetu, na kusitawisha mahusiano ya karibu zaidi na yenye upendo kati ya mzazi na mtoto, na pia kupata uradhi unaotokana na kusoma na kujifunza.

Zaidi ya yote, kupenda kujifunza kunaweza kuwasaidia watoto wako wawe watu wanaothamini mambo ya kiroho. Kupenda kujifunza ndio ufunguo ambao unafungua akili na mioyo ili kuelewa “upana na urefu na kimo na kina” cha kweli za Kimaandiko. (Efe. 3:18) Bila shaka, wazazi Wakristo wana mambo mengi ya kuwafundisha watoto wao. Wazazi wanapotumia wakati mwingi na kuwakazia uangalifu watoto wao na kujitahidi kadiri wanavyoweza kuwasaidia kuwa na mwanzo mzuri katika maisha, wanatumaini kwamba mwishowe watoto wao watachagua kuwa waabudu wa Yehova. Unapowafundisha watoto wako mazoea mazuri ya kujifunza unawasaidia kulinda hali yao nzuri ya kiroho na kujenga uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Hivyo basi, kwa kadiri unavyoweza, mwombe Yehova akubariki unapojitahidi kuwachochea watoto wako wapende kusoma na kujifunza.—Met. 22:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kusoma na kujifunza si rahisi kwa watoto ambao wamezaliwa wakiwa na matatizo ya kujifunza. Ili kuona jinsi wazazi wanavyoweza kuwasaidia watoto hao, ona gazeti la Amkeni! la Februari 22, 1997 (22/2/1997), ukurasa wa 3-10.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

Kusoma . . .

• Wape vitabu

• Soma kwa sauti

• Watie moyo washiriki

• Zungumzieni mambo mnayosoma

• Waombe watoto wako wasome huku ukisikiliza

• Watie moyo watoto wako waulize maswali

Kujifunza . . .

• Weka mfano mzuri ukiwa mzazi

• Wafundishe watoto jinsi ya . . .

○ kukaza fikira

○ kulinganisha mambo

○ kueleza habari kwa ufupi

○ kurudia

○ kuandika mambo machache

• Fanya kuwe na mazingira mazuri ya kujifunza

• Kazia thamani ya kujifunza