Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Usiogope. Mimi Mwenyewe Nitakusaidia”

“Usiogope. Mimi Mwenyewe Nitakusaidia”

“Usiogope. Mimi Mwenyewe Nitakusaidia”

YESU aliwaonya mapema wafuasi wake hivi: “Ibilisi ataendelea kuwatupa gerezani baadhi yenu ili mjaribiwe kwa ukamili.” Hata hivyo, kabla ya onyo hilo, Yesu alisema hivi: “Usiogope mateso ambayo yanakaribia kukupata.” Kwa kuwa Shetani anaendelea kutumia vitisho vya kututupa gerezani kama njia ya kusimamisha kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme, uwezekano wa kwamba serikali fulani zitawatesa Wakristo wa kweli ni halisi. (Ufu. 2:10; 12:17) Hivyo, ni nini kitakachotusaidia kujitayarisha kupambana na mbinu za Shetani na ‘kutoogopa,’ kama Yesu alivyohimiza?

Bila shaka, wengi wetu tumewahi kuhisi woga wakati fulani. Hata hivyo, Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba kwa msaada wa Yehova, tunaweza kuepuka kushindwa na woga. Jinsi gani? Njia moja ambayo Yehova anatumia ili kutusaidia kujitayarisha kupambana na upinzani ni kutuonyesha mbinu zinazotumiwa na Shetani na watumishi wake. (2 Kor. 2:11) Ili kuonyesha jambo hilo, acheni tuchunguze tukio moja lililotukia katika nyakati za Biblia. Tutachunguza pia mifano fulani ya wakati wetu ya waamini wenzetu waaminifu ambao ‘walisimama imara kupinga hila za Ibilisi.’—Efe. 6:11-13.

Mfalme Anayemwogopa Mungu Anakabiliana na Mtawala Mwovu

Katika karne ya nane K.W.K., Mfalme mwovu Senakeribu wa Ashuru alipata ushindi kwa mfululizo juu ya mataifa mengi. Akiwa mwenye uhakika sana baada ya ushindi huo, sasa aliazimia kuwashinda watu wa Yehova na mji wao mkuu, Yerusalemu, ambako Hezekia mwenye kumwogopa Mungu alikuwa akitawala akiwa mfalme. (2 Fal. 18:1-3, 13) Bila shaka, Shetani alikuwa akitumia nafasi hiyo kumchochea Senakeribu atimize mipango yake ili kwamba ibada ya kweli ikomeshwe kabisa duniani.—Mwa. 3:15.

Senakeribu alituma wajumbe Yerusalemu ili kuomba jiji hilo lisalimu amri. Rabshake ambaye alikuwa msemaji mkuu wa mfalme, alikuwa kati ya wajumbe hao. * (2 Fal. 18:17) Kusudi la Rabshake lilikuwa kuwavunja moyo Wayahudi na kuwalazimisha wasalimu amri bila kupigana. Rabshake alitumia mbinu gani katika jitihada zake za kuwaogopesha Wayahudi?

Wanabaki Waaminifu Hata Wakiwa Wametengwa

Rabshake aliwaambia wajumbe wa Hezekia hivi: “Mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru, amesema hivi: ‘Ni tumaini gani hili ambalo umelitegemea? . . . Tazama! umeweka tegemeo lako katika usaidizi wa tete hili lililopondeka, Misri, ambalo, mtu akiliegemea, hakika litaingia mkononi mwake na kuuchoma.’” (2 Fal. 18:19, 21) Shtaka la Rabshake lilikuwa la uwongo, kwa sababu Hezekia hakuwa amefanya mapatano na Misri. Hata hivyo, shtaka hilo lilikazia yale ambayo Rabshake alitaka Wayahudi wakumbuke waziwazi: ‘Hakuna mtu atakayekuja kuwasaidia. Mko peke yenu, mmetengwa.’

Katika nyakati za hivi karibuni, wapinzani wa ibada ya kweli walijaribu kuwaogopesha Wakristo wa kweli wakitumia vitisho hivyohivyo vya kuwatenga. Dada mmoja Mkristo, ambaye alifungwa gerezani kwa sababu ya imani yake na hivyo kutengana na waamini wenzake kwa miaka mingi, baadaye alieleza kile kilichomsaidia kutoshindwa na woga. Alisema hivi: “Sala ilinisaidia kumkaribia Yehova . . . Nilikumbuka uhakikisho ulio katika andiko la Isaya 66:2, kwamba Mungu anamtazama mtu ‘anayeteseka na kujuta rohoni.’ Sikuzote uhakikisho huo ulinitia nguvu na kunifariji sana.” Vivyo hivyo, ndugu mmoja ambaye alikaa kwa miaka mingi katika kifungo cha upweke alisema hivi: “Nilikuja kutambua kwamba hata hicho chumba kidogo cha gereza hakingeweza kunizuia kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.” Ndiyo, kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kuliwapa Wakristo hao wawili nguvu walizohitaji ili kuvumilia kifungo chao cha upweke. (Zab. 9:9, 10) Ni kweli kwamba watesaji wao wangewatenganisha na familia zao, marafiki, na waamini wenzao, lakini Mashahidi hao waliofungwa gerezani walijua kwamba wapinzani wao hawangewatenganisha kamwe na Yehova.—Rom. 8:35-39.

Hivyo basi, ni jambo la maana kama nini kwamba tutumie kila nafasi tunayopata kuutia nguvu uhusiano wetu pamoja na Yehova! (Yak. 4:8) Tunapaswa kujiuliza kwa ukawaida hivi: ‘Yehova ni halisi kwangu kadiri gani? Je, maneno yake yana uvutano mkubwa sana juu yangu ninapofanya maamuzi madogo na makubwa, katika maisha yangu ya kila siku?’ (Luka 16:10) Tukijitahidi sana kudumisha uhusiano wetu wa karibu pamoja na Mungu, hatuna sababu ya kuogopa. Nabii Yeremia, akizungumza kwa niaba ya Wayahudi wenye kuteseka, alisema hivi: “Nimeita jina lako, Ee Yehova, kutoka katika shimo la chini kabisa . . . Umekaribia katika siku ile ambayo niliendelea kukuita. Ukasema: ‘Usiogope.’”—Omb. 3:55-57.

Kupanda Mashaka Hakufanikiwi

Rabshake alitumia mawazo ya hila ili kujaribu kupanda mashaka katika akili za watu. Alisema: “Je, [Yehova] siye ambaye mahali pake pa juu na madhabahu zake Hezekia ameondoa? . . . Yehova mwenyewe aliniambia, ‘Nenda juu ya nchi hii, nawe lazima uiharibu.’” (2 Fal. 18:22, 25) Hivyo, Rabshake alidai kwamba Yehova hangewapigania watu Wake kwa sababu hakupendezwa nao. Lakini hiyo haikuwa kweli. Yehova alipendezwa na Hezekia na Wayahudi waliorudi kwenye ibada ya kweli.—2 Fal. 18:3-7.

Leo, huenda watesaji wenye nia mbaya wakasema habari fulani zilizo za kweli wakiwa na kusudi la kutushawishi, lakini wanachanganya kwa werevu habari hizo za kweli na uwongo wakiwa na kusudi la kupanda mashaka. Kwa mfano, nyakati fulani ndugu na dada ambao wamefungwa gerezani wameambiwa kwamba ndugu mmoja ambaye alikuwa akisimamia kazi ya kuhubiri katika nchi yao alikana imani yake na hivyo ni sawa wao pia watende vivyo hivyo na kukana imani yao. Hata hivyo, mawazo hayo hayafanikiwi kutokeza mashaka katika mioyo ya Wakristo walio na utambuzi.

Fikiria jambo lililompata dada mmoja Mkristo wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Akiwa gerezani, alionyeshwa karatasi yenye maandishi yaliyoonyesha kwamba ndugu mmoja aliyekuwa msimamizi alikana imani yake. Ofisa aliyekuwa akimhoji alimuuliza ikiwa ana imani na Shahidi huyo. Dada huyo alijibu hivi: “[Yeye] ni mwanadamu tu asiye mkamilifu.” Dada huyo aliongeza kwamba ndugu huyo alipokuwa akifuata kanuni za Biblia, Mungu alimtumia. “Lakini kwa kuwa maneno yake yanaonyesha kwamba ameacha kufuata Biblia, yeye si ndugu yangu tena.” Dada huyo mwaminifu alifuata kwa busara himizo hili la Biblia: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.”—Zab. 146:3.

Kuwa na ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na kufuata mashauri yake kutatusaidia kujilinda na mawazo ya udanganyifu ambayo yanaweza kudhoofisha azimio letu la kuvumilia. (Efe. 4:13, 14; Ebr. 6:19) Hivyo, ili tujitayarishe kuweza kufikiri sawasawa tunapokuwa chini ya mikazo, tunahitaji kutanguliza usomaji wetu wa Biblia kila siku na funzo la kibinafsi. (Ebr. 4:12) Ndiyo, huu sasa ndio wakati wa kuongeza kabisa ujuzi wetu na kuitia nguvu imani yetu. Ndugu mmoja ambaye alivumilia kifungo cha upweke kwa miaka mingi alisema hivi: “Ningependa kumtia moyo kila mtu aonyeshe uthamini wa kweli kwa ajili ya chakula chote cha kiroho ambacho tunapewa, kwa kuwa hatujui hasa jinsi kitakavyotusaidia sana wakati fulani.” Kwa kweli, ikiwa tunajifunza kwa uangalifu Neno la Mungu na vichapo vya Biblia vinavyotayarishwa na jamii ya mtumwa leo, basi, katika nyakati za taabu maishani, roho takatifu ‘itatukumbusha’ mambo ambayo tumejifunza.—Yoh. 14:26.

Kulindwa Kutokana na Vitisho

Rabshake alijaribu kuwaogopesha Wayahudi. Alisema hivi: “Tafadhali, mpeni dhamana bwana wangu mfalme wa Ashuru, nami niwape farasi elfu mbili tuone ikiwa mnaweza kuweka wapanda-farasi juu yao. Unawezaje, basi, kugeuza nyuma uso wa gavana mmoja wa watumishi wadogo zaidi wa bwana wangu?” (2 Fal. 18:23, 24) Kwa maoni ya wanadamu, lilikuwa jambo lisilowezekana kwa Hezekia na watu wake kupigana na jeshi lenye nguvu sana la Ashuru.

Leo pia, watesaji wanaweza kuonekana kuwa wenye nguvu nyingi sana, hasa wanapoungwa mkono na serikali. Bila shaka, ilikuwa hivyo na watesaji wa Nazi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Walijaribu kuwaogopesha watumishi wengi wa Mungu. Ndugu yetu mmoja, ambaye alifungwa gerezani kwa miaka mingi, alieleza baadaye jinsi alivyotishwa. Pindi moja, ofisa mmoja alimuuliza: “Je, uliona jinsi ndugu yako alivyopigwa risasi? Ulijifunza somo gani kutokana na hilo?” Jibu lake lilikuwa: “Mimi ni shahidi wa Yehova na nitabaki hivyo.” Kisha ofisa huyo akamtisha hivi: “Basi ni zamu yako kupigwa risasi.” Hata hivyo, ndugu yetu alibaki imara, na adui huyo akaacha kumtisha. Ni nini kilichomwezesha kukabiliana na vitisho hivyo? Alijibu hivi: “Niliweka tumaini langu katika jina la Yehova.”—Met. 18:10.

Kwa kuwa na imani kamili katika Yehova, tunakuwa na ngao kubwa inayotulinda na mambo yote ambayo Shetani anatumia ili kutuumiza kiroho. (Efe. 6:16) Hivyo, ni vizuri kumwomba Yehova katika sala ili atusaidie kutia nguvu imani yetu. (Luka 17:5) Pia, tunahitaji kutumia vizuri mipango ya kujenga imani inayoandaliwa na jamii ya mtumwa mwaminifu. Tunapotishwa, tunatiwa nguvu tunapokumbuka uhakikisho ambao Yehova alimpa nabii Ezekieli, ambaye alipaswa kushughulika na watu wakaidi. Yehova alimwambia hivi: “Nimeufanya uso wako uwe mgumu kama nyuso zao na paji la uso wako liwe gumu kama mapaji ya nyuso zao. Nimelifanya paji la uso wako kuwa kama almasi, gumu kuliko jiwe gumu.” (Eze. 3:8, 9) Ikiwa ni lazima, Yehova anaweza kutusaidia kuwa wagumu kama almasi kama Ezekieli alivyopaswa kuwa.

Kushinda Vishawishi

Wapinzani wameona kwamba mbinu zao zote zinaposhindwa, nyakati nyingine zawadi zenye kushawishi zinaweza kuvunja utimilifu wa mtu. Rabshake alitumia pia mbinu hiyo. Aliwaambia hivi wakaaji wa Yerusalemu: “Mfalme wa Ashuru amesema hivi: ‘Salimuni amri kwangu, mtoke nje mje kwangu . . . mpaka nije na kuwachukua ninyi na kwa kweli niwapeleke katika nchi iliyo kama nchi yenu wenyewe, nchi yenye nafaka na divai mpya, nchi yenye mkate na mashamba ya mizabibu, nchi yenye mizeituni ya mafuta na asali; nanyi mwendelee kuishi, msije mkafa.’” (2 Fal. 18:31, 32) Inaelekea kwamba tarajio la kula mkate na kunywa divai mpya liliwavutia sana watu ambao walikuwa wamefungiwa ndani ya jiji lenye kuta lililozingirwa!

Mbinu hiyo ilitumiwa kujaribu kudhoofisha azimio la mmishonari mmoja aliyekuwa amefungwa gerezani. Aliambiwa kwamba atahamishwa na kupelekwa katika “nyumba nzuri” yenye “bustani maridadi” kwa muda wa miezi sita ili aweze kufikiri. Hata hivyo, ndugu huyo alibaki macho kiroho na hakulegeza msimamo wake kwa kuvunja kanuni zake za Kikristo. Ni nini kilichomsaidia? Alisema hivi baadaye: “Niliendelea kutafakari juu ya Ufalme kuwa tumaini halisi. . . . Hawangeweza kunisadikisha kukana imani yangu kwa sababu nilitiwa nguvu na ujuzi kuhusu ufalme wa Mungu, nilikuwa na hakika kuhusu ufalme huo, na sikuwa na shaka hata kidogo.”

Ufalme wa Mungu ni halisi kwetu kadiri gani? Mzee wa ukoo Abrahamu, mtume Paulo, na Yesu mwenyewe, wote waliweza kuvumilia majaribu magumu kwa sababu Ufalme ulikuwa halisi kwao. (Flp. 3:13, 14; Ebr. 11:8-10; 12:2) Tukiendelea kutanguliza Ufalme katika maisha yetu na kukazia fikira baraka zake za milele, sisi pia tunaweza kushinda kishawishi cha kukubali zawadi ili kupata kitulizo cha muda kutokana na majaribu.—2 Kor. 4:16-18.

Yehova Hatatuacha

Ingawa Rabshake alijitahidi sana kuwaogopesha Wayahudi, Hezekia na watu wake walimtegemea Yehova bila kuyumba-yumba. (2 Fal. 19:15, 19; Isa. 37:5-7) Yehova naye kwa upande wake, alijibu sala zao za kuomba msaada kwa kumtuma malaika ili awaue askari-jeshi 185,000 kwa usiku mmoja katika kambi ya Waashuru. Siku iliyofuata, Senakeribu alirudi haraka Ninawi, mji wake mkuu, akiwa na aibu, pamoja na wanajeshi wake wachache waliobaki.—2 Fal. 19:35, 36.

Kwa wazi, Yehova hakuwaacha wale waliomtegemea. Mifano ya siku zetu ya ndugu na dada zetu ambao wanabaki imara chini ya majaribu inaonyesha kwamba Yehova anatenda vivyo hivyo leo. Hivyo basi, Baba yetu wa mbinguni ana sababu nzuri anapotuhakikishia hivi: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isa. 41:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 “Rabshake” lilikuwa jina la cheo la ofisa mashuhuri wa Ashuru. Jina la mwanamume huyo halitajwi katika simulizi hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Zaidi ya mara 30 katika Neno lake, Yehova mwenyewe anawahakikishia watumishi wake hivi: ‘Msiogope’

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mbinu za Rabshake zilifanana jinsi gani na zile zinazotumiwa na maadui wa watu wa Mungu leo?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Uhusiano wa karibu pamoja na Yehova unatuwezesha kudumisha utimilifu wetu chini ya majaribu