Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha “Sheria ya Fadhili Zenye Upendo” Ilinde Ulimi Wako

Acha “Sheria ya Fadhili Zenye Upendo” Ilinde Ulimi Wako

Acha “Sheria ya Fadhili Zenye Upendo” Ilinde Ulimi Wako

“Hufungua kinywa chake kwa hekima, na sheria ya fadhili zenye upendo ziko katika ulimi wake.”—MET. 31:26.

1, 2. (a) Waabudu wa Yehova wanatiwa moyo kusitawisha sifa gani? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika habari hii?

UJUMBE mzito ambao Mfalme Lemueli wa kale alipokea kutoka kwa mama yake ulitia ndani sifa moja ya maana ya mke mwema. Aliambiwa hivi: “Hufungua kinywa chake kwa hekima, na sheria ya fadhili zenye upendo ziko katika ulimi wake.” (Met. 31:1, 10, 26) Fadhili zenye upendo ni sifa yenye kupendeza katika ulimi wa mwanamke mwenye hekima na vilevile kwa watu wengine ambao wanataka kumpendeza Yehova Mungu. (Soma Methali 19:22.) Sifa ya fadhili zenye upendo inapaswa kuonekana wazi katika usemi wa waabudu wote wa kweli.

2 Fadhili zenye upendo ni nini? Ni nani wanaopaswa kuonyeshwa sifa hiyo? Ni nini kitakachotusaidia kuweka “sheria ya fadhili zenye upendo” katika ulimi wetu? Kufanya hivyo kutakuwa na matokeo gani kuelekea mawasiliano yetu na washiriki wa familia zetu na Wakristo wenzetu?

Fadhili Zinapochochewa na Upendo Mshikamanifu

3, 4. (a) Fadhili zenye upendo ni nini? (b) Sifa ya fadhili zenye upendo inatofautiana jinsi gani na fadhili za kawaida, au fadhili za kibinadamu?

3 Sifa ya “fadhili zenye upendo” inatia ndani sifa ya upendo na fadhili. Sifa hiyo inatia ndani fadhili, yaani, kupendezwa kibinafsi na wengine na kuonyesha kwamba unawajali au unawahangaikia kwa kuwasaidia na kwa kuwaambia maneno mazuri. Kwa kuwa upendo unahusika pia, kuonyesha fadhili zenye upendo kunatia ndani kupendezwa na hali nzuri ya wengine kwa sababu tunawapenda. Hata hivyo, neno la lugha ya awali linalotafsiriwa “fadhili zenye upendo” linamaanisha mambo mengi zaidi ya fadhili zinazochochewa na upendo. Fadhili zenye upendo ni fadhili ambazo zinashikamana kwa kupenda na kwa ushikamanifu na mtu fulani mpaka kusudi lake kuhusiana na mtu huyo litimie.

4 Sifa ya fadhili zenye upendo inatofautiana pia na sifa ya fadhili kwa njia nyingine. Fadhili za kawaida, au fadhili za kibinadamu, zinaweza kuonyeshwa hata kwa watu ambao hatuwajui. Mtume Paulo pamoja na watu wengine 275 ambao walivunjikiwa na meli walionyeshwa fadhili kama hizo na wakaaji wa kisiwa cha Malta—watu ambao hawakuwa wamewahi kukutana nao. (Mdo. 27:37–28:2) Kwa upande mwingine, fadhili zenye upendo zinahusisha kushikamana kwa ushikamanifu kati ya watu ambao tayari wamesitawisha uhusiano. * Watu walioitwa Wakeni waliwaonyesha fadhili zenye upendo “wana wote wa Israeli walipokuwa wakipanda kutoka Misri.”—1 Sam. 15:6.

Kutafakari na Kusali Ni Mambo ya Maana

5. Ni nini kitakachotusaidia kuuongoza ulimi wetu?

5 Inaweza kuwa vigumu kwetu kuonyesha fadhili zenye upendo katika usemi wetu. Akizungumza kuhusu ulimi, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Hakuna hata mmoja wa wanadamu anayeweza kuufuga. Huo ni kitu kitundu chenye kudhuru, umejaa sumu yenye kuua.” (Yak. 3:8) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuongoza kiungo hicho cha mwili ambacho ni vigumu sana kukizuia? Maneno ya Yesu kwa viongozi wa kidini katika siku zake yanaweza kutusaidia kuelewa jambo hilo. Alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt. 12:34) Ili fadhili zenye upendo zilinde ulimi wetu, tunahitaji kusitawisha sifa hiyo ndani ya moyo wetu, yaani, mtu wetu wa ndani. Acheni tuone jinsi kutafakari na kusali kunavyoweza kutusaidia kufanya hivyo.

6. Kwa nini tunapaswa kutafakari kwa shukrani kuhusu matendo ya Yehova ya fadhili zenye upendo?

6 Biblia inasema kwamba Yehova Mungu ni “mwingi wa fadhili zenye upendo.” (Kut. 34:6) Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Fadhili zako zenye upendo, Ee Yehova, zimeijaza dunia.” (Zab. 119:64) Maandiko yana masimulizi mengi yanayoonyesha jinsi Yehova alivyowaonyesha waabudu wake fadhili zenye upendo. Kutenga wakati ili kutafakari kuhusu ‘matendo ya Yehova’ tukiwa wenye shukrani kunaweza kusitawisha ndani yetu tamaa ya kukuza sifa hiyo ya kimungu.—Soma Zaburi 77:12.

7, 8. (a) Yehova alitenda tendo gani la fadhili zenye upendo kuelekea Loti na familia yake? (b) Daudi alihisi jinsi gani kwa sababu ya kuonyeshwa fadhili zenye upendo na Mungu?

7 Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyomwokoa Loti, mpwa wa Abrahamu, pamoja familia yake Alipoharibu Sodoma, jiji ambako waliishi. Wakati huo ulipozidi kukaribia, malaika waliokuwa wamekuja kwa Loti walimhimiza achukue familia yake na kuondoka haraka katika jiji hilo. Biblia inasema: “Alipoendelea kukawia, ndipo kwa huruma za Yehova kwake, wale [malaika] wakaushika mkono wake na mkono wa mke wake na mikono ya binti zake wawili. Wakamtoa nje na kumweka nje ya jiji.” Je, hatuguswi moyo tunapotafakari kuhusu tendo hilo la kuokoa, na je, hatuchochewi kukubali kwamba huo ulikuwa wonyesho wa fadhili zenye upendo za Mungu?—Mwa. 19:16, 19.

8 Fikiria pia mfano wa Mfalme Daudi wa Israeli la kale ambaye aliimba hivi: “[Yehova] anayesamehe makosa yako yote, [ndiye] anayeponya magonjwa yako yote.” Daudi alithamini kama nini kuonyeshwa msamaha kwa sababu ya dhambi yake na Bath-sheba! Alimtukuza Yehova kwa kusema hivi: “Kama mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo fadhili zake zenye upendo zilivyo kuu kuwaelekea wale wanaomwogopa.” (Zab. 103:3, 11) Kutafakari kuhusu masimulizi hayo na mengine katika Maandiko kunafanya mioyo yetu ijae shukrani kwa sababu ya fadhili zenye upendo za Yehova, na tunachochewa kumsifu na kumshukuru. Kadiri tunavyozidi kuwa na shukrani moyoni, ndivyo tunavyozidi kuwa na mwelekeo wa kumwiga Mungu wa kweli.—Efe. 5:1.

9. Ni sababu gani nzuri sana inayowachochea waabudu wa Yehova kuonyesha fadhili zenye upendo katika maisha yao ya kila siku?

9 Mifano mbalimbali katika Maandiko inafunua kwamba Yehova anawaonyesha fadhili zenye upendo, yaani, upendo wake mshikamanifu wale ambao tayari wana msimamo wenye kukubalika mbele zake. Namna gani wale ambao hawana uhusiano kama huo pamoja na Mungu aliye hai? Je, Yehova ni mkali kuwaelekea au hawatendei kwa fadhili? Hapana. “[Mungu] ni mwenye fadhili kuwaelekea wasio na shukrani na waovu,” linasema andiko la Luka 6:35. “Yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mt. 5:45) Kabla hatujajifunza kweli na kuanza kutenda kulingana na kweli hiyo, Mungu alikuwa akitutendea kwa fadhili, au kutuonyesha fadhili za kawaida. Hata hivyo, tukiwa waabudu wake tunafaidika na upendo wake mshikamanifu, yaani, fadhili zake zenye upendo ambazo hazibadiliki. (Soma Isaya 54:10.) Tunashukuru kama nini kwa sababu ya hilo! Na hiyo ni sababu nzuri kama nini ya kuonyesha fadhili zenye upendo katika usemi wetu na vilevile katika shughuli nyingine za maisha yetu ya kila siku!

10. Kwa nini sala ni msaada wenye thamani sana katika kufanya fadhili zenye upendo ziwe sehemu ya utu wetu?

10 Msaada mwingine wenye thamani sana unaotusaidia kusitawisha sifa ya fadhili zenye upendo ni pendeleo la sala. Hii ni kwa sababu upendo na fadhili —sifa zinazofanyiza fadhili zenye upendo—ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Yehova. (Gal. 5:22) Tunaweza kusitawisha fadhili zenye upendo ndani ya mioyo yetu kwa kujiruhusu tuongozwe na roho hiyo. Njia ya moja kwa moja ya kupokea roho takatifu ya Yehova ni kuomba katika sala tupewe roho hiyo. (Luka 11:13) Ni jambo linalofaa kwamba tusali tena na tena ili tupate roho ya Mungu na tukubali kuongozwa nayo. Ndiyo, kutafakari na kusali ni mambo ya maana ikiwa tunataka sheria ya fadhili zenye upendo iwe katika ulimi wetu.

Fadhili Zenye Upendo Katika Ulimi wa Wenzi wa Ndoa

11. (a) Tunajua jinsi gani kwamba Yehova anatazamia waume wawaonyeshe wake zao fadhili zenye upendo? (b) Ni kwa njia gani sheria ya fadhili zenye upendo inaweza kumsaidia mume aulinde ulimi wake?

11 Mtume Paulo anawahimiza waume hivi: “Endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Efe. 5:25) Paulo pia anawakumbusha maneno ambayo Yehova aliwaambia Adamu na Hawa. Mtume huyo anaandika hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.” (Efe. 5:31) Ni wazi kwamba Yehova anatazamia waume washikamane kwa ushikamanifu na wake zao, na wawaonyeshe fadhili zenye upendo sikuzote. Mume ambaye ulimi wake unaongozwa na upendo mshikamanifu hafunui hadharani makosa ya mke wake, au kuzungumza kumhusu kwa njia inayomvunjia heshima. Anafurahia kumsifu. (Met. 31:28) Ikiwa kwa sababu fulani matatizo yanatokea katika uhusiano wao, fadhili zenye upendo zinamchochea mume auzuie ulimi wake ili asimfedheheshe mke wake.

12. Usemi wa mke unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba sheria ya fadhili zenye upendo inaongoza ulimi wake?

12 Sheria ya fadhili zenye upendo inapaswa pia kuongoza ulimi wa mke. Usemi wake haupaswi kuongozwa na roho ya ulimwengu. Kwa kuwa ‘anamheshimu sana mume wake,’ anasema mambo mazuri kumhusu hadharani na hivyo kuongeza heshima ambayo huenda wengine tayari wanayo kumwelekea mume wake. (Efe. 5:33) Ili asipunguze heshima ambayo watoto wanayo kumwelekea baba yao, anaepuka kutokubaliana naye au kupinga maoni yake mbele ya watoto. Anatatua mambo kama hayo faraghani. Biblia inasema: “Mwanamke mwenye hekima kwelikweli amejenga nyumba yake.” (Met. 14:1) Nyumba yake ni mahali penye kupendeza na kustarehesha kwa familia nzima.

13. Ni wapi hasa ambapo sheria ya fadhili zenye upendo inapaswa kutawala, na inaweza kufanya hivyo jinsi gani?

13 Hata wakiwa faraghani katika nyumba zao, ni lazima wenzi wa ndoa waendelee kuutumia ulimi wao katika njia inayoonyesha kwamba wanaheshimiana. Paulo aliandika hivi: “Yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu.” Aliongezea hivi: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. . . . Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:8, 12-14) Ikiwa watoto wamezoea kuwasikia wazazi wao wakiongea kwa njia ya upendo na yenye fadhili nyumbani, watakuwa na furaha na vilevile inaelekea kwamba wataiga njia hiyo ya kuzungumza ya wazazi wao.

14. Vichwa vya familia wanaweza kutumia jinsi gani ulimi wao ili kuwafariji wale walio chini ya utunzaji wao?

14 Mtunga-zaburi aliandika hivi kumhusu Yehova: “Tafadhali, fadhili zako zenye upendo na zinifariji.” (Zab. 119:76) Njia kuu zaidi ambayo Yehova anawafariji watu wake ni kwa kuwahimiza na kuwapa mwongozo. (Zab. 119:105) Vichwa vya familia wanaweza kufaidika jinsi gani na mfano wa Baba yetu wa mbinguni na hivyo kuutumia ulimi wao kuwafariji wale walio chini ya utunzaji wao? Wanaweza kufanya hivyo kwa kuwatia moyo na kuwapa mwongozo unaohitajiwa. Jioni ya Ibada ya Familia ni nafasi nzuri kama nini ya kupata hazina za kiroho!—Met. 24:4.

Waonyeshe Waabudu Wenzako Upendo Mshikamanifu

15. Wazee na washiriki wengine wa kutaniko walio wakomavu wanaweza kuutumia jinsi gani ulimi wao kuwalinda wengine kutanikoni?

15 Mfalme Daudi alisali hivi: “Fadhili zako zenye upendo na ukweli wako zinilinde daima.” (Zab. 40:11) Wazee Wakristo na washiriki wengine wa kutaniko walio wakomavu wanaweza jinsi gani kumwiga Yehova katika jambo hilo? Bila shaka, kuutumia ulimi wetu kuelekeza uangalifu kwa habari ya Kimaandiko ni tendo la fadhili zenye upendo.—Met. 17:17.

16, 17. Tunaweza kuonyesha katika njia gani mbalimbali kwamba usemi wetu unaongozwa na sheria ya fadhili zenye upendo?

16 Tunapaswa kufanya nini tukiona Mkristo fulani akielekea kufanya jambo ambalo linapingana na kanuni za Biblia? Je, fadhili zenye upendo hazitatusukuma kuutumia ulimi wetu ili kujaribu kumrekebisha? (Zab. 141:5) Ikiwa tunajua kwamba mwabudu mwenzetu ametenda dhambi nzito, upendo mshikamanifu utatusukuma tumtie moyo mkosaji huyo “awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko” ili “wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova.” (Yak. 5:14) Ikiwa mkosaji huyo anakataa kuzungumza na wazee, hatutakuwa tukionyesha upendo wala fadhili kwa kutowajulisha wazee jambo hilo. Wengine kati yetu wanaweza kukata tamaa, kuhisi upweke, kusumbuliwa na hisia za kwamba hawafai, au kulemewa na mambo yanayovunja moyo. Njia nzuri ambayo tunaweza kuonyesha kwamba sheria ya fadhili zenye upendo iko katika ulimi wetu ni ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’—1 The. 5:14.

17 Tunapaswa kutenda jinsi gani wakati uvumi au habari za uwongo kuhusu waabudu wenzetu zinaposambazwa na maadui wa Mungu? Badala ya kuanza kutilia shaka utimilifu wa ndugu zetu, tunapaswa kukataa mazungumzo hayo bila kusema lolote au ikiwa mshtaki huyo ana usawaziko, tunaweza kumuuliza kama kweli ana uhakika kwamba mambo anayosema ni ya kweli. Ikiwa maadui wa watu wa Mungu wanawatafuta ndugu zetu Wakristo ili wawaumize, upendo mshikamanifu kwa ajili ya ndugu zetu utatuzuia kutoa habari kuwahusu.—Met. 18:24.

Mwanamume Mwenye “Fadhili Zenye Upendo Atapata Uzima”

18, 19. Kwa nini sheria ya fadhili zenye upendo haipaswi kuondoka kwenye ulimi wetu tunaposhughulika na waabudu wenzetu?

18 Tunapaswa kuonyesha upendo mshikamanifu katika mambo yote tunaposhughulika na waabudu wenzetu wa Yehova. Hata tunapokabiliana na hali ngumu, sheria ya fadhili zenye upendo haipaswi kuondoka kwenye ulimi wetu. Yehova alikasirika wakati fadhili zenye upendo za wana wa Israeli zilipokuwa “kama umande ambao hutoweka mapema.” (Hos. 6:4, 6) Kwa upande mwingine, Yehova anafurahi wakati tunapokuwa na zoea la kuonyesha fadhili zenye upendo kwa ukawaida. Hebu ona jinsi anavyowabariki wale wanaofuatilia fadhili zenye upendo.

19 Andiko la Methali 21:21 linasema hivi: “Anayefuatilia uadilifu na fadhili zenye upendo atapata uzima, uadilifu na utukufu.” Kati ya baraka ambazo mtu huyo atafurahia ni kwamba atapata uzima—si kwa kipindi kifupi tu lakini atapata uzima usio na mwisho. Yehova anamsaidia ‘kushika imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:12, 19) Hivyo basi, acheni tujitahidi kabisa kuendelea ‘kutendeana kwa fadhili zenye upendo na rehema.’—Zek. 7:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi fadhili zenye upendo zinavyotofautiana na ushikamanifu, upendo, na fadhili, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2002 (15/5/2002), ukurasa wa 12-13, 18-19.

Je, Unaweza Kueleza?

• Unaweza kueleza jinsi gani maana ya fadhili zenye upendo?

• Ni nini kitakachotusaidia kuwa na sheria ya fadhili zenye upendo katika ulimi wetu?

• Wenzi wa ndoa wanaweza kuonyesha jinsi gani upendo mshikamanifu katika usemi wao?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba sheria ya fadhili zenye upendo iko katika ulimi wetu tunaposhughulika na waamini wenzetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Daudi alitukuza fadhili zenye upendo za Yehova

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, mnakuwa na jioni ya Ibada ya Familia kwa ukawaida?