Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Fidia Inavyotuokoa

Jinsi Fidia Inavyotuokoa

Jinsi Fidia Inavyotuokoa

“Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu hukaa juu yake.”—YOH. 3:36.

1, 2. Gazeti Zion’s Watch Tower lilichapishwa kwa mara ya kwanza kwa sababu gani moja?

“IKIWA mtu anajifunza Biblia kwa uangalifu hawezi kukosa kutambua umuhimu wa kifo cha Kristo,” likasema toleo la nne la gazeti hili mnamo Oktoba 1879. Habari hiyo ilimalizia kwa maneno haya mazito: “Acheni tujihadhari na jambo lolote linalodharau, au kupuuza kwamba kifo cha Kristo ni toleo na upatanisho kwa ajili ya dhambi.”—Soma 1 Yohana 2:1, 2.

2 Sababu moja iliyofanya gazeti Zion’s Watch Tower lichapishwe kwa mara ya kwanza mnamo Julai (Mwezi wa 7) mwaka wa 1879 ilikuwa kutetea fundisho la Biblia la fidia au dhabihu ya ukombozi. Kurasa za gazeti hilo ziliandaa ‘chakula kwa wakati unaofaa,’ kwa kuwa mwishoni mwa miaka ya 1800, watu wengi waliodai kuwa Wakristo walianza kuwa na shaka kwamba kifo cha Yesu kingeweza kuwa fidia kwa ajili ya dhambi zetu. (Mt. 24:45) Wakati huo, wengi walianza kuamini fundisho la mageuzi ambalo linapingana na ukweli wa kwamba mwanadamu alipoteza hali ya ukamilifu. Wanamageuzi wanafundisha kwamba hali ya mwanadamu inaendelea kuwa bora zaidi na hivyo mwanadamu hahitaji fidia. Hivyo basi, shauri hili la mtume Paulo kwa Timotheo linafaa sana: “Linda lililowekwa amana kwako, ukigeuka mbali kutoka kwenye maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu na kutoka kwenye maneno yanayopingana ya ule unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi.’ Kwa maana kwa kujisifia ujuzi wa namna hiyo wengine wamegeuka kutoka kwenye imani.”—1 Tim. 6:20, 21.

3. Sasa tutachunguza maswali gani?

3 Bila shaka umeazimia ‘kutogeuka kutoka kwenye imani.’ Kwa sababu hiyo, itakuwa vizuri kuchunguza maswali au maulizo haya: Kwa nini ninahitaji fidia? Fidia iligharimu nini? Ninaweza kufaidika jinsi gani na uandalizi huo wenye thamani ambao unaweza kuniokoa kutokana na ghadhabu au hasira kali ya Mungu?

Kuokolewa Kutokana na Ghadhabu ya Mungu

4, 5. Ni nini kinachothibitisha kwamba ghadhabu ya Mungu inakaa juu ya mfumo huu mwovu wa mambo?

4 Biblia na mambo hakika ya historia yanaonyesha kwamba tangu Adamu atende dhambi, ghadhabu ya Mungu ‘imekaa juu ya’ jamii ya wanadamu. (Yoh. 3:36) Hilo linaonekana wazi kwa kuwa hakuna mwanadamu ambaye amewahi kuepuka kifo. Utawala wa mpinzani Shetani umeshindwa kabisa kuwalinda wanadamu kutokana na misiba inayoendelea, na hakuna serikali ya kibinadamu ambayo imeweza kuwatimizia raia wake wote mahitaji ya msingi. (1 Yoh. 5:19) Hivyo, wanadamu wanaendelea kuteseka kutokana na vita, uhalifu, na umaskini.

5 Hivyo basi, ni wazi kwamba mfumo huu mwovu wa mambo hauna baraka za Yehova. Paulo alisema kwamba “ghadhabu ya Mungu inafunuliwa kutoka mbinguni juu ya watu wote wasiomwogopa Mungu.” (Rom. 1:18-20) Kwa hiyo, wale wanaoishi maisha yasiyompendeza Mungu bila kutubu hawataepuka matokeo mabaya ya mwenendo wao. Leo, ghadhabu ya Mungu inajulishwa kupitia ujumbe wa hukumu ambao unamwagwa kama mapigo juu ya ulimwengu wa Shetani, na ujumbe huo unatolewa katika vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia.—Ufu. 16:1.

6, 7. Wakristo watiwa-mafuta wanaongoza katika kazi gani, na ni nafasi gani ambayo bado iko wazi kwa watu walio sehemu ya ulimwengu wa Shetani?

6 Je, hilo linamaanisha kwamba watu wamechelewa mno kuachana kabisa na utawala wa Shetani ili wakubaliwe na Mungu? Hapana, kwa sababu mlango unaoongoza katika hali ya kupatanishwa na Yehova bado ungali wazi kabisa. Wakristo watiwa-mafuta, ambao ni “mabalozi walio badala ya Kristo,” wanaongoza katika huduma ya hadharani ambayo kupitia hiyo watu wa mataifa yote wanasihiwa: “Mpatanishwe pamoja na Mungu.”—2 Kor. 5:20, 21.

7 Mtume Paulo alisema kwamba Yesu ‘anatukomboa sisi kutoka kwenye ghadhabu inayokuja.’ (1 The. 1:10) Wonyesho huo wa mwisho wa hasira ya Yehova utasababisha uharibifu wa milele kwa watenda-dhambi wasiotubu. (2 The. 1:6-9) Ni nani atakayeokoka? Biblia inasema hivi: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu hukaa juu yake.” (Yoh. 3:36) Ndiyo, mfumo huu unapofikia mwisho wake, wote walio hai ambao wanamwamini Yesu na fidia, hawataharibiwa katika siku ya mwisho ya ghadhabu ya Mungu.

Jinsi Fidia Inavyofanya Kazi

8. (a) Adamu na Hawa walikuwa na tumaini gani kubwa mbele yao? (b) Yehova alithibitisha jinsi gani kwamba yeye ni Mungu wa haki kamilifu?

8 Adamu na Hawa waliumbwa wakiwa wakamilifu. Ikiwa wangeendelea kumtii Mungu, dunia ingekuwa sasa imejaa wazao wao wenye furaha wakiishi pamoja nao katika Paradiso. Hata hivyo, inasikitisha kwamba wazazi wetu wa kwanza walivunja kimakusudi amri ya Mungu. Kwa sababu hiyo, walihukumiwa kifo cha milele na wakafukuzwa kutoka katika Paradiso ya kwanza. Kufikia wakati Adamu na Hawa walipopata watoto, wanadamu walikuwa wamerithi dhambi, na mwishowe mwanamume na mwanamke wa kwanza wakazeeka na kufa. Hilo linathibitisha kwamba sikuzote Yehova anatimiza neno lake. Zaidi ya hayo, yeye ni Mungu wa haki kamilifu. Yehova alimwonya Adamu kwamba akila tunda lililokatazwa atakufa, na ndivyo ilivyokuwa.

9, 10. (a) Kwa nini wazao wa Adamu wanakufa? (b) Tunaweza kuepuka kifo cha milele jinsi gani?

9 Tukiwa wazao wa Adamu, tumerithi mwili usio mkamilifu ambao una mwelekeo wa kutenda dhambi na mwishowe unakufa. Adamu alipotenda dhambi, ni kana kwamba bado tulikuwa katika viuno vyake. Kwa hiyo, hukumu ya dhambi ilituhusu sisi pia. Ikiwa Yehova angeondoa kifo bila kulipwa fidia, angeonekana kuwa mwongo. Kwa kweli, Paulo aliongea kwa niaba yetu sote aliposema hivi: “Tunajua kwamba Sheria ni ya kiroho; lakini mimi ni wa kimwili, nimeuzwa chini ya dhambi. Maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?”—Rom. 7:14, 24.

10 Ni Yehova Mungu peke yake angeweza kuweka msingi wa kisheria ambao angetumia kusamehe dhambi zetu kwa njia ya haki na kutuweka huru kutokana na hukumu ya kifo cha milele. Alifanya hivyo kwa kumtuma Mwana wake mpendwa kutoka mbinguni ili azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu, ambaye angeweza kutoa uhai wake kuwa fidia kwa ajili yetu. Tofauti na Adamu, Yesu alibaki mkamilifu. Kwa kweli, “yeye hakufanya dhambi.” (1 Pet. 2:22) Hivyo, Yesu alikuwa na uwezo wa kuzaa jamii ya wanadamu wakamilifu. Hata hivyo, badala ya kufanya hivyo, aliwaruhusu maadui wa Mungu wamuue ili aweze kuwanunua wazao wenye dhambi wa Adamu na hivyo kuwawezesha wale ambao wanamwamini wapate uzima wa milele. Maandiko yanasema hivi: “Kuna Mungu mmoja, na mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu, mwanadamu, Kristo Yesu, aliyejitoa kuwa fidia inayolingana kwa ajili ya wote.”—1 Tim. 2:5, 6.

11. (a) Tunaweza kulinganisha faida za fidia na nini? (b) Ni nani ambao watafaidika pia na fidia?

11 Tunaweza kulinganisha jinsi fidia inavyofanya kazi na hali ya watu ambao wameibiwa pesa zao zote na benki yenye ufisadi na hivyo kubaki na madeni. Kwa kufaa, wenye benki hiyo wanahukumiwa kifungo cha miaka mingi gerezani. Lakini namna gani watu wasio na hatia ambao waliweka pesa zao katika benki hiyo? Baada ya kuachwa wakiwa maskini, hawana lingine la kufanya kuhusu hali yao isipokuwa tu mtu fulani tajiri mwenye fadhili anunue benki hiyo na kuwarudishia watu hao pesa zao zote, na kuwalipia madeni yao. Vivyo hivyo, Yehova Mungu na Mwana wake mpendwa wamewanunua wazao wa Adamu na kufuta deni lao la dhambi kwa msingi wa damu ya Yesu iliyomwagwa. Ndiyo sababu Yohana Mbatizaji alisema hivi kumhusu Yesu: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” (Yoh. 1:29) Ulimwengu wa wanadamu ambao dhambi zao zimeondolewa unatia ndani si wale tu walio hai bali pia wale waliokufa.

Fidia Iligharimu Nini?

12, 13. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Abrahamu alivyokuwa tayari kumtoa Isaka?

12 Hatuwezi kuelewa kabisa jinsi fidia ilivyomgharimu Baba yetu wa mbinguni na Mwana wake mpendwa. Lakini Biblia ina masimulizi ambayo yanaweza kutusaidia kutafakari juu ya jambo hilo. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo huenda Abrahamu alihisi alipokuwa akisafiri kwa siku tatu kwenda Moria ili atii amri hii ya Mungu: “Tafadhali, mchukue mwana wako, mwana wako wa pekee unayempenda sana, Isaka, ufunge safari kwenda nchi ya Moria na huko umtoe kama toleo la kuteketezwa juu ya mmoja kati ya milima ambao nitakuonyesha.”—Mwa. 22:2-4.

13 Mwishowe Abrahamu alifika mahali alipoambiwa. Fikiria jinsi Abrahamu alivyohuzunika sana alipomfunga Isaka mikono na miguu na kumlaza juu ya madhabahu ambayo Abrahamu mwenyewe alikuwa amejenga. Abrahamu aliumia kama nini moyoni alipoinua kisu ambacho angetumia kumuua mwana wake! Fikiria jinsi Isaka alivyohisi alipolala juu ya madhabahu, akingoja kisu kimkate kwa uchungu mkali sana na kumuua. Malaika wa Yehova alimzuia Abrahamu kwa wakati unaofaa kabisa. Yale ambayo Abrahamu na Isaka walifanya katika pindi hiyo yanatusaidia kuelewa jinsi Yehova alivyohisi alipowaruhusu watumishi wa Shetani wamuue Mwana Wake. Namna Isaka alivyoshirikiana na Abrahamu ilionyesha vizuri jinsi Yesu alivyokuwa tayari kuteseka na kufa kwa ajili yetu.—Ebr. 11:17-19.

14. Ni jambo gani lililotukia katika maisha ya Yakobo ambalo linatusaidia kuthamini gharama ya fidia?

14 Gharama ya fidia inaweza pia kufananishwa na jambo fulani lililotukia katika maisha ya Yakobo. Kati ya watoto wake wote, Yakobo alimpenda Yosefu zaidi. Inasikitisha kwamba ndugu za Yosefu walimwonea wivu na walimchukia. Hata hivyo, Yosefu alikuwa tayari kutumwa na baba yake ili kuona ndugu zake walikuwa katika hali gani. Wakati huo, walikuwa wakichunga kundi la Yakobo umbali wa kilomita 100 upande wa kaskazini wa nyumbani kwao huko Hebroni. Fikiria jinsi Yakobo alivyohisi watoto wake waliporudi na nguo ya Yosefu iliyojaa damu! Yakobo alilia hivi: “Ni vazi la mwanangu! Mnyama-mwitu mkali amemrarua! Hakika Yosefu ameraruliwa vipande-vipande!” Yote hayo yalimfanya Yakobo aumie sana moyoni, akamwombolezea Yosefu kwa siku nyingi. (Mwa. 37:33, 34) Yehova hatendi kama wanadamu wasio wakamilifu wanavyotenda hali fulani inapotokea. Hata hivyo, kutafakari juu ya jambo hilo lililotukia katika maisha ya Yakobo kunaweza kutusaidia kuelewa, kwa kadiri fulani, jinsi Mungu alivyohisi wakati Mwana wake mpendwa alipoteswa na kuuawa kikatili akiwa mwanadamu duniani.

Jinsi Tunavyofaidika Kutokana na Fidia

15, 16. (a) Yehova alionyesha jinsi gani kwamba aliikubali fidia? (b) Umefaidika jinsi gani kutokana na fidia?

15 Yehova Mungu alimfufua Mwana wake mwaminifu akiwa na mwili wa roho wenye utukufu. (1 Pet. 3:18) Kwa muda wa siku 40, Yesu aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake, akatia nguvu imani yao na kuwatayarisha kwa ajili ya kazi kubwa ya kuhubiri habari njema iliyokuwa mbele yao. Kisha akapanda mbinguni. Akiwa huko alimtolea Mungu thamani ya damu yake iliyomwagwa ili itumiwe kwa faida ya wafuasi wake wa kweli, ambao wanaamini thamani ya dhabihu yake ya fidia au ukombozi. Yehova Mungu alionyesha kwamba ameikubali fidia ya Kristo kwa kumpa Yesu uwezo wa kumwaga roho takatifu juu ya wanafunzi wake ambao walikusanyika pamoja huko Yerusalemu siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K.—Mdo. 2:33.

16 Wafuasi hao watiwa-mafuta wa Kristo walianza papo hapo kuwahimiza wanadamu wenzao waepuke ghadhabu ya Mungu kwa kubatizwa katika jina la Yesu Kristo ili wasamehewe dhambi zao. (Soma Matendo 2:38-40.) Kuanzia siku hiyo ya kihistoria mpaka sasa, mamilioni ya watu kutoka katika mataifa yote wameingizwa katika uhusiano pamoja na Mungu kwa msingi wa imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yoh. 6:44) Kufikia hapa katika mazungumzo yetu, tunahitaji kuchunguza maswali mawili zaidi: Je, kuna yeyote kati yetu ambaye amepewa tumaini la uzima wa milele kwa sababu ya matendo yake mazuri? Baada ya kupata tumaini hilo zuri ajabu, je, tunaweza kulipoteza?

17. Unapaswa kuwa na maoni gani kuhusu baraka nzuri ajabu ya kuwa rafiki ya Mungu?

17 Fidia ni zawadi isiyostahiliwa kabisa. Lakini kwa kuonyesha imani katika fidia, mamilioni ya watu leo wamekuja kuwa marafiki wa Mungu, wakiwa na tumaini la kupata uzima wa milele katika paradiso duniani. Hata hivyo, kuwa marafiki wa Yehova si uhakikisho wa kwamba tutaendelea kuwa na uhusiano huo pamoja naye. Ili tuepuke siku ya Mungu inayokuja ya ghadhabu, ni lazima tuendelee kuonyesha kwamba tunathamini sana “fidia iliyolipwa na Kristo Yesu.”—Rom. 3:24; soma Wafilipi 2:12.

Endelea Kuonyesha Imani Katika Fidia

18. Kuonyesha imani katika fidia kunatia ndani nini?

18 Andiko la msingi la habari hii, Yohana 3:36, linaonyesha kwamba kumwamini Bwana Yesu Kristo kunatia ndani kumtii yeye. Kuithamini fidia kunapaswa kutuchochea kuishi kulingana na mafundisho ya Yesu, kutia ndani mambo aliyofundisha kuhusu maadili. (Marko 7:21-23) “Ghadhabu ya Mungu inakuja” juu ya wote ambao wanafanya bila kutubu matendo kama vile uasherati, mizaha michafu, na “ukosefu wa usafi wa kila namna,” ambao unatia ndani zoea la kutazama ponografia (picha au habari za ngono).—Efe. 5:3-6.

19. Ni katika njia gani nzuri tunaweza kuonyesha imani yetu katika fidia?

19 Uthamini wetu kwa ajili ya fidia unapaswa kutufanya tuwe na mengi ya kutimiza kuhusiana na “vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (2 Pet. 3:11) Basi na tutenge wakati wa kutosha wa kusali kwa bidii na kwa ukawaida, kujifunza Biblia kibinafsi, kuhudhuria mikutano, kuwa na ibada ya familia, na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Na acheni ‘tusisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.’—Ebr. 13:15, 16.

20. Wote wanaoendelea kuonyesha imani katika fidia wanaweza kutazamia baraka gani wakati ujao?

20 Ghadhabu ya Yehova inapouangukia mfumo huu mwovu wa mambo, tutafurahi kama nini kwamba tulionyesha imani katika fidia na kuendelea kuithamini! Na katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa, tutashukuru milele kwa ajili ya maandalizi hayo mazuri ajabu ambayo yalituokoa kutokana na ghadhabu ya Mungu.—Soma Yohana 3:16; Ufunuo 7:9, 10, 13, 14.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunahitaji fidia?

• Fidia iligharimu nini?

• Ni faida gani zinazotokana na fidia?

• Tunaonyesha imani katika fidia ya Yesu jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mlango unaoongoza katika hali ya kupatanishwa na Yehova bado ungali wazi kabisa

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kutafakari juu ya matukio haya yanayohusu Abrahamu, Isaka, na Yakobo kunaweza kutusaidia kuthamini gharama kubwa iliyolipwa kwa ajili ya fidia