Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Unapaswa Kufika kwa Wakati?

Kwa Nini Unapaswa Kufika kwa Wakati?

Kwa Nini Unapaswa Kufika kwa Wakati?

SI RAHISI kufika kwa wakati sikuzote. Huenda tukahitaji kukabiliana na matatizo kama vile kusafiri mbali sana, msongamano mkubwa wa magari, na ratiba zenye shughuli nyingi. Hata hivyo, kufika kwa wakati ni jambo la maana. Kwa mfano, kwa ujumla mtu anayefika kazini kwa wakati anaonwa kuwa mtu mwenye kutegemeka na mwenye bidii. Kwa upande mwingine, mtu ambaye anafika akiwa amechelewa anaweza kuvuruga kazi za wengine na kupunguza ubora wa kazi au huduma. Mwanafunzi anayechelewa anaweza kukosa vipindi fulani vya masomo na hilo linaweza kumzuia kufanya vizuri shuleni. Kuchelewa kufika kumwona daktari wa kitiba au wa meno kunaweza kufanya upokee matibabu yasiyofaa.

Hata hivyo, katika sehemu fulani, watu hawaoni kufika kwa wakati kuwa jambo la maana sana. Katika mazingira hayo, ni rahisi sana kuwa na zoea la kuchelewa. Ikiwa ndivyo ilivyo, ni jambo la maana kwamba tusitawishe tamaa ya kufika kwa wakati. Tukithamini umuhimu wa kufika kwa wakati, bila shaka hilo litatusaidia kutochelewa. Tuna sababu gani za kufika kwa wakati? Tunaweza kufanya nini ili tufike kwa wakati? Na ni faida gani tunazoweza kupata tukifika kwa wakati?

Yehova Ni Mungu Anayefuata Wakati

Sababu kuu zaidi ambayo inatufanya tusiwe na zoea la kuchelewa ni kwamba tunataka kumwiga Mungu tunayemwabudu. (Efe. 5:1) Yehova anaweka mfano bora kabisa katika kufuata wakati. Hachelewi kamwe. Anafuata kikamili ratiba yake ili atimize makusudi yake. Kwa mfano, Yehova alipoamua kuuharibu ulimwengu usiomwogopa Mungu kwa gharika, alimwambia Noa hivi: “Jifanyie safina ya mti wenye utomvu.” Mwisho ulipokuwa ukikaribia Yehova alimwambia Noa aingie ndani ya safina na kumweleza hivi: “Baada ya siku 7 nitanyesha mvua duniani siku 40 mchana na usiku; nami nitafutilia mbali kutoka uso wa nchi kila kitu kilichoko ambacho nimekifanya.” Kisha, kwa wakati unaofaa kabisa, “siku saba baadaye maji ya gharika yakaja juu ya dunia.” (Mwa. 6:14; 7:4, 10) Wazia jambo ambalo huenda lingetokea ikiwa Noa na familia yake wangechelewa kuingia ndani ya safina. Walihitaji kufuata wakati, kama Mungu waliyemwabudu alivyofuata wakati.

Miaka 450 hivi baada ya Gharika, Yehova alimwambia mzee wa ukoo Abrahamu kwamba angepata mwana ambaye kupitia kwake Uzao ulioahidiwa ungetokea. (Mwa. 17:15-17) Mungu alisema kwamba Isaka angezaliwa “wakati huu uliowekwa mwaka ujao.” Je, ndivyo ilivyotukia? Maandiko yanatuambia hivi: “Sara akapata mimba, kisha akamzalia Abrahamu mwana katika umri wake wa uzee kwa wakati uliowekwa ambao Mungu alikuwa amemwambia.”—Mwa. 17:21; 21:2.

Biblia ina mifano mingi inayoonyesha kwamba Mungu anafuata wakati. (Yer. 25:11-13; Dan. 4:20-25; 9:25) Biblia inatuambia tuendelee kungojea siku ya Yehova inayokuja ya hukumu. Hata ingawa wanadamu wanaona kwamba ‘inakawia,’ tunahakikishiwa kwamba ‘haitachelewa.’—Hab. 2:3.

Kufuata Wakati Ni Jambo la Maana Katika Ibada

Wanaume wote Waisraeli walipaswa kufika kwa wakati mahali palipochaguliwa kwa ajili ya “sherehe za majira za Yehova.” (Law. 23:2, 4) Pia, Mungu aliweka nyakati ambazo dhabihu fulani zilipaswa kutolewa. (Kut. 29:38, 39; Law. 23:37, 38) Je, hilo halionyeshi kwamba Mungu anataka watumishi wake wafuate wakati katika ibada yao?

Katika karne ya kwanza mtume Paulo alipowapa Wakorintho maagizo kuhusu jinsi mikutano ya Kikristo inavyopaswa kuongozwa, aliwahimiza hivi: “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Kwa hiyo, mikutano ya Wakristo ya ibada ilipaswa kuanza kwa wakati uliowekwa. Maoni ya Yehova kuhusu kufuata wakati hayajabadilika. (Mal. 3:6) Basi, tunaweza kuchukua hatua gani ili tufike kwa wakati kwenye mikutano hiyo ya Kikristo?

Yale Tunayoweza Kufanya ili Tufike kwa Wakati

Watu fulani wameona kwamba kufanya matayarisho mapema kunasaidia sana. (Met. 21:5) Kwa mfano, ikiwa tunahitaji kusafiri umbali fulani ili tufike kwa wakati fulani uliowekwa, je, lingekuwa jambo la hekima kutenga wakati wa kutosha tu kusafiri na kufika huko kwa wakati kamili? Je, halingekuwa jambo la busara kuhakikisha kwamba tuna dakika za ziada ili tusichelewe, hata tukipatwa na “tukio lisilotazamiwa” njiani? (Mhu. 9:11) “Jambo ambalo linaweza kumsaidia mtu yeyote afike kwa wakati ni kujua vizuri muda wa kusafiri ambao anahitaji,” anasema mwanamume mmoja kijana anayeitwa José. *

Huenda watu fulani wakahitaji kufanya mipango inayofaa ili kuondoka kazini mapema vya kutosha na hivyo kufika kwenye mikutano ya Kikristo kwa wakati mzuri. Hivyo ndivyo alivyofanya Shahidi mmoja huko Ethiopia alipotambua kwamba angechelewa kufika mikutanoni kwa dakika 45 kwa sababu ya mabadiliko ya zamu kazini. Alipanga ili mfanyakazi mwenzake aje mapema kazini na hivyo kumwezesha kuondoka siku za mikutano. Halafu, Shahidi huyo alikubali kumfanyia kazi mfanyakazi huyo mwenzake katika zamu ya ziada kwa muda wa saa saba.

Ikiwa tuna watoto wachanga, ni vigumu zaidi kufika kwa wakati kwenye mikutano. Kwa kawaida, mama ndiye anayeachiwa daraka la kuwatayarisha watoto, lakini washiriki wengine wa familia wanaweza na wanapaswa kumsaidia. Mama mmoja anayeitwa Esperanza huko Mexico amelea watoto wanane akiwa peke yake. Sasa, watoto hao wana umri wa kati ya miaka 5 na 23. Esperanza anaeleza jambo ambalo wanafanya wakiwa familia ili wafike kwa wakati: “Mabinti wangu wakubwa wananisaidia kuwatayarisha watoto wadogo. Hivyo ninapata nafasi ya kumaliza kazi yangu ya nyumbani na kujitayarisha kwenda kwenye mikutano kwa wakati tulioweka.” Familia hiyo imeweka wakati wa kuondoka nyumbani, na kila mtu anasaidia kazi ili waondoke kwa wakati huo.

Faida za Kufuata Wakati Katika Ibada Yako

Kutafakari kuhusu baraka ambazo tunapata tunapofika kwenye mikutano ya Kikristo kwa wakati kunaweza kuimarisha tamaa na azimio letu la kufanya yote tunayoweza ili tusichelewe. Mwanamke kijana anayeitwa Sandra, ambaye amesitawisha zoea la kufika kwenye mikutano kwa wakati mzuri, anasema hivi: “Ninachofurahia kuhusu kufika mapema ni kwamba ninapata nafasi ya kuwasalimu ndugu na dada, kuongea nao, na kuwafahamu vizuri zaidi.” Tunapofika mapema kwenye Jumba la Ufalme, tunaweza kufaidika kwa kusikia kuhusu uvumilivu na utumishi wa uaminifu wa wengine ambao wamehudhuria. Tunapohudhuria mikutano na kuzungumza nao mambo yenye kujenga, tunaweza kuwatia moyo ndugu na dada zetu na ‘kuwachochea katika upendo na matendo mazuri.’—Ebr. 10:24, 25.

Wimbo na sala ya kufungua kila mkutano wa Kikristo ni sehemu ya maana sana ya ibada yetu. (Zab. 149:1) Nyimbo zetu zinamsifu Yehova, na kutukumbusha sifa ambazo tunapaswa kusitawisha, na zinatutia moyo kushiriki kwa shangwe katika huduma. Namna gani sala ya kufungua? Katika nyakati za kale, Yehova aliliita hekalu ‘nyumba yake ya sala.’ (Isa. 56:7) Leo, tunakusanyika ili kusali kwa Mungu katika mikutano yetu. Sala ya kufungua inamwomba Yehova atuongoze na kutupatia roho takatifu na pia inatayarisha akili na mioyo yetu kupokea habari ambazo zitazungumziwa. Tunapaswa kuazimia kufika kwenye mikutano yetu kwa wakati ili tushiriki wimbo na sala ya kufungua.

Helen, mwenye umri wa miaka 23 anasema hivi kuhusu sababu zinazomfanya afike mapema mikutanoni: “Ninafikiri kwamba ni njia ya kumwonyesha Yehova upendo wangu, kwa kuwa anaandaa habari zote ambazo zinatolewa mikutanoni, kutia ndani na nyimbo na sala ya kufungua.” Je, hatupaswi kuona jambo hilo kwa njia hiyohiyo? Ndiyo, tunapaswa. Kwa hiyo, acheni tujitahidi kusitawisha zoea la kufuata wakati katika utendaji wetu wote, hasa ule unaohusu ibada yetu ya Mungu wa kweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Jitayarisheni mapema vya kutosha

[Picha katika ukurasa wa 26]

Acha wakati kwa ajili ya “tukio lisilotazamiwa”

[Picha katika ukurasa wa 26]

Pata faida za kufika mapema kwenye mikutano