Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Yesu alimwambia mwanamke aliyejulikana kuwa mtenda-dhambi kwamba dhambi zake zimesamehewa?—Luka 7:37, 48.

Yesu alipokuwa ameketi kwenye mlo katika nyumba ya Farisayo anayeitwa Simoni, mwanamke fulani ‘alikaa miguuni pa Yesu.’ Alilowesha miguu ya Yesu kwa machozi na kuifuta kwa nywele za kichwa chake. Kisha, akaibusu miguu yake kwa wororo na kuipaka mafuta yenye marashi. Simulizi hilo la Injili linasema kwamba mwanamke huyo ‘alijulikana jijini kuwa mtenda-dhambi.’ Bila shaka, kila mwanadamu asiye mkamilifu ni mtenda-dhambi, lakini kwa kawaida Maandiko yanatumia neno hilo kumhusu mtu ambaye dhambi zake ni mbaya sana au ambaye anajulikana kuwa mtenda-dhambi. Inaelekea kwamba mwanamke huyo alikuwa kahaba. Ni kwa mtu wa aina hiyo Yesu alisema hivi: “Dhambi zako zimesamehewa.” (Luka 7:36-38, 48) Yesu alimaanisha nini aliposema hivyo? Kwa kuwa dhabihu ya fidia au ukombozi bado haikuwa imetolewa, msamaha huo ungewezekana jinsi gani?

Baada ya mwanamke huyo kuisafisha miguu ya Yesu na kuipaka mafuta lakini kabla ya Yesu kumsamehe, Yesu alitumia mfano kumweleza jambo fulani la maana Simoni, ambaye alikuwa amemwalika. Akilinganisha dhambi na deni kubwa sana ambalo haliwezi kulipwa, Yesu alimwambia hivi Simoni: “Watu wawili walikuwa na deni kwa mkopeshaji fulani; mmoja alikuwa na deni la dinari 500, lakini yule mwingine la 50. Walipokuwa hawana kitu cha kulipa, aliwasamehe kwa hiari wote wawili. Kwa hiyo, ni nani kati yao atampenda zaidi?” Simoni akajibu akasema: “Nadhani ni yule ambaye alimsamehe kwa hiari zilizo nyingi zaidi.” Yesu akamjibu hivi: “Umeamua kwa usahihi.” (Luka 7:41-43) Sisi sote tuna deni la kumtii Mungu, kwa hiyo tunapokosa kumtii na kutenda dhambi, tunakosa kumlipa Mungu deni lake. Kwa hiyo, deni letu linaongezeka. Hata hivyo, Yehova ni kama mkopeshaji ambaye yuko tayari kusamehe madeni. Ndiyo sababu Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wasali kwa Mungu na kumwomba hivi: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mt. 6:12) Andiko la Luka 11:4 linafunua kwamba madeni hayo ni dhambi.

Mungu alisamehe dhambi kwa msingi gani nyakati zilizopita? Kulingana na haki yake kamilifu adhabu ya dhambi ni kifo. Hivyo, Adamu alilipia dhambi yake kwa uhai wake. Hata hivyo, chini ya Sheria ambayo Mungu alipatia taifa la Israeli, mtenda-dhambi angeweza kusamehewa dhambi zake kwa kumtolea Yehova dhabihu ya mnyama. Mtume Paulo alisema hivi: “Karibu vitu vyote husafishwa kwa damu kulingana na Sheria, na damu isipomwagwa hakuna msamaha unaotokea.” (Ebr. 9:22) Wayahudi walijua kwamba hiyo ndiyo njia pekee ambayo wangeweza kupata msamaha kutoka kwa Mungu. Kwa hiyo, haishangazi kwamba katika siku za Yesu watu waliokuwa wakitazama walipinga jambo ambalo alimwambia mwanamke huyo. Wale walioketi mezani pamoja na Yesu walisema hivi mioyoni mwao: “Ni nani mtu huyu ambaye hata husamehe dhambi?” (Luka 7:49) Basi, dhambi nyingi za mwanamke huyo zingeweza kusamehewa kwa msingi gani?

Unabii wa kwanza kabisa uliotangazwa baada ya wenzi wawili wa kwanza wanadamu kuasi ulitaja kusudi la Yehova la kutokeza “uzao” ambao ungetiwa jeraha kwenye kisigino na Shetani na “uzao” wake. (Mwa. 3:15) Uzao huo ulitiwa jeraha wakati Yesu alipouawa na maadui wa Mungu. (Gal. 3:13, 16) Damu ya Kristo iliyomwagwa ni fidia au dhabihu ya ukombozi ambayo inawaweka huru wanadamu kutoka katika dhambi na kifo. Kwa kuwa hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yehova asitimize kusudi lake, mara tu maneno ya Mwanzo 3:15 yaliposemwa, kwa maoni ya Mungu ni kana kwamba fidia hiyo ilikuwa tayari imelipwa. Sasa angeweza kuwasamehe wale walioonyesha kwamba wana imani katika ahadi zake.

Kabla ya nyakati za Ukristo, Yehova aliwahesabu watu fulani kuwa waadilifu. Watu hao walitia ndani Enoko, Noa, Abrahamu, Rahabu, na Ayubu. Kwa imani, walitazamia kutimizwa kwa ahadi za Mungu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova, na ikahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu.” Yakobo alisema hivi kumhusu Rahabu: “Vivyo hivyo, je, Rahabu yule kahaba hakutangazwa pia kuwa mwadilifu kwa matendo.”—Yak. 2:21-25.

Mfalme Daudi wa Israeli la kale alitenda dhambi mbalimbali nzito, lakini alikuwa na imani yenye nguvu katika Mungu wa kweli na kila mara alionyesha toba ya kweli. Zaidi ya hayo, Maandiko yanasema hivi: “Mungu alimweka [Yesu] kuwa toleo la kupatanisha kupitia imani katika damu yake. Ilikuwa hivyo ili kuonyesha wazi uadilifu wake mwenyewe, kwa sababu alikuwa akizisamehe dhambi zilizotokea wakati uliopita wakati Mungu alipokuwa akivumilia kwa subira; ili kuonyesha wazi uadilifu wake mwenyewe katika majira haya yaliyopo, ili awe mwadilifu hata anapomtangaza kuwa mwadilifu mtu aliye na imani katika Yesu.” (Rom. 3:25, 26) Kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu ambayo ingetolewa wakati ujao, Yehova angeweza kusamehe dhambi za Daudi bila kulegeza matakwa Yake mwenyewe ya haki.

Inaonekana kwamba hali ya mwanamke ambaye alipaka mafuta miguu ya Yesu ilikuwa kama ya Daudi. Mwanzoni, aliishi maisha mapotovu kiadili, lakini alikuwa ametubu. Alitambua kwamba alihitaji kukombolewa kutoka katika dhambi na akaonyesha kwa matendo yake kwamba alimthamini kikweli mtu ambaye Yehova alimtumia kutoa ukombozi huo. Hata ingawa dhabihu hiyo bado haikuwa imetolewa, ilikuwa hakika sana hivi kwamba thamani yake ingeweza kutumiwa wakati huo kwa ajili ya watu kama mwanamke huyo. Hivyo, Yesu alimwambia hivi: “Dhambi zako zimesamehewa.”

Kama simulizi hilo linavyoonyesha waziwazi, Yesu hakuwaepuka watenda-dhambi. Aliwatendea mema. Vivyo hivyo, Yehova yuko tayari kuwasamehe watenda-dhambi wanaotubu. Huo ni uhakikisho mzuri ajabu ambao unatuchangamsha moyo kama nini tukiwa wanadamu wasio wakamilifu!

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ilihesabiwa kwao kuwa ni uadilifu