Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usikubali Kushinikizwa Kufuata Maoni ya Watu Wengi

Usikubali Kushinikizwa Kufuata Maoni ya Watu Wengi

Usikubali Kushinikizwa Kufuata Maoni ya Watu Wengi

MAONI kuhusu mambo yanayofaa na yasiyofaa, mambo ya kusifika au ya kulaumika yanatofautiana kila mahali. Pia, yanabadilika baada ya muda kupita. Kwa hiyo, tunaposoma masimulizi ya Maandiko kuhusu mambo yaliyotukia zamani, tunahitaji kufikiria maoni ya watu wengi na viwango vilivyofuatwa nyakati za Biblia badala ya kuweka viwango vyetu wenyewe kuhusu mambo tunayosoma.

Kwa mfano, fikiria mambo mawili yanayotajwa tena na tena katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yaani, heshima na aibu. Ili kuelewa vizuri zaidi maandiko ambayo yanazungumza kuhusu heshima na aibu, tunapaswa kufikiria jinsi watu walioishi wakati huo walivyoyaona mambo hayo.

Viwango Katika Karne ya Kwanza

Msomi mmoja anasema hivi: “Wagiriki, Waroma, na Wayudea, wote waliona heshima na aibu kuwa mambo ya maana sana katika tamaduni zao. Wanaume waliishi na kufa wakitafuta heshima, sifa, umashuhuri, staha na kutambuliwa na watu.” Kwa kuwa waliongozwa na viwango hivyo ilikuwa rahisi kwao kufuata maoni ya wengine.

Cheo, umaarufu, na heshima ni mambo yaliyothaminiwa zaidi katika jamii kwa sababu watu walikazia sana cheo, kuanzia umashuhuri mpaka utumwa. Heshima haikutegemea tu jinsi mtu alivyojiona bali pia jinsi wengine walivyomwona. Kumheshimu mtu kulimaanisha kukiri waziwazi kwamba alijiendesha kwa njia ambayo watu walitazamia. Kumheshimu mtu kulimaanisha pia kuonyesha waziwazi kwamba unavutiwa na utajiri, cheo, au umaarufu wake na hivyo kumtendea kwa njia anayostahili. Mtu angeweza kuheshimiwa kwa kutenda mambo mema au kwa kuwashinda wengine. Kwa upande mwingine, mtu aliyefedheheshwa au kudhihakiwa mbele ya watu wote aliaibika au kukosa heshima. Mtu hakukosa heshima kwa sababu tu ya hisia zake mwenyewe au dhamiri yake, bali kwa sababu alishutumiwa na jamii.

Yesu aliposema kuhusu mtu kuketi “mahali penye kuonekana zaidi” au “mahali pa chini zaidi” kwenye karamu, alijua kwamba hilo lilikuwa jambo la heshima au la aibu kulingana na utamaduni wa wakati huo. (Luka 14:8-10) Katika angalau pindi mbili, wanafunzi wa Yesu walibishana kuhusu “ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote.” (Luka 9:46; 22:24) Walionyesha jambo ambalo liliwahangaisha sana watu wengi katika jamii. Wakati huo, viongozi wa kidini Wayahudi wenye kiburi na mashindano waliona kwamba mahubiri ya Yesu yalidharau heshima yao na mamlaka yao. Hata hivyo, sikuzote jitihada zao za kumshinda Yesu katika mazungumzo mbele ya umati wa watu, hazikufanikiwa.—Luka 13:11-17.

Katika karne ya kwanza, Wayahudi, Wagiriki, na Waroma walikuwa pia na maoni ya kwamba lilikuwa jambo la aibu “kushikwa na kushtakiwa mbele ya watu wengi kwa sababu ya kosa.” Pia, lilikuwa jambo la aibu sana kwa mtu kufungwa. Mtu aliyetendewa hivyo aliaibika mbele ya marafiki, familia, na watu kwa ujumla, iwe alikuwa na hatia ya kutenda uhalifu au hapana. Sifa mbaya aliyopata baadaye ingeweza kumfanya akose kabisa kujiheshimu na kuharibu uhusiano wake na wengine. Aibu ya kuvuliwa nguo au kupigwa viboko ilikuwa mbaya zaidi kuliko aibu ya kufungwa. Mtu aliyetendewa hivyo alidharauliwa na kudhihakiwa, na hivyo alipoteza heshima yake.

Tendo la aibu zaidi kuliko yote lilikuwa kuuawa juu ya mti wa mateso. Msomi Martin Hengel anasema kwamba “watumwa ndio waliopata adhabu hiyo. Hivyo, mtu aliyepata adhabu hiyo alifedheheka, aliteseka, na kupata aibu kubwa sana.” Familia na marafiki wake walishinikizwa na jamii kumkana mtu ambaye alipoteza heshima yake kwa njia hiyo. Kwa kuwa Kristo alikufa kwa njia hiyo, watu wote ambao walitaka kuwa Wakristo katika karne ya kwanza W.K. walilazimika kukubali hali ngumu ya kudhihakiwa na watu wote. Inaelekea kwamba watu wengi waliona kwamba ni jambo la kipumbavu kwa mtu yeyote yule kujitambulisha kuwa mfuasi wa mwanamume ambaye alitundikwa juu ya mti. Mtume Paulo aliandika hivi: “Sisi tunamhubiri Kristo aliyetundikwa mtini, kwa Wayahudi ni sababu ya kujikwaa lakini kwa mataifa ni upumbavu.” (1 Kor. 1:23) Wakristo wa karne ya kwanza walikabiliana jinsi gani na hali hiyo?

Viwango Tofauti

Wakristo wa karne ya kwanza walitii sheria na walijitahidi kuepuka kuaibishwa kwa sababu ya mwenendo mbaya. Mtume Petro aliandika hivi: “Yeyote kati yenu asiteseke kwa sababu yeye ni muuaji au mwizi au mtenda-maovu au mwenye kujiingiza katika mambo ya watu wengine.” (1 Pet. 4:15) Hata hivyo, Yesu alitabiri kwamba wafuasi wake wangeteswa kwa ajili ya jina lake. (Yoh. 15:20) Petro aliandika hivi: “[Mtu] akiteseka kwa sababu yeye ni Mkristo, asione aibu, bali na aendelee kumtukuza Mungu.” (1 Pet. 4:16) Mtu kutoona aibu alipoteseka akiwa mfuasi wa Kristo kulimaanisha kukataa kabisa maoni yaliyofuatwa na watu wengi siku hizo.

Wakristo hawangeweza kuruhusu viwango vya watu wengine viongoze mwenendo wao. Watu walioishi katika karne ya kwanza waliona kwamba ni upumbavu kumwona mtu aliyetundikwa mtini kuwa Masihi. Maoni hayo yangeweza kuwashinikiza Wakristo kufuata njia ya kufikiri iliyokubaliwa na wengi. Hata hivyo, walipaswa kumfuata Yesu hata wajapodhihakiwa kwa kuwa waliamini kwamba yeye ndiye Masihi. Yesu alisema hivi: “Mtu yeyote yule anayenionea aibu mimi na maneno yangu katika kizazi hiki chenye uzinzi na chenye dhambi, Mwana wa binadamu atamwonea aibu yeye pia atakapofika katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.”—Marko 8:38.

Leo, huenda tukapata mikazo inayokusudiwa kutufanya tuache Ukristo. Tunaweza kupata mikazo hiyo kutoka kwa wanafunzi wenzetu, majirani, au wafanyakazi wenzetu ambao wanajaribu kutushawishi tushiriki katika matendo mapotovu yasiyopatana na maadili, mambo yasiyo manyoofu, au mambo mengine yasiyofaa. Watu kama hao wanaweza kujaribu kutufanya tuonee aibu msimamo wetu wa kufuata kanuni zinazofaa. Tunapaswa kutenda namna gani?

Waige Wale Ambao Walidharau Aibu

Ili kudumisha utimilifu wake kwa Yehova, Yesu aliuawa kwa njia isiyo yenye heshima hata kidogo. “Alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu.” (Ebr. 12:2) Maadui wa Yesu walimpiga makofi, wakamtemea mate, wakamvua nguo, wakampiga viboko, wakamtundika mtini, na kumtukana. (Marko 14:65; 15:29-32) Hata hivyo, Yesu alidharau aibu ambayo walijaribu kumletea mbele ya wengine. Jinsi gani? Alikataa kulegeza msimamo wake hata alipotendewa mambo hayo. Yesu alijua kwamba bado alikuwa mwenye kuheshimika machoni pa Yehova, na bila shaka hakutafuta utukufu wa wanadamu. Hata ingawa Yesu alikufa kama mtumwa, Yehova alimheshimu kwa kumfufua na kumpa cheo chenye heshima zaidi kando Yake. Tunasoma hivi kwenye andiko la Wafilipi 2:8-11: “[Kristo Yesu] alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso. Kwa sababu hii pia Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Yesu alihisi uchungu moyoni kwa sababu ya aibu iliyosababishwa na kuuawa kwake. Yesu, Mwana wa Mungu, aliposhtakiwa kwamba amekufuru, alihangaishwa sana na aibu ambayo huenda shtaka hilo lingemletea Baba yake. Yesu alimwomba Yehova amwondolee aibu hiyo. Alisali hivi: “Niondolee kikombe hiki.” Lakini Yesu alijitiisha chini ya mapenzi ya Mungu. (Marko 14:36) Hata hivyo, Yesu alivumilia mikazo aliyokabili na kudharau aibu hiyo. Kwa kweli, wale ambao wangeona aibu ni wale tu ambao walikubali kikamili viwango vilivyofuatwa na watu siku hizo. Ni wazi kwamba Yesu hakukubali viwango hivyo.

Wanafunzi wa Yesu walikamatwa pia na kupigwa viboko. Kwa sababu ya kutendewa hivyo, hawakuheshimiwa na watu wengi. Walidharauliwa na kupuuzwa. Hata hivyo, hilo halikuwavunja moyo. Wanafunzi wa kweli hawakukubali kushinikizwa kufuata maoni ya watu wengi na walidharau aibu. (Mt. 10:17; Mdo. 5:40; 2 Kor. 11:23-25) Walijua kwamba walipaswa ‘kuuchukua mti wao wa mateso siku baada ya siku na kumfuata Yesu sikuzote.’—Luka 9:23, 26.

Namna gani sisi leo? Vitu ambavyo ulimwengu unaona kuwa vipumbavu, dhaifu, na vinavyodharauliwa, Mungu anaviona kuwa vitu vyenye hekima, vyenye nguvu, na vyenye kuheshimika. (1 Kor. 1:25-28) Je, halingekuwa jambo la kipumbavu na lisilo la hekima kwetu kufuata maoni ya watu wengi katika kila jambo?

Ni lazima mtu yeyote anayetamani kuheshimiwa afikirie kwa uzito maoni ya ulimwengu kumhusu. Kwa upande mwingine, kama Yesu na wafuasi wake katika karne ya kwanza, tunatamani Yehova awe Rafiki yetu. Kwa hiyo, tutaheshimu mambo ambayo anaona kuwa yenye kuheshimika na kuona mambo anayoyaona kuwa ya aibu kama yeye anavyoyaona.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Yesu hakufuata maoni ya ulimwengu kuhusu mambo ya kuonea aibu