Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kampeni ya Pekee Nchini Bulgaria Yafanikiwa

Kampeni ya Pekee Nchini Bulgaria Yafanikiwa

Kampeni ya Pekee Nchini Bulgaria Yafanikiwa

“Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.”—MT. 9:37, 38.

MANENO hayo ya Yesu yanafaa kabisa nchi ya Bulgaria, nchi maridadi ya Balkani iliyo kusini-mashariki mwa Ulaya! Kuna uhitaji mkubwa wa wafanyakazi zaidi wa kuwahubiria habari njema wakaaji zaidi ya milioni saba wa nchi hiyo. Kuna wahubiri 1,700 hivi nchini Bulgaria, lakini hawawezi kuhubiri eneo hilo lote. Hivyo basi, Baraza Linaloongoza lilikubali Mashahidi kutoka nchi mbalimbali za Ulaya wanaozungumza Kibulgaria waje na kushiriki katika kampeni ya pekee mwaka wa 2009. Kampeni hiyo ilipangwa kufanywa kwa majuma saba wakati wa majira ya joto, na ingekwisha wakati wa Kusanyiko la Wilaya la “Endeleeni Kukesha!” ambalo lilifanywa huko Sofia, Agosti 14-16, 2009 (14-16/8/2009).

Wengi Waunga Mkono

Akina ndugu katika ofisi ya tawi huko Sofia hawakujua ni wahubiri wangapi ambao wangekubali mwaliko huo kutoka Hispania, Italia, Poland, Ufaransa, Ugiriki, na Ujerumani. Hilo lingemaanisha kwamba wangesafiri kuja Bulgaria kwa gharama yao wenyewe na kutumia muda wao wa likizo wakihubiri. Lilikuwa jambo lenye kuchangamsha moyo sana kuona idadi ya wahubiri waliokuwa wakiomba kuja ikiongezeka juma baada ya juma, mpaka ilipofikia 292! Kwa sababu ya itikio hilo kubwa, wajitoleaji hao wangeweza kutumwa katika majiji matatu mbalimbali nchini Bulgaria: Kazanlak, Sandanski, na Silistra. Waangalizi wa mzunguko nchini Bulgaria waliwaalika mapainia wenyeji na wahubiri waunge mkono pia kampeni hiyo. Mwishowe, wajitoleaji 382 walikuwa wakihubiri kwa bidii katika maeneo ambayo hayakuwa yamehubiriwa habari njema kwa ukawaida.

Akina ndugu kutoka katika makutaniko ya karibu walitumwa mapema ili wawatafutie mahali pa kuishi. Walikodi nyumba za kuishi na wakahifadhi vyumba vya hoteli vya bei ya chini. Ndugu hao wenyeji walifanya kazi kwa bidii ili kuwasaidia wajitoleaji waliokuwa wakiwasili kupata mahali pa kuishi na kisha wakashughulikia mahitaji yao. Katika majiji yote matatu, walikodi mahali pa kufanyia mikutano. Mipango ilifanywa ili mikutano ya kutaniko iongozwe na ndugu waliotoka nchi nyingine. Ilisisimua kama nini kuona wahubiri 50 wakikutana ili kumsifu Yehova katika maeneo ambayo hakuna hata Shahidi mmoja anayeishi huko.

Wahubiri waliokuja kutoka nchi nyingine kwa ajili ya kampeni hiyo walikuwa na bidii nyingi sana. Wakati wa majira ya joto, kiwango cha joto nchini Bulgaria kinaweza kupita digrii 40 Selsiasi. Ingawa hivyo, hakuna jambo ambalo lingewazuia ndugu na dada hao wenye bidii. Silistra, jiji lililo kando ya Mto Danube ambalo lina wakaaji zaidi ya 50,000, lilipata ushahidi kamili kwa majuma matatu ya kwanza. Vivyo hivyo, akina ndugu waliendelea na bidii hiyohiyo na wakafika kwenye vijiji vilivyo karibu, hata walifika Tutrakan, kijiji kilicho kilomita 55 magharibi ya Silistra. Kwa kawaida walianza kuhubiri saa tatu na nusu asubuhi. Baada ya kupumzika kwa ajili ya chakula cha mchana, mara nyingi waliendelea mpaka saa moja jioni au hata usiku. Vivyo hivyo, kwa sababu ya bidii nyingi ya wajitoleaji hao, kampeni huko Kazanlak na Sandanski ilifanywa mpaka kwenye vijiji na majiji yaliyo karibu.

Ni Nini Kilichotimizwa?

Ushahidi mkubwa ulitolewa katika majuma hayo saba. Kama ilivyosemwa wakati wa mitume, wakaaji wa majiji hayo wangesema hivi: ‘Mmejaza majiji yetu na fundisho lenu.’ (Mdo. 5:28) Mashahidi walioshiriki waliwaachia watu magazeti 50,000 hivi na wakaanzisha mafunzo 482 ya Biblia. Jambo la kufurahisha ni kwamba kufikia Septemba 1, 2009, kutaniko lilianzishwa huko Silistra, na kuna vikundi huko Kazanlak na Sandanski. Inachangamsha moyo kuona watu ambao walisikia habari njema kwa mara ya kwanza wakati wa kampeni hiyo wakifanya maendeleo mazuri ya kiroho.

Katika juma la kwanza la kampeni hiyo, dada mmoja ambaye ni painia wa pekee kutoka Hispania na ambaye anazungumza Kibulgaria alimhubiria Karina, mwanamke fulani huko Silistra ambaye alikuwa akiuza magazeti barabarani. Karina alipendezwa na akahudhuria mkutano mmoja. Alikubali funzo la Biblia bila kusitasita. Mume wake anaamini kwamba hakuna Mungu, kwa hiyo Karina aliomba wajifunzie Biblia katika bustani. Binti zake wawili walishiriki katika funzo hilo la Biblia. Binti yake mkubwa anayeitwa Daniela, alithamini sana kweli za Biblia. Alisoma kitabu Biblia Inafundisha kwa muda wa juma moja na mara moja akafuata yale ambayo Biblia inasema kuhusu kutotumia mifano katika ibada. Kisha akaanza kuwaambia marafiki wake kweli hizo. Majuma matatu tu baada ya kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa mara ya kwanza, alimwambia hivi dada aliyekuwa akijifunza naye: “Ninahisi ni kana kwamba mimi ni mmoja wenu. Ninapaswa kufanya nini ili mimi pia nianze kuhubiri?” Daniela anaendelea kufanya maendeleo mazuri pamoja na mama yake na dada yake mdogo.

Huko Kazanlak, ndugu mmoja Mbulgaria anayeitwa Orlin, ambaye alikuja kwa ajili ya kampeni hiyo kutoka Italia, alikuwa akitembea baada ya utumishi wa shambani kurudi mahali alipokuwa akiishi. Akiwa njiani, Orlin aliwahubiria wanaume wawili vijana ambao walikuwa wameketi kwenye kiti katika bustani. Aliwaachia kitabu Biblia Inafundisha na akapanga kuwatembelea tena siku iliyofuata. Siku iliyofuata, Orlin alianzisha funzo la Biblia pamoja na Svetomir na walijifunza tena siku iliyofuata. Kwa muda wa siku tisa, Orlin alijifunza na Svetomir mara nane. Svetomir alisema hivi: “Siku mbili kabla ya kukutana na wewe, nilikuwa nimesali kwa Mungu ili anisaidie kumjua. Na nilimwahidi kwamba kama angenisaidia, ningeweka wakfu maisha yangu kwake.” Baada ya Orlin kurudi Italia, ndugu wenyeji waliendelea kujifunza na Svetomir, na anafanya kweli iwe mali yake.

Wale Waliojidhabihu Walipata Baraka Nyingi

Wale ambao walitumia muda wao wa likizo bila uchoyo na kusafiri kwa gharama yao wenyewe kwenda katika nchi nyingine ili kuhubiri habari njema wanahisi namna gani? Mzee mmoja anayetumika huko Hispania aliandika hivi: “Kampeni hiyo ilifanya ndugu wanaotumika katika eneo la watu wanaozungumza Kibulgaria nchini Hispania wawe na uhusiano wa karibu zaidi. Kampeni hiyo ilikuwa na matokeo makubwa juu ya ndugu walioshiriki.” Wenzi wawili wa ndoa kutoka Italia waliandika hivi: “Huo ndio uliokuwa mwezi wenye shangwe zaidi katika maisha yetu!” Waliongezea hivi: “Kampeni hiyo ilibadili maisha yetu! Sasa sisi ni watu tofauti.” Wenzi hao walianza kufikiria kwa uzito uwezekano wa kuhamia Bulgaria na kuishi huko ili watumike katika eneo ambalo lina uhitaji mkubwa zaidi. Carina ni dada mseja ambaye ni painia wa kawaida kutoka Hispania na aliunga mkono kampeni ya kuhubiri huko Silistra. Baada ya kampeni hiyo, aliacha kazi yake ya mshahara huko Hispania akahamia Bulgaria ili aunge mkono kutaniko jipya katika jiji hilo. Alikuwa ameweka akiba ya pesa za kutosha ambazo zingemsaidia kuishi Bulgaria kwa mwaka mmoja. Carina anasema hivi kuhusu uamuzi wake: “Ninafurahi sana kwamba Yehova ameniruhusu kutumika huku Bulgaria, na ninatumaini kwamba nitafaulu kubaki huku kwa muda mrefu zaidi. Tayari nina mafunzo matano ya Biblia na watatu kati yao wanahudhuria mikutano.”

Dada mmoja kutoka Italia alitaka kushiriki katika kampeni hiyo, lakini kwa sababu alikuwa tu amepata kazi mpya, hakuwa na siku za likizo. Bila kuogopa, aliomba likizo ya mwezi mmoja ambao hangelipwa mshahara na alikuwa tayari kuacha kazi ikiwa ombi lake lingekataliwa. Alishangaa msimamizi wa kazi alipomwambia hivi: “Ni sawa, lakini kuna sharti moja: Lazima unitumie kadi ya salamu ukiwa Bulgaria.” Bila shaka, dada huyo alihisi kwamba Yehova alikuwa amejibu sala zake.

Stanislava, dada ambaye ni kijana kutoka jiji la Varna huko Bulgaria na ambaye alikuwa anafanya kazi ya wakati wote ya mshahara mkubwa, aliomba ruhusa kazini ili ashiriki katika kampeni huko Silistra. Alipoona furaha ya mapainia wengi ambao walikuwa wamekuja kutoka mbali sana ili kuhubiri habari njema katika nchi yao, alitokwa na machozi. Alianza kufikiria jinsi alivyokuwa akitumia maisha yake, akifuatia kazi ya mshahara. Aliporudi nyumbani baada ya majuma mawili, aliacha kazi yake na akawa painia wa kawaida. Sasa ana furaha kwelikweli, akimkumbuka Muumba wake katika ujana wake.—Mhu. 12:1.

Ni baraka kama nini kushiriki kwa bidii katika utumishi wa Yehova. Hakuna jambo bora zaidi ambalo unaweza kufanya kuliko kutumia nguvu na wakati wako katika kazi ya maana ya kufundisha na kuhubiri habari njema. Je, kuna njia ambazo wewe binafsi unaweza kupanua utumishi wako katika huduma hii ya kuokoa uhai? Huenda kuna maeneo fulani katika nchi yenu ambayo yana uhitaji mkubwa zaidi. Je, unaweza kuhamia kwenye maeneo kama hayo? Au huenda ukafikiria kujifunza lugha nyingine ili uwasaidie watu katika nchi yenu ambao wana kiu ya kujua kweli ya Biblia. Haidhuru unafanya mabadiliko gani ili ushiriki zaidi katika huduma, unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakubariki sana.—Met. 10:22.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 32]

Siku ya Kukumbukwa

Wengi kati ya wale waliokuja kutoka nchi nyingine za Ulaya ili kuunga mkono kampeni ya pekee huko Bulgaria walipanga kuhudhuria Kusanyiko la Wilaya la “Endeleeni Kukesha!” huko Sofia. Lilikuwa jambo lenye kutia moyo sana kwa ndugu na dada wenyeji kukutana na wageni wengi sana kutoka nchi mbalimbali. Watu 2,039 waliohudhuria walisisimuka sana wakati Ndugu Geoffrey Jackson ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza alipotangaza kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kibulgaria! Wote waliokuwa wamehudhuria siku ya Ijumaa (Siku ya 5) walionyesha uthamini wao kutoka moyoni kwa kupiga makofi ya shangwe kwa muda mrefu. Wengi hata walitokwa na machozi ya shangwe. Tafsiri hiyo iliyo sahihi ambayo imeandikwa kwa lugha iliyo rahisi kueleweka itawasaidia Wabulgaria wenye mioyo minyoofu wamjue Yehova.

[Ramani katika ukurasa wa 30, 31]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

BULGARIA

SOFIA

Sandanski

Silistra

Kazanlak

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ushahidi mkubwa ajabu ulitolewa katika majuma hayo saba