Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutumika Wakati wa Ongezeko Kubwa Ajabu

Kutumika Wakati wa Ongezeko Kubwa Ajabu

Kutumika Wakati wa Ongezeko Kubwa Ajabu

Limesimuliwa na Harley Harris

Ilikuwa Septemba 2, 1950 (2/9/1950), huko Kennett, Missouri, Marekani. Tulikuwa katika kusanyiko la mzunguko, na tulikuwa tumezungukwa na umati wa watu. Meya wa mji huo alileta Jeshi la Kulinda Taifa ili kutulinda kutokana na umati huo wenye fujo. Askari-jeshi waliokuwa wameshika bunduki zenye visu walikuwa wamejipanga kando-kando ya barabara. Ingawa tulikuwa tukitukanwa na umati, tulitembea mpaka kwenye magari yetu na tukaelekea Cape Girardeau, Missouri, ili tuendelee na vipindi vya kusanyiko vilivyokuwa vimebaki. Nilibatizwa huko nikiwa na umri wa miaka 14. Lakini acheni niwasimulie jinsi nilivyoanza kumtumikia Yehova wakati huo wa msukosuko.

KATIKA miaka ya mapema ya 1930, babu yangu na nyanya yangu pamoja na watoto wao wanane walisikia hotuba fulani zilizokuwa zimerekodiwa za Ndugu Rutherford na wakasadiki kwamba walikuwa wamepata kweli. Wazazi wangu, Bay na Mildred Harris, walibatizwa mwaka wa 1935 kwenye kusanyiko lililofanywa huko Washington, D.C. Walisisimuka kama nini kuwa sehemu ya “mkutano mkubwa,” au “umati mkubwa,” ambao ulikuwa umetoka tu kutambulishwa kwenye kusanyiko hilo!—Ufu. 7:9, 14; Union Version.

Nilizaliwa mwaka uliofuata. Na mwaka mmoja baadaye, wazazi wangu wakahamia kwenye eneo la mbali huko Mississippi. Tulipokuwa tukiishi katika eneo hilo, hatukuwahi kamwe kutembelewa na mwangalizi anayesafiri. Familia yetu iliwasiliana na Betheli na tulihudhuria makusanyiko, na kwa muda fulani, huo tu ndio ushirika tuliokuwa nao na akina ndugu.

Kuvumilia Mateso

Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova waliteswa sana kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote katika vita. Tulikuwa tumehamia huko Mountain Home, Arkansas. Siku moja, mimi na baba yangu tulikuwa tukihubiri barabarani. Kwa ghafula, mwanamume fulani akamnyang’anya Baba magazeti, akayawasha moto, na kuyachoma papo hapo. Alituita waoga kwa sababu hatukwenda vitani. Kwa sababu nilikuwa na umri wa miaka mitano tu, nilianza kulia. Baba yangu alimtazama mwanamume huyo kwa utulivu bila kusema neno lolote mpaka mwanamume huyo alipoenda.

Kulikuwa pia na watu wazuri ambao walituunga mkono. Pindi moja, mwanasheria wa mashtaka aliyekuwa akiishi katika eneo hilo alipita na kuona umati ukiwa umezunguka gari letu. “Ni nini kinachoendelea hapa?” akauliza. Mwanamume mmoja akajibu hivi: “Hawa Mashahidi wa Yehova hawataki kupigania nchi yao!” Papo hapo mwanasheria huyo akapanda haraka juu ya sehemu ya kukanyagia ya gari letu na kusema hivi kwa sauti: “Nilipigana katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na nitapigana pia katika Vita vya Pili vya Ulimwengu! Waacheni watu hawa waende zao. Hawamuumizi mtu yeyote!” Umati huo ukatawanyika kimyakimya. Tuliwathamini sana watu wazuri kama hao ambao walituonyesha fadhili za kibinadamu.—Mdo. 27:3.

Tunatiwa Nguvu na Makusanyiko

Kusanyiko la mwaka wa 1941 lililofanyiwa huko St. Louis, Missouri, lilitupatia kitia-moyo tulichohitaji. Kulingana na kadirio moja, watu zaidi ya 115,000 walihudhuria. Idadi yenye kustaajabisha ya watu 3,903 walibatizwa! Ninakumbuka vizuri hotuba ya Ndugu Rutherford yenye kichwa “Watoto wa Mfalme.” Alizungumza moja kwa moja na sisi watoto, na sote tukapokea nakala ya kitabu maridadi cha rangi ya bluu kilichoitwa Children (Enfants). Kusanyiko hilo lilinitia nguvu kukabiliana na mambo yaliyofanyika mwaka uliofuata, mwaka ambao ningeanza kuhudhuria shule ya msingi. Mimi na binamu zangu tulifukuzwa shuleni kwa sababu ya kukataa kusalimu bendera. Tulirudi shuleni kila siku ili tuone kama wasimamizi wa shule walikuwa wamebadili maoni yao. Asubuhi nyingi tulitembea katikati ya msitu tukielekea shuleni na kila mara tulifukuzwa na kurudi nyumbani. Hata hivyo, niliona kwamba hiyo ilikuwa njia ya kuonyesha ushikamanifu wetu kwa Ufalme wa Mungu.

Hata hivyo, baada ya muda mfupi, Mahakama Kuu ya Marekani iliamua kwamba halikuwa jambo la lazima kusalimu bendera. Mwishowe, tulipata nafasi ya kuhudhuria shule. Mwalimu alitutendea kwa fadhili sana na akaturuhusu kujifunza masomo ambayo tulikuwa tumekosa. Wanafunzi wenzetu pia walitutendea kwa heshima.

Ninakumbuka pia kusanyiko lililofanywa huko Cleveland, Ohio, mwaka wa 1942, ambako Ndugu Nathan H. Knorr alitoa hotuba yenye kichwa “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Ufafanuzi huo wa Ufunuo sura ya 17 ulionyesha kwamba kipindi cha amani ya kadiri fulani kingekuwapo baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Kwa hiyo, ongezeko kubwa zaidi lilitarajiwa. Ili kujitayarisha kwa ajili ya maendeleo hayo, Shule ya Gileadi ilifunguliwa mwaka wa 1943. Sikujua kwamba shule hiyo ingekuwa na uvutano juu ya maisha yangu wakati ujao. Kwa kweli, baada ya vita, kipindi cha amani kilifuata na mateso yakakoma. Hata hivyo, Vita vya Korea vilipoanza mwaka wa 1950, kwa ghafula upinzani kuelekea kazi yetu ya kuhubiri ulianza tena, kama ilivyoelezwa mwanzoni.

Kushiriki Kikamili Zaidi Katika Ongezeko

Nilimaliza masomo yangu ya sekondari mwaka wa 1954, na mwezi mmoja baadaye nikaanza upainia. Baada ya kutumika huko Kennett, Missouri, ambako umati ulikuwa umetuzingira mwaka wa 1950, nilialikwa kutumika Betheli Machi (Mwezi wa 3) 1955. Kutaniko ambalo nilitumwa kushirikiana nalo lilihubiri pia katika eneo la Times Square, katikati ya jiji la New York City. Yalikuwa mabadiliko makubwa kwani nilikuwa nimezoea maisha ya mashambani! Niliweza kuanzisha mazungumzo na wakaaji wenye shughuli nyingi wa jiji la New York kwa kufungua gazeti kwenye makala yenye kuvuta fikira na kuuliza, “Je, umewahi kujiuliza swali hili?” Wengi walikubali kuchukua magazeti.

Moja kati ya pindi ambazo nilifurahia sana Betheli ni ibada ya asubuhi, ambayo ilikuwa ikiongozwa na Ndugu Knorr. Alikuwa akieleza vizuri sana maandiko ya Biblia na kuonyesha jinsi tunavyoweza kuyatumia kihalisi! Alizungumza nasi ndugu vijana tuliokuwa waseja kama vile baba anavyozungumza na mwana wake, mara nyingi akitupatia mashauri mazuri kuhusu jinsi tunavyopaswa kuwatendea watu wa jinsia tofauti. Kufikia mwaka wa 1960, nilikuwa nimeamua kufunga ndoa.

Nilituma ombi la kuondoka Betheli baada ya siku 30 lakini sikupokea majibu. Ingawa nilikuwa mwenye haya, baada ya siku hizo 30 kwisha, nilijipa ujasiri nikauliza kuhusu siku yangu ya kuondoka Betheli. Ndugu Robert Wallen ndiye aliyejibu simu yangu na akaja mahali nilipokuwa nikifanya kazi. Aliniuliza maoni yangu kuhusu kuwa painia wa pekee au mwangalizi wa mzunguko. Nikajibu hivi: “Lakini Bob, nina umri wa miaka 24 tu, na sina uzoefu.”

Naanza Kazi ya Mzunguko

Usiku huo nilipata bahasha kubwa ikiningoja chumbani. Ilikuwa na fomu mbili ndani yake, moja ya ombi la kuwa painia wa pekee na nyingine ya ombi la kazi ya mzunguko. Lo! Nilishangaa sana! Hivyo nikapata pendeleo ambalo sikustahili la kuwatumikia ndugu zangu nikiwa mwangalizi wa mzunguko katika eneo la kusini-magharibi mwa Missouri na mashariki mwa Kansas. Hata hivyo, kabla ya kuondoka Betheli nilihudhuria mkutano wa waangalizi wanaosafiri. Katika maneno yake ya kumalizia, Ndugu Knorr alisema hivi: “Kwa kuwa ninyi ni waangalizi wa mzunguko na waangalizi wa wilaya hilo halimaanishi kwamba mnajua mengi kuliko ndugu walio katika eneo. Wengine wao wana uzoefu mwingi kuliko ninyi. Lakini hali haziwaruhusu wawe na mapendeleo mliyo nayo. Mnaweza kujifunza mengi kutoka kwao.”

Hilo lilithibitika kuwa kweli kama nini! Ndugu Fred Molohan na mke wake pamoja na ndugu yake Charley aliyeishi huko Parsons, Kansas, walikuwa mifano bora kabisa. Walikuwa wamejifunza kweli katika miaka ya mapema ya 1900. Nilifurahi sana kusikia mambo waliyokuwa wamejionea hata kabla sijazaliwa! Ndugu mwingine ni John Wristen, ndugu mwenye fadhili aliyezeeka ambaye aliishi huko Joplin, Missouri, na ambaye alikuwa amefanya upainia kwa miaka mingi. Ndugu hao wapendwa waliheshimu sana mpango wa kitheokrasi. Walinifanya nihisi kwamba ninathaminiwa nikiwa mwangalizi wao wa mzunguko—ingawa bado nilikuwa kijana.

Mwaka wa 1962, nilimwoa Cloris Knoche, painia mchangamfu aliyekuwa na nywele nyekundu. Niliendelea katika kazi ya mzunguko pamoja na Cloris. Kwa sababu ya kuishi na akina ndugu, tuliwafahamu vizuri. Tuliwatia moyo vijana waanze utumishi wa wakati wote. Matineja wawili katika mzunguko wetu—Jay Kosinski na JoAnn Kresyman—walikuwa wakingojea kutiwa moyo kwa njia hiyo. Tulipohubiri pamoja nao na kuwaeleza kuhusu shangwe inayotokana na kuishi maisha ya kujinyima walichochewa kujiwekea miradi. JoAnn akawa painia wa pekee, na Jay akawa Mwanabetheli. Baadaye, hao wawili walioana, na wamekuwa wakifanya kazi ya mzunguko kwa miaka 30 hivi.

Utumishi wa Umishonari

Mwaka wa 1966, Ndugu Knorr alituuliza ikiwa tungependa kutumika katika nchi ya kigeni. Tulijibu hivi: “Tunafurahi kutumika mahali tulipo sasa lakini ikiwa kuna uhitaji mahali pengine, tuko tayari kusaidia.” Juma moja baadaye, tulialikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi. Nilisisimuka kama nini kurudi tena Betheli tulipohudhuria shule na kukutana na watu wengi ambao nilikuwa nimewapenda na kuwaheshimu! Tulianzisha urafiki pia na wanafunzi wenzetu, ambao bado wanatumikia kwa uaminifu mpaka leo.

Mimi na Cloris tulitumwa Ekuado huko Amerika Kusini, pamoja na Dennis na Edwina Crist, Ana Rodríguez, na Delia Sánchez. Ndugu na Dada Crist walienda kwenye jiji kuu, Quito. Sisi pamoja na Ana na Delia tulipewa mgawo wa kwenda Cuenca, ambalo ni jiji la tatu kwa ukubwa nchini Ekuado. Eneo letu lilitia ndani majimbo mawili. Kutaniko la kwanza huko Cuenca lilianzia katika chumba chetu cha sebule. Hudhurio lilitia ndani sisi wanne na watu wengine wawili. Tulijiuliza tungefanya jinsi gani kazi hiyo ya kuhubiri.

Jiji la Cuenca lilikuwa limejaa makanisa, na wakati wa siku zao takatifu, desturi za kidini zilifanywa kila mahali katika jiji hilo. Hata hivyo, wakaaji wa Cuenca walikuwa na maswali mengi. Kwa mfano, mara ya kwanza nilipokutana na Mario Polo, ambaye alikuwa mshindi wa mbio za baiskeli za Cuenca, alinishangaza kwa kuniuliza swali hili: “Ni nani kahaba anayetajwa katika kitabu cha Ufunuo?”

Pindi fulani, Mario alikuja nyumbani kwetu usiku akiwa na wasiwasi sana. Kasisi mmoja wa kanisa la kiinjilisti alikuwa amempa vitabu fulani ambavyo vilikuwa na mashtaka mazito kuhusu Mashahidi wa Yehova. Nilisababu naye kwamba mshtakiwa anapaswa kuruhusiwa ajitetee. Kwa hiyo siku iliyofuata, Mario alimwalika yule kasisi pamoja nami nyumbani kwake ili nijibu yale mashtaka. Katika mkutano huo nilipendekeza kwamba tuzungumzie fundisho la Utatu. Kasisi huyo aliposoma andiko la Yohana 1:1, Mario mwenyewe alieleza kwa usahihi maana ya andiko hilo. Na alifanya hivyo kwa kila mstari wa Biblia uliotajwa. Kwa hakika yule kasisi aliondoka bila kuthibitisha fundisho la Utatu. Hilo lilimsadikisha Mario na mke wake kwamba tulikuwa na kweli, nao wakawa wateteaji hodari wa mafundisho ya Biblia. Ni shangwe kama nini kuona makutaniko katika jiji la Cuenca yakiongezeka na kufikia 33 na jumla ya makutaniko 63 katika eneo kubwa ambalo lilikuwa mgawo wetu wa kwanza—ongezeko kubwa ajabu!

Kuona Ongezeko Nikiwa Katika Ofisi ya Tawi

Mwaka wa 1970, niliombwa niende kwenye ofisi ya tawi huko Guayaquil pamoja na Al Schullo. Sisi wawili tulifanya kazi ya ofisi ya tawi. Joe Sekerak alifanya kazi ya muda ya kupakia vichapo kwa ajili ya makutaniko 46 katika nchi yote. Kwa muda fulani, Cloris alifanya kazi ya kuhubiri akiwa mmishonari huku mimi nikitumika Betheli. Amewasaidia watu 55 kufikia ubatizo, mara nyingi alisaidia kati ya wanafunzi watatu na watano kubatizwa katika kusanyiko moja.

Kwa mfano, Cloris alijifunza na mwanamke mmoja anayeitwa Lucresia, ambaye alipingwa na mume wake. Ingawa hivyo, mwishowe Lucresia alibatizwa na akaanza kutumika akiwa painia wa kawaida. Aliwafundisha watoto wake njia za Yehova. Wanawe wawili sasa ni wazee wa kutaniko, na mmoja wao ni painia wa pekee; binti yake anatumika akiwa painia. Mjukuu wake aliolewa na ndugu mzuri, na wanatumika pia wakiwa mapainia wa pekee. Familia hiyo imewasaidia wengi kujifunza kweli.

Kufikia mwaka wa 1980, kulikuwa na wahubiri 5,000 hivi nchini Ekuado. Ofisi yetu ya tawi iliendelea kuwa ndogo kwa sababu ya ongezeko kubwa la wahubiri katika eneo. Ndugu mmoja alitupatia uwanja wa ekari 80 nje ya Guayaquil. Mwaka wa 1984 tulianza kujenga kwenye uwanja huo ofisi mpya ya tawi na Jumba la Kusanyiko, na majengo hayo yakawekwa wakfu mwaka wa 1987.

Watu Wengi Wajitolea Kusaidia Kuleta Ongezeko

Kwa miaka mingi ambayo imepita, limekuwa jambo lenye kuchangamsha moyo sana kuona wahubiri na mapainia wengi kutoka nchi nyingine wakija Ekuado ili kusaidia mahali penye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Mfano mmoja ambao ninakumbuka vizuri ni ule wa Andy Kidd, mwalimu wa shule aliyestaafu kutoka Kanada. Alihamia Ekuado mwaka wa 1985 akiwa na umri wa miaka 70 na akatumika kwa uaminifu mpaka alipokufa mwaka wa 2008 akiwa na umri wa miaka 93. Nilipomwona mara ya kwanza katika mgawo wake, alikuwa ndiye mwangalizi peke yake katika kutaniko moja dogo. Ingawa hakujua Kihispania vizuri, alitoa hotuba ya watu wote kisha akaongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi. Vilevile aliongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na akashughulikia sehemu nyingi katika Mkutano wa Utumishi! Katika eneo hilo, sasa kuna makutaniko mawili yanayofanya vizuri, ambayo yana wahubiri karibu 200 na wazee wengi wenyeji.

Ndugu mwingine, Ernesto Diaz, ambaye alihama kutoka Marekani pamoja na familia yake alisema hivi baada ya kuishi nchini Ekuado kwa miezi minane: “Watoto wetu watatu wamejifunza lugha ya huko na wamekuwa walimu bora. Nikiwa baba, nimefikia mradi ambao unaonekana kuwa mgumu kufikia katika mfumo huu—mradi wa kuwa painia wa kawaida, kushiriki katika utumishi wa wakati wote pamoja na familia yangu. Kwa ujumla, tunaongoza mafunzo 25 ya Biblia. Yote hayo yamefanya tuwe na umoja zaidi katika familia, na zaidi ya yote, nimemkaribia zaidi Yehova kuliko wakati mwingine wowote ule.” Tunawathamini kama nini ndugu na dada hao wapendwa!

Ofisi ya tawi ilipanuliwa tena mwaka wa 1994, ukubwa wake ukaongezeka mara mbili. Mwaka wa 2005, idadi ya wahubiri iliongezeka na kupita 50,000, na kukawa na uhitaji wa kupanua zaidi ofisi ya tawi. Kazi hiyo ilitia ndani kujenga Jumba kubwa zaidi la Kusanyiko na jengo jipya la makao, na pia ofisi za kutafsiri. Majengo hayo mapya yaliwekwa wakfu Oktoba 31, 2009.

Nilipofukuzwa shuleni mwaka wa 1942, kulikuwa na Mashahidi 60,000 hivi nchini Marekani. Sasa wako zaidi ya milioni moja. Tulipokuja Ekuado mwaka wa 1966, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme 1,400 hivi nchini. Sasa kuna wahubiri zaidi ya 68,000. Na bado wengine wengi watajiunga nasi kutokana na mafunzo ya Biblia 120,000 yanayoongozwa na zaidi ya watu 232,000 ambao walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka wa 2009. Kwa kweli, Yehova amewabariki watu wake kwa njia ambayo hatukuwahi kamwe kufikiria. Inasisimua kama nini kuishi wakati na mahali ambapo pamekuwa na ongezeko kubwa ajabu! *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 34 Habari hii ilipokuwa ikitayarishwa ili ichapishwe, Harley Harris alikufa akiwa mwaminifu kwa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kusanyiko lililofanywa nje (1981) na Jumba la Kusanyiko la Guayaquil (2009) kwenye uwanja uleule