Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafuta Baraka za Yehova kwa Bidii

Tafuta Baraka za Yehova kwa Bidii

Tafuta Baraka za Yehova kwa Bidii

“[Mungu] huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—EBR. 11:6.

1, 2. (a) Watu wengi wanatafuta jinsi gani baraka za Mungu? (b) Kwa nini tunapaswa kupendezwa kupata hasa baraka za Yehova?

“MUNGU akubariki!” Katika nchi nyingi, ni jambo la kawaida kuwasikia watu ambao wamekutana kwa mara ya kwanza wakisema maneno hayo mtu anapopiga chafya. Makasisi wa dini mbalimbali wanawabariki watu, wanyama, na vitu visivyo na uhai. Wasafiri wanavutiwa kutembelea maeneo fulani ya kidini wakitarajia kupata baraka. Mara nyingi, wanasiasa wanamwomba Mungu abariki taifa lao. Je, unafikiri kwamba sala kama hizo za kuomba baraka zinafaa? Je, sala hizo zina matokeo yoyote? Ni nani ambao kwa kweli wanapokea baraka za Mungu, na kwa nini?

2 Yehova alitabiri kwamba katika siku za mwisho, angekuwa na watu walio safi na wenye kufanya amani kutoka katika mataifa yote, ambao wangehubiri habari njema ya Ufalme mpaka miisho ya dunia hata ingawa wangechukiwa na kupingwa. (Isa. 2:2-4; Mt. 24:14; Ufu. 7:9, 14) Sisi ambao tumekubali daraka hilo la kuwa kati ya watu hao tunataka—na tunahitaji—baraka za Mungu, kwa sababu bila baraka hizo hatuwezi kufanikiwa. (Zab. 127:1) Hata hivyo, tunaweza kupata jinsi gani baraka za Mungu?

Watu Wanaotii Wanapata Baraka

3. Kungekuwa na matokeo gani ikiwa Waisraeli wangetii?

3 Soma Methali 10:6, 7Kabla tu ya taifa la Israeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Yehova alisema kwamba wangepata ufanisi mkubwa na ulinzi ikiwa wangetii sauti yake. (Kum. 28:1, 2) Baraka za Yehova hazingekuja tu juu ya watu wa Mungu lakini pia ‘zingewafikia.’ Kwa hakika kabisa, watu hao watiifu wangepata baraka hizo.

4. Kutii kikweli kunatia ndani nini?

4 Waisraeli walipaswa kutii wakiwa na mtazamo gani? Sheria ya Mungu ilisema kwamba hangefurahi ikiwa watu wake wangekosa kumtumikia “kwa kushangilia na shangwe ya moyo.” (Soma Kumbukumbu la Torati 28:45-47.) Yehova hataki tutii maagizo yake kidesturi tu, kama vile ambavyo wanyama au roho waovu wanavyoweza kutii. (Marko 1:27; Yak. 3:3) Tunapomtii Mungu kikweli tunaonyesha kwamba tunampenda. Utii huo unaonyeshwa kupitia shangwe inayotokana na imani ya kwamba amri za Yehova si mzigo mzito na kwamba Yehova “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Ebr. 11:6; 1 Yoh. 5:3.

5. Kuamini ahadi ya Yehova kungemsaidia jinsi gani mtu atii sheria iliyo katika Kumbukumbu la Torati 15:7, 8?

5 Hebu chunguza jinsi ambavyo utii huo unaotegemea imani ungeonyeshwa kwa kufuata sheria iliyoandikwa kwenye Kumbukumbu la Torati 15:7, 8. (Soma.) Huenda kutii sheria hiyo bila kupenda kungetokeza kitulizo cha muda kwa maskini, lakini je, kungetokeza mahusiano mazuri na hali ya uchangamfu kati ya watu wa Mungu? Na jambo la maana hata zaidi ni, je, kutii kwa aina hiyo kungeonyesha kwamba mtu ana imani katika uwezo wa Yehova wa kuwatimizia watumishi wake mahitaji yao na kwamba anathamini nafasi ya kuiga ukarimu wa Yehova? Hapana! Mungu aliona hali ya moyoni ya mtu aliye mkarimu kikweli na akaahidi kumbariki katika kila tendo lake na kila kazi ambayo angefanya. (Kum. 15:10) Kuamini ahadi hiyo kungemchochea mtu atende kwa ukarimu na hivyo kupata baraka nyingi.—Met. 28:20.

6. Andiko la Waebrania 11:6 linapaswa kutuhakikishia jambo gani?

6 Zaidi ya kuamini kwamba Yehova ni Mthawabishaji, andiko la Waebrania 11:6 linataja sifa nyingine ambayo tunahitaji ili tupate baraka za Mungu. Ona kwamba Yehova anawathawabisha wale “wanaomtafuta kwa bidii.” Neno la Kigiriki lililotumiwa hapa linamaanisha kuwa na bidii na juhudi nyingi sana. Hilo linatuhakikishia kabisa kwamba tunaweza kupata baraka! Chanzo cha baraka ni Mungu wa pekee wa kweli, “asiyeweza kusema uwongo.” (Tito 1:2) Ameonyesha kwa maelfu ya miaka kwamba mambo anayoahidi ni yenye kutegemeka kabisa. Maneno yake hayashindwi kamwe; sikuzote yanatimia. (Isa. 55:11) Hivyo basi, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba ikiwa tutaonyesha imani ya kweli, Mungu atathibitika kuwa Mthawabishaji wetu.

7. Tunaweza jinsi gani kujibariki kupitia “uzao” wa Abrahamu?

7 Yesu Kristo alithibitika kuwa sehemu ya msingi ya “uzao” wa Abrahamu. Wakristo waliotiwa mafuta ndio wanaofanyiza sehemu ya pili ya “uzao” huo uliotabiriwa. Wamepewa agizo la ‘kutangaza kotekote sifa bora zake yeye aliyewaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ (Gal. 3:7-9, 14, 16, 26-29; 1 Pet. 2:9) Hatuwezi kutazamia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova ikiwa tutawapuuza wale ambao Yesu amewachagua kutunza mali zake. Bila msaada wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” hatungeweza kamwe kuelewa kikamili yale tunayosoma katika Neno la Mungu wala hatungejua jinsi ya kuyatumia katika maisha yetu. (Mt. 24:45-47) Tukizoea kufanya yale ambayo tunajifunza katika Maandiko, tunaweza kujipatia baraka za Mungu.

Kukazia Fikira Mapenzi ya Mungu

8, 9. Mzee wa ukoo Yakobo alijitahidi jinsi gani kutenda kulingana na maombi yake?

8 Tunapofikiri kuhusu kujitahidi kabisa ili kupata baraka za Mungu, huenda tukamkumbuka mzee wa ukoo Yakobo. Hakujua jinsi ambavyo Mungu angetimiza ahadi yake kwa Abrahamu, lakini aliamini kwamba Yehova angewazidisha sana wazao wa babu yake, na wazao wao wangekuwa taifa kubwa. Kwa hiyo, mwaka wa 1781 K.W.K., Yakobo alisafiri kwenda Harani ili kutafuta mke. Hakuwa tu akitafuta mwanamke ambaye angekuwa mwenzi mzuri; badala yake, alitafuta mwanamke aliyemwabudu Yehova na kupenda mambo ya kiroho na ambaye angekuwa mama mzuri wa watoto wake.

9 Tunajua kwamba Yakobo alikutana na Raheli ambaye alikuwa mtu wake wa ukoo. Alikuja kumpenda Raheli na akakubali kumfanyia kazi baba yake, Labani, kwa miaka saba ili awe mke wake. Hii haikuwa hadithi tu ya uhusiano wa kimapenzi usioweza kusahaulika. Bila shaka, Yakobo alijua ahadi ambayo Mungu Mweza-Yote alikuwa amempa Abrahamu, babu yake, na alikuwa ameirudia tena ahadi hiyo kwa baba yake, Isaka. (Mwa. 18:18; 22:17, 18; 26:3-5, 24, 25) Naye Isaka akamwambia hivi Yakobo, mwana wake: “Mungu Mweza-Yote atakubariki na kukufanya uzae na kukuzidisha, nawe utakuwa kutaniko la vikundi vya watu. Naye atakupa baraka ya Abrahamu, wewe na uzao wako pamoja nawe, ili upate kumiliki nchi ya makao yako ya kigeni, ambayo Mungu amempa Abrahamu.” (Mwa. 28:3, 4) Kwa hiyo, jitihada ambazo Yakobo alifanya ili kumpata mke anayefaa na kutokeza familia zilionyesha uhakika wake katika maneno ambayo Yehova alikuwa amesema.

10. Kwa nini Yehova alipendezwa kumbariki Yakobo?

10 Yakobo hakuwa akitafuta utajiri ili aitunze familia yake. Alikuwa akifikiria ahadi za Yehova kuhusu wazao wake. Alikazia fikira kutimizwa kwa mapenzi ya Yehova. Yakobo alikuwa ameazimia kufanya yote ambayo angeweza ili kupata baraka za Mungu ingawa alikabili vizuizi. Aliendelea kuwa na mtazamo huo mpaka alipozeeka, na Yehova alimbariki kwa sababu ya mtazamo huo.—Soma Mwanzo 32:24-29.

11. Ni jitihada gani ambazo tunapaswa kufanya kulingana na kusudi la Mungu lililofunuliwa?

11 Kama Yakobo, hatujui mambo yote yanayohusika katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Hata hivyo, tunapojifunza Neno la Mungu, tunaona kwa ujumla mambo ambayo tunapaswa kutazamia kuhusiana na “siku ya Yehova.” (2 Pet. 3:10, 17) Kwa mfano, hatujui wakati kamili ambao siku hiyo itakuja, lakini tunajua kwamba iko karibu. Tunaamini Neno la Mungu linaposema kwamba tukitoa ushahidi kamili katika kipindi kifupi kilichobaki, tutajiokoa sisi wenyewe na wale wanaotusikiliza pia.—1 Tim. 4:16.

12. Tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo gani?

12 Tunatambua kwamba mwisho unaweza kuja wakati wowote; Yehova hatalazimika kungoja mpaka kila mtu duniani ahubiriwe. (Mt. 10:23) Zaidi ya hayo, tunapata mwongozo mzuri kuhusu jinsi ya kufanya kazi yetu ya kuhubiri kwa njia inayofaa. Kwa imani, tunashiriki katika kazi hiyo kwa uwezo wetu wote, tukitumia mali zozote tulizo nazo. Je, sikuzote tutahubiri katika eneo lenye matokeo zaidi? Kwa kweli, tunaweza jinsi gani kujua hilo kimbele? (Soma Mhubiri 11:5, 6.) Kazi yetu ni kuhubiri, tukiamini kwamba Yehova atatubariki. (1 Kor. 3:6, 7) Tunaweza kuwa na hakika kwamba anaona jitihada zetu nyingi, na kupitia roho yake takatifu atatupatia mwongozo wowote hususa ambao tunahitaji.—Zab. 32:8.

Kutafuta Roho Takatifu

13, 14. Uwezo wa roho takatifu ya Mungu wa kuwawezesha watumishi wake kufanya kazi umeonekana jinsi gani?

13 Namna gani ikiwa tunahisi kwamba hatustahili kufanya mgawo fulani au kushiriki katika kazi ya kuhubiri? Tunapaswa kumwomba Yehova atupatie roho yake takatifu ili tuboreshe uwezo wowote tulio nao katika utumishi wake. (Soma Luka 11:13.) Roho ya Mungu inaweza kufanya watu wastahili kutimiza kazi fulani au kupata pendeleo fulani la utumishi bila kutilia maanani hali zao au uzoefu waliokuwa nao mbeleni. Kwa mfano, mara tu baada ya Waisraeli kutoka Misri, roho ya Mungu iliwawezesha wachungaji na watumwa hao kuwashinda maadui wao katika vita ingawa hawakuwa na uzoefu katika vita. (Kut. 17:8-13) Muda mfupi baadaye, roho hiyohiyo ilimwezesha Bezaleli na Oholiabu kufanya kazi bora sana ya kutimiza mipango iliyoongozwa na roho ya Mungu ya kujenga maskani.—Kut. 31:2-6; 35:30-35.

14 Roho hiyo yenye nguvu iliwawezesha watumishi wa Mungu katika siku zetu kushughulikia mahitaji ya tengenezo wakati hali zilipowalazimisha kuanza kuchapisha wenyewe vichapo vyao. Ndugu R. J. Martin, ambaye alikuwa mwangalizi wa kiwanda wakati huo aliandika barua na kueleza hivi kuhusu kazi ambayo ilikuwa imetimizwa kufikia mwaka wa 1927: “Kwa wakati unaofaa, Bwana alifungua mlango; tukapata mashini kubwa ya kuchapisha, hata ingawa hatukujua jinsi ya kuiunganisha na kuitumia. Lakini Bwana anajua jinsi ya kuwazoeza haraka wale ambao wamejitoa kabisa kwake. . . . Katika muda wa majuma machache sana, tulifanikiwa kuendesha mashini hiyo; na bado inafanya kazi mpaka sasa, na inafanya kazi ambayo hata wale ambao waliitengeneza hawakujua kamwe kwamba inaweza kufanya.” Yehova ameendelea kubariki jitihada kama hizo zenye bidii mpaka leo.

15. Maneno ya Waroma 8:11 yanaweza kuwatia moyo jinsi gani wale ambao wanapambana na kishawishi?

15 Roho ya Yehova inafanya kazi katika njia mbalimbali. Watumishi wote wa Mungu wanaweza kuipata roho hiyo, na inawasaidia kushinda vizuizi vikubwa. Namna gani tukihisi kwamba tumelemewa na kishawishi fulani? Tunaweza kutiwa nguvu na maneno ya Paulo yaliyo katika Waroma 7:21, 25 na 8:11. Ndiyo, “roho ya yule aliyemfufua Yesu kutoka kwa wafu” inaweza kutenda kwa ajili yetu, na kututia nguvu ili tushinde vita juu ya tamaa za kimwili. Maneno hayo yaliandikwa kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta, hata hivyo, kanuni hiyo inawahusu watumishi wote wa Mungu. Sisi sote tunapata uzima kwa kuwa na imani katika Kristo, kwa kujitahidi kuua tamaa zisizofaa, na kwa kuishi kulingana na mwongozo wa roho.

16. Ni lazima tufanye nini ili tupate roho takatifu ya Mungu?

16 Je, tunaweza kumtazamia Mungu atupatie nguvu zake za utendaji ikiwa hatujitahidi hata kidogo? Hapana. Zaidi ya kusali ili tupewe roho hiyo, ni lazima tujilishe kwa bidii Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu. (Met. 2:1-6) Zaidi ya hayo, roho ya Mungu inakaa juu ya kutaniko la Kikristo. Tunapohudhuria mikutano kwa ukawaida tunaonyesha kwamba tunatamani ‘kusikia yale ambayo roho inayaambia makutaniko.’ (Ufu. 3:6) Kwa kuongezea, ni lazima tutii kwa unyenyekevu mambo tunayojifunza. Andiko la Methali 1:23 linatushauri hivi: “Geukeni mpate karipio langu. Ndipo mimi nitafanya roho yangu ibubujike juu yenu.” Kwa kweli, Mungu anawapa roho takatifu “wale wanaomtii yeye akiwa mtawala.”—Mdo. 5:32.

17. Tunaweza kulinganisha matokeo ya baraka za Mungu juu ya jitihada zetu na nini?

17 Ingawa tunahitaji kujitahidi kwa bidii ili kupata baraka za Mungu, kumbuka kwamba Yehova hawapi watu wake vitu vingi vizuri kwa sababu tu ya kazi yao ngumu. Tunaweza kulinganisha matokeo ya baraka zake juu ya jitihada zetu na jinsi miili yetu inavyofaidika kutokana na chakula kizuri. Mungu aliumba miili yetu kwa njia ya kwamba tunafurahia chakula na kupata lishe muhimu kutokana na chakula hicho. Yeye pia, anaandaa chakula hicho. Hatujui kikamili jinsi chakula chetu kinavyopata lishe au vitu vinavyojenga mwili, wala wengi wetu hatuwezi kueleza jinsi miili yetu inavyotokeza nguvu kutokana na chakula tunachokula. Tunachojua ni kwamba utaratibu huo unafanya kazi na tunashirikiana nao kwa kula chakula. Tunapochagua kula chakula kinachojenga mwili, matokeo yanakuwa bora hata zaidi. Vivyo hivyo, Yehova anaweka matakwa ya kupata uzima wa milele, na anatupatia msaada tunaohitaji ili kutimiza matakwa hayo. Ni wazi kwamba yeye ndiye anayefanya kazi nyingi na anastahili kusifiwa. Hata hivyo, ni lazima tushirikiane naye, na kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu, ili tupokee baraka hizo.—Hag. 2:18, 19.

18. Umeazimia kufanya nini, na kwa nini?

18 Kwa hiyo, jitahidi kabisa kutimiza kila mgawo kwa moyo wako wote. Mtegemee Yehova sikuzote ili ufanikiwe. (Marko 11:23, 24) Unapofanya hivyo, uwe na hakika kwamba “kila mtu anayetafuta hupata.” (Mt. 7:8) Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho watabarikiwa kwa kupewa “taji la uzima” huko mbinguni. (Yak. 1:12) “Kondoo wengine” wa Kristo, ambao wanajitahidi kujibariki kupitia uzao wa Abrahamu, watafurahi kumsikia Kristo akisema hivi: “Njooni, ninyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Yoh. 10:16; Mt. 25:34) Ndiyo, “wale wanaobarikiwa [na Mungu] wataimiliki dunia, . . . nao watakaa milele juu yake.”—Zab. 37:22, 29.

Je, Unaweza Kueleza?

• Utii wa kweli unatia ndani nini?

• Tunahitaji kufanya nini ili tupate baraka za Mungu?

• Tunaweza kupata jinsi gani roho takatifu ya Mungu, na inaweza kutenda kwa ajili yetu jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yakobo alipigana mweleka na malaika ili apate baraka za Yehova.

Je, unajitahidi kwa bidii vivyo hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Roho takatifu ya Mungu ilimwezesha Bezaleli na Oholiabu kufanya kazi bora kabisa